Askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia kutoka Mkoa wa Pwani, wakiongozwa na Sajini Taji Wandwi Patrick, wametoa msaada kwa watoto wanaolelewa katika Kituo cha kulea wahitaji cha Buloma kilichopo Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani.
Tukio hilo limefanyika leo ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa matendo ya huruma kwa jamii, hususan katika kipindi hiki kinachoelekea kwenye sikukuu za Eid na Pasaka ili kurudisha kwa jamii, kuonesha upendo, na kuleta faraja kwa watoto wahitaji.
Katika zoezi hilo, askari hao walikabidhi bidhaa mbalimbali muhimu za matumizi ya kila siku kwa watoto hao ikijumuisha unga wa sembe, wa ngano, sukari, chumvi, mafuta ya kula na ya kupaka.
Bidhaa nyingine zilizokabidhiwa ni sabuni, taulo za kike, mchele, biskuti, sharubati, maji ya kunywa, nguo na viatu pamoja na na fedha taslimu
Msaada huu unatarajiwa kusaidia kuboresha hali ya maisha ya watoto hao na kukidhi baadhi ya mahitaji yao ya msingi.
Akizungumza wakati wa kupokea msaada huo, mlezi wa kituo hicho, Baraka Kyando, alilishukuru Jeshi la Polisi pamoja na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani kwa kuruhusu askari kushiriki katika tendo hilo la huruma.
Alisema msaada huo ni muhimu sana kwa kituo hicho na kwamba utasaidia kukidhi mahitaji ya watoto wanaolelewa hapo.
“Hili ni jambo jema na la kupongezwa na tunawashukuru sana kwa upendo wao, na tunawaombea baraka zaidi ili waendelee kusaidia wengine”, alisema Kyando.
Tendo hili linaonesha umuhimu wa ushirikiano kati ya vyombo vya usalama na jamii, na nafasi yao katika kusaidia makundi yenye uhitaji maalum na unatajwa kama mfano mzuri wa kuigwa unaohamasisha mshikamano, upendo, na uwajibikaji wa kijamii.
Kadri jamii inavyoelekea kwenye sikukuu, matendo kama haya yanakumbusha umuhimu wa kushirikiana na kuwajali wale wanaohitaji msaada zaidi.
Makundi sogozi ya mitandao ya kijamii kama WhatsApp, Telegramu ni matokeo ya maendeleo ya sayansi, teknolojia ya habari na mawasiliano na yamekuwa ni njia rahisi na yenye nguvu ya kuwasiliana na kushirikiana.
Ikumbukwe kuwa matumizi ya makundi haya huwa na taratibu zinazoongoza uendeshaji wake na wakati mwingine yanapaswa kuwekewa vigezo au masharti lakini muhimu zaidi ni kuzingatia madhumuni ya kimawasiliano bila kuathiri shughuli za msingi za jumuiya ya watu wa kundi husika.
Kwa mfano makundi ya taasisi binafsi kama shule za msingi na sekondari hususani binafsi huwa wanatoa maharti na wakati mwingine kuwa na viongozi wachache (admin) wenye ruhusa ya kushirikisha au kutoa taarifa ya jambo lolote kulingana na taasisi husika ikiwemo matangazo kuhusu shughuli za msingi za taasisi husika.
Kwa mfano wa taasisi za elimu nilizotaja hapo juu ambazo ni shule binafsi zinatumia makundi sogozi ili kutoa taarifa kuhusu mambo kadha wa kadha ikiwemo kuwakumbusha wazazi au walezi masuala ya ulipaji ada, usafiri wa watoto kwa shule zenye mabasi na taarifa nyingine muhimu. Wao wapo kibiashara na wanalinda taswira, hadhi na utambulisho wa taasisi zao.
Kwa kundi au makundi ya mitandao ya kijamii ya taasisi za kidini ikiwemo makanisa au taasisi za elimu za kikanisa mambo hayana tofauti sana.
Kwa aina ya makundi katika muktadha wa dini mambo ya msingi yanayozingatiwa ni masuala ya kidini na taarifa kuhusu taratibu zao kama vile kuimarisha Imani, maadili mema, misaada ya kijamii lakini pia kujenga umoja na mshikamano miongoni mwa waumini.
Katika majukumu ya ujumla makundi sogozi yanakusudiwa kuwa njia kuu ya mawasiliano, husaidia uratibu wa shughuli za kiofisi na utoaji wa taarifa na matukio pamoja na uwasilishaji wa mipango mbalimbali.
Hatahivyo, wahusika wanapaswa kuzingatia maudhui yasiende nje na lengo mama. Sanjali na hilo, jamii ya watu katika makundi haya siyo tu wakristo wanaotegemea neno la Mungu pekee, ni sehemu ya jamii yenye mipango na shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi.
Kwa minajiri hiyo, ni muhimu kuwa tayari na kukubali faida ya uwepo pamoja kuwa ni fursa inayoweza kutumika kwa matokeo chanya kwa wahusika kuweka na kushirikishana fursa walizonazo ili kuapata wateja miongoni mwao au hata nje ya wao lakini kupitia wao.
Sidhani kama ni dhambi mtu kutoa taarifa ya biashara yake, au aina fulani ya shughuli inayoweza kumsaidia kupata kipato.
Vinginevyo hatuwezi kuliishi neno la Mungu ikiwa tutajitenga na shughuli za kimwili ambazo zinasaidia ustawi wa mwanajamii husika katika kundi.
Tukizungumzia dhana ya upatikanaji wa bidhaa au huduma na usambazaji naweza kuwa msharika wa kundi fulani ambalo lina washarika taja idadi yoyote na wanaweza kuwa ni miongoni mwa wahitaji wa huduma au bidhaa za msharika mwenzao lakini anawapaje taarifa kuhusu huduma zake?
Maudhui haya yanarandana na maoni yaliyotolewa na viongozi mbalimbali wa dini waliohojiwa na mwandishi juu ya matumizi ya makundi sogozi katika jamii. Viongozi hao wa dini walikuwa na maoni tofauti kuhusu jambo hili.
Mchungaji Kiongozi wa Kanisa Kuu la Kiinjili Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Dodoma, Daniel Sailowa anasema makundi haya ya WhatsApp ni muhimu kwa kuwa yanawaleta waumini wote na yanasaidia katika upokeaji wa taarifa zinazohitaji utekelezaji wa masuala mbalimbali ndani ya kanisa.
“Siyo ya kutoa na kupokea bali ni ya kupokea na kutekeleza, ndiyo maana yana viongozi wasimamizi (admin) wachache walioruhusiwa kushirikisha taarifa”, alisema Mchungaji Sailowa.
Alisema kutokana na kuwapa fursa wasimamizi wachache kushirikisha taarifa wamejitenga na changamoto ya kila mmoja kutoa taarifa na kuna taarifa zinaleta shida mpaka kutafuta ufumbuzi wake tayari kuna athari hivyo ni muhimu kuwa na vizuizi.
Mchungaji Sailowa anashauri kuwepo na makundi mengine madogomadogo yanaweza kuwa ya vijana, akina mama au akina baba ambayo yanaweza kutumika kwa taarifa nyingine na kuacha kundi kubwa kuhusika na dhima kuu za kikanisa.
Kwa upande wake, Mhadhiri Mwanadamizi wa Masuala ya Mawasiliano, Dr. Francis Ng’atigwa anasema masuala ya matangazo ya biashara katika makundi ya WhatsApp ya watu wa kanisa au jamii yoyote yanapaswa kuwa na makubaliano na uelewa na sheria za mitandao.
Wakati mwingine makubaliano ndiyo yaongoze namna ya kuwasilisha matangazo na labda wakati mwingine wangine wasiwe tu wakali sana, anasema Dr. Ngatigwa.
Mwandishi anaona kuwa kwa hali halisi na namna jamii ya sasa ilivyo na teknolojia ilipofikia hatuwezi kujitenga na masuala ya kijamii au kimwili hata kama waumini tulio kiroho. Kuna namna maisha yetu ya kiroho yanahusiana na ya kimwili.
Makundi ya WhatsApp ya kidini ni njia rahisi ya kuimarisha imani, kujifunza, na kusaidiana kiroho, lakini yanahitaji matumizi ya hekima ili yawe na manufaa kwa kila mtu ndani ya kundi husika. Zaidi yanapaswa kutmika kwa nidhamu na uwajibikaji ili kuepuka usumbufu au taarifa zisizo sahihi.
Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Ilala, Mrakibu Mwandamizi wa Jeshi la Polisi (SSP) Salum Morimori, amewataka wamiliki wa magari ya kusafirisha wanafunzi kuhakikisha wanaajiri madereva wenye sifa stahiki ili kuimarisha usalama wa watoto barabarani.
Akizungumza hivi karibuni katika viwanja vya Shule ya Msingi Olimpio wakati wa zoezi la ukaguzi wa mabasi ya shule, Morimori alisema ni muhimu kwa wamiliki kufuata taratibu za kisheria wanapoajiri madereva.
Ukaguzi huo ulifanywa na Jeshi la Polisi kwa lengo la kuhakikisha magari hayo yanakidhi viwango vinavyotakiwa kwa usafirishaji wa wanafunzi.
“Ni lazima mmiliki ahakikishe dereva anayeajiriwa ana leseni halali, angalau ya daraja C au C1, pamoja na kukidhi vigezo vingine vya kisheria,” alisisitiza Morimori.
Aliongeza kuwa pamoja na sifa za dereva, wamiliki wanapaswa kuhifadhi kumbukumbu muhimu za madereva wao na kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa magari yao ili kuepusha udanganyifu na kuwawajibisha wahusika pale matatizo yanapotokea.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa wa Ilala, SSP Sarah Bundala, aliwataka madereva kuwa makini na maudhui wanayowawekea wanafunzi wanapokuwa safarini na kuwataka kuchagua maudhui yenye maadili mema na kuepuka nyimbo au vipindi vinavyoweza kuathiri tabia za watoto.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Shule ya Upanga, Abel Kasabalala, alilishukuru Jeshi la Polisi kwa kuitikia mwaliko wao na kufanya ukaguzi huo kwa kuwa imewasaidia kubaini hali halisi ya magari yao ili waweze kuchukua hatua stahiki kuboresha huduma ya usafiri kwa wanafunzi.
Ukaguzi huo ni sehemu ya jitihada za kuimarisha usalama wa wanafunzi na kuhakikisha wanapata usafiri salama na wenye kuzingatia sheria za barabarani.
Serikali imezindua mradi maalum wa kuboresha huduma za dharura na usalama barabarani katika jiji la Dar es salaam kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo kutoka nchini Japan wenye lengo la kupunguza madhara kwa wahanga wa ajali za barabarani.
Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa huduma hizo jana jijini Dar es salaam, Mganga Mfawidhi Dkt. Bryceson Kiwelu al;isema Hospital ya Amana ni Iitakuwa ni kitovu cha uboreshaji wa huduma za dharura Katika mradi huo kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2025/2028.
Alisema serikali imeandaa mfumo wa ulinzi na sheria za barabarani kupitia taarifa za jeshi la polisi, wizara ya ujenzi na hospitali ziweze kusomana.
Alisema serikali kwa kushirikiana na wadau wa mfumo wanapaswa kutoa elimu ya matumizi sahihi ya barabara kwa wanafunzi wa shule za msingi ili kujenga uelewa na utamaduni wa usalama barabarani katika jamii.
“Hospitali ya Amana imechaguliwa kuwa kitovu cha mradi huo, ambapo huduma zitatolewa ndani ya kipenyo cha Kilomita tano kuzunguka hospitali hiyo,”alisema Dkt.Kiwelu.
Mratibu wa operesheni kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Dar es salaam, Michael Bachubila, amewataka wananchi kutumia namba ya dharura 114 wakati wowote wanaposhuhudia ajali au tukio la dharura Katika maeneombali mbali ya makazi yao.
Bachubila alisema Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limejiandaa kikamilifu kwa vifaa vya kisasa pamoja na wataalamu waliopata mafunzo maalum ya uokoaji na huduma za awali za dharura.
Aidha serikali imesema mradi huo utaanza kwa majaribio katika jiji la Dar es salaam na ikiwa utafanikiwa unatarajiwa kupanuliwa katika mikoa mingine nchini.
Mahakama ya Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma imemhukumu kijana mmoja mwenye umri wa miaka 20, James Hashimu Chingwaru, kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatikana na hatia ya kujaribu kumbaka bibi mwenye umri wa miaka 75.
Hukumu hiyo ilisomwa tarehe 16 Machi 2026 na Hakimu Mkazi Mfawidhi, F.M. Philip, katika Mahakama ya Wilaya ya Tunduru, baada ya ushahidi uliowasilishwa mahakamani kuthibitisha kosa hilo.
Kwa mujibu wa taarifa za mahakama, tukio hilo lilitokea tarehe 14 Desemba 2025 katika Kitongoji cha Nyerere, Kijiji cha Mtina, wilayani Tunduru. Baada ya tukio hilo, mtuhumiwa alikamatwa na kufikishwa mahakamani Januari 13, 2026 kwa hatua za kisheria.
Mshtakiwa huyo alipatikana na hataia chini ya kifungu cha 132(1) na 132(2)(a) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 (marejeo ya mwaka 2022), kinachohusiana na makosa ya kingono.
Mahakama ilisisitiza kuwa adhabu hiyo inalenga kutoa fundisho kwa jamii na kukomesha vitendo vya ukatili wa kijinsia, hasa dhidi ya watu walio katika mazingira hatarishi kama wazee
Chama Kikuu cha Ushirika RUNALI kinachohusisha wilaya za Nachingwea, Ruangwa na Liwale kimefanya kikao na wadau mbalimbali wa kampuni za usafirishaji ikiwa ni maandalizi ya kuelekea msimu mpya wa mazao wa mwaka 2026/2027.
Kikao hicho kilifanyika hivi karibuni katika ofisi za RUNALI zilizopo wilayani Nachingwea, ambapo viongozi wa chama hicho na wawakilishi wa kampuni za usafirishaji walijadili masuala mbalimbali yanayohusu usafirishaji wa mazao wakati wa msimu wa mavuno.
Akizungumza katika kikao hicho, Meneja wa Chama Kikuu cha Ushirika RUNALI, Jahida Hassan, alisema lengo la kikao hicho ni kufanya mazungumzo na wadau wa sekta ya usafirishaji, ikiwa ni sehemu ya utaratibu ambao chama hicho kimejiwekea kuelekea Mkutano Mkuu wa chama.
Alisema kupitia majadiliano hayo, RUNALI inalenga kusikiliza changamoto na maoni ya wadau ili kuboresha utendaji kazi, hususan katika sekta ya usafirishaji wa mazao wakati wa msimu wa mavuno.
Kwa upande wake, mmoja wa wadau wa kampuni za usafirishaji, Selemani Ramadhani Mukili, alisema wanaendelea kuvutiwa kufanya kazi na RUNALI kutokana na ushirikiano mzuri uliopo kati yao.
Alisema RUNALI imekuwa ikifanya malipo kwa wakati jambo ambalo limechangia kuongeza imani kwa kampuni za usafirishaji kuendelea kushirikiana na chama hicho.
Alisema kampuni zao zimejiandaa kikamilifu kwa msimu wa mazao wa mwaka 2026/2027 na ziko tayari kutoa huduma ya usafirishaji kwa weledi na ufanisi mkubwa ili kuhakikisha mazao yanafika kwa wakati katika maeneo husika.
Kwa mujibu wa uongozi wa RUNALI kikao hicho ni sehemu ya maandalizi ya kuhakikisha msimu wa mazao wa mwaka 2026/2027 unafanikiwa kupitia ushirikiano mzuri kati ya chama hicho na wadau wa sekta ya usafirishaji.
Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea imetoa mikopo ya asilimia 10 kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, sambamba na kukabidhi vifaa mbalimbali ikiwemo matrekta, maguta, magari madogo ya mizigo na pikipiki kwa wanufaika wa mpango huo.
Makabidhiano hayo yaliongozwa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Nachingwea, Ramadhani Maiga jana katika viwanja vya Halmashauri hiyo ambapo jumla ya mikopo hiyo ina thamani ya zaidi ya shilingi milioni 570.
Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Maiga aliipongeza serikali kwa kuendelea kuwezesha upatikanaji wa mikopo hiyo inayolenga kuwainua kiuchumi wananchi na kukuza shughuli za ujasiriamali.
Aidha, aliwataka wanufaika kuvitunza vifaa walivyokabidhiwa pamoja na kuhakikisha wanarejesha mikopo hiyo kwa wakati ili kutoa fursa kwa vikundi vingine kunufaika na mpango huo.
Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Stella Kategile, aliwahimiza wananchi kuchangamkia fursa ya mikopo hiyo.
“Ni muhimu kwa wanufaika kuzingatia maandiko ya miradi mliyoainisha na kwamba muiweze kutimiza malengo na kurejesha kwa wakati”, alisema Bi.Stella.
Baadhi ya wanufaika wa mikopo hiyo waliishukuru serikali kwa kutenga fedha hizo na kwamba vikundi vyao vitaendelea kuzitumia kwa ufanisi ili kujikwamua kiuchumi na kuongeza uzalishaji katika shughuli zao.
Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, watumishi wanawake wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) wametoa msaada wa vitu, mahitaji na vifaa mballimbali kwa watoto wa Kituo cha kulea watoto yatima na waliofanyiwa ukatili cha Shalom kilichopo Kidenge B, Kata ya Msangani, Halmashauri ya Mji wa Kibaha, mkoani Pwani.
Msaada huo unajumuisha mifuko 50 ya saruji, matofali 1,000 pamoja na mahitaji mbalimbali.
Akizungumza hivi karibuni wakati wa kukabidhi msaada huo, Meneja wa Udhibiti na Viwango wa Mamlaka hiyo Bi. Sultana Seiff, alisema wanawake wa e-GA wameamua kusherehekea siku hiyo na watoto wahitaji katika jamii na kukichagua kituo hicho ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii.
Bi. Seiff alisema baada ya kuwasiliana na kituo hicho na kupata changamoto mbalimbali zinazohitaji utatuzi ikiwemo ujenzi wa uzio ili kuhakikisha usalama wa watoto katika kituo hicho waliamua kuchangia vifaa vya ujenzi pamoja na mahitaji mengine muhimu kwa watoto.
“Napenda kuwasilisha salamu kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa e-GA ambaye ametuwezesha wanawake wa mamlaka hii kufika hapa Kibaha”, alisema Bi. Seiff.
Alisema mbali na vifaa vya ujenzi wametoa mahitaji mengine muhimu ikiwemo chupi za kuzuia mkojo kwa watoto yaani pampers, maziwa ya watoto wachanga, sukari na mahitaji mengine ya msingi kwa watoto wa kituo hicho.
Kwa upande wake, mbeba maono wa kituo hicho, Bi. Lilian Mbise, aliwashukuru wanawake wa Serikali Mtandao kwa kujitoa kwao kufika na kuwaona watoto hao pamoja na na msaada huo.
Alisema kwa niaba ya kituo anaishukuru sana Mamlaka ya Serikali Mtandao kupitia wanawake ambao wameacha shughuli zao na familia zao na kwenda kuwaunga mkono.
“Msaada huu wa saruji na tofali utasaidia sana katika ujenzi wa uzio,” alisema Bi. Mbise.
Akielezea historia ya kituo hicho alisema kilianzishwa Mei Mosi mwaka 2016, kikiwa na watoto wawili, lakini sasa kinahudumia watoto 66 wa kike na wa kiume, yatima na waliofanyiwa ukatili wa aina mbalimbali ambao hufikishwa kituoni hapo kupitia taratibu za kiserikali.
Katika kuadhimisha siku ya Wanawake Duniani kwa mwaka 2026 watumishi wanawake wa Bandari ya Tanga waliungana na wafanyakazi wanawake wa kutwa wa bandari hiyo kufanya matendo ya huruma.
Wanawake hao wametoa msaada wa mashine za kusaidia upumuaji aina ya “C- PAP Bubble Neonates, Oxygen Flowmeter” pamoja na vifaa mbalimbali katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga -Bombo vyenye thamani ya Shilingi Milioni 5.
Akizungumza baada ya kukabidhi mashine hizo, Afisa Rasilimali Watu Mkuu wa Bandari hiyo Bi. Sharifa Nuhu alisema wamekuwa na utaratibu wa kila mwaka kutumia siku hiyo kufanya matendo ya huruma kwa jamii na mwaka huu wameona wasaidie Hospital ya Rufaa ya Mkoa – Bombo.
“Mwaka huu tumeona tuunge mkono juhudi za serikali katika kuboresha afya za watoto, hivyo tumetoa msaada wa mashine hizo katika wodi ya watoto wachanga katika Hospitali ya Rufaa ya Bombo”, alisema Bi Sharifa.
Akipokea vifaa hivyo, Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo Dkt. Abdi Msangi aliwashukuru watumishi hao kwa msaada walioutoa kwani umetolewa wakati muafaka kutokana na upungufu wa mashine hizo katika wodi ya watoto wachanga wenye matatizo ya upumuaji.
Daktari Bingwa wa Watoto katika Hospitali hiyo, Dkt. Mohamed Salehe alisema kuwa mashine hizo zitasaidia hospitalini hapo ukizingatia ongezeko kubwa la watoto wanaozaliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya upumuaji na kwamba vifaa hivyo vitasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma kwa watoto.
Awali wanawake hao waliungana na wanawake wa Mkoa wa Tanga katika maandamano ya kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani Kiwilaya yaliyofanyika katika uwanja wa Shule ya Sekondari ya Usagara, ampabo kauli mbiu ya mwaka 2026 inasema “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana, Msingi Jumuishi Kufikia Dira 2050”
Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea, Mohamed Hassan Moyo, ameipongeza Kamati ya Lishe ya Wilaya pamoja na Maafisa Lishe kwa kufanya vizuri katika utekelezaji wa masuala ya lishe wilayani humo.
Moyo alitoa pongezi hizo jana wakati wa kikao cha tathmini ya Mkataba wa Lishe kwa robo ya pili ya mwaka wa fedha 2025/2026.
Aliwataka wataalamu wa lishe pamoja na maafisa watendaji wa Kata kuongeza bidii katika kazi zao ili kudumisha na kuendeleza mafanikio yaliyopatikana katika masuala ya lishe.
Alisisitiza kuwa ajenda ya lishe inapaswa kupewa kipaumbele na kuwa ajenda ya kudumu katika vikao mbalimbali vya maendeleo.
Moyo aliwataka watendaji kuhamasisha wanaume kushiriki katika siku ya maadhimisho ya Lishe ya Kijiji (SALIK), akieleza kuwa suala la lishe linamhusu kila mwananchi na si kundi maalumu pekee katika jamii.
Alisema kuna umuhimu wa kila mwanajamii kushiriki na kupata elimu ya lishe, akibainisha kuwa lishe bora ni jambo la muda mrefu na lenye umuhimu kwa afya ya jamii.
Vilevile, alimuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea kuandaa kikao maalumu kitakachowakutanisha viongozi wa dini na mila ili kuhamasisha wananchi kuondoa imani potofu kuhusu masuala ya lishe.
Kupitia kikao hicho, Moyo aliitaka jamii kuacha imani potofu kuhusu matumizi ya unga uliorutubishwa na badala yake kuutumia kwa manufaa ya afya zao kwa kuzingatia elimu wanayopewa na wataalamu.
Akizungumzia utoaji wa chakula shuleni, alisema bado hauwezi kuitwa lishe bora na kwamba unapaswa kuendelea kutolewa mara kwa mara kwa wananchi katika kuboresha afya zao.