
Na Jastini Bukebuke
Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Mbogwe, SP Yusuph Chiwanga, amewataka Sungusungu na wananchi wa Kijiji cha Luhala, Kata ya Lugunga, kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi wanapotekeleza majukumu yao ya ulinzi na usalama.
Akizungumza katika kikao cha uhamasishaji wa usalama wa jamii, SP Chiwanga alisema ni muhimu kwa Sungusungu kuzingatia nidhamu, maadili na taratibu za kisheria wakati wa kuwakamata watuhumiwa, badala ya kutumia nguvu kupita kiasi.
Alieleza kuwa utendaji unaozingatia sheria na haki huchangia kujenga imani kwa wananchi na kuondoa malalamiko yanayoweza kujitokeza katika jamii.
Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kushirikiana na Sungusungu pamoja na Jeshi la Polisi katika kudumisha amani na utulivu, huku akisisitiza kuwa kila mmoja ana wajibu wa kufuata sheria na taratibu zilizowekwa.
Kwa upande wake, Mkaguzi wa Polisi wa Kata ya Masumbwe, INSP Oliver Kasembe, aliwahimiza Sungusungu na wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za wahalifu na vitendo vya uhalifu vinavyotokea katika maeneo yao.

Alisema ushirikiano huo ni nguzo muhimu katika mapambano dhidi ya uhalifu, huku akiwataka wananchi kutofumbia macho vitendo vya kihalifu vinavyoweza kuhatarisha usalama wa jamii.
INSP Kasembe pia alitoa rai kwa wananchi kuachana na migogoro inayotokana na kulishiana mazao, akieleza kuwa migogoro hiyo imekuwa chanzo kikubwa cha migongano miongoni mwa wakazi wa kijiji hicho.
Naye Mkaguzi wa Polisi, INSP Nuru Mdugo, alikemea vitendo vya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto, huku akiwataka wananchi kujiepusha na matendo hayo ambayo yanaathiri ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.

Alisisitiza umuhimu wa wazazi na walezi kuwapatia watoto malezi bora yenye misingi ya maadili mema na kumcha Mungu, ili kujenga kizazi chenye nidhamu na kinachopinga vitendo vya ukatili.
“Malezi bora ndiyo msingi wa kujenga jamii salama na yenye maadili. Ni wajibu wa kila mzazi na mlezi kuhakikisha watoto wanakua katika mazingira yanayowajenga kuwa raia wema,” alisema INSP Mdugo.





















