• Na Farida Mkumba, Dodoma

    Hospitali ya Afya ya Akili ya Taifa Mirembe imeombwa kuimarisha ushirikiano na taasisi binafsi ili kuwezesha tathmini ya watoto wenye usonji kufanyika kila robo mwaka, hatua itakayosaidia kuboresha huduma za matibabu na ufuatiliaji wa karibu.

    Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Msaidizi wa Magonjwa Yasiyo ya Kuambukiza, Dkt. Omary Ubuguyu, kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Usonji Duniani yaliyofanyika leo katika Hospitali ya Mirembe mkoani Dodoma.

    Dkt. Ubuguyu aliipongeza hospitali hiyo kwa juhudi zake katika kutoa huduma kwa watoto wenye changamoto ya usonji, na kusisitiza umuhimu wa kuendelea kushirikiana na taasisi binafsi ikiwemo shule maalum ili kuboresha zaidi huduma hizo kwa jamii.

    Alieleza kuwa ushirikiano huo utaiwezesha Mirembe kutoa huduma bora zaidi na kuwasaidia watoto wenye usonji kupata matibabu sahihi kwa wakati.

    Kwa upande wake, Afisa Elimu Maalum wa Jiji la Dodoma, Issa Kambi, alisema halmashauri inaendelea kuwabaini watoto wenye usonji ili kuwaingiza katika mfumo wa bima ya afya kwa wote, hatua itakayorahisisha upatikanaji wa huduma za matibabu.

    Aliongeza kuwa lengo ni kuhakikisha watoto hao wanapata huduma bora za afya pamoja na elimu inayokidhi mahitaji yao.

    Naye Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Mirembe, Dkt. Godwin Mwisomba, alisema hospitali hiyo inaendelea kushirikiana kwa karibu na jamii ili kukuza uelewa, kuonesha upendo na kuhakikisha huduma bora za afya ya akili zinawafikia wananchi wengi zaidi.

    Maadhimisho hayo yalifanyika katika Hospitali ya Mirembe, Dodoma, yakiwa na lengo la kuongeza uelewa wa jamii kuhusu usonji na kuhamasisha mazingira jumuishi kwa watu wenye hali hiyo.

    Kauli mbiu ya mwaka huu ni: “Weka Tumaini Usoni Mwao, Furahia Utofauti.”

  • Na Cosmas Msuha

    Katika juhudi za kupunguza ajali za barabarani zinazohusiana na kazi, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) umesaini makubaliano ya ushirikiano na Chuo cha Usafirishaji cha Taifa (NIT) jijini Dar es Salaam.

    Ushirikiano huo unalenga kuimarisha usalama barabarani na kupunguza athari zake kwa wafanyakazi pamoja na uchumi wa taifa.

    Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma, alibainisha kuwa sehemu kubwa ya madai ya fidia yanayotolewa na mfuko huo yanatokana na ajali za barabarani.

    “Sehemu kubwa ya madai ya fidia tunayopokea yanatokana na ajali za barabarani, hususan kwa madereva na wafanyakazi wanaotumia usafiri kwenda na kutoka kazini”, alisema Dkt.Mduma.

    Alisema kupitia makubaliano hayo, taasisi hizo mbili zitashirikiana katika maeneo muhimu ikiwemo utoaji wa mafunzo, elimu ya usalama barabarani, kufanya tafiti, kubadilishana taarifa pamoja na kujengeana uwezo wa kitaalamu.

    “Ushirikiano huu utasaidia kuongeza uelewa na uwezo wa kitaalamu katika kukabiliana na ajali za barabarani nchini”, alisema Dkt.Mduma.

    Kwa upande wake, Mkuu wa NIT, Dkt. Prosper Mgaya, alisema ushirikiano huo unaashiria hatua muhimu katika kupunguza ajali za barabarani ambazo zimeendelea kuwa tatizo kubwa nchini.

    “Hii ni hatua muhimu katika juhudi za pamoja za kukabiliana na changamoto ya ajali za barabarani”, alisema Dkt.Mgaya.

    Alirejea takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinazoonesha kuwa takribani watu milioni 1.19 hupoteza maisha kila mwaka duniani kutokana na ajali za barabarani huku akifafanua zaidi kuwa nchi zinazoendelea kama Tanzania, ajali hizi husababisha hasara ya kati ya asilimia 3 hadi 5 ya Pato la Taifa kutokana na kupotea kwa nguvu kazi na gharama nyingine za kiuchumi.

    Kwa ujumla, ushirikiano huo unatarajiwa kusaidia kupunguza ajali za barabarani, kulinda maisha ya wafanyakazi, kuimarisha nguvu kazi ya taifa na kuboresha ustawi wa jamii kwa ujumla.

  • Na Mwandishi Wetu, Ruvuma

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Ruvuma linamshikilia mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Michael Ngonyani (38), mkazi wa Mtyangimbole, kwa tuhuma za kujihusisha na uhalifu mbalimbali ikiwemo wizi wa magari katika Mkoa wa Mbeya.

    Akizungumza kuhusu tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Marco Chilya, alisema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa Machi 31, 2026 katika kijiji cha Mtyangimbole, Halmashauri ya Madaba.

    Kwa mujibu wa Kamanda Chilya, baada ya kufanyika upekuzi katika makazi ya mtuhumiwa, polisi walifanikiwa kukamata mali mbalimbali zinazodhaniwa kuwa za wizi.

    Miongoni mwa mali hizo ni gari aina ya Toyota IST lenye namba za usajili T 829 DYH, leseni nne za udereva zenye majina tofauti, pamoja na vifaa vya kielektroniki ikiwemo sound bar aina ya Skywood, runinga mbili zenye ukubwa wa inchi 65 na 55, pamoja na pampu ya maji.

    Aidha, katika upekuzi huo, mtuhumiwa alikutwa na sare za vyombo vya ulinzi na usalama, zikiwemo sare za Jeshi la Polisi (kaki) jozi moja, pamoja na sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ambazo ni suruali moja na fulana moja.

    Kamanda Chilya alieleza kuwa inaaminika mtuhumiwa huyo alikuwa akitumia sare hizo kujifanya askari ili kurahisisha kutekeleza vitendo vya uhalifu katika maeneo mbalimbali.

    Aliongeza kuwa uchunguzi bado unaendelea ili kubaini namna mtuhumiwa alivyoweza kupata sare hizo na mtandao wake wa uhalifu, kabla ya kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

  • Na Mwandishi Wetu, Nachingwea – Lindi

    Chama Kikuu cha Ushirika (RUNALI), kinachojumuisha wilaya za Nachingwea, Ruangwa na Liwale, kimetoa mafunzo kwa viongozi wa vyama vya ushirika vya msingi (AMCOS) kutoka katika wilaya hizo, yakilenga kuongeza ufanisi na kuimarisha mipango ya vyama hivyo.

    Akizungumza wakati wa mafunzo hayo jana kwa naiba ya Mkuu wa Mkoa, wilayani Liwale, Mkuu wa Wilaya hiyo, Goodluck Milinga alisema yatachangia kuboresha utendaji na uwajibikaji wa viongozi na wanachama wa vyama vya ushirika.

    DC Milinga aliwamewapongeza wanachama wa ushirika kwa juhudi wanazozifanya katika kuendeleza sekta hiyo, huku akisisitiza umuhimu wa matumizi sahihi ya rasilimali fedha ili kuhakikisha maendeleo endelevu yanapatikana.

    A;isema mipango bora ni msingi muhimu katika kuelekeza mustakabali wa AMCOS, na kuonya dhidi ya kuchukua madeni yasiyo na tija pamoja na kuepuka migogoro isiyo ya lazima ndani ya vyama.

    Kwa upande wake, Mrajisi wa Ushirika Mkoa wa Lindi, Keneth Shemdoe, alisema RUNALI inaendelea kuimarisha sekta ya ushirika kupitia miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa hoteli na ukumbi wa kisasa kwa ajili ya mikutano na mafunzo.

    Alisema mradi wa ujenzi wa hoteli utachochea ukuaji wa uchumi wa eneo hilo kwa kuongeza fursa za huduma kwa jamii na kuzalisha ajira.

    Aidha, alivitaka vyama vya ushirika kuongeza mtaji wa hisa hadi kufikia angalau asilimia 51 ili kuhakikisha wanachama wengi zaidi wanashiriki kikamilifu katika umiliki na uwekezaji.

    Naye Mwenyekiti wa RUNALI, Odas Mpunga, alisema ushirika ni biashara, hivyo vyama vinapaswa kuendeshwa kwa misingi ya kibiashara ili kuongeza tija huku akibainisha kuwa baadhi ya vyama tayari vinamiliki mali kama magari ya mizigo, hatua inayoonesha ukuaji wa sekta hiyo.

    Kwa upande wao, baadhi ya wawakilishi wa AMCOS wameipongeza RUNALI kwa kuandaa mafunzo hayo kwani yatawasaidia kuboresha utendaji wao, usimamizi wa fedha, na mipango ya maendeleo ya vyama vya vyao.

  • Na Yusra Temba

    Wahudumu wa afya 58 wamehitimu mafunzo ya muda mfupi ya kipimo cha moyo kwa kutumia teknolojia ya Echo (Echocardiography), katika mahafali yaliyofanyika Ijumaa, tarehe 27 Machi, jijini Dar es Salaam.

    Mafunzo hayo yameandaliwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili kwa kushirikiana na Hospitali ya Taifa Muhimbili pamoja na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete. Programu hiyo imelenga kuimarisha ujuzi na weledi wa wahudumu wa afya katika uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo.

    Akizungumza katika hafla hiyo, Mgeni rasmi ambaye ni Makamu Mkuu wa Chuo, Profesa Appolinary Kamuhabwa, aliwapongeza wahitimu kwa kujituma kwao na kusisitiza umuhimu wa kutumia maarifa waliopata kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

    Kwa upande wake, Mratibu Mkuu wa mafunzo hayo, Profesa Pilly Chillo, alisema mafunzo hayo yameandaliwa kwa kuzingatia mahitaji halisi ya sekta ya afya.

    Alisema dhamira ya chuo ni kuendelea kutoa mafunzo bora yatakayochangia kuinua viwango vya huduma za afya nchini.

    Mahafali hayo yalifanyika katika viunga vya chuo hicho, yakihitimisha rasmi programu iliyolenga kujenga uwezo wa wataalamu wa afya. Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa chuo, wakufunzi pamoja na wahitimu wenyewe.

    Katika hotuba mbalimbali, umuhimu wa kujifunza na kuzingatia maadili ya taaluma ya afya vilisisitizwa kama nguzo muhimu katika kuboresha huduma kwa jamii.

  • Na Cosmas Msuha

    Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, amewataka wanahabari wanawake nchini kushirikiana kwa karibu na jamii ili kusaidia kuinua sauti ya mwanamke kupitia vyombo vya habari.

    Akizungumza katika Kongamano la “Malkia wa Habari” lililofanyika Machi 28, 2026 katika Ukumbi wa Hoteli ya Rungwe, Sinza jijini Dar es Salaam, Kairuki alisisitiza kuwa mchango wa wanahabari wanawake ni muhimu sana katika kushughulikia changamoto mbalimbali za kijamii, hususan zinazowahusu wanawake.

    Alieleza kuwa kalamu za wanahabari zina nguvu kubwa na zinaweza kuwa daraja la kuunganisha wananchi na serikali katika kutatua matatizo yaliyopo kwenye jamii.

    “Zipo fursa nyingi katika tasnia ya habari na mawasiliano, hivyo wanawake mnapaswa kuzichangamkia. Serikali ipo tayari kutoa ushirikiano,” alisema Kairuki.

    Aidha, aliwahimiza wanahabari wanawake kusimamia kikamilifu vikundi na vyama wanavyoanzisha ili viweze kuleta matokeo chanya, pamoja na kujenga umoja utakaowezesha kutambulika rasmi na serikali.

    Kwa upande wake, Mratibu wa kongamano hilo, Penina Malundo, alisema lengo la mkutano huo ni kujadili changamoto zinazowakabili wanahabari wanawake, kuimarisha ushirikiano wa kijamii, na kuinua sauti ya wanawake kupitia vyombo vya habari.

    Naye Mhariri wa Habari za Siasa wa gazeti la Mwananchi, Lilian Timbuka, aliwataka wanahabari wanawake kuwa na juhudi binafsi katika kutafuta maarifa badala ya kusubiri mafunzo rasmi pekee.

    Kwa upande mwingine, mmoja wa wahariri wa Clouds Media, Joyce Shebe, aliwashauri wanawake kujifunza mbinu mbalimbali za kukabiliana na taarifa hasi zinazosambaa mitandaoni.

    Naye Mhariri wa Habari wa gazeti la Tanzania Leo, Marry Geofrey, alisema kongamano hilo limewapa fursa wanahabari wanawake kujadili na kueleza changamoto zao wazi, pamoja na kubadilishana uzoefu.

    Kwa ujumla, kongamano hilo limeonyesha umuhimu wa mshikamano miongoni mwa wanahabari wanawake katika kuleta mabadiliko chanya ndani ya tasnia ya habari na jamii kwa ujumla.

    Top of Form

  • Na Mwandishi Wetu

    Tanzania inaelekea kufungua ukurasa mpya katika sekta ya madini kufuatia mipango ya kuendeleza uchimbaji wa madini ya niobium katika eneo la Panda Hill, mkoani Mbeya.

    Madini haya adimu yana umuhimu mkubwa duniani kutokana na matumizi yake katika kuimarisha chuma, sekta ya anga, pamoja na teknolojia za kisasa.

    Akizungumzia maendeleo hayo, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema kuwa mradi huo ni hatua muhimu katika kuiweka Tanzania kwenye ramani ya wazalishaji wa madini ya kimkakati duniani.

    Alisema serikali imejipanga kuhakikisha kuwa rasilimali hizo zinaleta manufaa makubwa kwa wananchi kupitia ajira, mapato, na maendeleo ya viwanda.

    Kwa upande wake, Patrick Cook, ambaye ni kiongozi wa kampuni ya Peak Rare Earths inayohusika na mradi huo, amesema kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na wadau wa kimataifa unaimarisha uwezekano wa kufanikisha mradi wa Panda Hill.

    Alisema mradi huo una uwezo wa kuiweka Tanzania katika nafasi ya nne duniani kwa uzalishaji wa niobium.

    Mradi huo unatarajiwa kujumuisha ujenzi wa mgodi, kituo cha uchenjuaji pamoja na kiwanda cha kuzalisha ferroniobium, bidhaa yenye thamani kubwa zaidi sokoni.

    Hatua hii inalenga kuongeza thamani ya madini ndani ya nchi badala ya kuyauza ghafi.

    Aidha, serikali kwa kushirikiana na wawekezaji inaendelea kukamilisha taratibu muhimu ikiwemo upatikanaji wa umeme, miundombinu, na leseni maalum za uchimbaji ili kuhakikisha mradi unaanza kwa wakati na kwa ufanisi.

    Kwa ujumla, mradi wa niobium wa Panda Hill unatarajiwa kuwa chachu ya mageuzi ya kiuchumi nchini, na kuifanya Tanzania kuwa na nafasi ya kipekee katika soko la kimataifa la madini adimu huku ukichochea maendeleo endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

  • Na Cosmas Msuha

    Tanzania imepiga hatua muhimu katika sekta ya madini baada ya kusaini makubaliano ya kimkakati na Marekani kwa ajili ya kuendeleza mradi wa madini ya Niobium wa Panda Hill. Hatua hii inalenga kuifanya Mbeya kuwa kitovu cha uzalishaji na usindikaji wa madini hayo adimu duniani.

    Akizungumza wakati wa hafla ya utiaji saini jijini Mbeya, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, alieleza kuwa mradi huo ni wa kipekee kutokana na umuhimu wa madini ya Niobium, ambayo hayapatikani kwa wingi duniani.

    Alisisitiza kuwa Tanzania inalenga kujipatia nafasi ya kipekee katika soko la kimataifa kwa kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa madini hayo.

    “Tanzania inalenga kuwa mzalishaji wa nne duniani kwa kuchangia takriban asilimia 4 ya mahitaji ya dunia, ikiwa na uzalishaji unaolengwa kufikia tani 100,000 kwa mwaka,” alisema Mavunde.

    Kwa sasa, Brazil inaongoza kwa kuzalisha takriban asilimia 80 ya mahitaji ya dunia, ikifuatiwa na mzalishaji mwingine kutoka Brazil (asilimia 11), huku Canada ikichangia takriban asilimia 6.

    Serikali imeeleza kuwa kupitia dira ya maendeleo ya mwaka 2025–2050, inalenga kuhakikisha madini yanachakatwa na kuongezewa thamani ndani ya nchi badala ya kusafirishwa ghafi ili kukuza ajira, kuongeza mapato ya taifa na kujenga viwanda vyenye ushindani wa kimataifa.

    Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa Panda Hill Tanzania Limited, Dennis Cook, alisema mradi huo umeingia hatua mpya ya utekelezaji baada ya maandalizi ya muda mrefu.

    Alisema hatua zinazofuata ni pamoja na kupata Leseni Maalum ya Uchimbaji Madini, kuunganisha mradi na umeme wa gridi ya taifa na kufanya tathmini ya masoko ya bidhaa ya ferroniobium.

    “Mradi utahusisha  ujenzi wa mgodi wa Niobium, kituo cha uchenjuaji na kiwanda cha kuzalisha ferroniobium”, alisema Cook..

    Kupitia mradi huu, Tanzania itakuwa mshiriki wa moja kwa moja katika minyororo ya ugavi ya viwanda vya kimataifa vinavyotumia teknolojia za hali ya juu—hatua inayoweza kubadilisha mwelekeo wa uchumi wa nchi.

    Katika hafla hiyo, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Samwel Maneno, pamoja na Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, walitia saini mkataba wa wanahisa kwa niaba ya serikali. Hatua hii imekamilisha rasmi muundo wa ushiriki wa serikali na mfumo wa usimamizi wa mradi.

    Mradi wa Niobium wa Panda Hill unaashiria mwanzo wa enzi mpya kwa Tanzania katika sekta ya madini. Ikiwa utatekelezwa kwa ufanisi, unaweza kuiweka nchi katika nafasi ya kipekee duniani na kuifanya kuwa kitovu cha uzalishaji wa madini ya kimkakati yenye thamani kubwa.

    Niobium ni madini ya kimkakati yanayotumika kuongeza uimara wa chuma na kutengeneza aloi maalum zenye utendaji wa juu. Madini haya ni muhimu katika ujenzi wa miundombinu mikubwa, sekta ya anga na usafiri na teknolojia za kisasa na viwanda vya hali ya juu na hii inaifanya Niobium kuwa rasilimali yenye thamani kubwa katika uchumi wa kisasa wa dunia.

  • Na Vincent Mpepo, (Kwa msaada wa mtandao).

    Makundi ya WhatsApp na Telegramu katika taasisi za kidini, kama makanisa na jumuiya za waumini, yamekuwa sehemu muhimu ya maisha ya kiroho na kijamii katika ulimwengu wa leo wa teknolojia.

    Kupitia makundi haya, waumini hupata nafasi ya kuwasiliana kwa haraka, kushirikishana taarifa muhimu na kuimarisha mshikamano wa kiimani na kijamii.

    Kwa asili, makundi haya huanzishwa kwa lengo la kuendeleza shughuli za kidini kama vile kuimarisha imani, kujifunza mafundisho ya dini, kutoa taarifa za ibada na matukio ya kijumuiya, pamoja na kuratibu misaada ya kijamii.

    Aidha, husaidia kujenga umoja na mshikamano miongoni mwa wanachama wa jumuiya husika.

    Ili kuhakikisha ufanisi wake, makundi haya huendeshwa kwa kuzingatia taratibu na kanuni maalum. Mara nyingi, kunakuwa na wasimamizi wachache (admins) wenye jukumu la kusimamia maudhui yanayoshirikishwa kundini.

    Hatua hii hulenga kudhibiti mtiririko wa taarifa na kuepusha mkanganyiko au usumbufu unaoweza kujitokeza pale kila mwanachama anapokuwa na uhuru wa kuchapisha bila mwongozo.

    Hata hivyo, ni muhimu kutambua kuwa wanachama wa makundi haya si watu wa kiroho pekee bali pia ni sehemu ya jamii pana yenye mahitaji ya kijamii na kiuchumi.

    Katika muktadha huu, makundi haya yanaweza pia kuwa jukwaa la kushirikishana fursa mbalimbali za kimaendeleo, ikiwemo biashara na huduma.

    Swali linalojitokeza ni iwapo ni sahihi kutumia makundi ya kidini kwa matangazo ya biashara. Kwa mtazamo wa usawa, si kosa kwa mwanachama kushirikisha taarifa ya huduma au bidhaa anayotoa, mradi tu jambo hilo linafanyika kwa kuzingatia makubaliano ya kundi, halivurugi malengo ya msingi ya kundi, na linafanywa kwa nidhamu.

    Kwa upande mwingine, baadhi ya viongozi wa dini wanasisitiza kuwa makundi makubwa ya taasisi yabaki kwa matumizi rasmi ya mawasiliano ya msingi, huku makundi madogo ya vikundi maalum kama vijana, kina mama au kina baba yakitumika kwa mawasiliano mengine yasiyo rasmi zaidi. Mtazamo huu husaidia kulinda hadhi na mwelekeo wa kundi kuu.

    Wataalamu wa mawasiliano pia wanashauri kuwa uwepo wa mwongozo au sera ya matumizi ya makundi haya ni muhimu, hasa inapohusisha masuala ya matangazo ya biashara, ili kuepusha migongano na kulinda maslahi ya wanachama wote.

    Kwa ujumla, makundi ya WhatsApp ya taasisi za kidini ni nyenzo muhimu inayochangia kuimarisha maisha ya kiroho na kijamii. Hata hivyo, mafanikio yake yanategemea matumizi ya hekima, nidhamu na uwajibikaji wa wanachama wake.

    Makundi haya vizuri, yanaweza kuwa daraja linalounganisha maisha ya kiroho na maendeleo ya kijamii; lakini yasipotumika ipasavyo, yanaweza kuleta changamoto zisizo za lazima.

    Hivyo basi, ni wajibu wa kila mshiriki kuhakikisha anatumia jukwaa hili kwa kuzingatia madhumuni yake ili kuleta manufaa kwa wote ndanI ya jamii husika.