• Na Cosmas Msuha

    Wananchi wa Kimara, Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam, wanatarajia kuondokana na changamoto za usafiri baada ya ujenzi wa Barabara ya TRA–King’ong’o unaoendelea kwa kiwango cha zege kufikia hatua nzuri.

    Hayo yalisemwa na Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), Catherine Sungura, wakati wa Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma.

    Alisema katika ujenzi wa barabara hiyo zimebaki kilomita 1.6, ambapo mita 800 zinatarajiwa kujengwa kuanzia Julai mwaka huu, huku sehemu iliyosalia ikikamilishwa katika awamu inayofuata.

    Sungura alisema TARURA itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara ili kurahisisha usafiri, kuimarisha mawasiliano na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

    Akizungumzia huduma zinazotolewa katika banda la TARURA, alisema wananchi wanaowasilisha kero zao huunganishwa moja kwa moja na mameneja wa mikoa au wilaya husika ili kupata majibu na ufumbuzi kwa wakati.

    Kwa upande wake, mkazi wa Kimara, Sarah James Joseph, alisema ameridhishwa na maelezo aliyopata kuhusu maendeleo ya ujenzi wa barabara hiyo baada ya kuwasiliana na Meneja wa TARURA Wilaya ya Ubungo kupitia banda la wakala huo.

    Tangu kuanza kwa Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, zaidi ya wananchi 300 wametembelea banda la TARURA kupata taarifa na ufafanuzi kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya barabara nchini.

  • Na George Mwamba

    Viongozi na maafisa kutoka taasisi mbalimbali za usalama za Tanzania na Msumbiji wamekutana mjini Songea kujadili na kubadilishana uzoefu kuhusu makosa na uhalifu wa kuvuka mipaka, pamoja na kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya kiusalama.

    Mkutano huo wa siku mbili ulioanza jana katika Ukumbi wa Heritage Cottage, Manispaa ya Songea, Mkoa wa Ruvuma, umezikutanisha pande hizo mbili kwa lengo la kuweka mikakati ya pamoja ya kudhibiti uhalifu wa kuvuka mipaka na kuimarisha usalama wa wananchi.

    Akifungua mkutano huo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Mkuu wa Wilaya ya Nyasa, Perres Magiri, alisema ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na Msumbiji ni muhimu katika kudumisha amani, usalama na utulivu katika maeneo ya mipakani.

    Alisema mikutano ya aina hiyo imeendelea kuwa jukwaa muhimu la kujenga mahusiano mazuri, kuimarisha mawasiliano na kutafuta suluhisho la pamoja kwa changamoto za kiusalama zinazojitokeza katika maeneo ya mipaka.

    Kwa mujibu wa Magiri, washiriki wa mkutano huo wanatarajiwa kujadili masuala mbalimbali yanayohusu usalama wa wananchi, udhibiti wa uhalifu wa kuvuka mipaka, usimamizi wa mipaka na namna ya kuendeleza ushirikiano wa kiutendaji kati ya vyombo vya usalama vya Tanzania na Msumbiji kwa manufaa ya mataifa yote mawili.

    Kabla ya kuanza kwa kikao hicho, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Marco Chilya, alimtambulisha Kamanda wa Jimbo la Niassa, Kamishna Msaidizi wa Polisi Celestino Albano Vianeque, kwa washiriki wa mkutano.

  • Na Cartace Ngajiro, Tanga

    Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Wilaya ya Temeke, Mhe. Uzairu Athumani, ameipongeza Serikali kwa uwekezaji mkubwa uliofanyika katika Bandari ya Tanga, akisema umeongeza uwezo wa bandari hiyo kuhudumia hadi meli 600 kwa mwaka na kufungua fursa nyingi za kiuchumi.

    Mhe. Athumani alitoa kauli hiyo alipofanya ziara ya mafunzo katika Bandari ya Tanga, akiwa ameambatana na madiwani pamoja na watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Temeke. Ujumbe huo ulipokelewa na Meneja wa Bandari ya Tanga, Bw. Salehe Mbega.

    Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Athumani alisema wamevutiwa na historia, maendeleo na maboresho makubwa yaliyofanyika katika Bandari ya Tanga, akieleza kuwa uwekezaji huo umeifanya bandari kuwa kitovu muhimu cha biashara na uchumi katika ukanda wa kaskazini mwa Tanzania.

    “Kwa maelezo tuliyoyapata hapa, ni wazi kuwa Bandari ya Tanga ni mfano wa mafanikio ya uwekezaji wa kimkakati unaochochea ukuaji wa uchumi na kufungua fursa za biashara na uwekezaji,” alisema Mhe. Athumani.

    Aliongeza kuwa lengo la ziara hiyo halikuwa kujifunza shughuli za bandari pekee, bali pia kutambua na kutathmini fursa mbalimbali za uwekezaji zinazopatikana ili kuona namna Halmashauri ya Temeke na wadau wake wanavyoweza kunufaika nazo.

    Kwa upande wake, Meneja wa Bandari ya Tanga, Bw. Salehe Mbega, alisema bandari hiyo imeendelea kupanua wigo wa huduma zake kwa kuhudumia masoko ya nchi jirani, ikiwemo Zimbabwe, huku matarajio yakiwa ni kuanza kuhudumia pia shehena za kutoka Sudan Kusini.

    Alisema maboresho yaliyofanyika yameongeza kwa kiasi kikubwa uwezo wa bandari, ambapo kiwango cha shehena kinachohudumiwa kimeongezeka kutoka tani 700,000 hadi tani milioni mbili kwa mwaka huku kukiwa na ongezeko la meli zinazotia nanga kutokana na kuimarika kwa miundombinu na ufanisi wa huduma.

    Bw. Mbega aliwahimiza madiwani na wadau wengine kutumia fursa zilizopo kuwekeza katika miradi ya bandari kavu na shughuli nyingine zinazochochea ukuaji wa biashara na uchumi.

  • Na Jastini Bukebuke

    Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, SACP Safia Jongo, ameongoza maofisa na askari wa Jeshi la Polisi, wanachama wa Ulinzi Shirikishi pamoja na Geita Jogging Club kushiriki mazoezi maalumu yaliyoandaliwa na Idara ya Afya ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita ikiwa ni sehemu ya kuhitimisha maadhimisho ya Siku ya Sikoseli Duniani.

    Akizungumza wakati wa shughuli hiyo, Mratibu wa Magonjwa Yasiyoambukiza kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita, Dkt. Glory Temba, alisema maadhimisho hayo yamelenga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu ugonjwa wa sikoseli, athari zake, mbinu za kujikinga nao pamoja na kuhamasisha mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.

    Dkt. Temba alisema kufanya mazoezi ya mwili kwa angalau dakika 30 kila siku ni muhimu katika kuboresha afya ya mwili na akili, huku akisisitiza umuhimu wa kuzingatia mtindo bora wa maisha ili kupunguza hatari ya magonjwa yasiyoambukiza.

    Aidha, aliwataka wananchi kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara na kufuata ushauri wa wataalamu wa afya ili kuimarisha ustawi wa jamii na kuongeza tija katika shughuli za maendeleo.

    Mazoezi hayo ya mchakamchaka yaliwakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya afya pamoja na wananchi, yakianzia Viwanja vya Kalangalala na kuhitimishwa katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Kalangalala.

    Maadhimisho hayo yalihitimishwa kwa wito wa kuendeleza ushirikiano kati ya wadau mbalimbali katika kuelimisha jamii kuhusu ugonjwa wa sikoseli, kuhamasisha uchunguzi wa afya na kuimarisha mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.

  • Na Jastini Bukebuke

    Mkuu wa Wilaya ya Chato, Mhe. Louis Bura, amefunga rasmi mafunzo maalumu ya Ulinzi Shirikishi kwa washiriki 1,001 kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Geita na Manispaa ya Geita, akisisitiza umuhimu wa ushiriki wa wananchi katika kuimarisha usalama na kulinda mali za umma na binafsi.

    Hafla ya kufunga mafunzo hayo ilifanyika jana katika Viwanja vya GGM, Kata ya Kalangalala, mkoani Geita, ambapo Mhe. Bura alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela. Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML), Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita pamoja na viongozi mbalimbali wa serikali na wadau wa usalama.

    Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Bura alisema mafunzo hayo yamewajengea washiriki uelewa na ujuzi wa kutekeleza dhana ya ulinzi shirikishi kwa ufanisi, ikiwemo mbinu za kukabiliana na vitendo vya uvamizi, wizi wa mawe ya madini na uhalifu mwingine unaolenga mali za GGML pamoja na maeneo mengine muhimu ya kiuchumi.

    Alisema usalama wa jamii na uwekezaji ni msingi muhimu wa maendeleo, hivyo wananchi wanapaswa kushiriki kikamilifu katika kuzuia na kutoa taarifa za vitendo vya uhalifu vinavyoweza kuhatarisha amani na ustawi wa jamii.

    Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, SACP Safia Jongo, alisema kuwa ulinzi na usalama ni jukumu la kila mwananchi na kwamba washiriki wa mafunzo hayo wamewezeshwa kushiriki kikamilifu katika kubaini, kuzuia na kupambana na vitendo vya uhalifu ndani ya maeneo yao.

    Alieleza kuwa mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi endelevu za Jeshi la Polisi za kuimarisha ushirikiano kati ya wananchi na vyombo vya dola katika kudumisha amani, usalama na utulivu wa jamii.

    Naye Mtendaji Mkuu wa GGML, Ashraf Suryaningrat, aliwapongeza wahitimu wote pamoja na Jeshi la Polisi kwa ushirikiano mkubwa uliofanikisha utekelezaji wa programu ya Ulinzi Shirikishi, akibainisha kuwa programu hiyo imeendelea kuleta matokeo chanya katika kuimarisha usalama wa mgodi na maeneo yanayouzunguka.

    Suryaningrat alisema GGML itaendelea kushirikiana na serikali pamoja na vyombo vya usalama katika kutekeleza mipango mbalimbali inayolenga kulinda rasilimali za taifa na kuchangia maendeleo ya jamii zinazozunguka mgodi.

    Akihitimisha hafla hiyo, Mhe. Bura aliwataka wahitimu kutumia maarifa na ujuzi walioupata kuendelea kuimarisha ulinzi wa raia na mali zao, kuongeza weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku, kushiriki doria katika maeneo muhimu na kulinda miundombinu ya kimkakati.

    Alisisitiza kuwa mazingira salama na yenye utulivu ni nguzo muhimu katika kuvutia uwekezaji, kukuza shughuli za kiuchumi na kuharakisha maendeleo ya Mkoa wa Geita na Taifa kwa ujumla.

  • Na Jastini Bukebuke

    Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Mbogwe, SP Yusuph Chiwanga, amewataka Sungusungu na wananchi wa Kijiji cha Luhala, Kata ya Lugunga, kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi wanapotekeleza majukumu yao ya ulinzi na usalama.

    Akizungumza katika kikao cha uhamasishaji wa usalama wa jamii, SP Chiwanga alisema ni muhimu kwa Sungusungu kuzingatia nidhamu, maadili na taratibu za kisheria wakati wa kuwakamata watuhumiwa, badala ya kutumia nguvu kupita kiasi.

    Alieleza kuwa utendaji unaozingatia sheria na haki huchangia kujenga imani kwa wananchi na kuondoa malalamiko yanayoweza kujitokeza katika jamii.

    Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kushirikiana na Sungusungu pamoja na Jeshi la Polisi katika kudumisha amani na utulivu, huku akisisitiza kuwa kila mmoja ana wajibu wa kufuata sheria na taratibu zilizowekwa.

    Kwa upande wake, Mkaguzi wa Polisi wa Kata ya Masumbwe, INSP Oliver Kasembe, aliwahimiza Sungusungu na wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za wahalifu na vitendo vya uhalifu vinavyotokea katika maeneo yao.

    Alisema ushirikiano huo ni nguzo muhimu katika mapambano dhidi ya uhalifu, huku akiwataka wananchi kutofumbia macho vitendo vya kihalifu vinavyoweza kuhatarisha usalama wa jamii.

    INSP Kasembe pia alitoa rai kwa wananchi kuachana na migogoro inayotokana na kulishiana mazao, akieleza kuwa migogoro hiyo imekuwa chanzo kikubwa cha migongano miongoni mwa wakazi wa kijiji hicho.

    Naye Mkaguzi wa Polisi, INSP Nuru Mdugo, alikemea vitendo vya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto, huku akiwataka wananchi kujiepusha na matendo hayo ambayo yanaathiri ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.

    Alisisitiza umuhimu wa wazazi na walezi kuwapatia watoto malezi bora yenye misingi ya maadili mema na kumcha Mungu, ili kujenga kizazi chenye nidhamu na kinachopinga vitendo vya ukatili.

    “Malezi bora ndiyo msingi wa kujenga jamii salama na yenye maadili. Ni wajibu wa kila mzazi na mlezi kuhakikisha watoto wanakua katika mazingira yanayowajenga kuwa raia wema,” alisema INSP Mdugo.

  • Na Cosmas Msuha

    SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) imeingia makubaliano ya ushirikiano (MoU) na Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa maafa nchini kupitia matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu.

    Akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Dkt. Jim James Yonazi, alisema hatua hiyo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya kujenga mifumo madhubuti ya kiutendaji inayoongozwa na maarifa, sayansi na teknolojia, ikiwemo matumizi ya Akili Unde (AI) katika kukabiliana na maafa.

    Alisema makubaliano hayo yanatekeleza mapendekezo ya Mkutano wa Nane wa Umoja wa Mataifa wa Jukwaa la Dunia la Upunguzaji wa Vihatarishi vya Maafa uliofanyika Geneva, Uswisi, mwezi Juni 2025.

    “Vyuo vikuu na taasisi za utafiti, ikiwemo Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam, vina jukumu muhimu la kuzalisha maarifa na suluhisho za kisayansi zitakazosaidia kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini,” alisema Dkt. Yonazi.

    Alisema ili kuhakikisha utekelezaji madhubuti wa makubaliano hayo, Serikali itaandaa mpango kazi wa utekelezaji pamoja na Ajenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Usimamizi wa Maafa, ambayo itabainisha maeneo ya kipaumbele yanayohitaji ufumbuzi wa kisayansi na kiteknolojia.

    Aidha, alisisitiza kuwa mafanikio ya makubaliano hayo yatapimwa kwa matokeo halisi yatakayochangia kuongeza usalama wa wananchi, kulinda rasilimali za taifa na kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam, Prof. Preksedis Marco Ndomba, alisema taasisi hiyo imeandika historia kwa kusaini makubaliano ya ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu, akibainisha kuwa mchakato wa kufanikisha ushirikiano huo ulianza muda mrefu na sasa umeanza kuzaa matunda.

    “Tunaahidi kutekeleza na kufanikisha makubaliano haya kwa kuwa tuna uwezo na utaalamu wa kutosha. Tutaendelea kushirikiana katika masuala ya vihatarishi vya kitaifa ili kufanikisha adhima hii ya Serikali,” alisema Prof. Ndomba.

    Ushirikiano huo unaelezwa kuendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inaweka msisitizo katika matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu kama nguzo muhimu za maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii nchini.

  • Na Cosmas Msuha

    Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo amekutana na watanzania waishio Jamhuri ya Korea na kuwahimiza kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa Tanzania kwa kuitangaza nchi na fursa mbalimbali katika sekta za uwekezaji, biashara na utalii.

    Akizungumza katika mkutano uliofanyika jana jijini Seoul, Balozi Dkt. Kombo alisema ni muhimu kwa watanzania kuifahamu vizuri nchi wanayoishi, ikiwemo tamaduni, lugha, sheria na mifumo ya kijamii ili waweze kujumuika na kujenga uhusiano chanya unaoweza kuleta manufaa kwa Taifa.

    Balozi Dkt. Kombo aliwakumbusha kutumia majukwaa mbalimbali ya kitaaluma, kijamii na kibiashara kuitangaza Tanzania na fursa zinazopatikana katika nchi wanazoishi ili kuvutia wawekezaji, watalii na wadau wa maendeleo kushirikiana na Tanzania.

    Aidha aliwaasa wanafunzi wa elimu ya juu nchini humo kujikita katika tafiti zinazolenga kutatua changamoto mbalimbali nchini Tanzania hususan katika sekta za afya, maji, elimu na mazingira.

    Kwa upande wake, Rais wa Jumuiya ya watanzania nchini Korea, Eliusta Filikunjombe alieleza utayari wao wa kuendelea kushirikiana na serikali katika kutangaza fursa na kuimarisha mahusiano kati ya Tanzania na Jamhuri ya Korea.

    Balozi wa Tanzania nchini Korea, Mhe. Noel Kaganda alisema idadi ya watanzania nchini humo inafikia 300 ambayo inajumuisha wafanyakazi, wafanyabiashara na wanafunzi.

    Balozi Dkt. Kombo yupo nchini Korea kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Korea na Afrika, unaolenga kuimarisha ushirikiano na mahusiano ya kidiplomasia, kiuchumi na maendeleo kati ya Korea na nchi za Afrika.

  • Na Cosmas Msuha

    WAZIRI Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amekagua ujenzi wa Barabara ya Noranga (Doroto)–Itigi (Mlongojii) yenye urefu wa kilomita 25 inayojengwa katika Halmashauri ya Itigi, Wilaya ya Manyoni, mkoani Singida kwa gharama ya shilingi bilioni 29.6.

    Dkt. Mwigulu amefanya ukaguzi huo leo wakati akipokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kutoka kwa Mkurugenzi wa Miradi wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mhandisi Japherson Nnko.

    Katika taarifa hiyo, Dkt. Mwigulu alielezwa kuwa hadi Mei 30, 2026, mradi huo ulikuwa umefikia asilimia 83.25 ya utekelezaji ambapo kati ya kilomita 25 zinazojengwa, kilomita 20.2 zimekamilika kwa kiwango cha lami, huku kilomita 4.8 zilizobaki zikiwa zimefikia hatua ya tabaka la juu la msingi na zinatarajiwa kukamilika mwezi Juni 2026.

    Mhandisi Nnko alisema kipande hicho ni sehemu ya Barabara ya Mbeya–Chunya–Makongolosi–Rungwa–Itigi–Mkiwa yenye urefu wa kilomita 524, inayounganisha mikoa ya Mbeya, Singida na Tabora na kwamba barabara hiyo inatarajiwa kuboresha usafirishaji wa watu, bidhaa na mazao katika ukanda huo hivyo kuchochea shughuli za kiuchumi.

    Aliongeza kuwa mradi huo unagharamiwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Tanzania na unatekelezwa na Kampuni ya China Henan International Cooperation Group Co. Ltd (CHICO) kwa gharama ya shilingi bilioni 29.6, bila kujumuisha Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).

    Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kazi za ujenzi zilianza Septemba 16, 2022 na zinatarajiwa kukamilika mwezi Agosti 2026 baada ya mkandarasi kuongezewa muda wa utekelezaji kwa mujibu wa masharti ya mkataba.

    Hadi Mei 30, 2026, mkandarasi ameshalipwa shilingi bilioni 12.9, huku akiidai Serikali shilingi bilioni 3.84. Aidha, Mhandisi Mshauri amelipwa shilingi bilioni 1.49 na anadai shilingi milioni 586.6.

    Taarifa hiyo pia ilieleza kuwa wananchi 578 walioathiriwa na utekelezaji wa mradi huo wamelipwa fidia ya jumla ya shilingi milioni 721.4 kwa mujibu wa sheria.

    Katika utekelezaji wa mradi huo, jumla ya ajira 305 zimezalishwa, ambapo ajira 278 sawa na asilimia 91 zimetolewa kwa wazawa na ajira 27 sawa na asilimia 9 zimetolewa kwa wageni.