
Na Yusra Temba
Imeelezwa kuwa matumizi ya teknolojia ya kidijitali katika ununuzi wa umma yanaendelea kupewa kipaumbele nchini kufuatia hitimisho la Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma lililofanyika jijini Arusha mwishoni mwa mweziu Julai. Kongamano hilo liliwakutanisha wadau kutoka sekta za umma na binafsi kujadili namna ya kuimarisha ufanisi, uwazi na ushindani katika michakato ya ununuzi wa umma kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Alnason Nguvila, alisema matumizi ya teknolojia ni muhimu katika kuimarisha mfumo wa ununuzi wa umma, akieleza kuwa mifumo ya kidijitali inaweza kuongeza uwazi, ushindani na ufanisi katika utekelezaji wa miradi na utoaji wa huduma za umma.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Denis Simba, alisema dhima kuu ya kongamano hilo ilikuwa kutumia fursa zinazotokana na ununuzi wa umma kidijitali ili kufikia uchumi endelevu, shirikishi, jumuishi na wenye ushindani kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Alisema matumizi ya mifumo ya kidijitali yanaendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuongeza uwazi, kuimarisha ushindani wa haki na kuhakikisha thamani ya fedha katika utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma.
Naye Afisa Masoko wa Kampuni ya Blueberry Travel, Laylati Twaha, ambaye alipokea tuzo ya Mdhamini Bora katika kongamano hilo, alisema tukio hilo limewasaidia kujifunza zaidi kuhusu mfumo wa ununuzi wa umma na kuwapatia fursa za kupanua biashara zao kwa kushirikiana na serikali.
Kongamano hilo liliwakutanisha maafisa manunuzi, maafisa sheria, wafanya maamuzi kutoka idara mbalimbali, wazabuni, wakandarasi pamoja na wataalamu wa sekta ya ununuzi wa umma, ambapo walijadili kwa kina matumizi ya teknolojia na uzingatiaji wa sheria katika hatua mbalimbali za ununuzi wa umma.
Aidha, PPRA ilitambua mchango wa wadau mbalimbali kwa kutoa tuzo kwa taasisi na washiriki waliofanya vizuri katika nyanja tofauti za ununuzi wa umma. Hatua hiyo imelenga kuhamasisha ubora, uwajibikaji na uzingatiaji wa sheria ili kuongeza ufanisi katika sekta hiyo.





















