• Na Cosmas Msuha

    Serikali imewaagiza wazalishaji wote nchini kutumia alama ya ‘Made in Tanzania’ ili kuongeza utambulisho na imani kwa bidhaa zinazozalishwa nchini, pamoja na kuimarisha ushindani wake katika masoko ya kimataifa.

    Agizo hilo limetolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Emmanuel Nchimbi, wakati wa kilele cha maadhimisho ya Usiku wa Jubilei ya Dhahabu (Miaka 50) ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

    Makamu wa Rais alizitaka taasisi zinazosimamia viwango na huduma za kifedha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ili kuhakikisha bidhaa za Tanzania zinakidhi viwango vinavyokubalika katika soko la kimataifa.

    “Matumizi ya alama ya ‘Made in Tanzania’ yataongeza utambulisho wa bidhaa zenye ubora na kuimarisha heshima ya taifa katika biashara za kimataifa,” alisema Mhe. Balozi Nchimbi.

    Aidha, aliwapongeza wadau wa sekta ya fedha kwa kuendelea kutoa mikopo yenye masharti nafuu kwa viwanda vidogo na vya kati, akisema hatua hiyo imechangia kupunguza changamoto ya upatikanaji wa mitaji kwa wajasiriamali na kuchochea ukuaji wa uzalishaji nchini.

    Alisema Serikali itaendelea kuweka sera rafiki kwa uwekezaji, kuboresha miundombinu na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi ili kujenga uchumi wa viwanda wenye ushindani.

    Kwa upande wake, Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mbunge), alisema Tanzania itanufaika zaidi na rasilimali zake endapo itawekeza katika uchakataji na uzalishaji wa bidhaa za mwisho zenye thamani kubwa, badala ya kuendelea kuuza malighafi ghafi nje ya nchi.

    Alibainisha kuwa hatua hiyo itafungua masoko mapya, kuongeza thamani ya mauzo ya bidhaa nje ya nchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa wananchi.

    Mhe. Kapinga alisisitiza kuwa ili kujenga uchumi imara wa viwanda wenye ushindani, ni muhimu kubadili mtazamo wa uzalishaji kwa kuhakikisha mazao ya kilimo, mifugo, uvuvi, misitu na madini yanaongezewa thamani kwa kuchakatwa, kufungashwa vizuri na kuzalishwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.

    Aidha, alisema uwekezaji katika teknolojia za kisasa una mchango mkubwa katika kuongeza uzalishaji, kuboresha ubora wa bidhaa zinazozalishwa nchini, kupunguza gharama za uzalishaji na kuziwezesha bidhaa za Tanzania kushindana katika masoko ya kimataifa.

    Hafla hiyo iliambatana na utoaji wa tuzo kwa washirika muhimu wa TANTRADE pamoja na taasisi zinazochangia maendeleo ya biashara, viwango na huduma za kifedha nchini.

    Kwa mujibu wa Makamu wa Rais, Mhe. Balozi Nchimbi maadhimisho ya Jubilei ya Dhahabu ya TANTRADE ni fursa muhimu ya kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 50, ikiwemo kuongezeka kwa viwanda, uzalishaji, ajira na upanuzi wa masoko ya bidhaa na huduma za Tanzania duniani.

  • Na Cosmas Msuha

    Ofisi ya Waziri Mkuu imewawezesha watu wenye ulemavu kushiriki katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kupitia Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA).

    Ushiriki huo umewawezesha kuonesha bidhaa na huduma mbalimbali wanazozalisha na kuzitoa, pamoja na kufanya biashara katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.

    Akitembelea mabanda ya washiriki hao, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Ummy Nderiananga, alieleza kuridhishwa na kiwango cha ushiriki wa watu wenye ulemavu, akibainisha kuwa ushiriki wao umeongeza fursa za kiuchumi na kuonesha uwezo wao katika uzalishaji na biashara.

    Aidha, Nderiananga aliipongeza Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) pamoja na taasisi nyingine zilizowezesha ushiriki huo na kuzitaka mamlaka za serikali za mitaa kuendelea kutenga na kutoa mikopo ya asilimia mbili kwa watu wenye ulemavu ili kuwawezesha kukuza shughuli zao za kiuchumi.

    “Ni wakati sasa kwa watu wenye ulemavu kuendelea kuonesha uwezo wao katika uzalishaji na biashara. Kupitia maonesho haya tumejionea matokeo chanya ya uwezeshaji wa kiuchumi unaotokana na mikopo na fursa zinazotolewa na Serikali,” alisema Nderiananga.

    Kwa upande wake, mwakilishi wa washiriki hao, Bi. Pili Bilahi, aliishukuru Serikali kwa kuwawezesha kushiriki katika maonesho hayo bila kulipia gharama yoyote.

    Vilevile, Bi. Bilahi aliishukuru serikali kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi yanayowapa watu wenye ulemavu fursa za kiuchumi, ikiwemo kupitia mikopo ya asilimia mbili ya mapato ya ndani inayotolewa na halmashauri.

    Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, “Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania,” yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu nchini. Maonesho hayo yalianza Juni 28 na yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13, 2026.

  • Na George Gabriel, Mtwara

    Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Mtwara imetoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa Hospitali ya Mangaka iliyopo Wilaya ya Nanyumbu, mkoani Mtwara, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa wajibu wake kwa jamii na kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuboresha huduma za afya.

    Akizungumza wakati wa makabidhiano ya vifaa hivyo, Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Mtwara, Mashauli Elisante, alisema msaada huo unaonesha dhamira ya taasisi hiyo ya kushiriki katika maendeleo ya jamii sambamba na kutekeleza jukumu lake la kuzuia na kupambana na rushwa.

    “Tunaamini afya bora ni msingi wa maendeleo ya jamii, na ni wajibu wa kila taasisi kushiriki pale inapowezekana katika kuboresha huduma zinazowagusa wananchi moja kwa moja,” alisema.

    Vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na magauni ya wajawazito na wazazi, viatu, vipima joto, sabuni pamoja na nepi za watoto (pampers), ambavyo vinatarajiwa kusaidia kuboresha huduma kwa akina mama, watoto na wagonjwa wengine wanaopatiwa huduma katika hospitali hiyo.

    Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mangaka, Benedict Mbai, aliishukuru TAKUKURU kwa msaada huo, akisema vifaa hivyo vitasaidia kuboresha utoaji wa huduma na kupunguza changamoto zinazowakabili wahudumu wa afya, hususan katika wodi za akina mama na watoto.

    Kwa upande wake, mmoja wa wazazi wanaopata huduma hospitalini hapo, Faudhia Geugeu, alitoa shukrani kwa TAKUKURU kwa msaada huo, akieleza kuwa umefika wakati muafaka na utanufaisha wananchi wengi wanaotegemea huduma za hospitali hiyo.

    Msaada huo unaakisi umuhimu wa ushirikiano kati ya taasisi za umma na sekta ya afya katika kuboresha ustawi wa wananchi na kuhakikisha huduma bora za afya zinaendelea kuwafikia Watanzania.

  • Na Yusra Temba, Iringa

    Msimu wa tano wa Great Ruaha Marathon umefanyika ndani ya Hifadhi ya Taifa Ruaha ukilenga kuhamasisha uhifadhi wa mazingira na kukuza utalii wa michezo.

    Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Msajili wa Hazina na mlezi wa Great Ruaha Marathon, Nehemiah Mchechu, ambaye alimwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na katika hotuba yake, alisema uhifadhi wa mazingira una mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi.

    Alisema pia, Mto Ruaha Mkuu ni rasilimali muhimu inayochangia shughuli za kilimo, ufugaji na uzalishaji wa umeme, huku akiwahimiza watanzania kutembelea hifadhi za taifa na kushiriki katika juhudi za kuhifadhi maliasili.

    Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Massana Gibril Mwishawa, alisema mbio hizo ni sehemu ya mkakati wa kuendeleza utalii wa michezo na kuitangaza Tanzania kupitia vivutio vyake vya kipekee vya utalii.

    Kwa upande wake, Mratibu wa Great Ruaha Marathon, Hamim Kilahama, alisema marathon hiyo inalenga kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wa mazingira na rasilimali za asili kupitia michezo

    Msimu wa tano wa Great Ruaha Marathon umeandaliwa kwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, wakiwemo Airtel Tanzania, Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Maji ya Mkwawa, NMB Bank, Ununio Beach Park na Mkuu Creatives.

  • Na Cosmas Msuha

    Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) imeshiriki Jukwaa la Biashara lililofanyika sambamba na Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), kwa lengo la kutangaza fursa za uwekezaji, biashara na kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali wa sekta ya madini.

    Jukwaa hilo limewakutanisha wafanyabiashara, wawekezaji na wadau kutoka mataifa mbalimbali kujadili mikakati ya kukuza biashara, uwekezaji na masoko ya ndani na kimataifa.

    Akifungua mkutano huo, Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara ya Ndani kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara, Semeo Manongi, alisema Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuwezesha sekta binafsi kufanya shughuli zake kwa ufanisi, usalama na tija, hatua inayochangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

    Alieleza kuwa jukwaa hilo, lililoandaliwa na Benki ya Equity Tanzania katika Viwanja vya Mwalimu Julius K. Nyerere jijini Dar es Salaam, limewakutanisha wajumbe 51 kutoka mataifa mbalimbali na kufanyika sambamba na maonesho ya Sabasaba.

    Manongi alibainisha kuwa maonesho ya Sabasaba yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza bidhaa, huduma na fursa za uwekezaji, huku yakifungua masoko mapya kwa taasisi, kampuni na wafanyabiashara wa ndani na nje ya nchi.

    Kwa upande wake, Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Benki kwa Wateja Binafsi wa Benki ya Equity Tanzania, Theresia Mayanie, aliwahimiza wawekezaji na wafanyabiashara kutumia huduma za benki hiyo, akieleza kuwa Equity imejipanga kutoa huduma bora na ushirikiano wa karibu kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa.

    Ushiriki wa GST katika jukwaa hilo unaonyesha dhamira ya taasisi hiyo ya kutangaza huduma zake, kuonesha fursa zilizopo katika sekta ya madini na kujenga ushirikiano na wawekezaji pamoja na wadau wengine kwa lengo la kuendeleza sekta hiyo na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Tanzania.

    Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yalianza rasmi Juni 28, 2026 na yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13, 2026. Maonesho hayo yamewakutanisha zaidi ya kampuni 200 za kimataifa na washiriki kutoka mataifa mbalimbali, yakitoa fursa za biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi.

  • Na Jastini Bukebuke

    Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Geita, kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi pamoja na watumishi kutoka idara mbalimbali za serikali, limeendesha msako maalum wa ukaguzi wa miundombinu ya umeme katika Mtaa wa Mwambageni, Kata ya Nyarugusu, Wilaya ya Geita.

    Akizungumza wakati wa msako huo, Afisa Uendeshaji wa TANESCO Mkoa wa Geita, Elthemius Katemana, amewataka wakazi wa eneo hilo kuacha tabia ya kujiunganishia umeme kinyume cha sheria.

    Alisema wananchi wanapaswa kufuata taratibu zilizowekwa na TANESCO ili kupata huduma ya umeme kwa njia halali, salama na endelevu.

    Kwa upande wake, Mtendaji wa Kata ya Nyarugusu, Abas Masune, akiwa ameambatana na wajumbe wa kata, alitembelea eneo hilo kujionea vitendo vya udanganyifu vilivyofanywa na baadhi ya wakazi kwa miundombinu ya umeme.

    aliwawataka wananchi kuacha mara moja vitendo hivyo, akisisitiza kuwa vinahatarisha miundombinu ya umeme, usalama wa wananchi na vinaikosesha serikali mapato.

    TANESCO imeeleza kuwa itaendelea kufanya operesheni kama hiyo katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Geita na nchini kote kwa lengo la kudhibiti wizi wa umeme, kulinda miundombinu ya umeme na kuhakikisha matumizi ya nishati yanafuata sheria, taratibu na viwango vya usalama.

  • Na Mwandishi Wetu

    Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amewataka Watanzania kuendelea kudumisha amani na kutopuuza viashiria vya uvunjifu wa amani, akisisitiza kuwa vinaweza kuchafua taswira ya taifa.

    Dkt. Nchemba alitoa wito huo jana wakati wa ibada maalumu ya kilele cha harambee iliyofanyika Usharika wa Amani, mjini Singida, katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kati.

    Alisema ulinzi wa taifa ni jukumu la kila Mtanzania, hivyo wananchi wanapaswa kuendelea kuhamasishana kulinda amani na kutoa taarifa mapema kuhusu viashiria vinavyoweza kuhatarisha usalama wa nchi.

    “Sasa hivi hatupaswi kupuuzia viashiria vya uvunjifu wa amani hapa nchini. Hatutakiwi kuvipuuza kwa sababu vinaweza kulitia doa taifa letu,” alisema Dkt. Nchemba.

    Harambee hiyo, ambayo ni ya nne kufanyika, ililenga kukusanya Sh. bilioni 1.4 kwa ajili ya kuboresha huduma za afya, elimu, utumishi na uinjilisti katika Dayosisi ya Kati. Jumla ya Sh. bilioni 1.331 zilipatikana kupitia michango ya fedha taslimu na ahadi.

    Dkt. Nchemba alisema kiasi kilichobaki cha Sh. milioni 69 kitakamilishwa ndani ya wiki ijayo kupitia utekelezaji wa ahadi mbalimbali zilizotolewa pamoja na timu aliyoiunda kusimamia zoezi hilo.

    Akihubiri katika ibada hiyo, Mkuu wa Kanisa la KKKT, Askofu Dkt. Alex Gehazi Malasusa, alisema harambee hiyo imewapa waumini nafasi ya kumshukuru Mungu kwa baraka na mafanikio aliyowajalia.

    “Kila tunachokifanya kinapaswa kumtukuza Mungu. Mali na fedha zetu ziwe za halali na zisipatikane kwa kuwaonea au kuwakanyaga wengine,” alisema Askofu Malasusa.

    Kwa upande wake, Askofu wa KKKT Dayosisi ya Kati, Dkt. Cyprian Hilinti, alisema kanisa linaendelea kuwaombea viongozi wa nchi kila Jumapili pamoja na kuombea amani na maridhiano kati ya makundi mbalimbali ya jamii, ikiwemo makabila, wakulima na wafugaji, pamoja na vyama vya siasa.

    “Tunatamani kuona msamaha ukitawala katika nyanja mbalimbali za maisha. Msamaha ni dawa,” alisema Dkt. Hilinti.

    Aliongeza kuwa tangu kuanzishwa kwa harambee hiyo miaka minne iliyopita, Dayosisi imeanzisha majimbo manane mapya, sharika 27, imepokea waumini wapya 17,364 na kupata wachungaji wapya 65.

    Akizungumzia huduma za jamii, alisema Dayosisi pia imefanikiwa kusajili shule mbili mpya za sekondari na shule moja ya msingi inayotoa elimu kwa lugha ya Kiingereza, huku akiwashukuru waumini wote kwa kujitolea na kuchangia maendeleo ya kanisa na jamii.

  • Na Cosmas Msuha

    Serikali ya Tanzania imeingia makubaliano na kampuni mbili kutoka Japan ili kufungua fursa za soko la biashara ya kaboni kupitia Mpango wa Uratibu wa Pamoja wa Mikopo (JCM).

    Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo iliyofanyika Juni 25, 2026, jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Mayungi, alisema hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 kupitia uwekezaji katika nishati safi, biashara ya kaboni na usimamizi endelevu wa taka.

    Dkt. Mayungi alisema ushirikiano huo pia unalenga kuongeza ushiriki wa sekta binafsi katika utekelezaji wa miradi ya mazingira na maendeleo endelevu, sambamba na kuchochea ukuaji wa uchumi wa kijani.

    Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Biashara ya Kaboni (NCMC), Ngenda Kigaraba, alisema mfumo wa utoaji wa mikopo ya pamoja utachangia kuimarisha uhifadhi wa mazingira, kukuza biashara ya kaboni na kuongeza mapato ya Serikali kupitia uwekezaji wa miradi rafiki kwa mazingira.

    Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya 3T kutoka Japan, Kan Shimizu, alisema Tanzania itanufaika kwa kiwango kikubwa kupitia ushirikiano huo, hususan katika kuendeleza miradi ya utunzaji wa mazingira na biashara ya kaboni, ambayo pia itasaidia kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi.

    Makubaliano hayo kati ya NCMC na kampuni hizo za Japan yanatarajiwa kuchochea ushiriki wa sekta binafsi katika utekelezaji wa miradi ya mazingira, sambamba na kuunga mkono utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050, hususan nguzo ya tatu inayosisitiza ukuaji wa uchumi unaozingatia maendeleo endelevu na uhifadhi wa mazingira.

  • Na Jastini Bukebuke

    Mtandao wa Polisi Wanawake Mkoa wa Geita (TPF-NET) umetembelea na kutoa msaada katika Kituo cha Kulelea Watoto Yatima cha Bin Ghanimu kilichopo Bwanga, Wilaya ya Chato, ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kuwafariji na kusaidia watoto wenye uhitaji katika jamii.

    Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mkuu wa Kituo cha Polisi Bwanga, ASP Neema Nhaluke, alisema TPF-NET imeendelea kuwa daraja la ulinzi, upendo na matumaini kwa jamii, hususan kwa watoto wenye mazingira magumu. Alisisitiza kuwa jukumu la askari wanawake haliishii katika kulinda usalama pekee, bali linajumuisha pia kushiriki katika shughuli za kijamii zinazogusa makundi yenye uhitaji.

    ASP Nhaluke aliwataka walezi kuendelea kusimamia maadili, uzalendo na malezi bora ili kuwajengea watoto msingi imara wa kuwa raia wema na wenye manufaa kwa taifa.

    Kwa upande wao, Wakaguzi wa Polisi Paschazia Nunda na Shida Samweli waliwahimiza watoto hao kuzingatia nidhamu na maadili mema, wakieleza kuwa tabia njema ndiyo msingi wa kufikia ndoto na malengo yao ya maisha.

    Aidha, walitoa wito kwa watoto na walezi kutovumilia vitendo vya unyanyasaji na ukatili, wakisisitiza umuhimu wa kuripoti matukio hayo kwa mamlaka husika bila hofu ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.

    Naye Mkuu wa Shule na Mlezi wa kituo hicho, Seleiman Shila, alilishukuru Jeshi la Polisi kwa upendo, faraja na msaada walioutoa, akiahidi kuendelea kuwalea watoto hao katika misingi ya nidhamu, maadili na elimu ili wawe tegemeo la taifa siku zijazo.