
Na Cosmas Msuha
Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) imeshiriki Jukwaa la Biashara lililofanyika sambamba na Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), kwa lengo la kutangaza fursa za uwekezaji, biashara na kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali wa sekta ya madini.
Jukwaa hilo limewakutanisha wafanyabiashara, wawekezaji na wadau kutoka mataifa mbalimbali kujadili mikakati ya kukuza biashara, uwekezaji na masoko ya ndani na kimataifa.
Akifungua mkutano huo, Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara ya Ndani kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara, Semeo Manongi, alisema Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuwezesha sekta binafsi kufanya shughuli zake kwa ufanisi, usalama na tija, hatua inayochangia ukuaji wa uchumi wa taifa.
Alieleza kuwa jukwaa hilo, lililoandaliwa na Benki ya Equity Tanzania katika Viwanja vya Mwalimu Julius K. Nyerere jijini Dar es Salaam, limewakutanisha wajumbe 51 kutoka mataifa mbalimbali na kufanyika sambamba na maonesho ya Sabasaba.
Manongi alibainisha kuwa maonesho ya Sabasaba yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza bidhaa, huduma na fursa za uwekezaji, huku yakifungua masoko mapya kwa taasisi, kampuni na wafanyabiashara wa ndani na nje ya nchi.
Kwa upande wake, Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Benki kwa Wateja Binafsi wa Benki ya Equity Tanzania, Theresia Mayanie, aliwahimiza wawekezaji na wafanyabiashara kutumia huduma za benki hiyo, akieleza kuwa Equity imejipanga kutoa huduma bora na ushirikiano wa karibu kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa.
Ushiriki wa GST katika jukwaa hilo unaonyesha dhamira ya taasisi hiyo ya kutangaza huduma zake, kuonesha fursa zilizopo katika sekta ya madini na kujenga ushirikiano na wawekezaji pamoja na wadau wengine kwa lengo la kuendeleza sekta hiyo na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Tanzania.
Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yalianza rasmi Juni 28, 2026 na yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13, 2026. Maonesho hayo yamewakutanisha zaidi ya kampuni 200 za kimataifa na washiriki kutoka mataifa mbalimbali, yakitoa fursa za biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi.


























