• Na Cosmas Msuha

    WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), amemuapisha Massana Gibril Mwishawa kuwa Kamishna mpya wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), akisema uteuzi wake unaashiria imani ya Serikali katika uwezo wake wa kuendeleza sekta ya uhifadhi na utalii nchini.

    Akizungumza katika hafla ya uapisho iliyofanyika jana katika Makao Makuu ya TANAPA jijini Arusha, Dkt. Kijaji alimtaka Kamishna Mwishawa kuimarisha mapambano dhidi ya ujangili na uhalifu wa wanyamapori kwa kutumia teknolojia za kisasa pamoja na mifumo madhubuti ya kiintelijensia.

    Alisema Serikali ina matarajio makubwa kwamba Kamishna huyo atailinda na kuiendesha TANAPA kwa weledi, uadilifu, nidhamu, umoja na maono yatakayoiwezesha taasisi hiyo kuendelea kuwa mfano wa kuigwa katika uhifadhi na utalii ndani na nje ya nchi.

    Aidha, Dkt. Kijaji alisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za Serikali, huku akimtaka Kamishna huyo kuboresha maslahi ya watumishi kwa kuongeza nyumba za askari na watumishi, kuboresha vitendea kazi, kuimarisha mafunzo pamoja na huduma za afya.

    “Hapa Kamishna wa Uhifadhi, naomba upigie mstari. Ninatarajia kuona TANAPA ikiwa taasisi inayojivunia watumishi wenye maadili, nidhamu, ari ya kazi na uzalendo wa hali ya juu,” alisisitiza Dkt. Kijaji.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya TANAPA, Jenerali Mstaafu George Waitara, alisema bodi itaendelea kutoa ushirikiano na ushauri unaohitajika ili kufanikisha azma ya kuendeleza sekta ya maliasili na utalii nchini.

    Naye Kamishna mpya wa Uhifadhi wa TANAPA, Massana Gibril Mwishawa, alisema Hifadhi za Taifa ni hazina muhimu ya ikolojia, uchumi na jamii, yenye mchango mkubwa katika kuongeza pato la Taifa.

    Aliahidi kutekeleza majukumu yake kwa weledi, uwazi na uwajibikaji, huku akisisitiza ushirikiano na wadau mbalimbali wa uhifadhi ili kuendelea kulinda rasilimali za taifa na kukuza sekta ya utalii.

    Hafla hiyo ilihudhuriwa na wakuu wa taasisi mbalimbali za uhifadhi, wakiwemo wawakilishi kutoka TAWA, TFS na NCAA, pamoja na viongozi wa Serikali, wadau wa uhifadhi na utafiti, maafisa na askari wa TANAPA.

  • Na Cosmas Msuha

    Wakazi wa Jiji la Dodoma wamesema ujenzi wa barabara za mzunguko umeleta manufaa makubwa kwao, ikiwemo kuongeza fursa za biashara, kurahisisha usafiri na kuchochea ukuaji wa uchumi katika maeneo yanayozunguka barabara hizo.

    Mmoja wa wakazi wa eneo la Nala, Bi. Minnael Msanga, alisema uwepo wa barabara hiyo umeongeza idadi ya watu wanaopita katika eneo hilo na hivyo kuwapatia wakazi fursa zaidi za kufanya biashara.

    Kwa upande wake, Mussa Rajab, mkazi wa Nala anayejishughulisha na kazi za ubebaji mizigo, alisema sehemu ya kisasa ya kuegesha magari iliyojengwa kandokando ya barabara imeongeza ajira na kipato kwao.

    “Mwanzoni eneo hili halikuwepo, hivyo kusimama kwa magari hapa kulitegemea udharura wa dereva, nasi tulipata kazi kwa uchache sana. Lakini sasa magari yanasimama, mizigo inashushwa hapa na sisi tunapata ridhiki,” alisema Rajab.

    Naye Simon Ndamanyilu, dereva wa lori la mizigo kutoka Dar es Salaam kwenda Rwanda, alisema barabara hiyo imewaondolea ulazima wa kupita katikati ya Jiji la Dodoma, jambo linalopunguza muda wa safari na matumizi ya mafuta.

    “Imeturahisishia sana. Safari imekuwa fupi kwa sababu njia hii haina foleni hata kidogo,” alisema Ndamanyilu.

    Akizungumzia mradi huo, Mhandisi Morice Mlay kutoka kampuni ya mzawa ya Inter-Consult Ltd, ambayo ni Mhandisi Mshauri wa mradi, alisema barabara za mzunguko zimechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza msongamano wa magari katikati ya Jiji la Dodoma, hasa malori yanayosafirisha mizigo kwenda nchi jirani.

    Alisema sehemu ya kwanza ya mradi imefikia hatua za mwisho za utekelezaji na tayari imeanza kutumika, huku uzinduzi rasmi ukitarajiwa kufanyika Oktoba 2026 baada ya kukamilika kwa kazi zilizobaki.

    “Ujenzi wa sehemu ya kwanza umefikia ukingoni. Kilichobaki ni baadhi ya kazi ndogo, ikiwemo ufungaji wa taa za barabarani na umaliziaji wa njia za watembea kwa miguu,” alisema Mhandisi Mlay.

    Alifafanua kuwa mradi huo wa barabara ya njia nne kwa kiwango cha lami unaunganisha mikoa ya Morogoro, Arusha, Singida na Iringa. Barabara hiyo ina urefu wa kilometa 112.3, ambapo kipande cha kwanza chenye kilometa 52.3 kimekamilika kwa asilimia 93.3.

    Mradi wa kipande cha kwanza unagharimu shilingi bilioni 100.84 na unatarajiwa kuendelea kuwa suluhisho la msongamano wa magari katikati ya Jiji la Dodoma, huku ukichochea ukuaji wa uchumi wa mkoa wa Dodoma, mikoa jirani na Taifa kwa ujumla.

  • Na Cosmas Msuha

    Serikali imesema mageuzi yanayoendelea kutekelezwa katika sekta ya madini yameifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zenye mazingira bora ya uwekezaji barani Afrika, huku yakifungua fursa mbalimbali katika utafiti, uchimbaji, uchenjuaji, uchakataji na uongezaji thamani wa madini.

    Naibu Waziri wa Madini, Dkt. Steven Kiruswa, alitoa kauli hiyo jana alipofungua Kongamano la Madini lililofanyika katika Ukumbi wa Dome, ndani ya Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF), maarufu Sabasaba.

    Alisema maboresho ya sera, sheria na mifumo ya usimamizi wa sekta ya madini yameongeza uwazi, uwajibikaji na ushiriki wa sekta binafsi, hatua zilizochochea ongezeko la uwekezaji, ajira na mchango wa sekta hiyo katika ukuaji wa uchumi wa taifa.

    Dkt. Kiruswa alisema Tanzania imebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi za madini, zikiwemo dhahabu, almasi, tanzanite, nikeli, makaa ya mawe, niobium, madini adimu pamoja na madini ya viwandani na ujenzi.

    “Serikali haiwaaliki wawekezaji kuja kuchimba madini pekee, bali pia kuwekeza katika tafiti za kijiolojia, teknolojia za uchenjuaji, uchakataji, uongezaji thamani wa madini na viwanda vinavyotumia madini kama malighafi,” alisema Dkt. Kiruswa.

    Akizungumzia kongamano hilo, alisema linatarajiwa kufungua fursa mpya za biashara na uwekezaji, huku akiwakaribisha wadau kushiriki Mkutano wa Kimataifa wa Madini utakaofanyika Novemba 19 hadi 21, 2026, katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam. Alisema mkutano huo unalenga kuendelea kuitangaza Tanzania kama kitovu cha uwekezaji katika sekta ya madini barani Afrika.

    Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini wa Tume ya Madini, CPA Venance Kasiki, alisema Tume inaendelea kusimamia utoaji wa leseni za utafutaji, uchimbaji, uongezaji thamani na biashara ya madini kwa kuzingatia Sheria ya Madini ili kuhakikisha rasilimali hizo zinawanufaisha Watanzania na taifa kwa ujumla.

    Alisema serikali pia inaendelea kuimarisha utekelezaji wa Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania, zinazolenga kuwawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika usambazaji wa bidhaa na huduma ndani ya mnyororo wa thamani wa sekta ya madini.

    Aidha, aliwahimiza Watanzania kutumia fursa zilizopo kwa kuwekeza katika viwanda vinavyozalisha bidhaa na vifaa vinavyotumika migodini, pamoja na kutoa huduma mbalimbali zinazohitajika katika shughuli za uchimbaji na uongezaji thamani wa madini.

    Awali, Katibu Tawala wa Mkoa wa Geita, Mohamed Jumanne, alisema sekta ya madini imeendelea kutoa ajira kwa maelfu ya vijana na kuchangia ukuaji wa uchumi katika maeneo yenye shughuli za uchimbaji.

    Alisema serikali itaendelea kuimarisha ushirikiano katika masuala ya ulinzi na usalama ili shughuli za uchimbaji zifanyike kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo, hatua itakayochochea maendeleo endelevu ya sekta hiyo na kuongeza mchango wake katika uchumi wa taifa.

  • Na Cosmas Msuha

    Serikali imewaagiza wazalishaji wote nchini kutumia alama ya ‘Made in Tanzania’ ili kuongeza utambulisho na imani kwa bidhaa zinazozalishwa nchini, pamoja na kuimarisha ushindani wake katika masoko ya kimataifa.

    Agizo hilo limetolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Emmanuel Nchimbi, wakati wa kilele cha maadhimisho ya Usiku wa Jubilei ya Dhahabu (Miaka 50) ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

    Makamu wa Rais alizitaka taasisi zinazosimamia viwango na huduma za kifedha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ili kuhakikisha bidhaa za Tanzania zinakidhi viwango vinavyokubalika katika soko la kimataifa.

    “Matumizi ya alama ya ‘Made in Tanzania’ yataongeza utambulisho wa bidhaa zenye ubora na kuimarisha heshima ya taifa katika biashara za kimataifa,” alisema Mhe. Balozi Nchimbi.

    Aidha, aliwapongeza wadau wa sekta ya fedha kwa kuendelea kutoa mikopo yenye masharti nafuu kwa viwanda vidogo na vya kati, akisema hatua hiyo imechangia kupunguza changamoto ya upatikanaji wa mitaji kwa wajasiriamali na kuchochea ukuaji wa uzalishaji nchini.

    Alisema Serikali itaendelea kuweka sera rafiki kwa uwekezaji, kuboresha miundombinu na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi ili kujenga uchumi wa viwanda wenye ushindani.

    Kwa upande wake, Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mbunge), alisema Tanzania itanufaika zaidi na rasilimali zake endapo itawekeza katika uchakataji na uzalishaji wa bidhaa za mwisho zenye thamani kubwa, badala ya kuendelea kuuza malighafi ghafi nje ya nchi.

    Alibainisha kuwa hatua hiyo itafungua masoko mapya, kuongeza thamani ya mauzo ya bidhaa nje ya nchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa wananchi.

    Mhe. Kapinga alisisitiza kuwa ili kujenga uchumi imara wa viwanda wenye ushindani, ni muhimu kubadili mtazamo wa uzalishaji kwa kuhakikisha mazao ya kilimo, mifugo, uvuvi, misitu na madini yanaongezewa thamani kwa kuchakatwa, kufungashwa vizuri na kuzalishwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.

    Aidha, alisema uwekezaji katika teknolojia za kisasa una mchango mkubwa katika kuongeza uzalishaji, kuboresha ubora wa bidhaa zinazozalishwa nchini, kupunguza gharama za uzalishaji na kuziwezesha bidhaa za Tanzania kushindana katika masoko ya kimataifa.

    Hafla hiyo iliambatana na utoaji wa tuzo kwa washirika muhimu wa TANTRADE pamoja na taasisi zinazochangia maendeleo ya biashara, viwango na huduma za kifedha nchini.

    Kwa mujibu wa Makamu wa Rais, Mhe. Balozi Nchimbi maadhimisho ya Jubilei ya Dhahabu ya TANTRADE ni fursa muhimu ya kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 50, ikiwemo kuongezeka kwa viwanda, uzalishaji, ajira na upanuzi wa masoko ya bidhaa na huduma za Tanzania duniani.

  • Na Cosmas Msuha

    Ofisi ya Waziri Mkuu imewawezesha watu wenye ulemavu kushiriki katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kupitia Shirikisho la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA).

    Ushiriki huo umewawezesha kuonesha bidhaa na huduma mbalimbali wanazozalisha na kuzitoa, pamoja na kufanya biashara katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.

    Akitembelea mabanda ya washiriki hao, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Ummy Nderiananga, alieleza kuridhishwa na kiwango cha ushiriki wa watu wenye ulemavu, akibainisha kuwa ushiriki wao umeongeza fursa za kiuchumi na kuonesha uwezo wao katika uzalishaji na biashara.

    Aidha, Nderiananga aliipongeza Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) pamoja na taasisi nyingine zilizowezesha ushiriki huo na kuzitaka mamlaka za serikali za mitaa kuendelea kutenga na kutoa mikopo ya asilimia mbili kwa watu wenye ulemavu ili kuwawezesha kukuza shughuli zao za kiuchumi.

    “Ni wakati sasa kwa watu wenye ulemavu kuendelea kuonesha uwezo wao katika uzalishaji na biashara. Kupitia maonesho haya tumejionea matokeo chanya ya uwezeshaji wa kiuchumi unaotokana na mikopo na fursa zinazotolewa na Serikali,” alisema Nderiananga.

    Kwa upande wake, mwakilishi wa washiriki hao, Bi. Pili Bilahi, aliishukuru Serikali kwa kuwawezesha kushiriki katika maonesho hayo bila kulipia gharama yoyote.

    Vilevile, Bi. Bilahi aliishukuru serikali kwa kuendelea kuweka mazingira wezeshi yanayowapa watu wenye ulemavu fursa za kiuchumi, ikiwemo kupitia mikopo ya asilimia mbili ya mapato ya ndani inayotolewa na halmashauri.

    Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, “Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania,” yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu nchini. Maonesho hayo yalianza Juni 28 na yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13, 2026.

  • Na George Gabriel, Mtwara

    Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Mtwara imetoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa Hospitali ya Mangaka iliyopo Wilaya ya Nanyumbu, mkoani Mtwara, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa wajibu wake kwa jamii na kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuboresha huduma za afya.

    Akizungumza wakati wa makabidhiano ya vifaa hivyo, Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Mtwara, Mashauli Elisante, alisema msaada huo unaonesha dhamira ya taasisi hiyo ya kushiriki katika maendeleo ya jamii sambamba na kutekeleza jukumu lake la kuzuia na kupambana na rushwa.

    “Tunaamini afya bora ni msingi wa maendeleo ya jamii, na ni wajibu wa kila taasisi kushiriki pale inapowezekana katika kuboresha huduma zinazowagusa wananchi moja kwa moja,” alisema.

    Vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na magauni ya wajawazito na wazazi, viatu, vipima joto, sabuni pamoja na nepi za watoto (pampers), ambavyo vinatarajiwa kusaidia kuboresha huduma kwa akina mama, watoto na wagonjwa wengine wanaopatiwa huduma katika hospitali hiyo.

    Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mangaka, Benedict Mbai, aliishukuru TAKUKURU kwa msaada huo, akisema vifaa hivyo vitasaidia kuboresha utoaji wa huduma na kupunguza changamoto zinazowakabili wahudumu wa afya, hususan katika wodi za akina mama na watoto.

    Kwa upande wake, mmoja wa wazazi wanaopata huduma hospitalini hapo, Faudhia Geugeu, alitoa shukrani kwa TAKUKURU kwa msaada huo, akieleza kuwa umefika wakati muafaka na utanufaisha wananchi wengi wanaotegemea huduma za hospitali hiyo.

    Msaada huo unaakisi umuhimu wa ushirikiano kati ya taasisi za umma na sekta ya afya katika kuboresha ustawi wa wananchi na kuhakikisha huduma bora za afya zinaendelea kuwafikia Watanzania.

  • Na Yusra Temba, Iringa

    Msimu wa tano wa Great Ruaha Marathon umefanyika ndani ya Hifadhi ya Taifa Ruaha ukilenga kuhamasisha uhifadhi wa mazingira na kukuza utalii wa michezo.

    Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Msajili wa Hazina na mlezi wa Great Ruaha Marathon, Nehemiah Mchechu, ambaye alimwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na katika hotuba yake, alisema uhifadhi wa mazingira una mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi.

    Alisema pia, Mto Ruaha Mkuu ni rasilimali muhimu inayochangia shughuli za kilimo, ufugaji na uzalishaji wa umeme, huku akiwahimiza watanzania kutembelea hifadhi za taifa na kushiriki katika juhudi za kuhifadhi maliasili.

    Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Massana Gibril Mwishawa, alisema mbio hizo ni sehemu ya mkakati wa kuendeleza utalii wa michezo na kuitangaza Tanzania kupitia vivutio vyake vya kipekee vya utalii.

    Kwa upande wake, Mratibu wa Great Ruaha Marathon, Hamim Kilahama, alisema marathon hiyo inalenga kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wa mazingira na rasilimali za asili kupitia michezo

    Msimu wa tano wa Great Ruaha Marathon umeandaliwa kwa ushirikiano wa wadau mbalimbali, wakiwemo Airtel Tanzania, Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Maji ya Mkwawa, NMB Bank, Ununio Beach Park na Mkuu Creatives.

  • Na Cosmas Msuha

    Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) imeshiriki Jukwaa la Biashara lililofanyika sambamba na Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), kwa lengo la kutangaza fursa za uwekezaji, biashara na kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali wa sekta ya madini.

    Jukwaa hilo limewakutanisha wafanyabiashara, wawekezaji na wadau kutoka mataifa mbalimbali kujadili mikakati ya kukuza biashara, uwekezaji na masoko ya ndani na kimataifa.

    Akifungua mkutano huo, Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara ya Ndani kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara, Semeo Manongi, alisema Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuwezesha sekta binafsi kufanya shughuli zake kwa ufanisi, usalama na tija, hatua inayochangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

    Alieleza kuwa jukwaa hilo, lililoandaliwa na Benki ya Equity Tanzania katika Viwanja vya Mwalimu Julius K. Nyerere jijini Dar es Salaam, limewakutanisha wajumbe 51 kutoka mataifa mbalimbali na kufanyika sambamba na maonesho ya Sabasaba.

    Manongi alibainisha kuwa maonesho ya Sabasaba yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kutangaza bidhaa, huduma na fursa za uwekezaji, huku yakifungua masoko mapya kwa taasisi, kampuni na wafanyabiashara wa ndani na nje ya nchi.

    Kwa upande wake, Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Benki kwa Wateja Binafsi wa Benki ya Equity Tanzania, Theresia Mayanie, aliwahimiza wawekezaji na wafanyabiashara kutumia huduma za benki hiyo, akieleza kuwa Equity imejipanga kutoa huduma bora na ushirikiano wa karibu kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa.

    Ushiriki wa GST katika jukwaa hilo unaonyesha dhamira ya taasisi hiyo ya kutangaza huduma zake, kuonesha fursa zilizopo katika sekta ya madini na kujenga ushirikiano na wawekezaji pamoja na wadau wengine kwa lengo la kuendeleza sekta hiyo na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Tanzania.

    Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) yalianza rasmi Juni 28, 2026 na yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13, 2026. Maonesho hayo yamewakutanisha zaidi ya kampuni 200 za kimataifa na washiriki kutoka mataifa mbalimbali, yakitoa fursa za biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kiuchumi.