
Na Mwandishi Wetu, Haydom, Manyara
Madereva wa magari na pikipiki katika Mji Mdogo wa Haydom, Wilaya ya Mbulu mkoani Manyara, wamekumbushwa kuendelea kuzingatia sheria za usalama barabarani ili kupunguza ajali na kulinda maisha ya watumiaji wa barabara.
Wito huo umetolewa na Koplo (CPL) Andrea Mbona wa Kikosi cha Usalama Barabarani Haydom, ambaye aliwataka madereva kuzingatia taratibu zote za usalama, ikiwemo kufunga mikanda wanapoendesha magari na kuzingatia alama mbalimbali za barabarani.
Alisisitiza umuhimu wa kuwa makini wanapofika kwenye vivuko vya watembea kwa miguu na maeneo yanayovukwa na wanyama, akieleza kuwa kufuata sheria na tahadhari hizo kutasaidia kupunguza ajali za barabarani.
Mmoja wa madereva, Emanuel Evarist, alisema anashukuru kwa elimu hiyo ya usalama barabarani, akieleza kuwa wakati mwingine madereva huendesha kwa mazoea na kusahau kuzingatia sheria.

Alisema elimu hiyo ni muhimu kwa kuwa inawakumbusha madereva wajibu wao wa kuendesha kwa kuzingatia sheria na kuongeza kuwa inapaswa kutolewa mara kwa mara ili kuendelea kujenga uelewa na nidhamu barabarani.
Naye dereva, Israel Mohe, amelipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kutoa elimu kwa madereva na watumiaji wengine wa barabara.

“Kwa kweli, mimi kama dereva ninalipongeza Jeshi la Polisi kwa namna linavyoendelea kutoa elimu ya usalama barabarani. Kwa kipindi hiki, jeshi limejikita zaidi katika utoaji wa elimu kuliko ilivyokuwa hapo awali,” alisema Mohe.
Alisema utoaji wa elimu una mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa madereva na watumiaji wengine wa barabara, hatua inayosaidia kuimarisha usalama na kupunguza ajali.


























