Tanzania imeeleza dhamira yake ya kuimarisha ushirikiano wa kibunge kimataifa kupitia ushiriki wake katika Mkutano wa 5 wa Mabunge ya Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote (NAM-PN).
Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo (MB), akimwakilisha Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azzan Zungu, alitoa msimamo huo wakati wa mkutano huo uliofanyika katika Hoteli ya Hilton Istanbul, nchini Uturuki, Aprili 15, 2026.
Katika mkutano huo, Mhe. Sillo alieleza kuwa Bunge la Tanzania linaunga mkono azimio la kulipa hadhi Bunge la Kiarabu kuwa mwangalizi katika Umoja wa Mabunge ya nchi hizo, hatua inayolenga kupanua wigo wa ushirikiano wa kibunge kimataifa.
Alibainisha kuwa Tanzania inatambua umuhimu wa kuendeleza uhusiano na taasisi za kimataifa kama sehemu ya kuimarisha taasisi za kibunge na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya NAM-PN.
Katika ziara hiyo, Mhe. Sillo aliambatana na Mbunge wa Singida Mashariki, Mhe. Elibariki Kingu, ambapo walishiriki kikamilifu katika majadiliano ya mkutano huo.
Kwa mujibu wa azimio hilo, Bunge la Kiarabu sasa litashiriki vikao na shughuli za NAM-PN kama mwangalizi, baada ya ombi lake rasmi kukubaliwa na nchi wanachama. Hatua hiyo inatarajiwa kuimarisha ushirikiano wa kibunge na kukuza malengo ya pamoja ya nchi wanachama wa Harakati ya Nchi Zisizofungamana na Upande Wowote.
Uamuzi huo unaonesha dhamira ya Tanzania katika kujenga na kuendeleza ushirikiano na nchi za Kiarabu pamoja na jumuiya nyingine za kimataifa kwa maslahi ya maendeleo ya pamoja.
Wanafunzi wa Shule ya Msingi Juhudi iliyopo Kata ya Ruvuma, Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wametakiwa kuzingatia nidhamu na kujituma katika masomo ili waweze kutimiza ndoto zao za kielimu na kuwa raia bora wa baadaye.
Wito huo umetolewa na Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Wilaya ya Songea, Mkaguzi wa Polisi Koladina Mahundi, Aprili 15, 2026, alipofanya ziara shuleni hapo kwa lengo la kutoa elimu ya ushirikishwaji wa jamii katika masuala ya usalama.
Mahundi, ambaye aliambatana na Polisi Kata ya Ruvuma, Mkaguzi wa Polisi Frank Makuwa, alisema nidhamu ni msingi muhimu katika kufanikisha malengo ya wanafunzi, huku akiwahimiza kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuharibu mustakabali wao.
Aliongeza kuwa wanafunzi ni miongoni mwa makundi yaliyo katika hatari ya kufanyiwa vitendo vya ukatili, hivyo wanapaswa kuwa mstari wa mbele kuripoti viashiria vya matukio hayo kwa mamlaka husika ili hatua zichukuliwe dhidi ya wahusika.
Kwa upande wake, Mkaguzi Makuwa aliwataka wanafunzi kuepuka utoro na mahusiano ya kimapenzi wakiwa shuleni, akisisitiza kuwa tabia hizo ni kinyume na maadili na zinaweza kuathiri masomo yao na ndoto zao za baadaye.
Mahakama ya Wilaya ya Tunduru, mkoani Ruvuma, imemhukumu kifungo cha miaka mitatu jela Saidi Saidi Chalamanda (49), mkazi wa Kijiji cha Fundimbaga, baada ya kupatikana na hatia ya kumiliki pombe haramu aina ya gongo.
Hukumu hiyo ilisomwa Aprili 14, 2026 na Hakimu wa Mahakama hiyo, S.J. Mwampashe, kufuatia ushahidi uliowasilishwa mahakamani kuthibitisha kosa hilo pasipo shaka.
Kwa mujibu wa taarifa za mahakama, mtuhumiwa alikamatwa Machi 19, 2026 katika Kijiji cha Fundimbaga, wilayani Tunduru, akiwa na lita 4.5 za pombe haramu ya moshi (gongo). Baadaye alifikishwa mahakamani Aprili 14, 2026 kujibu shtaka hilo.
Mahakama ilimtia hatiani mshtakiwa huyo chini ya Kifungu cha 30 cha Sheria ya Udhibiti wa Vileo, Sura ya 384 (marejeo ya mwaka 2023), kinachokataza umiliki na usambazaji wa pombe haramu.
Katika juhudi za kudumisha amani, mshikamano na maendeleo ya taifa, vijana wametakiwa kuwa wakakamavu, wazalendo na kuichukia rushwa inavyochangia mmomonyoko wa maadili nchini.
Hayo yameelezwa na Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando, wakati akizindua programu ya “Vijana Plattform” iliyoambatana na semina ya makundi mbalimbali ya vijana katika Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salaam kuanzia Aprili 13 hadi 14, 2026.
Akizungumza katika hafla hiyo, Msando alisema serikali kupitia programu ya “Vijana Tuijenge Tanzania Yetu” inalenga kuwaandaa vijana kwa ajira endelevu, pamoja na kuboresha huduma za afya hasa kwa mama na mtoto kwa kuhakikisha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba.
“Hakikisha unalinda usalama wa nchi yako. Uzalendo wa kweli ni kuipenda nchi, kutoa taarifa sahihi na kuwa raia mwema,” alisema Msando.
Alisema kupitia sera ya ajira, serikali imepanua wigo wa upatikanaji wa elimu kwa kujenga shule katika kila kata, pamoja na kutoa ajira na mikopo yenye riba nafuu kwa zaidi ya vijana laki tisa.
Kwa upande wake, Afisa Vijana wa Manispaa ya Ubungo, Allen Mjindo, aliipongeza serikali kwa kuandaa kongamano hilo, akisema litawawezesha vijana kutambua na kutumia fursa zilizopo katika maeneo yao.
“Kongamano hili linawaleta pamoja vijana wa kada mbalimbali kama wanafunzi, bodaboda, wanasiasa na wafanyabiashara ili kushirikiana katika kujenga taifa,” alisema Mjindo.
Diwani wa Kata ya Mbezi, Pius Nyatori, alisema mafunzo hayo yatawasaidia vijana kuelewa vizuri namna ya kunufaika na mikopo ya halmashauri yenye riba nafuu, ambayo ni chachu muhimu ya maendeleo yao kiuchumi.
“Kijana unatakiwa kujifunza kutengeneza vitega uchumi na kutumia fursa ipasavyo; ukifanya hivyo, fedha itakufuata,” alisisitiza Nyatori.
Kwa upande wake, mama mjasiriamali kutoka Kata ya Mbezi, Elizabeth Ngonera, alisema vijana wakijitambua na kutumia vizuri fursa zilizopo, wanaweza kubadilisha maisha yao na kuchangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya taifa.
Ngonera alishauri kuwepo kwa ushirikiano kati ya serikali, wazazi na jamii ili kufanikisha jukumu la kuwawezesha vijana kwa kuwapatia elimu, mafunzo na mazingira rafiki yatakayowawezesha kukuza uchumi wao binafsi, jamii inayowazunguka na taifa kwa ujumla.
A hiker celebrates a breathtaking view over Moraine Lake in Banff National Park.
Na Vincent Mpepo
Makundi sogozi ya mitandao ya kijamii kama WhatsApp, Telegramu na programu tumizi nyingine tunazozifahamu ni matokeo ya maendeleo ya sayansi, teknolojia ya habari na mawasiliano na yamekuwa ni njia yenye nguvu na rahisi katika mawasiliano na kujenga ushirikiano katika jamii.
Ikumbukwe kuwa matumizi ya makundi haya huwa na taratibu zinazoongoza uendeshaji wake na wakati mwingine yanapaswa kuwekewa vigezo au masharti lakini muhimu zaidi ni kuzingatia madhumuni ya kimawasiliano bila kuathiri shughuli za msingi za jumuiya ya watu wa kundi husika.
Kwa mfano makundi ya taasisi binafsi kama shule za msingi na sekondari hususani binafsi huwa wanatoa maharti na wakati mwingine kuwa na viongozi wachache (admin) wenye ruhusa ya kushirikisha au kutoa taarifa ya jambo lolote kulingana na taasisi husika ikiwemo matangazo kuhusu shughuli za msingi za taasisi husika.
Kwa mfano wa taasisi za elimu nilizotaja hapo juu ambazo ni shule binafsi zinatumia makundi sogozi ili kutoa taarifa kuhusu mambo kadha wa kadha ikiwemo kuwakumbusha wazazi au walezi masuala ya ulipaji ada, usafiri wa watoto kwa shule zinazotoa huduma hiyo na taarifa nyingine muhimu za kiuendeshaji katika taasisi zao.
Wapo sawa na sahihi kwa kuwa madhumuni yao ni kulinda taswira, hadhi na utambulisho wa taasisi zao. Na hu oni mlengo wa kibishara.
Kwa kundi au makundi ya mitandao ya kijamii ya taasisi za kidini ikiwemo makanisa au taasisi za elimu za kikanisa mambo hayana tofauti sana.
Kwa aina ya makundi katika muktadha wa dini mambo ya msingi yanayozingatiwa ni masuala ya kidini na taarifa kuhusu taratibu zao kama vile kuimarisha Imani, maadili mema, misaada ya kijamii lakini pia kujenga umoja na mshikamano miongoni mwa waumini.
Katika majukumu ya ujumla makundi sogozi yanakusudiwa kuwa njia kuu ya mawasiliano, husaidia uratibu wa shughuli za kiofisi na utoaji wa taarifa na matukio pamoja na uwasilishaji wa mipango mbalimbali.
Hatahivyo, wahusika wanapaswa kuzingatia maudhui yasiende nje na lengo mama. Sanjali na hilo jamii ya watu katika makundi haya siyo tu wakristo wanaotegemea neno la Mungu pekee, bali ni sehemu ya jamii yenye mipango na shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi zinazofanya maisha yao ya kimwili na kiroho yaende vyema.
Kwa minajiri hiyo, ni muhimu kuwa tayari na kukubali faida ya uwepo pamoja kuwa ni fursa inayoweza kutumika kwa matokeo chanya kwa wahusika kuweka na kushirikishana fursa walizonazo ili kuapata wateja miongoni mwao au hata nje ya wao lakini kupitia wao.
Sidhani kama ni dhambi mtu kutoa taarifa ya biashara yake, au aina fulani ya shughuli inayoweza kumsaidia kupata kipato.
Vinginevyo hatuwezi kuliishi neno la Mungu ikiwa tutajitenga na shughuli za kimwili ambazo zinasaidia ustawi wa mwanajamii husika katika kundi.
Tukizungumzia dhana ya upatikanaji wa bidhaa au huduma na usambazaji naweza kuwa muumini au msharika wa kundi fulani ambalo lina washarika taja idadi yoyote na wanaweza kuwa ni miongoni mwa wahitaji wa huduma au bidhaa za msharika mwenzao lakini anawapaje taarifa kuhusu huduma zake?
Maudhui haya yanarandana na maoni yaliyotolewa na viongozi mbalimbali wa dini waliohojiwa na mwandishi juu ya matumizi ya makundi sogozi katika jamii. Viongozi hao wa dini walikuwa na maoni tofauti kuhusu jambo hili.
Mchungaji Kiongozi wa Kanisa Kuu la Kiinjili Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Dodoma, Daniel Sailowa anasema makundi haya ya WhatsApp ni muhimu kwa kuwa yanawaleta waumini wote na yanasaidia katika upokeaji wa taarifa zinazohitaji utekelezaji wa masuala mbalimbali ndani ya kanisa.
“Siyo ya kutoa na kupokea bali ni ya kupokea na kutekeleza, ndiyo maana yana viongozi wasimamizi (admin) wachache walioruhusiwa kushirikisha taarifa”, alisema Mchungaji Sailowa.
Alisema kutokana na kuwapa fursa wasimamizi wachache kushirikisha taarifa wamejitenga na changamoto ya kila mmoja kutoa taarifa na kuna taarifa zinaleta shida mpaka kutafuta ufumbuzi wake tayari kuna athari hivyo ni muhimu kuwa na vizuizi.
Mchungaji Sailowa anashauri kuwepo na makundi mengine madogomadogo yanaweza kuwa ya vijana, akina mama au akina baba ambayo yanaweza kutumika kwa taarifa nyingine na kuacha kundi kubwa kuhusika na dhima kuu za kikanisa.
Kwa upande wake, Mhadhiri Mwanadamizi wa Masuala ya Mawasiliano, Dr. Francis Ng’atigwa anasema masuala ya matangazo ya biashara katika makundi ya WhatsApp ya watu wa kanisa au jamii yoyote yanapaswa kuongozwa na vitu vikuu viwili ambavyo ni uelewa wa sheria za mawasiliano na makubaliano.
“Wakati mwingine makubaliano ndiyo yaongoze namna ya kuwasilisha matangazo na labda wakati mwingine wengine wasiwe tu wakali sana”, alisema Dr. Ng’atigwa.
Mwandishi anaona kuwa kwa hali halisi na namna jamii ya sasa ilivyo na teknolojia ilipofikia hatuwezi kujitenga na masuala ya kijamii au kimwili hata kama waumini tulio kiroho.
Na ukweli ni kuwa kuna namna maisha ya kila siku na jamii zetu zinahusiana kiroho na kimwili.
Makundi sogozi ya WhatsApp ya kidini ni njia rahisi ya kuimarisha imani, kujifunza, na kusaidiana kiroho, lakini yanahitaji matumizi ya kiwango cha juu cha hekima ili yawe na manufaa kwa kila mtu ndani ya kundi husika.
Zaidi yanapaswa kutmika kwa nidhamu na uwajibikaji ili kuepuka usumbufu au taarifa zisizo sahihi. Na huenda kupanga ni kuchagua, wahusika wanaweza kuona njia ipi itawafaa kuenenda katika namna bora kimawasiliano ili kutoharibu madhumuni ya uwepo wao pamoja.
Hospitali ya Afya ya Akili ya Taifa Mirembe imeombwa kuimarisha ushirikiano na taasisi binafsi ili kuwezesha tathmini ya watoto wenye usonji kufanyika kila robo mwaka, hatua itakayosaidia kuboresha huduma za matibabu na ufuatiliaji wa karibu.
Wito huo umetolewa na Mkurugenzi Msaidizi wa Magonjwa Yasiyo ya Kuambukiza, Dkt. Omary Ubuguyu, kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Usonji Duniani yaliyofanyika leo katika Hospitali ya Mirembe mkoani Dodoma.
Dkt. Ubuguyu aliipongeza hospitali hiyo kwa juhudi zake katika kutoa huduma kwa watoto wenye changamoto ya usonji, na kusisitiza umuhimu wa kuendelea kushirikiana na taasisi binafsi ikiwemo shule maalum ili kuboresha zaidi huduma hizo kwa jamii.
Alieleza kuwa ushirikiano huo utaiwezesha Mirembe kutoa huduma bora zaidi na kuwasaidia watoto wenye usonji kupata matibabu sahihi kwa wakati.
Kwa upande wake, Afisa Elimu Maalum wa Jiji la Dodoma, Issa Kambi, alisema halmashauri inaendelea kuwabaini watoto wenye usonji ili kuwaingiza katika mfumo wa bima ya afya kwa wote, hatua itakayorahisisha upatikanaji wa huduma za matibabu.
Aliongeza kuwa lengo ni kuhakikisha watoto hao wanapata huduma bora za afya pamoja na elimu inayokidhi mahitaji yao.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Mirembe, Dkt. Godwin Mwisomba, alisema hospitali hiyo inaendelea kushirikiana kwa karibu na jamii ili kukuza uelewa, kuonesha upendo na kuhakikisha huduma bora za afya ya akili zinawafikia wananchi wengi zaidi.
Maadhimisho hayo yalifanyika katika Hospitali ya Mirembe, Dodoma, yakiwa na lengo la kuongeza uelewa wa jamii kuhusu usonji na kuhamasisha mazingira jumuishi kwa watu wenye hali hiyo.
Kauli mbiu ya mwaka huu ni: “Weka Tumaini Usoni Mwao, Furahia Utofauti.”
Katika juhudi za kupunguza ajali za barabarani zinazohusiana na kazi, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) umesaini makubaliano ya ushirikiano na Chuo cha Usafirishaji cha Taifa (NIT) jijini Dar es Salaam.
Ushirikiano huo unalenga kuimarisha usalama barabarani na kupunguza athari zake kwa wafanyakazi pamoja na uchumi wa taifa.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dkt. John Mduma, alibainisha kuwa sehemu kubwa ya madai ya fidia yanayotolewa na mfuko huo yanatokana na ajali za barabarani.
“Sehemu kubwa ya madai ya fidia tunayopokea yanatokana na ajali za barabarani, hususan kwa madereva na wafanyakazi wanaotumia usafiri kwenda na kutoka kazini”, alisema Dkt.Mduma.
Alisema kupitia makubaliano hayo, taasisi hizo mbili zitashirikiana katika maeneo muhimu ikiwemo utoaji wa mafunzo, elimu ya usalama barabarani, kufanya tafiti, kubadilishana taarifa pamoja na kujengeana uwezo wa kitaalamu.
“Ushirikiano huu utasaidia kuongeza uelewa na uwezo wa kitaalamu katika kukabiliana na ajali za barabarani nchini”, alisema Dkt.Mduma.
Kwa upande wake, Mkuu wa NIT, Dkt. Prosper Mgaya, alisema ushirikiano huo unaashiria hatua muhimu katika kupunguza ajali za barabarani ambazo zimeendelea kuwa tatizo kubwa nchini.
“Hii ni hatua muhimu katika juhudi za pamoja za kukabiliana na changamoto ya ajali za barabarani”, alisema Dkt.Mgaya.
Alirejea takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinazoonesha kuwa takribani watu milioni 1.19 hupoteza maisha kila mwaka duniani kutokana na ajali za barabarani huku akifafanua zaidi kuwa nchi zinazoendelea kama Tanzania, ajali hizi husababisha hasara ya kati ya asilimia 3 hadi 5 ya Pato la Taifa kutokana na kupotea kwa nguvu kazi na gharama nyingine za kiuchumi.
Kwa ujumla, ushirikiano huo unatarajiwa kusaidia kupunguza ajali za barabarani, kulinda maisha ya wafanyakazi, kuimarisha nguvu kazi ya taifa na kuboresha ustawi wa jamii kwa ujumla.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Ruvuma linamshikilia mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Michael Ngonyani (38), mkazi wa Mtyangimbole, kwa tuhuma za kujihusisha na uhalifu mbalimbali ikiwemo wizi wa magari katika Mkoa wa Mbeya.
Akizungumza kuhusu tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Marco Chilya, alisema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa Machi 31, 2026 katika kijiji cha Mtyangimbole, Halmashauri ya Madaba.
Kwa mujibu wa Kamanda Chilya, baada ya kufanyika upekuzi katika makazi ya mtuhumiwa, polisi walifanikiwa kukamata mali mbalimbali zinazodhaniwa kuwa za wizi.
Miongoni mwa mali hizo ni gari aina ya Toyota IST lenye namba za usajili T 829 DYH, leseni nne za udereva zenye majina tofauti, pamoja na vifaa vya kielektroniki ikiwemo sound bar aina ya Skywood, runinga mbili zenye ukubwa wa inchi 65 na 55, pamoja na pampu ya maji.
Aidha, katika upekuzi huo, mtuhumiwa alikutwa na sare za vyombo vya ulinzi na usalama, zikiwemo sare za Jeshi la Polisi (kaki) jozi moja, pamoja na sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ambazo ni suruali moja na fulana moja.
Kamanda Chilya alieleza kuwa inaaminika mtuhumiwa huyo alikuwa akitumia sare hizo kujifanya askari ili kurahisisha kutekeleza vitendo vya uhalifu katika maeneo mbalimbali.
Aliongeza kuwa uchunguzi bado unaendelea ili kubaini namna mtuhumiwa alivyoweza kupata sare hizo na mtandao wake wa uhalifu, kabla ya kuchukuliwa hatua kali za kisheria.
Chama Kikuu cha Ushirika (RUNALI), kinachojumuisha wilaya za Nachingwea, Ruangwa na Liwale, kimetoa mafunzo kwa viongozi wa vyama vya ushirika vya msingi (AMCOS) kutoka katika wilaya hizo, yakilenga kuongeza ufanisi na kuimarisha mipango ya vyama hivyo.
Akizungumza wakati wa mafunzo hayo jana kwa naiba ya Mkuu wa Mkoa, wilayani Liwale, Mkuu wa Wilaya hiyo, Goodluck Milinga alisema yatachangia kuboresha utendaji na uwajibikaji wa viongozi na wanachama wa vyama vya ushirika.
DC Milinga aliwamewapongeza wanachama wa ushirika kwa juhudi wanazozifanya katika kuendeleza sekta hiyo, huku akisisitiza umuhimu wa matumizi sahihi ya rasilimali fedha ili kuhakikisha maendeleo endelevu yanapatikana.
A;isema mipango bora ni msingi muhimu katika kuelekeza mustakabali wa AMCOS, na kuonya dhidi ya kuchukua madeni yasiyo na tija pamoja na kuepuka migogoro isiyo ya lazima ndani ya vyama.
Kwa upande wake, Mrajisi wa Ushirika Mkoa wa Lindi, Keneth Shemdoe, alisema RUNALI inaendelea kuimarisha sekta ya ushirika kupitia miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa hoteli na ukumbi wa kisasa kwa ajili ya mikutano na mafunzo.
Alisema mradi wa ujenzi wa hoteli utachochea ukuaji wa uchumi wa eneo hilo kwa kuongeza fursa za huduma kwa jamii na kuzalisha ajira.
Aidha, alivitaka vyama vya ushirika kuongeza mtaji wa hisa hadi kufikia angalau asilimia 51 ili kuhakikisha wanachama wengi zaidi wanashiriki kikamilifu katika umiliki na uwekezaji.
Naye Mwenyekiti wa RUNALI, Odas Mpunga, alisema ushirika ni biashara, hivyo vyama vinapaswa kuendeshwa kwa misingi ya kibiashara ili kuongeza tija huku akibainisha kuwa baadhi ya vyama tayari vinamiliki mali kama magari ya mizigo, hatua inayoonesha ukuaji wa sekta hiyo.
Kwa upande wao, baadhi ya wawakilishi wa AMCOS wameipongeza RUNALI kwa kuandaa mafunzo hayo kwani yatawasaidia kuboresha utendaji wao, usimamizi wa fedha, na mipango ya maendeleo ya vyama vya vyao.