
Na Pilastus Nyaulingo, Tanga
Wito umetolewa kwa madereva wa bodaboda nchini kuongeza tahadhari wanapopokea abiria, hasa wanaowaomba safari za umbali mrefu, kufuatia kifo cha dereva mwenye umri wa miaka 18, Rajab Arufan, aliyefariki baada ya kwenda katika safari ya Lukozi, Wilaya ya Lushoto.
Rajab, aliyekuwa akifanya kazi katika kituo cha bodaboda Mabanda ya Papa jijini Tanga, aliondoka kwa safari hiyo akiamini ni ya kawaida, lakini baadaye mwili wake uligundulika katika eneo la Magamba, Lushoto.
Kwa mujibu wa watu waliokuwa karibu naye, Rajab alikuwa amemfahamu abiria aliyempa safari hiyo kwa takribani wiki mbili na awali alikuwa amewahi kumsafirisha katika maeneo ya Pangani na Horohoro.
Rafiki yake, Hemed Said, alisema Rajab alikuwa kijana mwenye bidii aliyejiajiri kupitia kazi ya bodaboda na siku ya safari alimweleza kuwa alikuwa amepata safari ya kwenda Lushoto.
Said alisema baada ya Rajab kutorejea na simu yake kutopatikana, walitoa taarifa kwa familia yake na baadaye walipata taarifa za kifo chake baada ya mwili kugundulika Magamba.
Dereva mwenzake, Karim Abdallah, alisema abiria huyo hakufahamika katika kituo cha Mabanda ya Papa, huku Rajab akiwa amewaeleza wenzake kuwa alikuwa akimpa safari ndefu na malipo mazuri.
Naye Salum Bakari, aliyewahi kufanya biashara pamoja na Rajab, alisema alimshauri kutosafiri peke yake baada ya kumweleza kuhusu safari hiyo, akisisitiza kuwa si rahisi kumwamini kila mteja.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Madereva Bodaboda Mkoa wa Tanga, Mohamed Chande, alisema madereva wanapaswa kuwa makini zaidi wanapochukua abiria wasiowafahamu, hasa wanaowaomba safari ndefu.
Chande alisema ingawa matukio ya mauaji ya madereva yamepungua ikilinganishwa na kipindi kilichopita, bado kuna haja ya madereva kutoa taarifa mapema wanapokuwa na mashaka kuhusu abiria au safari wanazopewa.
Alisema chama hicho kinaendelea kuhimiza ushirikiano kati ya madereva na vyombo vya usalama ili kuzuia matukio kama hayo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Almachius Mchunguzi, alisema Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi kuhusu tukio hilo na kuwataka wananchi kushirikiana na vyombo vya usalama kuwabaini wahusika wa vitendo vya uhalifu.

Kifo cha Rajab kimeongeza wito wa kuimarishwa kwa usalama wa madereva wa bodaboda, huku wadau wakisisitiza umuhimu wa madereva kuchukua tahadhari kabla ya kukubali safari za umbali mrefu au kwenda maeneo wasiyoyafahamu.
























