• Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Rukwa, Jacqueline Mzindakaya akizungumza na baadhi ya vyombo vya habari kuhusu utekelezaji wa bima ya afya kwa wote.

    Na Cosmas Msuha

    Serikali imepongezwa kwa kuendelea kutekeleza mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, hatua inayolenga kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za afya bila kujali uwezo wake wa kifedha.

    Pongezi hizo zimetolewa na Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Rukwa, Jacqueline Mzindakaya, wakati akishiriki katika zoezi la kugawa kadi za mfano za bima ya afya kwa walengwa wenye mahitaji maalum, wakiwemo watoto na mama wajawazito.

    Katika tukio hilo, Mbunge huyo aligawa kadi 30 za mfano kati ya jumla ya kadi 48,500 zilizotengwa kwa Mkoa wa Rukwa kwa ajili ya kaya zisizo na uwezo.

    Akizungumza katika semina iliyowakutanisha walengwa wa kaya maskini pamoja na wadau wa maendeleo mkoani humo, Mzindakaya alisema kuwa mpango huo ni hatua muhimu ya kusaidia wananchi wasio na uwezo kupata huduma za afya bila vikwazo vya kifedha.

    Katika hotuba yake, alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutimiza ahadi yake aliyoitoa katika siku 100 za mwanzo wa uongozi wake ya kuhakikisha Watanzania wasiojiweza wanapatiwa bima ya afya bure.

    “Mpango huu unalenga kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa na uhakika wa kupata matibabu bila kujali hali yake ya kipato,” alisema Mzindakaya.

    Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Rukwa, Amos Edward, alisema serikali imejipanga kuhakikisha mpango huo unatekelezwa kwa ufanisi ili wananchi waweze kunufaika kikamilifu.

    Alisema juhudi zinafanyika kuhakikisha vituo vyote vya afya vinavyotoa huduma chini ya mpango huo vinakuwa na dawa na vifaa tiba vya kutosha.

    Aidha, aliwakumbusha watoa huduma katika hospitali kuhakikisha wanatoa huduma bora kwa wananchi wote bila ubaguzi, huku wakizingatia matumizi ya lugha ya staha na kuwahudumia kwa usawa wote wanaofika hospitalini, ikiwemo wanaolipia huduma kwa fedha taslimu.

    “Tunatarajia kuwa na vifurushi mbalimbali vitakavyowezesha kila kaya kupata bima itakayowanufaisha katika kupata huduma bora zaidi za afya,” alisema Edward.

    Naye Mwenyekiti wa Kata ya Kiwango, Paulin Nikasi, aliipongeza serikali kwa kuanzisha mpango huo na kuwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kujiunga na bima ya afya ili kupata matibabu kwa urahisi.

    Alisisitiza umuhimu wa kuwapa kipaumbele makundi maalum kama wazee, mama wajawazito na watoto wanapofika hospitalini ili wapate huduma kwa wakati.

    “Ni jambo jema kwa sababu mpango wa bima ya afya kwa wote utamfikia kila Mtanzania. Zamani watu wengi walipoteza maisha kutokana na kushindwa kumudu gharama za matibabu,” alisema Nikasi.

    Sambamba na masuala ya afya, semina hiyo pia ilitoa elimu ya ujasiriamali kwa wananchi, ambapo washiriki walipata mafunzo kuhusu fursa za mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri.

    Mafunzo hayo yaliwasilishwa na Afisa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga, Noela Munis, ikiwa ni sehemu ya jitihada za serikali kuwawezesha wananchi kujikwamua kiuchumi na kuboresha maisha yao.

  • Na Mwandishi Wetu

    Mtandao wa Polisi Wanawake Mkoa wa Ruvuma (TPF–NET) umeendelea kuonyesha moyo wa kujali jamii baada ya kutembelea na kutoa msaada kwa watoto wenye mahitaji katika Kituo cha kulelea watoto yatima cha Mfaranyaki, kilichopo Manispaa ya Songea, mkoani Ruvuma.

    Ziara hiyo iliongozwa na Mwenyekiti wa TPF–NET Mkoa wa Ruvuma, Mrakibu wa Polisi (SP) Atupakisye Mwakasutu, aliyewaongoza polisi wanawake wa mkoa huo kukabidhi msaada wa mahitaji mbalimbali yenye thamani ya Shilingi 800,000 kwa watoto wanaolelewa katika kituo hicho.

    Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, SP Mwakasutu alisema kuwa hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa wajibu wa Mtandao wa Polisi Wanawake katika kushirikiana na jamii na kuwasaidia watu wenye mahitaji maalum.

    “Lengo letu ni kuwashika mkono watoto hawa kwa kuwasaidia mahitaji mbalimbali, lakini pia kuendelea kuwa karibu na jamii inayotuzunguka,” alisema SP Mwakasutu.

    Aliongeza kuwa TPF–NET imeamua kufanya hivyo ili kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha huduma kwa jamii, hususan kwa makundi maalumu yanayohitaji msaada.

    SP Mwakasutu pia alieleza kuwa Jeshi la Polisi limekuwa na utaratibu wa kutembelea vituo vya kulelea watoto wenye mahitaji maalumu na kutoa misaada mbalimbali, huku akihimiza jamii, taasisi za umma na binafsi kujitokeza kusaidia makundi hayo ili kujenga jamii yenye mshikamano, upendo na kujali.

    Mbali na msaada huo, Jeshi la Polisi pia linaendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu lishe bora kwa watoto, malezi bora pamoja na kupinga ukatili wa kijinsia, ili kuongeza uelewa kwa watoto na jamii kwa ujumla.

    Kwa upande wake, uongozi wa Kituo cha Mfaranyaki ulilishukuru Jeshi la Polisi kwa msaada huo, ukieleza kuwa umekuwa faraja kubwa kwa watoto wanaolelewa hapo, hasa katika kipindi hiki cha kuelekea sikukuu za Eid El Fitri na Pasaka.

  • Na Cosmas Msuha

    Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, TAKUKURU Mkoani Rukwa imefanikiwa kudhibiti vitendo vya rushwa katika miradi ya maendeleo yenye thamani ya shilingi bilioni 1.7 kwa kipindi cha Oktoba hadi Disemba mwaka 2025.

    Mkuu waTAKUKURU Mkoa wa Rukwa,  Mzalendo Widege  aliyasema hayo katika taarifa yake kwa umma ambapo inaonesha kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2026, TAKUKURU Mkoani humo imepanga  kufuatilia matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo pamoja na mali za watuhumiwa ili kufidia hasara zinazotokana na vitendo vya rushwa.

    Alisema katika kuboresha utekelezaji wa miradi, TAKUKURU ilitoa mapendekezo kadhaa ikiwemo matumizi ya wahandisi waliosajiliwa, matumizi ya vifaa vya kujikinga kwa mafundi, kutangaza zabuni mapema kupitia mfumo wa NeST pamoja na kuimarisha vikao katika eneo la mradi na utunzaji wa nyaraka.

     Katika hatua nyingine, alisema TAKUKURU ilifanikiwa kumrejesha mkandarasi aliyekuwa ameacha ujenzi wa bweni na madarasa katika Shule ya Sekondari Mzindakaya.

    “Mradi huo wenye thamani ya shilingi milioni 380 ulisimama kwa miezi miwili kuanzia Oktoba hadi Novemba 2025 kutokana na mkandarasi huyo kuwa na zabuni nyingi, alisema Widege.

    Sanjali na hayo alitoa taarifa ya kuhusu uchambuzi wa mifumo ambapo taasisi hiyo imefanya tathmini ya ukusanyaji mapato katika Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo na usimamizi wa Jumuiya za Maji ngazi ya Jamii katika Wilaya ya Sumbawanga, ambapo mapendekezo yametolewa na ufuatiliaji unaendelea.

    Katika taarifa yake alibainisha jumla ya malalamiko 64 yalipokelewa katika kipindi hicho ambapo kati ya hayo, malalamiko 35 sawa na asilimia 55 yalihusu rushwa, huku 29 sawa na asilimia 45 hayakuhusu rushwa.

    “Malalamiko yasiyohusu rushwa yalifungwa baada ya ushauri, wakati yale yanayohusu rushwa uchunguzi unaendelea”, alisema Widege.

    Akizungumzia suala la elimu kwa umma, TAKUKURU imeendesha semina 19, mikutano ya hadhara 15, maonesho matano, kuimarisha klabu 10 za wapinga rushwa na kufungua klabu moja mpya na kudai kuwa hatua hiyo imeongeza mwitikio wa wananchi kutoa taarifa za vitendo vya rushwa.

    Widege aliwataka wananchi kuepuka vitendo vya  rushwa na kuendelea kutoa taarifa kupitia simu ya bure 113 au namba ya Mkuu wa TAKUKURU Mkoa 0738150186.

  • Na Cosmas Msuha

    Waziri wa Mifugo na Uvuvi Balozi Dkt. Bashiru Ally amefanya ziara mkoani Geita na kugagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya Soko la Kimataifa Samaki la Chato na kumtaka mkandarasi kukamilisha ujenzi wa mtambo wa kukaushia dagaa kabla ya mwezi April mwaka huu.

    Dkt. Bashiru alitoa maagizo hayo Februari 28, 2026 baada ya kukagua ujenzi wa miundombinu ya soko hilo ambapo ameonesha kutoridhishwa na kasi ya kazi zinazofanywa na mkandarasi huyo licha ya changamoto za malipo zinazomkabiri.A

    Aliagiza kufanyika tathmini mpya ya gharama za mtambo huo ili upatikane kwa haraka  ambapo kukamilika kwa ujenzi huo kutachangia upatikanaji wa ajira kwa makundi mbali mbali ya vijana katika soko hilo.

    “Nataka kazi ifanyike kwa kasi na Jumatatu barua iwe imejibiwa na mpaka Jumatano mkandarasi awe ameipata na mimi nipate nakala”, alisema Dkt. Bashiru

    Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Miundombinu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhandisi George Kwandu alisema kuchelewa kwa malipo kwa mkandarasi kulitokana na changamoto kadhaa ambazo zilisababisha mkandarasi kushindwa kununua mtambo kwa wakati hatahivyo wamejipanga kujadiliana na kuzifanyia kazi ili kuharakisha malipo hayo.

    Sanjali na maagizo hayo, Dkt. Bashiru amemtaka mkandarasi huyo kushirikiana na taasisi nyingine katika uimarishaji wa miundombinu na huduma za kijamii ikiwemo miundombinu ya maji, umeme, barabara ili soko hilo litambuliwe kimataifa na kuanza kufanya kazi kwa manufaa ya wananchi.

  • Na Mwandishi Wetu, Nachingwea – Lindi

    Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea, Mohamed Hassan Moyo ameongoza zoezi la ugawaji wa miche zaidi ya elfu sabini ya mikorosho kwa wananchi, ikiwa ni juhudi za kuongeza uzalishaji wa zao la korosho wilayani humo.

    Akizungumza wakati wa zoezi hilo tarehe 23/02/2026, Moyo alisema serikali imeamua kuwapatia wakulima miche hiyo bila malipo ili kupunguza gharama za uzalishaji na kuwawezesha kuongeza kipato chao.

    Ameeleza kuwa mpango huo unatekelezwa kwa lengo la kuimarisha sekta ya kilimo na kuinua uchumi wa wananchi.

    Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Adinan Mpyagila, ambaye ameshiriki katika zoezi hilo, amesema ugawaji wa miche hiyo ya mikorosho utachochea ongezeko la uzalishaji na kuboresha ubora wa zao la korosho wilayani hapo.

    Kwa upande wao, wakulima walishukuru kupata miche hiyo, walisema hapo awali walikuwa wakisubiri kwa muda mrefu kupata mavuno walipopanda miche ya zamani tofauti ni miche mipya waliyopewa ambayo itawawezesha kupata mavuno kwa muda mfupi zaidi.

    Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa serikali wa kuendeleza mazao ya kimkakati, ikiwemo korosho, kwa lengo la kuongeza mapato ya wakulima na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

  • Na Vincent Mpepo

    Waumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Mtaa wa Kwembe, wameungana na watu wengine duniani kuadhimisha Siku ya Wapendanao kwa namna ya kipekee, ambapo wanandoa walipatiwa mafunzo na uzoefu mbalimbali kama njia ya kukumbushana wajibu na haki zao katika ndoa taasisi inayotajwa kuwa msingi wa familia, jamii na taifa kwa ujumla.

    Hafla hiyo iliyofanyika jana katika ukumbi wa kanisa hilo, iliongozwa na viongozi wa mtaa wa kanisa pamoja na wawezeshaji kutoka ndani na nje ya kanisa.

    Katika mafundisho yaliyotolewa, ilibainika kuwa ukosefu wa elimu ya ndoa katika jamii ni moja ya vikwazo vikubwa vinavyosababisha ndoa kushindwa kukua, kutoeleweka na kuyumba.

    Akitoa mada katika maadhimisho hayo, Mwalimu na Mwanasaikolojia, Bupe Mwabenga, alisema jamii imekuwa haijali uwekezaji wa kutosha katika elimu ya ndoa, hali inayosababisha baadhi ya wanandoa kutoitambua ndoa kwa uzito unaostahili na kuichukulia kama jambo la kawaida.

    “Kumekuwa na mtazamo kuwa elimu ya ndoa ni jambo la kawaida na hivyo kutopewa kipaumbele, jambo ambalo si sahihi,” alisema Mwanasaikolojia Bupe.

    Alisema athari za ukosefu wa elimu ya ndoa ni pamoja na migogoro ya kifamilia, kuvunjika kwa ndoa na kuathirika kwa afya ya akili miongoni mwa wanandoa, hali inayowaacha watoto wakikua katika mazingira yasiyo salama kihisia na kimaadili.

    “Ifike wakati kila mwanandoa aache kumchukulia poa mwenza wake,” alisisitiza.

    Aidha, alitaja sababu nyingine zinazosababisha changamoto katika ndoa kuwa ni pamoja na athari za utandawazi, baadhi ya wanandoa kutojua kusudi la kuingia katika ndoa, pamoja na kutoelewa haki na wajibu wao ndani ya ndoa.

    Akizungumzia tabia ya wanandoa kujikita zaidi katika udhaifu wa wenza wao, Bupe alisema hali hiyo huchangia migogoro isiyo ya lazima, huku akisisitiza kuwa hakuna mwanadamu mkamilifu.

    “Mbinu mojawapo ya kuishi vyema katika ndoa ni kuyatambua madhaifu na mazuri ya mwenza wako, na zaidi kujikita katika kuyakuza mazuri yake badala ya kuganda na madhaifu,” alisema.

    Kuhusu changamoto za utandawazi, Bupe alisema jamii imejikita mno katika utafutaji wa mali na vyeo kana kwamba pesa ndiyo suluhisho la kila changamoto, hali inayochochea kiburi na kuathiri mahusiano ya ndoa.

    “Baadhi ya athari za pesa au cheo, hususan kwa wanawake, zimesababisha wanaume kujenga ukuta wa kujihami, jambo linalodhoofisha ustawi wa ndoa,” alifafanua.

    Kwa upande wake, mwezeshaji mwingine wa mada, James Betram, alisisitiza umuhimu wa kila mwanandoa kujijengea sababu ya kupendwa na mwenza wake, licha ya mafundisho ya kibiblia yanayoeleza kuwa upendo haujivuni wala haufanyi ubaguzi.

    Aliongeza kuwa baadhi ya mabadiliko ya kisasa yamesababisha wanandoa kutochukulia ndoa kwa uzito unaostahili, hali inayofanya ndoa kuonekana kama jambo la mazoea.

    “Ni muhimu kwa wanandoa kudumisha mawasiliano, kujali hisia za wenza wao na kuwa na moyo wa kusameheana ili kujenga mahusiano yenye afya na ustawi wa familia,” alisema Betram.

    Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Malezi na Uinjilisti ya kanisa hilo, Mratibu wa shughuli hiyo, Michael Mwambage, alisema ni wajibu wa kanisa kuendelea kuimarisha taasisi ya ndoa kwa kutoa elimu na jukwaa la kubadilishana uzoefu.

    “Ni vyema wanandoa kukutana kanisani, kujifunza na kubadilishana uzoefu badala ya kusherehekea Siku ya Wapendanao kwa namna nyingine zisizo na tija ya kudumu,” alisema Mwambage.

  • Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

    Katika mwendelezo wa utoaji wa elimu kwa umma, Jeshi la polisi limeendelea na kazi hiyo ambapo jana, Mratibu wa Program ya Usalama Wetu Kwanza Wilaya ya Kati na Kariakoo Mkaguzi Msaidizi wa Polisi (Insp) Martin Shila alifika katika Shule ya Msingi Olympio Iliyopo Upanga Dar es salaam na kuzungumza na wanafunzi wa Shule hiyo.

    Katika tukio hilo Insp Shilla aliwaeleza watoto hao kuwa kila mtu ana mchango katika kuzuia ukatili hivyo kuwataka kuwajibika katika kupambana na changamoto hiyo katika katika jamii.

    Aidha katika hatua nyingine Insp Shilla alibainisha mazingira hatarishi yanayoweza kusababisha ukatili kutokea na kuwaasa kutoa taarifa katika vituo vya polisi, ofisi za serikali za mitaa na mamlaka nyingine za kisheria.