• Na Issa Mwadangala.

    Madereva wa vyombo vya moto wanaofanya safari zao Barabara ya Mbeya-Tunduma wametakiwa kuacha tabia ya kuendesha vyombo hivyo kwa mazoea ili kupunguza ajali za barabarani.


    Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Raphael Magoma aliyasema hayo jana wakati akitoa elimu kwa madereva na abiria katika eneo la ukaguzi wa magari lililopo Chimbuya Wilaya ya Mbozi Mkoa wa Songwe huku akiwataka kufuata sheria na miongozo ya usalama barabarani.


    “Mnapaswa kujitathmini na kuacha tabia ya kufanya kazi kwa mazoea”,alisema Magoma.

    Alisema kila safari ni ya kipekee na inahitaji umakini wa hali ya juu kulinda maisha maisha ya watu wasio na hatia.

    Aidha, aliwataka madereva hao kuzingatia sheria za usalama barabarani ikiwemo kutozidisha mwendo, kutoendesha wakiwa wamelewa na kuhakikisha vyombo vyao vya usafiri vipo katika hali nzuri kabla ya safari.

    “Ninawataka abria mtoe taarifa kuhusu madereva wazembe ili hatua za haraka zichukuliwe dhidi yao”, alisema Magoma.

  • Na Vincent Mpepo

    Vijana wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Mtaa wa Kwembe wameelezea mafanikio, fursa na changamoto zinazowakabili katika safari ya kujikwamua kichumi kama sehemu ya jamii huku wakitoa rai kwa washarika na jamii kuwaunga mkono katika harakati zao.

    Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa Vijana Mtaani hapo, Abel Mvungi Siku ya Jumapili ambayo kwa kalenda ya KKKT ilikuwa ni Siku ya vijana ambapo vijana hao walitumia siku hiyo kuonesha talanta zao katika maonesho ya kazi za mikono, bidhaa na huduma wazitoazo kama sehemu ya shuhguli wazifanyazo ili kukuza mfuko wao na kujikwamua kichumi.

    Alisema pamoja na kumtumikia Mungu katika utume na shughuli mbalimbali za kikanisa wanahitaji kuungwa mkono na washarika na jamii ya wanakwembe ili waendelee kuwa imara kiuchumi na hivyo kupunguza utegemezi kwa wazazi na walezi.

    “Tunaomba muendelee kutushika mkono katika miradi mbalimbali ikiwemo huu wa matunda na mbogamboga ili kuisukuma mbele idara ya vijana katika kutekeleza malengo yake ya kuwainua vijana”, alisema Abel.

    Akizungumzia mafanikio ya umoja huo mtaani hapo, alisema wa Mwaka jana 2024 umoja huo ulifanikiwa kuhudhuria Kongamano la vijana jijini Arusha amabalo lililenga kuwafundisha vijana kumjua Mungu na namna bora ya kuishi katika jamii inayowazunguka.

    “Viongozi walipata safari ya kwenda Dodoma kwa ajili ya kongomano la kiuongozi”, alisema Abel.

    Alibainisha mafanikio mengine kuwa ni kuwawezesha vijana 103 kushiriki Tamasha la Twen’zetu kwa Yesu lililofanyika Kawe jijini Dar es salaam na kuwashukuru washarika wa Mtaa huo kwa kuwaunga mkono katika ununuzi wa tiketi kwa baadhi ya vijana ili washiriki katika kongamano hilo.

    Alisema Mwaka 2024 umoja huo uliazimia kuanzisha mradi wa pikipiki tatu yaani bodaboda kwa kufanya harambee ndogo Tarehe 7/7/2024 ambazo zingetumiwa na vijana kanisani kama sehemu ya ajira na kuuzalishia mfuko wa vijana fedha. 

    “Katika harambee hiyo tulifanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi 1,300,000/ taslimu na ahadi za shilingi 2,600,000/ ambazo hazijalipwa mpaka leo hivyo kufanya mradi huo kutokufanikiwa kwa wakati”, alisema Abel.

    Mhubiri wa siku hiyo, Kresensia Kabala alizungumzia umuhimu wa vijana kuwa na nidhamu katika kila walifanyalo kwani kupitia nidhamu ndio inaonesha thamani ya ujana katika jamii  kinyume na hilo ni kuonekana hawafai.

    “Jitengenezee mazingira yatakayowakosesha watu na jamii sababu za kukukudharau”, alisema Kresensia.

    Aliwataka vijana kufanya kazi na wakati mwingine kutochagua kazi hata kama wamesoma hususani wakati huu ambapo kuna changamoto ya upatikanaji wa ajira.

    Aidha aliwaasa wazazi kuwafundisha kazi watoto wao ili waweze kujitegemea badala ya kuwalea kama mayai kitu ambacho ni janga katika masiha yao ya baadaye kama akina baba na akina mama watarajiwa.

    “Matatizo mengi katika ndoa yanatokana  na msingi mbovu wa malezi katika familia”, alisema Kresensia.

    Aliwaasa vijana wa kike na wa kiume wanaosoma kutumia vizuri muda wao shuleni na vyuoni katika kuandaa kesho yao na kuacha tamaa kwani itasababisha upotevu wao na kuwapa majonzi wazazi na walezi amabao hutumia rasilimali zao kuhakikisha wanapata elimu.

    Mchunganji Dkt. Mwatumai Mwanjota alihudumu katika ibada hiyo na huduma za kichungaji kadhaa zilifanyika ikiwemo ubatizo na huduma ya chakula cha Bwana.

    Siku hiyo ilipambwa na uimbaji kutoka kwa vijana huku huduma zote kanisani hapo zikiendeshwa nao jambo  lililoonesha hazina kubwa ya talanta na vipawa mbalimbali kwa vijana hao ambao wakipewa nafasi wanaweza kuidhihirishia jamii thamani yao.

  • Wimbo maalum kwa ajili ya kumpa heshima Mt. Yosefu. Ni wa kusikiliza (Audio), kutafakari, na kuomba ulinzi wa Mt. Yosefu. Furahia kazi ya sanaa kutoka kwa Wanakwaya wa Kwaya ya Damu Takatifu ya Yesu, Tegeta, Dar es Salaam, Tanzania.

  • Na Vincent Mpepo

    Makamu Mkuu wa chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Profesa Alex Makulilo amewataka wafanyakazi wa chuo hicho kubadilika kifikra na kiutendaji ili kuendana na ushindani katika mifumo ya uendeshaji taasisi za elimu ya juu kutoka ndani na nje ya nchi.

    Profesa Makulilo alitoa wito huo jana wakati wa mkutano wake wa kwanza na wafanyakazi wa chuo hicho akihudumu kwa nafasi hiyo mara baada ya uteuzi wake mapema Mwezi Juni, 2025.

    Alisema sura ya elimu ya juu hivi sasa imebadilika sana na kwamba kwa kuangalia mwenendo wanaweza kuelewa kinachoendelea huku mabadiliko hayo yakiathiri soko la chuo hicho.

    “Idadi ya vyuo vikuu na vyuo vikuu huria imeongezeka kwenye nchi ambazo hazikuwa navyo”, alisema Profesa Makulilo.

    Alisema idadi ya wanafunzi wa kimataifa kutoka nje ya nchi imepungua akitolea mfano wa idadi ya wanafunzi wa uzamili kutoka Kenya kwa mwaka wa masomo wa 2022/2023.

    “Takwimu zinaonesha idadi ya wanafunzi wa uzamili kutoka Kenya imepungua kutoka wanane (08) hadi sita (06) maana yake ushindani umeongezeka”, alisema Profesa Makulilo.

    Aidha alizungumzia ushindani kutoka ndani ambao umetokana na vyuo vikuu vingine hapa nchini kutoka kwenye mfumo wa mazoea wa madarasa na kuingia kwenye mfumo wa elimu huria na masafa yaani (ODL).

    “Wengine wameenda mbele zaidi na kuanza kujenga vituo vya mikoa na wanaviita majina kama kampasi za kilimo, elimu bahari au madini na kadhalika”, alisema Profesa Makulilo.

    Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Mipango, Fedha na Utawala, Profesa Josiah Katani aliwakumbusha wafanyakazi wa chuo hicho taratibu za utumishi wa umma ikiwemo kuwahi kazini, kuomba ruhusa wanapokuwa safari au kukumbwa na changamoto yoyote.

    “Barua zinazoenda uongozi wa juu lazima zipitishwe kwa msimamizi wako wa kazi”, alisema Profesa Katani.

    Aliwaasa watumishi kuomba likizo kwa kutumia mfumo, kuhakiki taarifa zao na waende likizo kwa tarehe walizojaza kwenye kwenye mfumo na ikitokea kuna mabadiliko ni lazima wapate kibali kwa uongozi.

    Profesa Katani aliwakumbusha  wafanyakazi wa chuo hicho kujaza kujaza kwa wakati majukumu yao katika mfumo wa usimamizi wa utendaji kazi katika utumishi wa umma yaani (PEPMIS)ili kuondokana na adha ya kutopanda vyeo.

    “Alama za chini kabisa kwa mfanyakazi ni 75%”, alisema Profesa Katani.

    Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Taaluma, Utafiti wa Ushauri wa Kitaalamu, Profesa Saganga Kapaya aliezea maendeleo ya uhuishaji na utengenezaji wa mitaala na kubainisha kuwa zoezi hilo linaendelea vizuri.

    Alisema idadi ya mitaala ya programu katika shahada za awali, uzamili na uzamivu zilizowasilishwa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania ni 109 baada ya kupitishwa kwenye kamati za maamuzi za juu za chuo hicho.

    Aidha aliwataka wafanyakazi wa chuo hicho kuboresha huduma kwa mteja ili kutoa huduma nzuri zitakazowafanya wanafaunzi waliodahiliwa kuendelea na masomo chuoni hapo badala ya kuhama au kuacha.

    Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za. Elimu ya Juu Tanzania tawi la Chuo Kikuu Huria cha Tanzania Salatiel Chaula akizungumza kwa niaba ya wafanyakazi wa chuo hicho alisema wamepokea maelekezo wapo tayari kwa utekelezaji  ili kusukuma mbele gurudumu la taasisi hiyo.

  • Na Mwandishi Wetu

    Mtangazaji mstaafu wa Redio Tanzania Dar es Salaam (RTD), Edda Sanga, ameelezea kukerwa na utangazaji wa mzaha na ucheshi unaovunja miiko ya tasnia hiyo kwa kuwa madai kuwa studio ni eneo la kuheshimiwa sio kupiga kelele au kurushiana maneno.

    Sanga alitoa kauli hiyo jana wakati wa mafunzo kwa watangazaji chipukizi kutoka vyuo vya kati, yaliyoandaliwa kama sehemu ya maadhimisho ya miaka 74 ya utangazaji Tanzania.

    Alisema heshima ya utangazaji imepungua kwa sababu baadhi ya walipewa nafasi za utangazaji hawana wala maadili jambo linalosababisha wasikilizaji kuacha kufuatilia vipindi na maudhui kwa ujumla.

    “Studio ni eneo la heshima, utangazaji sio kupiga kelele wala eneo lakurushiana maneno,” alisema Sanga.

    Akizungumzia eneo la uandaaji wa maudhui katika vipindi vya mahojiano, Sanga alisema lina udhaifu mkubwa kwa sababu baadhi ya waandishi wa habari hususani wa kizazi kipya,hawajiandai wanapotaka kufanya mahojiano na kuzalisha maudhui ambayo hailengi kuisaidia jamii.

    Alisema suala la waandishi wa habari kushindwa kuwatafuta watu mahususi ambao ni vyanzo vya kuaminika kuzungumzia mada badala yake huwatumia wale wanaopatikana mara kwa mara na kushauri kuwatafuta watu wenye weledi na maarifa ya kuzunngumza mada husika.

    “Eneo la mahojiano bado lina changamoto kwa baadhi ya waandishi hawajiandai ipasavyo, wala hawatafuti watu sahihi wenye ujuzi wa kuzungumzia mada husika hivyo kuathiri ubora wa taarifa zinazozalishwa,” alisema Bi Edda.

    Katika mafunzo hayo, washiriki walijadili kuhusu hali ya kizazi kipya katika kulinda maadili ya kitaifa na uzalendo ambapo wazungumzaji walieleza hofu yao juu ya kupotea kwa misingi ya mshikamano wa kijamii kutokana na mabadiliko ya kiteknolojia.

    Balozi Christopher Liundi, alisema kukosekana kwa uzalendo miongoni mwa vijana kunachangiwa na kutopatiwa elimu mapema kuhusu umuhimu wa suala hilo,pamoja na athari zamatumizi ya simu na mitandao ya kijamii.

    “Siku hizi rafiki mkubwa wa watu amekuwa ni simu hakuna tena upendo wa kweli wala urafiki wa dhati kama zamani, watu hawatembeleani, hawatafutani tena kama enzi zetu,” alisema Balozi Liundi.

    Alisema redio na vyombo vya habari kwa ujumla vina nafasi kubwa ya kusaidia kurejesha maadili ya kijamii, lakini hilo linawezekana tu endapo watangazaji na waandishi wa habari watafanya kazi zao kwa kuzingatia weledi, maadili na dhamira ya kuelimisha jamii.

    Debora Mwenda ni miongoni mwa waandishi wakongwe tangu uhuru alisema anakerwa na baadhi ya matamshi ya baadhi ya watangazaji wa kisasa ambao hushindwa kutamka majina ya nchi ikiwemo Tanzania na miji mingine mikubwa duniani.

    Mjumbe wa Bodi ya Chama cha Watangazaji Wakongwe wa Redio Tanzania Dar es Salaam (RTD), Judica Losai alisema kutokana na kukua kwa teknolojia kunahitajika kuandaliwa vipindi au maudhui inayotumia dakika chache ikiwa na ubora unaotakiwa ili kumvutia msikilizaji.

  • Na Vincent Mpepo

    Watangazaji wakongwe wa iliyokuwa Redio Tanzania Dar es salaam (RTD) ambayo kwa sasa ni sehemu ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) wametumia siku ya maadhimisho ya miaka 74 ya utangazaji Tanzania kubalishana uzoefu na waandishi wa habari watangazaji chipukizi ili kuhakikisha wanarithisha amali njema katika tasnia ya hiyo.

    Wakizungumza wakati wa mafunzo ya siku moja yaliyofanyika jana katika Ukumbi wa Break Point Kijiji cha Makumbusho jijini Dar es salaam, wakongwe hao wamesema licha ya kukua kwa sayansi na teknolojia kunakoigusa tasnia ya habari hususani utangazaji misingi ya uandishi wa habari haijabadilika.

    Akifungua mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Chama cha Wakongwe wa Redio Tanzania Dar es salaam, Suleiman Kumchaya alisema madhumuni ya mafunzo hayo ni kubadishana mawazo na waandishi wa habari watangazaji kwa kuelezea uzoefu waliokuwa nao kwa miaka kadhaa kama sehemu ya mchango wao kwa tasnia ya habari.

    “Unapojali kazi yako siku zote utasikiliza na kufuatilia kinachoendelea katika tasnia yako”, alisema Kumchaya.

    Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini ya chama hicho, Balozi Mstaafu, Christopher Liundi alisema mafunzo hayo ni muhimu kwa waandishi wa habari watangazaji kwa kuwa yatasaidia kurudisha taaluma hiyo katika misingi lakini imekuwa fursa nzuri ya pamoja kujadili changamoto na fursa zilizopo.

    Balozi Liundi alisema msingi wa taaluma ya uandishi wa habari umejikita katika kulinda maslahi ya umma kwa kuwa wafanyacho kila seku ni sehemu ya elimu waitowayo na hawana budi kujiongezea maarifa kila iitwapo leo na ndio maana hata miundo ya ajira na kiserikali inatambua suala hilo.

    “Uandishi wa habari ni taaluma yenye mifumo yenye viwango vya juu vinavyofahamika na kupimika hivyo ni muhimu kwa waandishi kuiheshimu kwa kufuata taratibu, kanuni na sharia ambazo kila mhusika atawajibika kwazo”, alisema Balozi Liundi.

    Alisema ni muhimu kwa waandishi watangazaji kuzingatia misingi ya taaluma hiyo inayowataka wawajibike kwa umma kwa uadilifu unaozingatia usahihi, umahiri na weledi katika kazi zao.

    Makamu Mwenyekiti wa Wakongwe RTD, Jacob Tesha alizungumzia changamoto ya maudhui ya vyombo vya habari kutoka nje yanayotumiwa na baadhi ya vyombo vya habari na athari zake katika utamaduni wetu na kuwataka waandishi wa habari wasomi kuzalisha vipindi vyenye asili ya kitanzania ili kulinda utamaduni wetu.

    Kwa upande wake Mkufunzi wa Masomo ya Habari na Mawasilinao ya Umma kutoka Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Bujo Ambosisye aliwashukuru wakongwe hao kwa kujali na kujitoa kwao kwa ajili ya waandishi wa habari chipukizi na kwamba ni mara ya pili kwake kukutana na wakongwe hao katika mafunzo hayo.

    ‘Niliwahi kukutana na baadhi ya wakongwe katika tasnia ya habari miaka kadhaa ilyopita wakati wa maazimisho ya wiki ya ukombozi wa bara Afrika na kimsingi tunanafaika sana na uwepo wenu”, alisema Ambosisye.

    Katika mafunzo hayo mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwemo misingi ya uandishi wa habari za redio, uandishi wa habari za redio kabla na baada ya maendeleo ya teknolojia, changamoto katika kipindi kisichokuwa cha uchaguzi na kipindi cha uchaguzi.

  • Na Vincent Mpepo

    Wanawake walio kwenye ndoa wametakiwa kuwasaidia waume zao katika majukumu ya kifamilia kwa kufanya kazi badala ya kuwa wategemezi na walalamishi ili kuwapunguzia msongo wa mawazo na vifo waume zao.

    Kauli hiyo imetolewa jana na Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Kiinjili Kilutheri Tanzania (KKKT), Ismail Mwipile wa Usharika wa Segerea jijini Dar es salaam wakati wa mahubiri ya ibada ya ndoa ambapo Mfanyakazi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania Stewart Kaberege alifunga pingu za masiha na Bi Suzana Kweka.

    Alisema kwa miaka ya hivi karibuni kumekuwa na ongezeko la wajane linatokana na changamoto za ndoa ambazo kwa kiasi fulani zinasababisha na msongo wa mawazo kwa wanaume kutokana na kuzidiwa kimawazo, majukumu na wakati mwingine kutopata msaada kutoka kwa wake zao.

    “Niwakumbushe wanawake mlio kwenye ndoa kuwatii, kuwaheshimu na kuwasaidia waume zenu majukumu ili mzeeke pamoja”, alisema Mchungaji Mwipile.

    Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Profesa Alex Makulilo ambaye aliongoza wafanyakazi wa chuo hicho katika hafla za sherehe ya ndoa ya Stewart Kaberege alisema ndoa si jambo lelemama kwani linahitaji wawili walioamua kuishi pamoja kuwa na akili za ziada.

    Aliwapongeza maharusi hao kwa hatua hiyo muhimu na kuwataka kuishi kwa kadiri ya maelekezo ya dini na Imani yao.

    Aidha aliwaasa kuzaa watoto wengi ili kuijaza dunia kama maandiko yanavyowataka wakristo kufanya hivyo.

    “Stewart na mkeo msijibane sana, nendeni mkazae kuijaza dunia”, alisema Profesa Makulilo

    Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi, Ntimi Kasumo aliwakaribisha wageni na kuwashukuru kwa michango yao ya hali na mali ambayo imesaidia kufanikisha hafla hiyo na kwamba alisimia 20 ya michango hiyo imewekwa kwenye akaunti ya maharusi hao kama zawadi.

    Uchunguzi uliofanywa na mwandishi umebaini kutokuwepo kwa umoja kati ya wafanyakazi wa chuo hicho husasani kati ya watumishi wanataaluma na waendeshaji kutokuwa na mizania katika matukio mengi ya kijamii.

  • Na Tabia Mchakama

    Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imeshuhudia ulipwaji wa fidia kwa Bi. Bahati Ngowi kufuatia kufuatia kifo cha mume wake Profesa Ngowi aliyepata ajali ya gari maeneo ya Mlandizi Kibaha mkoani Pwani tarehe 28 Machi 2022.

    Akishuhudia tukio hilo Kamishna wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania, Dkt. Baghayo Saqware alizitaka kampuni za bima kuhakikisha zinalinda na kutetea haki za wateja wao wa bima wanapopatwa na majanga ili kuleta utulivu na ahueni kwa waathirika.

    Aidha alimshukuru Mhe. Waziri Mkuu, Kassimu Majaliwa kwa kumuelekeza mhanga huyo mahali sahihi lakini na kuipongeza kampuni ya bima ya Mayfair kwa kumpatia mama huyo fidia stahiki iliyoendana na janga bila ya usumbufu wowote.  

    “Ninawaalika watanzania kuja TIRA ikiwa mtakutana na changamoto yoyote ya kibima”, alisema Kamishna Dkt. Saqware.

    Kwa upande wake, mnufaika wa bima, Bi. Bahati Ngowi alisema TIRA imekuwa msaada mkubwa kwa sababu alianza kufuatilia madai hayo mahakamani mara baada ya ajali kutokea na mwaka 2025 alielekezwa kufika TIRA na Mhe. Waziri Mkuu wa Tanzania, Majaliwa Kasim Majaliwa.

    Kampuni ya bima ya Mayfair imemlipa Bi. Bahati Ngowi kiasi cha shilingi milioni mia moja na arobaini na tano (145,000,000).

  • Kwaya ya watoto wa shule ya Jumapili wakihudumu katika ibada SiKu ya Jumapili (picha na Vincent Mpepo).

    Na Vincent Mpepo

    Mtenda Kazi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Anna Mauki amewataka washarika wa kanisa hilo kuona fahari ya umoja wa makanisa yaliyoungana na kuwa kanisa moja kwa kuwa ndani yake kuna mafanikio mengi.

    Bi. Anna Mauki aliyasema hayo Siku ya Jumapili wakati wa mahubiri na kuwataka wakristo wa sasa kuona kuwa wana sehemu ya kufanya ili kuhakikisha historia ya kanisa hilo kwa miaka 62 ijayo inakuwa na kumbukumbu nzuri zaidi kwa wao kuhusika katika mambo mbalimbali.

    Alisema waasisi wa umoja huo walifanya vitu na maono yao ndiyo yanayoonesha mafanikio ya kanisa kwa sasa kupitia kazi, shughuli na huduma mbalimbali zilizopo akitaja baadhi kama hospitali, vyombo vya habari, shule za msingi na sekondari pamoja na vyuo vikuu ambavyo vinamilikiwa na kanisa na vina mchango kwa jamii.

    “Tupende kazi za umoja kwakuwa ni kazi za Mungu”, alkisema Bi.Mauki.

    Alisema kanisa liendelee kuwaandaa watoto kuja kuwa wakristo wawajibikaji siku zijazo na kwamba maanadalizi hayo huanzia katika ngazi ya familia.

    “Kanisa lina utaratibu mzuri wa kuwapokea watoto tangu wakiwa wadogo na limeendelea na programu mbalimbali katika makuzi yao mpaka utu uzima”, alisema Bi.Mauki.

     Alisema na bado familia ina wajibu mkubwa kuhakikisha inafuatilia makuzi na mwenendo wa mtoto ili awe mkristu mwajibikaji.

    Aidha aliwataka wakristo kuacha tabia ya kufuatilia mambo yasiyowahusu na badala yake wajikite katika yanayowahusu.

    Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi Mtaani hapo, Exaud Mchome alitoa taarifa ya maendelep ya ujenzi na kwamba kwa kwa wiki ile ujenzi haukuenda vizuri kutokana na mafundi wanaofanya kazi hiyo kutofikia viwango stahiki.

    Aliwashukuru washarika kwa kuendelea kujitoa kwa ajili ya kazi ya ujenzi unaoendelea kanisani hapo na kusisitiza ambao bado hawajakamilisha ahadi zao kwa awamu ya kwanza ya Januari hadi Juni kukamilisha ili kupisha zoezi la mavuno lililopo mbele.

    Wakati huo huo, Mwinjilsti Kiongozi wa Mtaa huo, Emeline Mnzava aliwashukuru wazazi waliowaruhusu vijana wao kushiriki Tamasha la Twenzetu kwa Yesu kwani licha ya kuwa ni mtoko ni sehemu ambayo imewapa mafunzo yatakayowasaidia kuikulia Imani.

    Aidha, aliwakumbusha washarika kuendelea kutoa sadaka ya mfuko wa elimu kwa kuwa ina majukumu ya kusaidia watoto wengi kupata elimu.