Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limemfikisha katika Mahakama ya Wilaya ya Chato, Lufuta Magoma (40), mganga wa kienyeji na mkazi wa Kijiji cha Rutunguru, akikabiliwa na shtaka la kumuua mama yake mzazi, Dotto Magoma Nyara (70).
Mshtakiwa alipandishwa kizimbani jana, Julai 10, 2026, ambapo alisomewa shtaka la mauaji mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Erick Kagimbo.
Akisoma shauri la jinai namba 15471/2026, Wakili wa Serikali, Mashaka Said, alidai kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Juni 4, 2026, katika Kijiji cha Rutunguru, Wilaya ya Chato, Mkoa wa Geita.
Upande wa mashtaka ulidai kuwa Lufuta Magoma alimuua mama yake mzazi, Dotto Magoma Nyara, kinyume na vifungu vya 196 na 197 vya Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16, kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2023.
Hata hivyo, mshtakiwa hakutakiwa kujibu shtaka hilo kwa kuwa Mahakama ya Wilaya haina mamlaka ya kusikiliza kesi za mauaji.
Hakimu Kagimbo alisema kuwa kutokana na aina ya shtaka linalomkabili mshtakiwa, kesi hiyo haina dhamana, hivyo ataendelea kuwa mahabusu hadi upelelezi utakapokamilika na hatua nyingine za kisheria kuchukuliwa.
Kesi hiyo imeahirishwa mpaka Julai 23, 2026, kwa ajili ya kutajwa, huku mshtakiwa akirejeshwa rumande akisubiri maendeleo ya upelelezi.
Mjiolojia kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Abbas Mruma, amesema Tanzania inaendelea kujijengea nafasi muhimu duniani kutokana na kuwa na hifadhi kubwa ya madini ya kimkakati, yakiwemo graphite, lithium na rare earth elements, ambayo ni nguzo muhimu katika maendeleo ya teknolojia za kisasa na nishati safi.
Mruma alitoa kauli hiyo wakati akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Stanslaus Muyungi, alipotembelea banda la Tume ya Madini katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).
Alisema mahitaji ya madini ya lithium yanaongezeka kwa kasi duniani kutokana na matumizi yake katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme, simu za mkononi, kompyuta mpakato na vifaa vingine vya kisasa vya kielektroniki.
Kwa mujibu wa Mruma, nchini Tanzania madini ya lithium yanapatikana zaidi katika maeneo ya Dodoma na Ikungi, mkoani Singida, hali inayoiweka nchi katika nafasi nzuri ya kunufaika na ongezeko la mahitaji ya madini hayo katika soko la kimataifa.
Akizungumzia madini ya graphite, alisema Tanzania ndiyo nchi inayoongoza barani Afrika kwa kuwa na hifadhi kubwa ya madini hayo, ambayo ni malighafi muhimu katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme pamoja na matumizi mbalimbali ya viwandani.
Aidha, alisema Tanzania pia ina hifadhi kubwa ya madini ya rare earth elements katika Ukanda wa Afrika Mashariki, yanayopatikana katika eneo la Ngualla mkoani Songwe na Wigu mkoani Morogoro. Madini hayo yanatumika katika utengenezaji wa vifaa vya teknolojia ya juu, ikiwemo vifaa vya mawasiliano, nishati jadidifu na vifaa vya ulinzi.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Stanslaus Muyungi, aliipongeza Tume ya Madini kwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu rasilimali za madini na fursa zinazopatikana katika sekta hiyo.
Alisema elimu hiyo ina mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa rasilimali za madini, kuvutia uwekezaji na kuonesha nafasi ya sekta ya madini katika kukuza uchumi na kufanikisha maendeleo endelevu ya Taifa.
KAIMU Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino, Dkt. Sophia Nchimbi, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, amezindua mradi wa Mama Tembe unaolenga kuhifadhi urithi wa kiutamaduni wa Wagogo, kuwawezesha wanawake na wasichana, pamoja na kukuza uchumi kupitia ubunifu wa asili.
Uzinduzi wa mradi huo umefanyika hivi karibuni wilayani Chamwino, mkoani Dodoma. Mradi unasimamiwa na Shirika la Innovation Development for Future Generation (IDFG) kwa ufadhili wa Serikali za Uswisi na Norway kupitia programu ya Articipate.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt. Nchimbi alisema mradi unawahusisha wanawake wazee 15 wa kabila la Kigogo, mabinti 20 na wanafunzi kutoka shule tatu ambao watarithi mbinu za uchoraji wa jadi kwa kutumia zana na malighafi za asili zilizokuwa zikitumika kupamba nyumba za tembe.
Alisema uchoraji wa nyumba za tembe si mapambo ya kawaida bali ni sehemu muhimu ya historia na utambulisho wa Wagogo, hivyo kurejeshwa kwake kutasaidia kuitangaza Chamwino kama kitovu cha utalii wa utamaduni kupitia kazi za ubunifu zinazofanywa na wananchi.
“Tunafungua ukurasa mpya wa kuhifadhi utamaduni wetu. Kupitia mradi huu, Chamwino itanufaika kwa kuitangaza historia na utamaduni wake,” alisema Dkt. Nchimbi.
Aliongeza kuwa mradi huo pia utawawezesha wananchi kujiongezea kipato kupitia shughuli za sanaa, huku Halmashauri ikiendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha unafanikiwa.
Kwa upande wake, Afisa Utamaduni wa Wilaya ya Chamwino, Jackson Kitija, alisema mradi umefika kwa wakati muafaka kwani baadhi ya maarifa ya jadi yalikuwa yameanza kupotea kutokana na wazee waliokuwa nayo kuzeeka huku vijana wengi wakikosa fursa ya kuyajifunza.
Kitija alisema hatua inayofuata ni kuhakikisha ubunifu wa wanawake hao unalindwa kwa kupata hati miliki, huku michoro hiyo ikitumika kutengeneza bidhaa mbalimbali zenye thamani ya kiuchumi, ikiwemo mavazi yatakayobeba utambulisho wa sanaa ya Wagogo.
Mkurugenzi wa Shirika la Innovation Development for Future Generation (IDFG), Bi. Victoria Mponda, alisema mradi wa Mama Tembe umebuniwa baada ya utafiti kubaini kuwa wanawake wa Kigogo walikuwa na mchango mkubwa katika kuhifadhi utamaduni kupitia michoro ya nyumba za tembe.
Alisema mradi hautaishia kutoa mafunzo pekee, bali utakusanya historia ya michoro hiyo, kueleza maana ya kila mchoro na kuhifadhi taarifa zote kidijitali ili ziwe rejea kwa vizazi vijavyo.
“Tunataka wanawake hawa watambulike kama wabunifu wa sanaa hii. Tutahifadhi kazi zao kidijitali, tutazisajili kwa hati miliki na baadaye kuzigeuza kuwa bidhaa zitakazoweza kuuzwa,” alisema Mponda.
Alieleza kuwa changamoto kubwa mwanzoni mwa utekelezaji wa mradi ilikuwa kuwashawishi wanawake wazee kushiriki, kwa kuwa wengi hawakuamini kuwa uchoraji walioutumia kwa miaka mingi kupamba nyumba ungeweza kuwa chanzo cha kipato.
“Kwa kushirikiana na viongozi wa serikali na wa kimila tuliwafikia na kuwajengea uelewa kuwa sanaa nayo ni uchumi. Leo wamekubali kurithisha maarifa yao kwa mabinti, jambo ambalo tunaamini litakuwa mwanzo wa kufufua sanaa iliyokuwa ikielekea kutoweka,” alisema Mponda.
Miongoni mwa wanufaika wa mradi huo ni Bi. Esteli Chibaya (84), mkazi wa Chamwino, ambaye alisema amefurahishwa na hatua ya kupewa nafasi ya kurithisha ujuzi alioupata tangu akiwa msichana, akiamini kuwa vijana wataendelea kuuenzi utamaduni wa Wagogo badala ya kuuacha upotee.
“Tulikuwa tunachora nyumba kwa ajili ya kuzipamba bila kujua kuwa siku moja ujuzi huu ungekuwa sehemu ya maendeleo yetu. Leo nina furaha kuona watoto na wajukuu wetu wataurithi na kuutumia kujenga maisha yao,” alisema Bi. Chibaya.
Mradi wa Mama Tembe unatarajiwa kukamilika Oktoba 2026. Wadau wanaamini kuwa, mbali na kufufua sanaa ya uchoraji wa nyumba za tembe, utasaidia kuhifadhi urithi wa kabila la Wagogo, kuimarisha utalii wa utamaduni na kuwawezesha wanawake kutumia maarifa ya jadi kama nyenzo ya kujiletea maendeleo.
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), amemuapisha Massana Gibril Mwishawa kuwa Kamishna mpya wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), akisema uteuzi wake unaashiria imani ya Serikali katika uwezo wake wa kuendeleza sekta ya uhifadhi na utalii nchini.
Akizungumza katika hafla ya uapisho iliyofanyika jana katika Makao Makuu ya TANAPA jijini Arusha, Dkt. Kijaji alimtaka Kamishna Mwishawa kuimarisha mapambano dhidi ya ujangili na uhalifu wa wanyamapori kwa kutumia teknolojia za kisasa pamoja na mifumo madhubuti ya kiintelijensia.
Alisema Serikali ina matarajio makubwa kwamba Kamishna huyo atailinda na kuiendesha TANAPA kwa weledi, uadilifu, nidhamu, umoja na maono yatakayoiwezesha taasisi hiyo kuendelea kuwa mfano wa kuigwa katika uhifadhi na utalii ndani na nje ya nchi.
Aidha, Dkt. Kijaji alisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za Serikali, huku akimtaka Kamishna huyo kuboresha maslahi ya watumishi kwa kuongeza nyumba za askari na watumishi, kuboresha vitendea kazi, kuimarisha mafunzo pamoja na huduma za afya.
“Hapa Kamishna wa Uhifadhi, naomba upigie mstari. Ninatarajia kuona TANAPA ikiwa taasisi inayojivunia watumishi wenye maadili, nidhamu, ari ya kazi na uzalendo wa hali ya juu,” alisisitiza Dkt. Kijaji.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya TANAPA, Jenerali Mstaafu George Waitara, alisema bodi itaendelea kutoa ushirikiano na ushauri unaohitajika ili kufanikisha azma ya kuendeleza sekta ya maliasili na utalii nchini.
Naye Kamishna mpya wa Uhifadhi wa TANAPA, Massana Gibril Mwishawa, alisema Hifadhi za Taifa ni hazina muhimu ya ikolojia, uchumi na jamii, yenye mchango mkubwa katika kuongeza pato la Taifa.
Aliahidi kutekeleza majukumu yake kwa weledi, uwazi na uwajibikaji, huku akisisitiza ushirikiano na wadau mbalimbali wa uhifadhi ili kuendelea kulinda rasilimali za taifa na kukuza sekta ya utalii.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na wakuu wa taasisi mbalimbali za uhifadhi, wakiwemo wawakilishi kutoka TAWA, TFS na NCAA, pamoja na viongozi wa Serikali, wadau wa uhifadhi na utafiti, maafisa na askari wa TANAPA.
Wakazi wa Jiji la Dodoma wamesema ujenzi wa barabara za mzunguko umeleta manufaa makubwa kwao, ikiwemo kuongeza fursa za biashara, kurahisisha usafiri na kuchochea ukuaji wa uchumi katika maeneo yanayozunguka barabara hizo.
Mmoja wa wakazi wa eneo la Nala, Bi. Minnael Msanga, alisema uwepo wa barabara hiyo umeongeza idadi ya watu wanaopita katika eneo hilo na hivyo kuwapatia wakazi fursa zaidi za kufanya biashara.
Kwa upande wake, Mussa Rajab, mkazi wa Nala anayejishughulisha na kazi za ubebaji mizigo, alisema sehemu ya kisasa ya kuegesha magari iliyojengwa kandokando ya barabara imeongeza ajira na kipato kwao.
“Mwanzoni eneo hili halikuwepo, hivyo kusimama kwa magari hapa kulitegemea udharura wa dereva, nasi tulipata kazi kwa uchache sana. Lakini sasa magari yanasimama, mizigo inashushwa hapa na sisi tunapata ridhiki,” alisema Rajab.
Naye Simon Ndamanyilu, dereva wa lori la mizigo kutoka Dar es Salaam kwenda Rwanda, alisema barabara hiyo imewaondolea ulazima wa kupita katikati ya Jiji la Dodoma, jambo linalopunguza muda wa safari na matumizi ya mafuta.
“Imeturahisishia sana. Safari imekuwa fupi kwa sababu njia hii haina foleni hata kidogo,” alisema Ndamanyilu.
Akizungumzia mradi huo, Mhandisi Morice Mlay kutoka kampuni ya mzawa ya Inter-Consult Ltd, ambayo ni Mhandisi Mshauri wa mradi, alisema barabara za mzunguko zimechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza msongamano wa magari katikati ya Jiji la Dodoma, hasa malori yanayosafirisha mizigo kwenda nchi jirani.
Alisema sehemu ya kwanza ya mradi imefikia hatua za mwisho za utekelezaji na tayari imeanza kutumika, huku uzinduzi rasmi ukitarajiwa kufanyika Oktoba 2026 baada ya kukamilika kwa kazi zilizobaki.
“Ujenzi wa sehemu ya kwanza umefikia ukingoni. Kilichobaki ni baadhi ya kazi ndogo, ikiwemo ufungaji wa taa za barabarani na umaliziaji wa njia za watembea kwa miguu,” alisema Mhandisi Mlay.
Alifafanua kuwa mradi huo wa barabara ya njia nne kwa kiwango cha lami unaunganisha mikoa ya Morogoro, Arusha, Singida na Iringa. Barabara hiyo ina urefu wa kilometa 112.3, ambapo kipande cha kwanza chenye kilometa 52.3 kimekamilika kwa asilimia 93.3.
Mradi wa kipande cha kwanza unagharimu shilingi bilioni 100.84 na unatarajiwa kuendelea kuwa suluhisho la msongamano wa magari katikati ya Jiji la Dodoma, huku ukichochea ukuaji wa uchumi wa mkoa wa Dodoma, mikoa jirani na Taifa kwa ujumla.
Serikali imesema mageuzi yanayoendelea kutekelezwa katika sekta ya madini yameifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zenye mazingira bora ya uwekezaji barani Afrika, huku yakifungua fursa mbalimbali katika utafiti, uchimbaji, uchenjuaji, uchakataji na uongezaji thamani wa madini.
Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, alitoa kauli hiyo jana alipofungua Kongamano la Madini lililofanyika katika Ukumbi wa Dome, ndani ya Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF), maarufu Sabasaba.
Alisema maboresho ya sera, sheria na mifumo ya usimamizi wa sekta ya madini yameongeza uwazi, uwajibikaji na ushiriki wa sekta binafsi, hatua zilizochochea ongezeko la uwekezaji, ajira na mchango wa sekta hiyo katika ukuaji wa uchumi wa taifa.
Dkt. Kiruswa alisema Tanzania imebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi za madini, zikiwemo dhahabu, almasi, tanzanite, nikeli, makaa ya mawe, niobium, madini adimu pamoja na madini ya viwandani na ujenzi.
“Serikali haiwaaliki wawekezaji kuja kuchimba madini pekee, bali pia kuwekeza katika tafiti za kijiolojia, teknolojia za uchenjuaji, uchakataji, uongezaji thamani wa madini na viwanda vinavyotumia madini kama malighafi,” alisema Dkt. Kiruswa.
Akizungumzia kongamano hilo, alisema linatarajiwa kufungua fursa mpya za biashara na uwekezaji, huku akiwakaribisha wadau kushiriki Mkutano wa Kimataifa wa Madini utakaofanyika Novemba 19 hadi 21, 2026, katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam. Alisema mkutano huo unalenga kuendelea kuitangaza Tanzania kama kitovu cha uwekezaji katika sekta ya madini barani Afrika.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini wa Tume ya Madini, CPA Venance Kasiki, alisema Tume inaendelea kusimamia utoaji wa leseni za utafutaji, uchimbaji, uongezaji thamani na biashara ya madini kwa kuzingatia Sheria ya Madini ili kuhakikisha rasilimali hizo zinawanufaisha Watanzania na taifa kwa ujumla.
Alisema serikali pia inaendelea kuimarisha utekelezaji wa Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania, zinazolenga kuwawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika usambazaji wa bidhaa na huduma ndani ya mnyororo wa thamani wa sekta ya madini.
Aidha, aliwahimiza Watanzania kutumia fursa zilizopo kwa kuwekeza katika viwanda vinavyozalisha bidhaa na vifaa vinavyotumika migodini, pamoja na kutoa huduma mbalimbali zinazohitajika katika shughuli za uchimbaji na uongezaji thamani wa madini.
Awali, Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita, Mohamed Jumanne, alisema sekta ya madini imeendelea kutoa ajira kwa maelfu ya vijana na kuchangia ukuaji wa uchumi katika maeneo yenye shughuli za uchimbaji.
Alisema serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano katika masuala ya ulinzi na usalama ili shughuli za uchimbaji zifanyike kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo, hatua itakayochochea maendeleo endelevu ya sekta hiyo na kuongeza mchango wake katika uchumi wa taifa.
Serikali imewaagiza wazalishaji wote nchini kutumia alama ya ‘Made in Tanzania’ ili kuongeza utambulisho na imani kwa bidhaa zinazozalishwa nchini, pamoja na kuimarisha ushindani wake katika masoko ya kimataifa.
Agizo hilo limetolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Emmanuel Nchimbi, wakati wa kilele cha maadhimisho ya Usiku wa Jubilei ya Dhahabu (Miaka 50) ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam hivi karibuni.
Makamu wa Rais alizitaka taasisi zinazosimamia viwango na huduma za kifedha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ili kuhakikisha bidhaa za Tanzania zinakidhi viwango vinavyokubalika katika soko la kimataifa.
“Matumizi ya alama ya ‘Made in Tanzania’ yataongeza utambulisho wa bidhaa zenye ubora na kuimarisha heshima ya taifa katika biashara za kimataifa,” alisema Mhe. Balozi Nchimbi.
Aidha, aliwapongeza wadau wa sekta ya fedha kwa kuendelea kutoa mikopo yenye masharti nafuu kwa viwanda vidogo na vya kati, akisema hatua hiyo imechangia kupunguza changamoto ya upatikanaji wa mitaji kwa wajasiriamali na kuchochea ukuaji wa uzalishaji nchini.
Alisema Serikali itaendelea kuweka sera rafiki kwa uwekezaji, kuboresha miundombinu na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi ili kujenga uchumi wa viwanda wenye ushindani.
Kwa upande wake, Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mbunge), alisema Tanzania itanufaika zaidi na rasilimali zake endapo itawekeza katika uchakataji na uzalishaji wa bidhaa za mwisho zenye thamani kubwa, badala ya kuendelea kuuza malighafi ghafi nje ya nchi.
Alibainisha kuwa hatua hiyo itafungua masoko mapya, kuongeza thamani ya mauzo ya bidhaa nje ya nchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa wananchi.
Mhe. Kapinga alisisitiza kuwa ili kujenga uchumi imara wa viwanda wenye ushindani, ni muhimu kubadili mtazamo wa uzalishaji kwa kuhakikisha mazao ya kilimo, mifugo, uvuvi, misitu na madini yanaongezewa thamani kwa kuchakatwa, kufungashwa vizuri na kuzalishwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.
Aidha, alisema uwekezaji katika teknolojia za kisasa una mchango mkubwa katika kuongeza uzalishaji, kuboresha ubora wa bidhaa zinazozalishwa nchini, kupunguza gharama za uzalishaji na kuziwezesha bidhaa za Tanzania kushindana katika masoko ya kimataifa.
Hafla hiyo iliambatana na utoaji wa tuzo kwa washirika muhimu wa TANTRADE pamoja na taasisi zinazochangia maendeleo ya biashara, viwango na huduma za kifedha nchini.
Kwa mujibu wa Makamu wa Rais, Mhe. Balozi Nchimbi maadhimisho ya Jubilei ya Dhahabu ya TANTRADE ni fursa muhimu ya kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 50, ikiwemo kuongezeka kwa viwanda, uzalishaji, ajira na upanuzi wa masoko ya bidhaa na huduma za Tanzania duniani.
Ofisi ya Waziri Mkuu imewawezesha watu wenye ulemavu kushiriki katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kupitia Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA).
Ushiriki huo umewawezesha kuonesha bidhaa na huduma mbalimbali wanazozalisha na kuzitoa, pamoja na kufanya biashara katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.
Akitembelea mabanda ya washiriki hao, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Ummy Nderiananga, alieleza kuridhishwa na kiwango cha ushiriki wa watu wenye ulemavu, akibainisha kuwa ushiriki wao umeongeza fursa za kiuchumi na kuonesha uwezo wao katika uzalishaji na biashara.
Aidha, Nderiananga aliipongeza Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) pamoja na taasisi nyingine zilizowezesha ushiriki huo na kuzitaka mamlaka za serikali za mitaa kuendelea kutenga na kutoa mikopo ya asilimia mbili kwa watu wenye ulemavu ili kuwawezesha kukuza shughuli zao za kiuchumi.
“Ni wakati sasa kwa watu wenye ulemavu kuendelea kuonesha uwezo wao katika uzalishaji na biashara. Kupitia maonesho haya tumejionea matokeo chanya ya uwezeshaji wa kiuchumi unaotokana na mikopo na fursa zinazotolewa na Serikali,” alisema Nderiananga.
Kwa upande wake, mwakilishi wa washiriki hao, Bi. Pili Bilahi, aliishukuru Serikali kwa kuwawezesha kushiriki katika maonesho hayo bila kulipia gharama yoyote.
Vilevile, Bi. Bilahi aliishukuru serikali kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi yanayowapa watu wenye ulemavu fursa za kiuchumi, ikiwemo kupitia mikopo ya asilimia mbili ya mapato ya ndani inayotolewa na halmashauri.
Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, “Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania,” yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu nchini. Maonesho hayo yalianza Juni 28 na yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13, 2026.