
Na Cosmas Msuha
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), amemuapisha Massana Gibril Mwishawa kuwa Kamishna mpya wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), akisema uteuzi wake unaashiria imani ya Serikali katika uwezo wake wa kuendeleza sekta ya uhifadhi na utalii nchini.

Akizungumza katika hafla ya uapisho iliyofanyika jana katika Makao Makuu ya TANAPA jijini Arusha, Dkt. Kijaji alimtaka Kamishna Mwishawa kuimarisha mapambano dhidi ya ujangili na uhalifu wa wanyamapori kwa kutumia teknolojia za kisasa pamoja na mifumo madhubuti ya kiintelijensia.
Alisema Serikali ina matarajio makubwa kwamba Kamishna huyo atailinda na kuiendesha TANAPA kwa weledi, uadilifu, nidhamu, umoja na maono yatakayoiwezesha taasisi hiyo kuendelea kuwa mfano wa kuigwa katika uhifadhi na utalii ndani na nje ya nchi.
Aidha, Dkt. Kijaji alisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za Serikali, huku akimtaka Kamishna huyo kuboresha maslahi ya watumishi kwa kuongeza nyumba za askari na watumishi, kuboresha vitendea kazi, kuimarisha mafunzo pamoja na huduma za afya.
“Hapa Kamishna wa Uhifadhi, naomba upigie mstari. Ninatarajia kuona TANAPA ikiwa taasisi inayojivunia watumishi wenye maadili, nidhamu, ari ya kazi na uzalendo wa hali ya juu,” alisisitiza Dkt. Kijaji.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya TANAPA, Jenerali Mstaafu George Waitara, alisema bodi itaendelea kutoa ushirikiano na ushauri unaohitajika ili kufanikisha azma ya kuendeleza sekta ya maliasili na utalii nchini.
Naye Kamishna mpya wa Uhifadhi wa TANAPA, Massana Gibril Mwishawa, alisema Hifadhi za Taifa ni hazina muhimu ya ikolojia, uchumi na jamii, yenye mchango mkubwa katika kuongeza pato la Taifa.
Aliahidi kutekeleza majukumu yake kwa weledi, uwazi na uwajibikaji, huku akisisitiza ushirikiano na wadau mbalimbali wa uhifadhi ili kuendelea kulinda rasilimali za taifa na kukuza sekta ya utalii.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na wakuu wa taasisi mbalimbali za uhifadhi, wakiwemo wawakilishi kutoka TAWA, TFS na NCAA, pamoja na viongozi wa Serikali, wadau wa uhifadhi na utafiti, maafisa na askari wa TANAPA.


















