• Na Jastini Bukebuke

    Mkuu wa Wilaya ya Chato, Mhe. Louis Bura, amefunga rasmi mafunzo maalumu ya Ulinzi Shirikishi kwa washiriki 1,001 kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Geita na Manispaa ya Geita, akisisitiza umuhimu wa ushiriki wa wananchi katika kuimarisha usalama na kulinda mali za umma na binafsi.

    Hafla ya kufunga mafunzo hayo ilifanyika jana katika Viwanja vya GGM, Kata ya Kalangalala, mkoani Geita, ambapo Mhe. Bura alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela. Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML), Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita pamoja na viongozi mbalimbali wa serikali na wadau wa usalama.

    Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Bura alisema mafunzo hayo yamewajengea washiriki uelewa na ujuzi wa kutekeleza dhana ya ulinzi shirikishi kwa ufanisi, ikiwemo mbinu za kukabiliana na vitendo vya uvamizi, wizi wa mawe ya madini na uhalifu mwingine unaolenga mali za GGML pamoja na maeneo mengine muhimu ya kiuchumi.

    Alisema usalama wa jamii na uwekezaji ni msingi muhimu wa maendeleo, hivyo wananchi wanapaswa kushiriki kikamilifu katika kuzuia na kutoa taarifa za vitendo vya uhalifu vinavyoweza kuhatarisha amani na ustawi wa jamii.

    Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, SACP Safia Jongo, alisema kuwa ulinzi na usalama ni jukumu la kila mwananchi na kwamba washiriki wa mafunzo hayo wamewezeshwa kushiriki kikamilifu katika kubaini, kuzuia na kupambana na vitendo vya uhalifu ndani ya maeneo yao.

    Alieleza kuwa mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi endelevu za Jeshi la Polisi za kuimarisha ushirikiano kati ya wananchi na vyombo vya dola katika kudumisha amani, usalama na utulivu wa jamii.

    Naye Mtendaji Mkuu wa GGML, Ashraf Suryaningrat, aliwapongeza wahitimu wote pamoja na Jeshi la Polisi kwa ushirikiano mkubwa uliofanikisha utekelezaji wa programu ya Ulinzi Shirikishi, akibainisha kuwa programu hiyo imeendelea kuleta matokeo chanya katika kuimarisha usalama wa mgodi na maeneo yanayouzunguka.

    Suryaningrat alisema GGML itaendelea kushirikiana na serikali pamoja na vyombo vya usalama katika kutekeleza mipango mbalimbali inayolenga kulinda rasilimali za taifa na kuchangia maendeleo ya jamii zinazozunguka mgodi.

    Akihitimisha hafla hiyo, Mhe. Bura aliwataka wahitimu kutumia maarifa na ujuzi walioupata kuendelea kuimarisha ulinzi wa raia na mali zao, kuongeza weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku, kushiriki doria katika maeneo muhimu na kulinda miundombinu ya kimkakati.

    Alisisitiza kuwa mazingira salama na yenye utulivu ni nguzo muhimu katika kuvutia uwekezaji, kukuza shughuli za kiuchumi na kuharakisha maendeleo ya Mkoa wa Geita na Taifa kwa ujumla.

  • Na Jastini Bukebuke

    Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Mbogwe, SP Yusuph Chiwanga, amewataka Sungusungu na wananchi wa Kijiji cha Luhala, Kata ya Lugunga, kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi wanapotekeleza majukumu yao ya ulinzi na usalama.

    Akizungumza katika kikao cha uhamasishaji wa usalama wa jamii, SP Chiwanga alisema ni muhimu kwa Sungusungu kuzingatia nidhamu, maadili na taratibu za kisheria wakati wa kuwakamata watuhumiwa, badala ya kutumia nguvu kupita kiasi.

    Alieleza kuwa utendaji unaozingatia sheria na haki huchangia kujenga imani kwa wananchi na kuondoa malalamiko yanayoweza kujitokeza katika jamii.

    Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kushirikiana na Sungusungu pamoja na Jeshi la Polisi katika kudumisha amani na utulivu, huku akisisitiza kuwa kila mmoja ana wajibu wa kufuata sheria na taratibu zilizowekwa.

    Kwa upande wake, Mkaguzi wa Polisi wa Kata ya Masumbwe, INSP Oliver Kasembe, aliwahimiza Sungusungu na wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za wahalifu na vitendo vya uhalifu vinavyotokea katika maeneo yao.

    Alisema ushirikiano huo ni nguzo muhimu katika mapambano dhidi ya uhalifu, huku akiwataka wananchi kutofumbia macho vitendo vya kihalifu vinavyoweza kuhatarisha usalama wa jamii.

    INSP Kasembe pia alitoa rai kwa wananchi kuachana na migogoro inayotokana na kulishiana mazao, akieleza kuwa migogoro hiyo imekuwa chanzo kikubwa cha migongano miongoni mwa wakazi wa kijiji hicho.

    Naye Mkaguzi wa Polisi, INSP Nuru Mdugo, alikemea vitendo vya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto, huku akiwataka wananchi kujiepusha na matendo hayo ambayo yanaathiri ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.

    Alisisitiza umuhimu wa wazazi na walezi kuwapatia watoto malezi bora yenye misingi ya maadili mema na kumcha Mungu, ili kujenga kizazi chenye nidhamu na kinachopinga vitendo vya ukatili.

    “Malezi bora ndiyo msingi wa kujenga jamii salama na yenye maadili. Ni wajibu wa kila mzazi na mlezi kuhakikisha watoto wanakua katika mazingira yanayowajenga kuwa raia wema,” alisema INSP Mdugo.

  • Na Cosmas Msuha

    SERIKALI kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) imeingia makubaliano ya ushirikiano (MoU) na Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa maafa nchini kupitia matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu.

    Akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo, Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Dkt. Jim James Yonazi, alisema hatua hiyo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya kujenga mifumo madhubuti ya kiutendaji inayoongozwa na maarifa, sayansi na teknolojia, ikiwemo matumizi ya Akili Unde (AI) katika kukabiliana na maafa.

    Alisema makubaliano hayo yanatekeleza mapendekezo ya Mkutano wa Nane wa Umoja wa Mataifa wa Jukwaa la Dunia la Upunguzaji wa Vihatarishi vya Maafa uliofanyika Geneva, Uswisi, mwezi Juni 2025.

    “Vyuo vikuu na taasisi za utafiti, ikiwemo Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam, vina jukumu muhimu la kuzalisha maarifa na suluhisho za kisayansi zitakazosaidia kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini,” alisema Dkt. Yonazi.

    Alisema ili kuhakikisha utekelezaji madhubuti wa makubaliano hayo, Serikali itaandaa mpango kazi wa utekelezaji pamoja na Ajenda ya Kitaifa ya Utafiti wa Usimamizi wa Maafa, ambayo itabainisha maeneo ya kipaumbele yanayohitaji ufumbuzi wa kisayansi na kiteknolojia.

    Aidha, alisisitiza kuwa mafanikio ya makubaliano hayo yatapimwa kwa matokeo halisi yatakayochangia kuongeza usalama wa wananchi, kulinda rasilimali za taifa na kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam, Prof. Preksedis Marco Ndomba, alisema taasisi hiyo imeandika historia kwa kusaini makubaliano ya ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu, akibainisha kuwa mchakato wa kufanikisha ushirikiano huo ulianza muda mrefu na sasa umeanza kuzaa matunda.

    “Tunaahidi kutekeleza na kufanikisha makubaliano haya kwa kuwa tuna uwezo na utaalamu wa kutosha. Tutaendelea kushirikiana katika masuala ya vihatarishi vya kitaifa ili kufanikisha adhima hii ya Serikali,” alisema Prof. Ndomba.

    Ushirikiano huo unaelezwa kuendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inaweka msisitizo katika matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu kama nguzo muhimu za maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii nchini.

  • Na Cosmas Msuha

    Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Mahmoud Thabit Kombo amekutana na watanzania waishio Jamhuri ya Korea na kuwahimiza kuendelea kuwa mabalozi wazuri wa Tanzania kwa kuitangaza nchi na fursa mbalimbali katika sekta za uwekezaji, biashara na utalii.

    Akizungumza katika mkutano uliofanyika jana jijini Seoul, Balozi Dkt. Kombo alisema ni muhimu kwa watanzania kuifahamu vizuri nchi wanayoishi, ikiwemo tamaduni, lugha, sheria na mifumo ya kijamii ili waweze kujumuika na kujenga uhusiano chanya unaoweza kuleta manufaa kwa Taifa.

    Balozi Dkt. Kombo aliwakumbusha kutumia majukwaa mbalimbali ya kitaaluma, kijamii na kibiashara kuitangaza Tanzania na fursa zinazopatikana katika nchi wanazoishi ili kuvutia wawekezaji, watalii na wadau wa maendeleo kushirikiana na Tanzania.

    Aidha aliwaasa wanafunzi wa elimu ya juu nchini humo kujikita katika tafiti zinazolenga kutatua changamoto mbalimbali nchini Tanzania hususan katika sekta za afya, maji, elimu na mazingira.

    Kwa upande wake, Rais wa Jumuiya ya watanzania nchini Korea, Eliusta Filikunjombe alieleza utayari wao wa kuendelea kushirikiana na serikali katika kutangaza fursa na kuimarisha mahusiano kati ya Tanzania na Jamhuri ya Korea.

    Balozi wa Tanzania nchini Korea, Mhe. Noel Kaganda alisema idadi ya watanzania nchini humo inafikia 300 ambayo inajumuisha wafanyakazi, wafanyabiashara na wanafunzi.

    Balozi Dkt. Kombo yupo nchini Korea kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Korea na Afrika, unaolenga kuimarisha ushirikiano na mahusiano ya kidiplomasia, kiuchumi na maendeleo kati ya Korea na nchi za Afrika.

  • Na Cosmas Msuha

    WAZIRI Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amekagua ujenzi wa Barabara ya Noranga (Doroto)–Itigi (Mlongojii) yenye urefu wa kilomita 25 inayojengwa katika Halmashauri ya Itigi, Wilaya ya Manyoni, mkoani Singida kwa gharama ya shilingi bilioni 29.6.

    Dkt. Mwigulu amefanya ukaguzi huo leo wakati akipokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kutoka kwa Mkurugenzi wa Miradi wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mhandisi Japherson Nnko.

    Katika taarifa hiyo, Dkt. Mwigulu alielezwa kuwa hadi Mei 30, 2026, mradi huo ulikuwa umefikia asilimia 83.25 ya utekelezaji ambapo kati ya kilomita 25 zinazojengwa, kilomita 20.2 zimekamilika kwa kiwango cha lami, huku kilomita 4.8 zilizobaki zikiwa zimefikia hatua ya tabaka la juu la msingi na zinatarajiwa kukamilika mwezi Juni 2026.

    Mhandisi Nnko alisema kipande hicho ni sehemu ya Barabara ya Mbeya–Chunya–Makongolosi–Rungwa–Itigi–Mkiwa yenye urefu wa kilomita 524, inayounganisha mikoa ya Mbeya, Singida na Tabora na kwamba barabara hiyo inatarajiwa kuboresha usafirishaji wa watu, bidhaa na mazao katika ukanda huo hivyo kuchochea shughuli za kiuchumi.

    Aliongeza kuwa mradi huo unagharamiwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Tanzania na unatekelezwa na Kampuni ya China Henan International Cooperation Group Co. Ltd (CHICO) kwa gharama ya shilingi bilioni 29.6, bila kujumuisha Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).

    Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kazi za ujenzi zilianza Septemba 16, 2022 na zinatarajiwa kukamilika mwezi Agosti 2026 baada ya mkandarasi kuongezewa muda wa utekelezaji kwa mujibu wa masharti ya mkataba.

    Hadi Mei 30, 2026, mkandarasi ameshalipwa shilingi bilioni 12.9, huku akiidai Serikali shilingi bilioni 3.84. Aidha, Mhandisi Mshauri amelipwa shilingi bilioni 1.49 na anadai shilingi milioni 586.6.

    Taarifa hiyo pia ilieleza kuwa wananchi 578 walioathiriwa na utekelezaji wa mradi huo wamelipwa fidia ya jumla ya shilingi milioni 721.4 kwa mujibu wa sheria.

    Katika utekelezaji wa mradi huo, jumla ya ajira 305 zimezalishwa, ambapo ajira 278 sawa na asilimia 91 zimetolewa kwa wazawa na ajira 27 sawa na asilimia 9 zimetolewa kwa wageni.

  • Na Vincent Mpepo, OUT

    Imeelezwa kuwa elimu ya darasani pamoja na mafunzo ya ufundi yanayotolewa katika mfumo rasmi bado hayajawawezesha wahitimu kuwa wabunifu, mahiri na wenye uwezo wa kukabiliana na changamoto za maisha na ajira katika mazingira halisi.

    Hayo yamebainishwa leo katika mhadhara wa wazi uliofanyika katika ukumbi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, ambapo Profesa Mara Huber kutoka University at Buffalo aliwasilisha mada kuhusu mfumo wa kukuza stadi za ufundi kwa maendeleo ya uchumi wa viwanda.

    Profesa Mara alisema kuna umuhimu wa kuanzishwa kwa mfumo wa kitaifa utakaounganisha elimu, mafunzo ya ufundi stadi, tafiti, ubunifu, viwanda pamoja na mahitaji ya soko la ajira ili kujenga wataalamu wenye ujuzi wa vitendo na uwezo wa kujitegemea.

    Aidha, aliwasilisha matumizi ya nyenzo yake ya PEARL, inayolenga kuwawezesha watafiti, wanafunzi wa vyuo na ufundi pamoja na wadau wa maendeleo kujifunza kwa vitendo katika kutatua changamoto halisi za maendeleo, kuongeza thamani ya bidhaa na kubaini fursa mpya za ubunifu.

    “Hata wahitimu wa shahada mara nyingi hawapati uwezo wa kukidhi mahitaji ya soko la ajira na mazingira halisi ya kazi,” alisema Profesa Mara.

    Aliongeza kuwa kutokana na kasi ya maendeleo ya sayansi, teknolojia na matumizi ya akili unde, kuna umuhimu mkubwa wa elimu inayotolewa nje ya darasa kupitia uzoefu wa vitendo ili kuwajengea wahitimu umahiri wa kweli katika taaluma zao.

    “Kujenga uwezo katika elimu ya ufundi kutasaidia kuongeza thamani ya elimu kwa kuwapa wahitimu ujuzi wa vitendo, mfano katika fani za uchomeleaji,” alisisitiza.

    Akifungua mjadala huo, Mratibu wa Kigoda cha Viwanda na Maendeleo chuoni hapo, Dkt. Christopher Awinia alisema uchumi wa kati unaenda sambamba na maendeleo ya miundombinu ya kisasa, huku sekta ya uchomeleaji ikiwa miongoni mwa maeneo yanayokua kwa kasi na yanayohitaji kupewa kipaumbele maalumu.

    Alitaja maeneo mbalimbali yanayotegemea stadi za uchomeleaji, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya gesi, madini, afya pamoja na mitambo ya viwandani, akisisitiza kuwa sekta hiyo ni muhimu kwa maendeleo ya taifa.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Kitivo cha Sanaa na Sayansi za Jamii, Dkt. Dunlop Ochieng, aliwashukuru washiriki wa mhadhara huo na kueleza kuwa kigoda hicho ni jukwaa muhimu linalowakutanisha watafiti, wanazuoni na jamii kujadili masuala yenye manufaa kwa umma.

    Akizungumzia elimu ya ufundi na stadi za maisha, alisema waliopata elimu miaka 30 au 40 iliyopita wanakumbuka namna shule za msingi na sekondari zilivyotoa elimu ya kujitegemea iliyowajengea wanafunzi ujuzi wa vitendo na kuwafanya kuwa mahiri katika shughuli mbalimbali hata baada ya kuhitimu.

    Naye mhadhiri wa Sayansi ya Siasa, Dkt. Emmanuel Mallya, alisema mjadala kuhusu elimu ya ufundi unapaswa kuangalia namna mifumo ya elimu ya sasa isivyoendana na mahitaji halisi ya vijana.

    “Tatizo si vijana, bali ni mifumo. Haiwezekani kijana aliyesomea taaluma fulani akaambiwa aende kuzalisha parachichi au mafuta bila kuwa na uhakika wa soko na kipato,” alisema Dkt. Mallya.

    Alisisitiza umuhimu wa kuwa na mfumo wa elimu unaoanzia ngazi za chini ili kujenga kizazi kitakachoendana na mahitaji ya elimu ya ufundi na uchumi wa kisasa.

  • Na Cosmas Msuha

    Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi imesema katika mwaka wa fedha 2026/27 inatarajia kuajiri watumishi wapya 10,919 pamoja na kutekeleza vipaumbele vinane vinavyolenga kuimarisha usalama, huduma za uraia na matumizi ya teknolojia nchini.

    Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo bungeni jijini Dodoma Mei 25, 2026, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi alisema ajira hizo ni sehemu ya mkakati wa kuongeza ufanisi katika vyombo vya usalama vilivyo chini ya wizara hiyo.

    Aidha, Idara ya Uhamiaji Tanzania inatarajia kuajiri watumishi 1,000 huku Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) ikipanga kuajiri watumishi 84 ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

    Katika bajeti hiyo, Waziri Katambi alisema wizara itaendelea kuboresha miundombinu ya vyombo vya usalama ikiwemo makazi ya maofisa, wakaguzi, askari pamoja na watumishi wasio askari ili kuongeza mazingira bora ya kazi na ufanisi wa utendaji.

    Pia wizara imepanga kuimarisha upatikanaji wa vitendea kazi, ikiwemo vyombo vya usafiri na usafirishaji kwa taasisi zote zilizo chini yake, hatua inayolenga kuongeza kasi ya utekelezaji wa majukumu ya kiusalama nchini.

    Mheshimiwa Katambi alisema wizara itaendelea kufanya tafiti mbalimbali kubaini sababu za kuongezeka kwa makosa mapya pamoja na kuweka mikakati madhubuti ya kuyadhibiti. Aliongeza kuwa matumizi ya TEHAMA yataendelea kupewa kipaumbele katika utoaji wa huduma na usimamizi wa shughuli za wizara hiyo.

    Katika miradi ya maendeleo, wizara itaanza ujenzi wa makao makuu ya NIDA jijini Dodoma, pamoja na ofisi 31 za usajili katika wilaya mbalimbali na kituo cha mafunzo na matengenezo ya vifaa vya TEHAMA mjini Kibaha.

    Mbali na hilo, wizara imesema itaendelea kuimarisha shughuli za uzalishaji mali kupitia sekta za kilimo, mifugo, viwanda pamoja na utunzaji wa mazingira.

  • Na Cosmas Msuha

    Shughuli za uchimbaji madini katika Mgodi wa Namungo uliopo Wilaya ya Ruangwa zimeendelea kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa eneo hilo, huku wachimbaji waliokuwa wakihangaika kimaisha wakianza kunufaika na maendeleo kupitia sekta ya madini.

    Akizungumza kwa niaba ya Afisa Madini Mkazi wa Lindi, Dickson Joram alisema shughuli za uchimbaji katika mgodi huo zimechangia kuboresha huduma za maji, elimu, afya pamoja na miundombinu huku zikifungua fursa za ajira na kukuza biashara kwa wananchi wa maeneo yanayouzunguka mgodi huo.

    Alieleza kuwa hali ya maisha ya wachimbaji na wananchi wa Namungo imebadilika kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na mwaka 2019, ambapo wachimbaji wengi walikuwa wakitumia njia duni za uzalishaji na kushindwa kumudu mahitaji muhimu ya kila siku.

    “Leo Namungo imebadilika kwa kiasi kikubwa, wananchi wanajitegemea na wanaendesha shughuli kubwa kupitia sekta ya madini,” alisema Mhandisi Joram.

    Kwa upande wake, Afisa Uhusiano wa kampuni ya Elianje Limited, Joseph Shayo alisema kampuni hiyo ilianza shughuli za utafiti na uchimbaji mwaka 2020 na imekuwa ikihakikisha jamii inayozunguka mgodi inanufaika kupitia miradi mbalimbali ya kijamii.

    Alisema kampuni hiyo imechimba visima na kusambaza maji katika Kijiji cha Tongwe pamoja na Kitongoji cha Namungo, huku ikiendelea kuboresha huduma ya maji safi na salama katika maeneo yenye changamoto ya upatikanaji wa maji.

    Katika sekta ya elimu, kampuni hiyo imejenga shule ya awali, kuboresha madarasa, kujenga vyoo vya kisasa na kushiriki katika ujenzi wa shule ya msingi katika Kitongoji cha Namungo ili kupunguza umbali wa wanafunzi kufuata elimu.

    Aidha, mgodi huo umechangia uboreshaji wa barabara zinazounganisha vijiji na kata jirani pamoja na kusaidia shule mbalimbali kwa vifaa vya elimu ikiwemo kompyuta na mashine za uchapishaji.

    Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Chingumbwa, Kata ya Mbekenyela Wilaya ya Ruangwa, Abdallah Manjakali alisema uwepo wa mgodi huo umefungua fursa nyingi za ajira, biashara na huduma za kijamii ambazo hapo awali zilikuwa changamoto kubwa kwa wananchi.

    “Leo wananchi wanapata kipato na maisha yameimarika, pia kampuni imenunua gari la wagonjwa linalowahudumia wananchi bure wakati wa dharura bila kuchangishwa fedha yoyote,” alisema Manjakali.

    Aidha, alisisitiza kuwa ushirikiano kati ya mgodi na jamii inayouzunguka unapaswa kuwa mfano kwa wawekezaji wengine wa sekta ya madini, huku akizitaka kampuni zenye leseni ambazo bado hazijaanza uzalishaji kuharakisha uwekezaji ili wananchi wanufaike zaidi na rasilimali zilizopo katika maeneo yao.

  • Na Cosmas Msuha

    Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imeridhishwa na maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa Msalato Satellite City unaotekelezwa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia programu ya Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi (KKK) katika eneo la Msalato jijini Dodoma.

    Ziara hiyo ya ukaguzi ililenga kujionea maendeleo ya mradi huo wenye ukubwa wa takribani ekari 971, unaotarajiwa kutumika kwa shughuli mbalimbali za maendeleo na unatarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa na maeneo yanayozunguka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato.

    Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Timotheo Mnzava, amepongeza juhudi zinazofanywa na wizara katika usimamizi wa sekta ya ardhi na kusisitiza kuwa utekelezaji wa mradi huo unaendana na mipango ya serikali ya upimaji na upangaji bora wa ardhi.

    Kwa upande wake, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapo, aliishukuru kamati hiyo kwa kutembelea mradi na kupokea taarifa ya utekelezaji wake. Pia aliahidi kuyafanyia kazi maelekezo yaliyotolewa ili kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa ufanisi, tija na kwa kuzingatia masilahi ya Taifa.

    Aidha, Dkt. Akwilapo alisema mradi huo utasaidia kuongeza thamani ya ardhi, kuboresha mipango ya matumizi ya ardhi, kuvutia wawekezaji na kufungua fursa mpya za kiuchumi katika maeneo yanayozunguka Uwanja wa Ndege wa Msalato.

    Katika ziara hiyo, Waziri Akwilapo aliambatana na Naibu Waziri wa wizara hiyo Kaspar Mmuya, Katibu Mkuu Anthony Sanga pamoja na wajumbe wa menejimenti na wataalamu mbalimbali wa wizara hiyo.