Timu ya Nanyumbu Veterans imezindua rasmi jezi zake mpya katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Lindi Veterans uliochezwa kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Mangaka, Wilaya ya Nanyumbu.
Mchezo huo ulimalizika kwa sare ya mabao 1-1, huku ukishuhudiwa na mashabiki wengi na kuambatana na ushindani mkubwa. Lengo la mchezo huo lilikuwa kuimarisha afya, umoja na mshikamano miongoni mwa wanamichezo na jamii.
Mgeni rasmi katika hafla ya uzinduzi huo alikuwa Diwani wa Kata ya Mangaka, Salvatory Lyimo, ambaye aliipongeza Nanyumbu Veterans kwa hatua ya kuzindua jezi mpya na kuendelea kushiriki shughuli za michezo zinazochochea afya, urafiki na ushirikiano wa wananchi.
Akizungumza baada ya mchezo huo, Nahodha wa Nanyumbu Veterans, Hassan Simoje, alimshukuru Diwani Lyimo kwa ushirikiano na uungaji mkono wake, akisema umeongeza ari kwa wachezaji na kuhamasisha maendeleo ya michezo katika kata hiyo.
“Tunamshukuru sana Mheshimiwa Diwani kwa kuwa nasi wakati wote. Mchango wake umetupa nguvu na motisha wa kuendelea kuitangaza Mangaka kupitia michezo,” alisema Simoje.
Kwa upande wake, shabiki wa timu hiyo, Matajabu Juma, alisema uzinduzi wa jezi mpya ni hatua muhimu kwa Nanyumbu Veterans na utaongeza hamasa kwa wachezaji pamoja na mashabiki.
“Tunajivunia kuona timu yetu inaendelea kupiga hatua. Tunampongeza Diwani kwa kuendelea kuwa karibu na timu, na tunaamini ushirikiano huu utaifanya Nanyumbu Veterans kufikia mafanikio makubwa zaidi,” alisema Juma.
Mashabiki waliojitokeza kushuhudia mchezo huo walieleza kufurahishwa na kiwango kilichoonyeshwa na timu zote mbili, wakiahidi kuendelea kuiunga mkono Nanyumbu Veterans katika michezo ijayo. Walisisitiza kuwa michezo ni nyenzo muhimu ya kuimarisha afya, urafiki na maendeleo ya jamii.
Mzize Foundation kwa kushirikiana na GSM Foundation imeandaa Tamasha la ‘Washike Mkono’, lililofanyika jana katika Uwanja wa Samora mkoani Iringa, likiwa na lengo la kukusanya rasilimali kwa ajili ya kuwapatia madereva wa bodaboda kofia ngumu (helmeti) na kuchangia vifaa tiba katika vituo mbalimbali vya afya mkoani humo.
Mgeni rasmi katika tamasha hilo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James, ambaye aliungana na mamia ya wakazi wa mkoa huo kushiriki tukio hilo lililolenga kuhamasisha mshikamano wa jamii kupitia michezo na shughuli za kijamii.
Mbali na kampeni ya kuchangisha rasilimali, Mzize Foundation ilitoa mafuta bure kwa madereva wa bodaboda walioshiriki tamasha hilo ikiwa ni sehemu ya kuthamini mchango wao katika jamii na kuhamasisha usalama barabarani.
Akizungumza baada ya tamasha hilo, mshambuliaji wa Klabu ya Young Africans (Yanga SC) na Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars), Clement Mzize, aliwashukuru wakazi wa Mkoa wa Iringa kwa mwitikio mkubwa waliouonesha na kueleza kufurahishwa na mafanikio ya tukio hilo.
“Kwa kweli nina furaha sana. Matarajio niliyokuwa nayo yametimia kwa kiwango kikubwa. Watu wamejitokeza kwa wingi kunipa ushirikiano kwa sababu ni ndugu yao. Huu ni mwanzo mzuri, na naamini mambo mengi mazuri zaidi yanakuja,” alisema Mzize.
Kwa upande wake, Msemaji wa Klabu ya Yanga, Ali Kamwe, aliwapongeza wakazi wa Mkoa wa Iringa kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki tamasha hilo, akisema mwitikio huo unaonesha mshikamano mkubwa wa wananchi katika kuunga mkono shughuli zenye manufaa kwa jamii.
Tamasha hilo lilianza kwa mazoezi ya pamoja yaliyowakutanisha wananchi na wadau mbalimbali, kisha kufuatiwa na mchezo wa utangulizi kati ya Iringa All Stars Veterans na Ruaha National Park, uliomalizika kwa sare ya mabao 1-1.
Baadaye kulichezwa mechi ya hisani kati ya Timu ya Mzize na Timu ya Oscar, ambapo Timu ya Mzize iliibuka na ushindi wa mabao 2-0.
Tamasha hilo lilifanikishwa kwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, wakiwemo Ruaha National Park, K4S Security, Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa, ASAS pamoja na taasisi nyingine zilizojitokeza kuunga mkono jitihada za Mzize Foundation za kutumia michezo kama chachu ya maendeleo na ustawi wa jamii.
Harakati za kukuza utalii nchini zimeendelea kushika kasi baada ya mamia ya washiriki kutoka ndani na nje ya Tanzania kushiriki mbio za Arusha Tourism Marathon zilizofanyika jana ndani ya Hifadhi ya Taifa Arusha, zikilenga kuhamasisha utalii kupitia michezo.
Mashindano hayo yalijumuisha mbio za kilometa 2.5, 5, 10 na 21, mbio za baiskeli, burudani ya muziki, michezo ya watoto pamoja na shughuli mbalimbali zilizowapa washiriki fursa ya kujionea vivutio vya kipekee vinavyopatikana ndani ya hifadhi hiyo.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Arusha, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Witness Shoo, ambaye alikuwa mgeni rasmi, alisema mbio hizo zimekuwa jukwaa muhimu la kutangaza utalii kwa kuwaunganisha wananchi na wageni na vivutio vya asili vinavyopatikana nchini.
Alisema matukio yanayounganisha michezo na utalii yana mchango mkubwa katika kuitangaza Tanzania kimataifa na kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea hifadhi za taifa na maeneo mengine ya vivutio vya utalii.
Kwa upande wake, Mkurugenzi na Mwanzilishi wa Ruaha Tourism Marathon, Cornell Magoti, alisema lengo la mbio hizo ni kuunganisha sekta ya michezo na utalii ili kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea vivutio vya Tanzania na hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia sekta ya utalii.
Baadhi ya washiriki wa mbio hizo walieleza kufurahishwa na mandhari ya kuvutia pamoja na vivutio mbalimbali walivyopata fursa ya kuviona ndani ya Hifadhi ya Taifa Arusha, wakisema tukio hilo limewapa uzoefu wa kipekee na kuwahamasisha kuendelea kutembelea maeneo ya utalii nchini.
Waandaaji wa mbio hizo walieleza kuwa wanaendelea kutumia michezo kama jukwaa la kuitangaza Tanzania, wakiamini kuwa matukio ya aina hiyo yanaongeza mwamko wa utalii wa ndani na kuvutia wageni kutoka mataifa mbalimbali.
Mafundi ujenzi wapatao 460 kutoka mikoa ya Geita na Mwanza wamehimizwa kufanya kazi kwa weledi, uaminifu na uadilifu ili kujenga imani kwa wateja, kuboresha huduma wanazotoa na kuinua ustawi wa maisha yao.
Wito huo umetolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, SACP Safia Jongo, wakati akifungua semina maalum iliyoandaliwa na Kampuni ya Magic Builders International ya Dar es Salaam. Semina hiyo ilifanyika jana katika Ukumbi wa Golden Social Hall uliopo Manispaa ya Geita.
Akizungumza katika semina hiyo, SACP Jongo aliwakumbusha mafundi hao umuhimu wa kuzingatia sheria katika utekelezaji wa shughuli zao za kila siku, kuepuka vitendo vya uhalifu na ulaghai dhidi ya wananchi, pamoja na kutoshirikiana na wahalifu katika wizi wa vifaa vya ujenzi.
Alisisitiza kuwa mafundi wanapaswa kutekeleza majukumu yao katika mazingira salama yanayozingatia sheria, huku wakidumisha amani, utulivu na mahusiano mema na jamii ili kuchochea maendeleo ya sekta ya ujenzi na taifa kwa ujumla.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Magic Builders International, David Barongo, aliwahimiza mafundi hao kuendelea kujiendeleza kitaaluma kwa kupata mafunzo kutoka katika vyuo vinavyotambulika na mamlaka husika ili kuongeza maarifa, ujuzi na uzoefu unaowawezesha kutoa huduma bora na zenye ushindani.
Barongo pia alilishukuru Jeshi la Polisi kwa kushiriki semina hiyo na kutoa elimu iliyolenga kuimarisha uzingatiaji wa sheria, maadili ya kazi na usalama katika sekta ya ujenzi.
Alisema ushirikiano kati ya taasisi za umma na sekta binafsi una mchango mkubwa katika kuwajengea mafundi uwezo, kuongeza taaluma na kukuza sekta ya ujenzi nchini.
Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Petro Magoti, amepongeza mchango wa Chuo cha Serikali za Mitaa (LGTI) katika kuandaa wataalamu wenye uwezo wa kusimamia na kuendeleza utawala wa Serikali za Mitaa nchini.
Magoti alitoa pongezi hizo alipotembelea banda la LGTI katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.
Alisema LGTI imeendelea kujijengea sifa kwa kutoa elimu na mafunzo yenye ubora, yaliyowezesha kuzalishwa kwa wataalamu wenye weledi wanaochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya Serikali za Mitaa na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Magoti alisema anajivunia kuwa mmoja wa wahitimu wa chuo hicho, akibainisha kuwa elimu aliyoipata imekuwa msingi muhimu katika safari yake ya utumishi wa umma.
“Elimu niliyopata LGTI imekuwa msingi imara wa utendaji wangu wa kazi na ndiyo imenisaidia kufikia mafanikio haya niliyoyapata katika utumishi wa umma,” alisema Magoti.
Aidha, aliwataka vijana na watumishi wa umma kuendelea kuthamini elimu na mafunzo ya kitaaluma, akisisitiza kuwa taasisi kama LGTI zina nafasi kubwa katika kujenga watumishi wenye ujuzi, maadili na uwezo wa kusimamia maendeleo ya nchi.
Akihitimisha ziara yake katika banda la chuo hicho, Magoti alikabidhiwa zawadi maalum yenye nembo ya LGTI kama kumbukumbu ya kutembelea banda hilo katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam.
Maonesho ya SABASABA yameendelea kuwa jukwaa muhimu kwa taasisi za umma na binafsi kuonesha huduma, bidhaa na mafanikio yao. Kupitia maonesho hayo, LGTI inaendelea kutumia fursa hiyo kutangaza programu zake za mafunzo na kuonesha mchango wake katika kuimarisha utawala wa Serikali za Mitaa nchini.
Mkaguzi wa Polisi Kata ya Nyakafulu, INSP Denis Rwehumbiza, amewataka wanafunzi kutovumilia wala kuficha vitendo vya ukatili wanavyofanyiwa nyumbani au shuleni, badala yake watoe taarifa kwa walimu, wazazi, viongozi wa maeneo yao au Jeshi la Polisi ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi ya wahusika.
Rai hiyo ameitoa leo alipokuwa akitoa elimu kuhusu kinga dhidi ya ukatili kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Ilolangulu, iliyopo Kata ya Ilolangulu, Wilaya ya Mbogwe, mkoani Geita.
INSP Rwehumbiza aliwataka wanafunzi kuwa waangalifu dhidi ya vishawishi kutoka kwa watu wasiowafahamu, ikiwemo kupokea zawadi kama pipi, chipsi, fedha au msaada wa usafiri (lifti), akieleza kuwa mazingira hayo yanaweza kutumika kuwarubuni na hatimaye kuwaingiza katika vitendo vinavyohatarisha maisha na mustakabali wao.
Alisema baadhi ya madhara yanayoweza kujitokeza ni pamoja na kuacha shule, kupata mimba za utotoni na kujiingiza katika mazingira hatarishi yanayoweza kuathiri maendeleo yao.
Kwa upande wake, Mwalimu wa Nidhamu wa Shule ya Sekondari Ilolangulu, Fanuel Wilfred, aliwahimiza wanafunzi kuwa mstari wa mbele kutoa taarifa kuhusu watu wanaowadanganya au kuwarubuni ili hatua za kisheria zichukuliwe mapema.
Alisema ushirikiano kati ya wanafunzi, walimu, wazazi na vyombo vya dola ni muhimu katika kuzuia vitendo vya ukatili na kuhakikisha mazingira salama ya kujifunzia.
Elimu hiyo imelenga kuongeza uelewa wa wanafunzi kuhusu namna ya kujilinda dhidi ya ukatili na unyanyasaji, pamoja na kuwajengea ujasiri wa kutoa taarifa kwa mamlaka husika wanapokumbana na vitendo hivyo.
Akihitimisha, INSP Rwehumbiza aliwahimiza wanafunzi kusoma kwa bidii, kuzingatia nidhamu na kujituma ili kutimiza ndoto zao za kielimu na kujenga maisha yenye mafanikio.
Afisa Tawala wa Wilaya ya Geita, Lucy Beda, kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Geita, Hashimu Komba, amefunga rasmi hafla ya kuwaaga wajumbe 15 wanaotarajia kupanda Mlima Kilimanjaro kupitia programu ya GGML Kili Challenge, inayofadhiliwa na Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML).
Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika jana, Beda aliwataka watumishi wa umma na wananchi wa Mkoa wa Geita kuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya magonjwa kwa kuzingatia afya zao, akisisitiza kuwa afya bora ni msingi muhimu wa maendeleo ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, SACP Safia Jongo, aliwahimiza askari wa Jeshi la Polisi kuendelea kuzingatia sheria, kanuni na taratibu katika utekelezaji wa majukumu yao. Pia aliwasisitiza kuweka afya zao mbele ili kuongeza ufanisi na ubora wa utendaji kazi.
Naye Dkt. Omar Sukari alisema tukio hilo limewanufaisha wananchi wa Mkoa wa Geita kwa kuwapatia huduma za upimaji wa afya bila malipo, zikiwemo kupima makundi ya damu na kupata elimu kuhusu magonjwa ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza na kwamba hatua hiyo inasaidia kugundua na kudhibiti magonjwa mapema.
Shughuli hiyo ilijumuisha matembezi ya kuhamasisha afya kwa jamii, utoaji wa elimu ya afya pamoja na huduma za upimaji wa Virusi vya UKIMWI (VVU), ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za kitaifa za kudhibiti maambukizi ya VVU na UKIMWI kupitia programu ya The Kili Challenge Initiatives.
Akihitimisha hafla hiyo, Kaimu Meneja Mkuu wa GGML, Duan Campbell, alilishukuru Jeshi la Polisi, viongozi wa serikali, watumishi wa taasisi mbalimbali na wananchi kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki Siku ya Afya Geita na hafla ya kuwaaga washiriki wa GGML Kili Challenge.
Alisema ushiriki wao unaonyesha dhamira ya pamoja ya kujenga jamii yenye afya bora na kuimarisha ushirikiano katika kuendeleza ustawi wa wananchi wa Mkoa wa Geita.
Programu ya GGML Kili Challenge inalenga kuhamasisha jamii kuchukua hatua dhidi ya maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (VVU) na kuongeza uelewa kuhusu masuala ya afya kwa ujumla. Hafla hiyo ilifanyika katika viwanja vya GGML vilivyopo Manispaa ya Geita, mkoani Geita.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limemfikisha katika Mahakama ya Wilaya ya Chato, Lufuta Magoma (40), mganga wa kienyeji na mkazi wa Kijiji cha Rutunguru, akikabiliwa na shtaka la kumuua mama yake mzazi, Dotto Magoma Nyara (70).
Mshtakiwa alipandishwa kizimbani jana, Julai 10, 2026, ambapo alisomewa shtaka la mauaji mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Erick Kagimbo.
Akisoma shauri la jinai namba 15471/2026, Wakili wa Serikali, Mashaka Said, alidai kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Juni 4, 2026, katika Kijiji cha Rutunguru, Wilaya ya Chato, Mkoa wa Geita.
Upande wa mashtaka ulidai kuwa Lufuta Magoma alimuua mama yake mzazi, Dotto Magoma Nyara, kinyume na vifungu vya 196 na 197 vya Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16, kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2023.
Hata hivyo, mshtakiwa hakutakiwa kujibu shtaka hilo kwa kuwa Mahakama ya Wilaya haina mamlaka ya kusikiliza kesi za mauaji.
Hakimu Kagimbo alisema kuwa kutokana na aina ya shtaka linalomkabili mshtakiwa, kesi hiyo haina dhamana, hivyo ataendelea kuwa mahabusu hadi upelelezi utakapokamilika na hatua nyingine za kisheria kuchukuliwa.
Kesi hiyo imeahirishwa mpaka Julai 23, 2026, kwa ajili ya kutajwa, huku mshtakiwa akirejeshwa rumande akisubiri maendeleo ya upelelezi.
Mjiolojia kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Njombe, Abbas Mruma, amesema Tanzania inaendelea kujijengea nafasi muhimu duniani kutokana na kuwa na hifadhi kubwa ya madini ya kimkakati, yakiwemo graphite, lithium na rare earth elements, ambayo ni nguzo muhimu katika maendeleo ya teknolojia za kisasa na nishati safi.
Mruma alitoa kauli hiyo wakati akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Stanslaus Muyungi, alipotembelea banda la Tume ya Madini katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).
Alisema mahitaji ya madini ya lithium yanaongezeka kwa kasi duniani kutokana na matumizi yake katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme, simu za mkononi, kompyuta mpakato na vifaa vingine vya kisasa vya kielektroniki.
Kwa mujibu wa Mruma, nchini Tanzania madini ya lithium yanapatikana zaidi katika maeneo ya Dodoma na Ikungi, mkoani Singida, hali inayoiweka nchi katika nafasi nzuri ya kunufaika na ongezeko la mahitaji ya madini hayo katika soko la kimataifa.
Akizungumzia madini ya graphite, alisema Tanzania ndiyo nchi inayoongoza barani Afrika kwa kuwa na hifadhi kubwa ya madini hayo, ambayo ni malighafi muhimu katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme pamoja na matumizi mbalimbali ya viwandani.
Aidha, alisema Tanzania pia ina hifadhi kubwa ya madini ya rare earth elements katika Ukanda wa Afrika Mashariki, yanayopatikana katika eneo la Ngualla mkoani Songwe na Wigu mkoani Morogoro. Madini hayo yanatumika katika utengenezaji wa vifaa vya teknolojia ya juu, ikiwemo vifaa vya mawasiliano, nishati jadidifu na vifaa vya ulinzi.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Stanslaus Muyungi, aliipongeza Tume ya Madini kwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu rasilimali za madini na fursa zinazopatikana katika sekta hiyo.
Alisema elimu hiyo ina mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa rasilimali za madini, kuvutia uwekezaji na kuonesha nafasi ya sekta ya madini katika kukuza uchumi na kufanikisha maendeleo endelevu ya Taifa.
KAIMU Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino, Dkt. Sophia Nchimbi, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, amezindua mradi wa Mama Tembe unaolenga kuhifadhi urithi wa kiutamaduni wa Wagogo, kuwawezesha wanawake na wasichana, pamoja na kukuza uchumi kupitia ubunifu wa asili.
Uzinduzi wa mradi huo umefanyika hivi karibuni wilayani Chamwino, mkoani Dodoma. Mradi unasimamiwa na Shirika la Innovation Development for Future Generation (IDFG) kwa ufadhili wa Serikali za Uswisi na Norway kupitia programu ya Articipate.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt. Nchimbi alisema mradi unawahusisha wanawake wazee 15 wa kabila la Kigogo, mabinti 20 na wanafunzi kutoka shule tatu ambao watarithi mbinu za uchoraji wa jadi kwa kutumia zana na malighafi za asili zilizokuwa zikitumika kupamba nyumba za tembe.
Alisema uchoraji wa nyumba za tembe si mapambo ya kawaida bali ni sehemu muhimu ya historia na utambulisho wa Wagogo, hivyo kurejeshwa kwake kutasaidia kuitangaza Chamwino kama kitovu cha utalii wa utamaduni kupitia kazi za ubunifu zinazofanywa na wananchi.
“Tunafungua ukurasa mpya wa kuhifadhi utamaduni wetu. Kupitia mradi huu, Chamwino itanufaika kwa kuitangaza historia na utamaduni wake,” alisema Dkt. Nchimbi.
Aliongeza kuwa mradi huo pia utawawezesha wananchi kujiongezea kipato kupitia shughuli za sanaa, huku Halmashauri ikiendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha unafanikiwa.
Kwa upande wake, Afisa Utamaduni wa Wilaya ya Chamwino, Jackson Kitija, alisema mradi umefika kwa wakati muafaka kwani baadhi ya maarifa ya jadi yalikuwa yameanza kupotea kutokana na wazee waliokuwa nayo kuzeeka huku vijana wengi wakikosa fursa ya kuyajifunza.
Kitija alisema hatua inayofuata ni kuhakikisha ubunifu wa wanawake hao unalindwa kwa kupata hati miliki, huku michoro hiyo ikitumika kutengeneza bidhaa mbalimbali zenye thamani ya kiuchumi, ikiwemo mavazi yatakayobeba utambulisho wa sanaa ya Wagogo.
Mkurugenzi wa Shirika la Innovation Development for Future Generation (IDFG), Bi. Victoria Mponda, alisema mradi wa Mama Tembe umebuniwa baada ya utafiti kubaini kuwa wanawake wa Kigogo walikuwa na mchango mkubwa katika kuhifadhi utamaduni kupitia michoro ya nyumba za tembe.
Alisema mradi hautaishia kutoa mafunzo pekee, bali utakusanya historia ya michoro hiyo, kueleza maana ya kila mchoro na kuhifadhi taarifa zote kidijitali ili ziwe rejea kwa vizazi vijavyo.
“Tunataka wanawake hawa watambulike kama wabunifu wa sanaa hii. Tutahifadhi kazi zao kidijitali, tutazisajili kwa hati miliki na baadaye kuzigeuza kuwa bidhaa zitakazoweza kuuzwa,” alisema Mponda.
Alieleza kuwa changamoto kubwa mwanzoni mwa utekelezaji wa mradi ilikuwa kuwashawishi wanawake wazee kushiriki, kwa kuwa wengi hawakuamini kuwa uchoraji walioutumia kwa miaka mingi kupamba nyumba ungeweza kuwa chanzo cha kipato.
“Kwa kushirikiana na viongozi wa serikali na wa kimila tuliwafikia na kuwajengea uelewa kuwa sanaa nayo ni uchumi. Leo wamekubali kurithisha maarifa yao kwa mabinti, jambo ambalo tunaamini litakuwa mwanzo wa kufufua sanaa iliyokuwa ikielekea kutoweka,” alisema Mponda.
Miongoni mwa wanufaika wa mradi huo ni Bi. Esteli Chibaya (84), mkazi wa Chamwino, ambaye alisema amefurahishwa na hatua ya kupewa nafasi ya kurithisha ujuzi alioupata tangu akiwa msichana, akiamini kuwa vijana wataendelea kuuenzi utamaduni wa Wagogo badala ya kuuacha upotee.
“Tulikuwa tunachora nyumba kwa ajili ya kuzipamba bila kujua kuwa siku moja ujuzi huu ungekuwa sehemu ya maendeleo yetu. Leo nina furaha kuona watoto na wajukuu wetu wataurithi na kuutumia kujenga maisha yao,” alisema Bi. Chibaya.
Mradi wa Mama Tembe unatarajiwa kukamilika Oktoba 2026. Wadau wanaamini kuwa, mbali na kufufua sanaa ya uchoraji wa nyumba za tembe, utasaidia kuhifadhi urithi wa kabila la Wagogo, kuimarisha utalii wa utamaduni na kuwawezesha wanawake kutumia maarifa ya jadi kama nyenzo ya kujiletea maendeleo.