• Na Mwandishi Wetu, Haydom, Manyara

    Madereva wa magari na pikipiki katika Mji Mdogo wa Haydom, Wilaya ya Mbulu mkoani Manyara, wamekumbushwa kuendelea kuzingatia sheria za usalama barabarani ili kupunguza ajali na kulinda maisha ya watumiaji wa barabara.

    Wito huo umetolewa na Koplo (CPL) Andrea Mbona wa Kikosi cha Usalama Barabarani Haydom, ambaye aliwataka madereva kuzingatia taratibu zote za usalama, ikiwemo kufunga mikanda wanapoendesha magari na kuzingatia alama mbalimbali za barabarani.

    Alisisitiza umuhimu wa kuwa makini wanapofika kwenye vivuko vya watembea kwa miguu na maeneo yanayovukwa na wanyama, akieleza kuwa kufuata sheria na tahadhari hizo kutasaidia kupunguza ajali za barabarani.

    Mmoja wa madereva, Emanuel Evarist, alisema anashukuru kwa elimu hiyo ya usalama barabarani, akieleza kuwa wakati mwingine madereva huendesha kwa mazoea na kusahau kuzingatia sheria.

    Alisema elimu hiyo ni muhimu kwa kuwa inawakumbusha madereva wajibu wao wa kuendesha kwa kuzingatia sheria na kuongeza kuwa inapaswa kutolewa mara kwa mara ili kuendelea kujenga uelewa na nidhamu barabarani.

    Naye dereva, Israel Mohe, amelipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kutoa elimu kwa madereva na watumiaji wengine wa barabara.

    “Kwa kweli, mimi kama dereva ninalipongeza Jeshi la Polisi kwa namna linavyoendelea kutoa elimu ya usalama barabarani. Kwa kipindi hiki, jeshi limejikita zaidi katika utoaji wa elimu kuliko ilivyokuwa hapo awali,” alisema Mohe.

    Alisema utoaji wa elimu una mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa madereva na watumiaji wengine wa barabara, hatua inayosaidia kuimarisha usalama na kupunguza ajali.

  • Na George Gabriel

    Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Edward Magala, amefungua rasmi mafunzo ya awali ya Jeshi la Akiba kwa mwaka 2026 yanayofanyika katika Kata ya Likokona, yakilenga kuwajengea washiriki uzalendo, nidhamu na ujuzi wa msingi wa ulinzi na usalama wa Taifa.

    Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo uliofanyika Julai 13, 2026, katika viwanja vya Shule ya Msingi Likokona B, Magala alisema Jeshi la Akiba lina nafasi muhimu katika kuimarisha usalama wa nchi na kujenga uzalendo miongoni mwa wananchi. Aliwataka washiriki kuyatumia vyema mafunzo hayo na kuwa tayari kulitumikia Taifa watakapohitajika.

    Jumla ya washiriki 82 wamejiunga na mafunzo hayo, wakiwemo wanaume 73 na wanawake 9. Washiriki hao wanatarajiwa kupata mafunzo ya msingi ya kinadharia na vitendo yatakayowawezesha kutekeleza majukumu ya Jeshi la Akiba kwa ufanisi.

    Mmoja wa washiriki, Said Mtailika, alisema ameridhishwa na uamuzi wa Serikali kuendelea kutoa mafunzo ya Jeshi la Akiba kwa wananchi, akieleza kuwa yatamjengea uwezo wa kujitambua, kuimarisha nidhamu na kuongeza uzalendo.

    Aliwahimiza vijana wengine kutumia fursa hiyo badala ya kuipuuzia, akisema mafunzo hayo yana manufaa makubwa kwa maendeleo yao binafsi na kwa Taifa kwa ujumla.

    Naye mzazi Kalanje Abdarah aliwashukuru viongozi wa Serikali kwa kuanzisha mafunzo hayo wilayani Nanyumbu, akisema yatasaidia kuwajenga vijana katika maadili mema, nidhamu na kuwajibika kwa jamii.

    Aidha, aliwasihi washiriki wote kutokukata tamaa au kukimbia mafunzo kutokana na changamoto zinazoweza kujitokeza, bali wavumilie hadi watakapohitimu, kwani maarifa na stadi watakazopata yatakuwa msingi muhimu katika maisha yao ya baadaye.

    Mafunzo hayo yanatarajiwa kuendelea kwa kipindi kilichopangwa, huku washiriki wakipatiwa mafunzo mbalimbali ya kinadharia na vitendo yatakayowawezesha kutekeleza majukumu ya Jeshi la Akiba kwa weledi, nidhamu na uzalendo.

  • Na  Jastini Bukebuke

    Madereva wa bodaboda na bajaji za mizigo katika Mtaa wa Shinyanga A, Kata ya Nyakafulu, Wilaya ya Mbogwe mkoani Geita, wamepatiwa elimu kuhusu umuhimu wa ulinzi shirikishi na malezi bora ya watoto, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha usalama na ustawi wa jamii.

    Akitoa elimu hiyo juzi, Staff Sajenti (SSGT) wa Jeshi la Polisi, Mohamed Bujiku, aliwataka madereva hao kuacha tabia ya kufumbia macho vitendo vya uhalifu, akieleza kuwa baadhi ya wahalifu hutegemea ushirikiano wa madereva kusafirisha watuhumiwa, mali za wizi au mizigo inayohusishwa na vitendo vya kihalifu.

    Alisisitiza kuwa ushiriki wa madereva katika kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kuhusu watu au matukio yanayotiliwa shaka ni hatua muhimu ya kuzuia uhalifu na kulinda amani, usalama wa wananchi pamoja na mali zao.

    Aidha, aliwahimiza kushiriki kikamilifu katika shughuli za ulinzi shirikishi, akieleza kuwa mfumo huo ni nguzo muhimu ya kudumisha usalama, kuimarisha ushirikiano kati ya wananchi na Jeshi la Polisi, na kujenga jamii yenye amani, mshikamano na uwajibikaji.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kijiwe hicho, Amon Kidenya, aliwataka madereva hao kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za usafirishaji barabarani ili kuepuka ajali.

    Pia alisisitiza kuwa malezi bora ya watoto ni jukumu la kila mwanajamii, akieleza kuwa ushirikiano wa wananchi katika kuhakikisha watoto wanalelewa katika maadili mema unachangia kwa kiasi kikubwa kupunguza vitendo vya uhalifu na kujenga kizazi chenye nidhamu, uzalendo na uwajibikaji.

  • Na Mwandishi Wetu

    Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), kwa kushirikiana na Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC), wamezindua programu maalum ya kuwajengea uwezo na kuwathibitisha Maafisa Ulinzi wa Taarifa Binafsi nchini.

    Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Prof. Alex Makulilo, alisema programu hiyo si semina ya kawaida, bali ni mafunzo ya kina yatakayojumuisha nadharia na vitendo.

    Alisema uteuzi wa Afisa Ulinzi wa Taarifa Binafsi pekee hautoshi kumwezesha kusimamia kikamilifu utekelezaji wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi.

    “Msingi wa Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi kukichagua Chuo Kikuu Huria cha Tanzania ni uwezo wake wa kutoa mafunzo hayo bila kuathiri utekelezaji wa majukumu ya washiriki ya kila siku,” alisema Prof. Makulilo.

    Prof. Makulilo alisema awamu ya kwanza ya programu hiyo itaanza rasmi tarehe 10 Agosti 2026. Mafunzo hayo yatakuwa na moduli tano, yataendeshwa kwa muda wa siku 14, na kila mshiriki atachangia Sh milioni 2.5.

    Aliongeza kuwa baada ya mafunzo, washiriki watafanyiwa tathmini ya kina kabla ya kuthibitishwa rasmi na PDPC.

    Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa PDPC, Dkt. Emmanuel Mkilia, alisema licha ya taasisi nyingi kutekeleza matakwa ya sheria kwa kuteua Maafisa Ulinzi wa Taarifa Binafsi, imebainika kuwa maafisa hao wana viwango tofauti vya taaluma na uelewa kuhusu dhana ya ulinzi wa taarifa binafsi.

    Alisema ushirikiano kati ya PDPC na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania ni msingi imara wa kujenga wataalamu wenye weledi katika fani ya ulinzi wa taarifa binafsi.

    “Mafunzo haya yapo kwa mujibu wa sheria na ni lazima kwa kila Afisa Ulinzi wa Taarifa Binafsi aliyeteuliwa kuyapata ili kuhakikisha anatekeleza kikamilifu Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi,” alisema Dkt. Mkilia.

    Dkt. Mkilia aliwataka viongozi wa taasisi zote kuwawezesha Maafisa Ulinzi wa Taarifa Binafsi wa taasisi zao kushiriki katika programu hiyo ili kuimarisha utawala bora na kujenga imani ya wananchi katika huduma zinazotolewa.

    Alisema dhamira ya Tume ni kuona Tanzania inakuwa na Maafisa Ulinzi wa Taarifa Binafsi wenye ujuzi, weledi na umahiri wa kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa sheria, huku wakilinda faragha na taarifa za wananchi.

  • Na George Gabriel

    Timu ya Nanyumbu Veterans imezindua rasmi jezi zake mpya katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Lindi Veterans uliochezwa kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Mangaka, Wilaya ya Nanyumbu.

    Mchezo huo ulimalizika kwa sare ya mabao 1-1, huku ukishuhudiwa na mashabiki wengi na kuambatana na ushindani mkubwa. Lengo la mchezo huo lilikuwa kuimarisha afya, umoja na mshikamano miongoni mwa wanamichezo na jamii.

    Mgeni rasmi katika hafla ya uzinduzi huo alikuwa Diwani wa Kata ya Mangaka, Salvatory Lyimo, ambaye aliipongeza Nanyumbu Veterans kwa hatua ya kuzindua jezi mpya na kuendelea kushiriki shughuli za michezo zinazochochea afya, urafiki na ushirikiano wa wananchi.

    Akizungumza baada ya mchezo huo, Nahodha wa Nanyumbu Veterans, Hassan Simoje, alimshukuru Diwani Lyimo kwa ushirikiano na uungaji mkono wake, akisema umeongeza ari kwa wachezaji na kuhamasisha maendeleo ya michezo katika kata hiyo.

    “Tunamshukuru sana Mheshimiwa Diwani kwa kuwa nasi wakati wote. Mchango wake umetupa nguvu na motisha wa kuendelea kuitangaza Mangaka kupitia michezo,” alisema Simoje.

    Kwa upande wake, shabiki wa timu hiyo, Matajabu Juma, alisema uzinduzi wa jezi mpya ni hatua muhimu kwa Nanyumbu Veterans na utaongeza hamasa kwa wachezaji pamoja na mashabiki.

    “Tunajivunia kuona timu yetu inaendelea kupiga hatua. Tunampongeza Diwani kwa kuendelea kuwa karibu na timu, na tunaamini ushirikiano huu utaifanya Nanyumbu Veterans kufikia mafanikio makubwa zaidi,” alisema Juma.

    Mashabiki waliojitokeza kushuhudia mchezo huo walieleza kufurahishwa na kiwango kilichoonyeshwa na timu zote mbili, wakiahidi kuendelea kuiunga mkono Nanyumbu Veterans katika michezo ijayo. Walisisitiza kuwa michezo ni nyenzo muhimu ya kuimarisha afya, urafiki na maendeleo ya jamii.

  • Na Yusra Temba

    Mzize Foundation kwa kushirikiana na GSM Foundation imeandaa Tamasha la ‘Washike Mkono’, lililofanyika jana katika Uwanja wa Samora mkoani Iringa, likiwa na lengo la kukusanya rasilimali kwa ajili ya kuwapatia madereva wa bodaboda kofia ngumu (helmeti) na kuchangia vifaa tiba katika vituo mbalimbali vya afya mkoani humo.

    Mgeni rasmi katika tamasha hilo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, ambaye aliungana na mamia ya wakazi wa mkoa huo kushiriki tukio hilo lililolenga kuhamasisha mshikamano wa jamii kupitia michezo na shughuli za kijamii.

    Mbali na kampeni ya kuchangisha rasilimali, Mzize Foundation ilitoa mafuta bure kwa madereva wa bodaboda walioshiriki tamasha hilo ikiwa ni sehemu ya kuthamini mchango wao katika jamii na kuhamasisha usalama barabarani.

    Akizungumza baada ya tamasha hilo, mshambuliaji wa Klabu ya Young Africans (Yanga SC) na Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars), Clement Mzize, aliwashukuru wakazi wa Mkoa wa Iringa kwa mwitikio mkubwa waliouonesha na kueleza kufurahishwa na mafanikio ya tukio hilo.

    “Kwa kweli nina furaha sana. Matarajio niliyokuwa nayo yametimia kwa kiwango kikubwa. Watu wamejitokeza kwa wingi kunipa ushirikiano kwa sababu ni ndugu yao. Huu ni mwanzo mzuri, na naamini mambo mengi mazuri zaidi yanakuja,” alisema Mzize.

    Kwa upande wake, Msemaji wa Klabu ya Yanga, Ali Kamwe, aliwapongeza wakazi wa Mkoa wa Iringa kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki tamasha hilo, akisema mwitikio huo unaonesha mshikamano mkubwa wa wananchi katika kuunga mkono shughuli zenye manufaa kwa jamii.

    Tamasha hilo lilianza kwa mazoezi ya pamoja yaliyowakutanisha wananchi na wadau mbalimbali, kisha kufuatiwa na mchezo wa utangulizi kati ya Iringa All Stars Veterans na Ruaha National Park, uliomalizika kwa sare ya mabao 1-1.

    Baadaye kulichezwa mechi ya hisani kati ya Timu ya Mzize na Timu ya Oscar, ambapo Timu ya Mzize iliibuka na ushindi wa mabao 2-0.

    Tamasha hilo lilifanikishwa kwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, wakiwemo Ruaha National Park, K4S Security, Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa, ASAS pamoja na taasisi nyingine zilizojitokeza kuunga mkono jitihada za Mzize Foundation za kutumia michezo kama chachu ya maendeleo na ustawi wa jamii.

  • Na Yusra Temba

    Harakati za kukuza utalii nchini zimeendelea kushika kasi baada ya mamia ya washiriki kutoka ndani na nje ya Tanzania kushiriki mbio za Arusha Tourism Marathon zilizofanyika jana ndani ya Hifadhi ya Taifa Arusha, zikilenga kuhamasisha utalii kupitia michezo.

    Mashindano hayo yalijumuisha mbio za kilometa 2.5, 5, 10 na 21, mbio za baiskeli, burudani ya muziki, michezo ya watoto pamoja na shughuli mbalimbali zilizowapa washiriki fursa ya kujionea vivutio vya kipekee vinavyopatikana ndani ya hifadhi hiyo.

    Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Arusha, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Witness Shoo, ambaye alikuwa mgeni rasmi, alisema mbio hizo zimekuwa jukwaa muhimu la kutangaza utalii kwa kuwaunganisha wananchi na wageni na vivutio vya asili vinavyopatikana nchini.

    Alisema matukio yanayounganisha michezo na utalii yana mchango mkubwa katika kuitangaza Tanzania kimataifa na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea hifadhi za taifa na maeneo mengine ya vivutio vya utalii.

    Kwa upande wake, Mkurugenzi na Mwanzilishi wa Ruaha Tourism Marathon, Cornell Magoti, alisema lengo la mbio hizo ni kuunganisha sekta ya michezo na utalii ili kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea vivutio vya Tanzania na hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia sekta ya utalii.

    Baadhi ya washiriki wa mbio hizo walieleza kufurahishwa na mandhari ya kuvutia pamoja na vivutio mbalimbali walivyopata fursa ya kuviona ndani ya Hifadhi ya Taifa Arusha, wakisema tukio hilo limewapa uzoefu wa kipekee na kuwahamasisha kuendelea kutembelea maeneo ya utalii nchini.

    Waandaaji wa mbio hizo walieleza kuwa wanaendelea kutumia michezo kama jukwaa la kuitangaza Tanzania, wakiamini kuwa matukio ya aina hiyo yanaongeza mwamko wa utalii wa ndani na kuvutia wageni kutoka mataifa mbalimbali.

  • Na Jastini Bukebuke, Geita

    Mafundi ujenzi wapatao 460 kutoka mikoa ya Geita na Mwanza wamehimizwa kufanya kazi kwa weledi, uaminifu na uadilifu ili kujenga imani kwa wateja, kuboresha huduma wanazotoa na kuinua ustawi wa maisha yao.

    Wito huo umetolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, SACP Safia Jongo, wakati akifungua semina maalum iliyoandaliwa na Kampuni ya Magic Builders International ya Dar es Salaam. Semina hiyo ilifanyika jana katika Ukumbi wa Golden Social Hall uliopo Manispaa ya Geita.

    Akizungumza katika semina hiyo, SACP Jongo aliwakumbusha mafundi hao umuhimu wa kuzingatia sheria katika utekelezaji wa shughuli zao za kila siku, kuepuka vitendo vya uhalifu na ulaghai dhidi ya wananchi, pamoja na kutoshirikiana na wahalifu katika wizi wa vifaa vya ujenzi.

    Alisisitiza kuwa mafundi wanapaswa kutekeleza majukumu yao katika mazingira salama yanayozingatia sheria, huku wakidumisha amani, utulivu na mahusiano mema na jamii ili kuchochea maendeleo ya sekta ya ujenzi na taifa kwa ujumla.

    Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Magic Builders International, David Barongo, aliwahimiza mafundi hao kuendelea kujiendeleza kitaaluma kwa kupata mafunzo kutoka katika vyuo vinavyotambulika na mamlaka husika ili kuongeza maarifa, ujuzi na uzoefu unaowawezesha kutoa huduma bora na zenye ushindani.

    Barongo pia alilishukuru Jeshi la Polisi kwa kushiriki semina hiyo na kutoa elimu iliyolenga kuimarisha uzingatiaji wa sheria, maadili ya kazi na usalama katika sekta ya ujenzi.

    Alisema ushirikiano kati ya taasisi za umma na sekta binafsi una mchango mkubwa katika kuwajengea mafundi uwezo, kuongeza taaluma na kukuza sekta ya ujenzi nchini.

  • Na Farida Mkumba

    Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Petro Magoti, amepongeza mchango wa Chuo cha Serikali za Mitaa (LGTI) katika kuandaa wataalamu wenye uwezo wa kusimamia na kuendeleza utawala wa Serikali za Mitaa nchini.

    Magoti alitoa pongezi hizo alipotembelea banda la LGTI katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.

    Alisema LGTI imeendelea kujijengea sifa kwa kutoa elimu na mafunzo yenye ubora, yaliyowezesha kuzalishwa kwa wataalamu wenye weledi wanaochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya Serikali za Mitaa na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

    Magoti alisema anajivunia kuwa mmoja wa wahitimu wa chuo hicho, akibainisha kuwa elimu aliyoipata imekuwa msingi muhimu katika safari yake ya utumishi wa umma.

    “Elimu niliyopata LGTI imekuwa msingi imara wa utendaji wangu wa kazi na ndiyo imenisaidia kufikia mafanikio haya niliyoyapata katika utumishi wa umma,” alisema Magoti.

    Aidha, aliwataka vijana na watumishi wa umma kuendelea kuthamini elimu na mafunzo ya kitaaluma, akisisitiza kuwa taasisi kama LGTI zina nafasi kubwa katika kujenga watumishi wenye ujuzi, maadili na uwezo wa kusimamia maendeleo ya nchi.

    Akihitimisha ziara yake katika banda la chuo hicho, Magoti alikabidhiwa zawadi maalum yenye nembo ya LGTI kama kumbukumbu ya kutembelea banda hilo katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam.

    Maonesho ya SABASABA yameendelea kuwa jukwaa muhimu kwa taasisi za umma na binafsi kuonesha huduma, bidhaa na mafanikio yao. Kupitia maonesho hayo, LGTI inaendelea kutumia fursa hiyo kutangaza programu zake za mafunzo na kuonesha mchango wake katika kuimarisha utawala wa Serikali za Mitaa nchini.

  • Na Jastini Bukebuke, Geita

    Mkaguzi wa Polisi Kata ya Nyakafulu, INSP Denis Rwehumbiza, amewataka wanafunzi kutovumilia wala kuficha vitendo vya ukatili wanavyofanyiwa nyumbani au shuleni, badala yake watoe taarifa kwa walimu, wazazi, viongozi wa maeneo yao au Jeshi la Polisi ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi ya wahusika.

    Rai hiyo ameitoa leo alipokuwa akitoa elimu kuhusu kinga dhidi ya ukatili kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Ilolangulu, iliyopo Kata ya Ilolangulu, Wilaya ya Mbogwe, mkoani Geita.

    INSP Rwehumbiza aliwataka wanafunzi kuwa waangalifu dhidi ya vishawishi kutoka kwa watu wasiowafahamu, ikiwemo kupokea zawadi kama pipi, chipsi, fedha au msaada wa usafiri (lifti), akieleza kuwa mazingira hayo yanaweza kutumika kuwarubuni na hatimaye kuwaingiza katika vitendo vinavyohatarisha maisha na mustakabali wao.

    Alisema baadhi ya madhara yanayoweza kujitokeza ni pamoja na kuacha shule, kupata mimba za utotoni na kujiingiza katika mazingira hatarishi yanayoweza kuathiri maendeleo yao.

    Kwa upande wake, Mwalimu wa Nidhamu wa Shule ya Sekondari Ilolangulu, Fanuel Wilfred, aliwahimiza wanafunzi kuwa mstari wa mbele kutoa taarifa kuhusu watu wanaowadanganya au kuwarubuni ili hatua za kisheria zichukuliwe mapema.

    Alisema ushirikiano kati ya wanafunzi, walimu, wazazi na vyombo vya dola ni muhimu katika kuzuia vitendo vya ukatili na kuhakikisha mazingira salama ya kujifunzia.

    Elimu hiyo imelenga kuongeza uelewa wa wanafunzi kuhusu namna ya kujilinda dhidi ya ukatili na unyanyasaji, pamoja na kuwajengea ujasiri wa kutoa taarifa kwa mamlaka husika wanapokumbana na vitendo hivyo.

    Akihitimisha, INSP Rwehumbiza aliwahimiza wanafunzi kusoma kwa bidii, kuzingatia nidhamu na kujituma ili kutimiza ndoto zao za kielimu na kujenga maisha yenye mafanikio.