
Na Yusra Temba
Mlimbwende Jihan Dimack ameibuka mshindi wa taji la Miss Grand Tanzania 2026, baada ya kuwashinda washiriki wengine kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania katika shindano lililojumuisha vipengele vya mahojiano, mawasilisho, matembezi ya jukwaani na uwezo wa kujieleza mbele ya majaji na hadhira.
Ushindi huo ulishuhudiwa na wadau mbalimbali wa tasnia ya burudani, urembo na ulimwengu wa mitindo katika fainali zilizofanyika usiku wa Jumamosi katika Ukumbi wa The Super Dome, Masaki, Dar es Salaam.
Ushindi wa Jihan Dimack unaendelea kuimarisha safari ya Tanzania katika mashindano ya Miss Grand International, baada ya mwakilishi wa mwaka 2025, Beatrice Alex, kuweka rekodi ya kuwa Mtanzania aliyefika mbali zaidi katika historia ya mashindano hayo.
Matokeo hayo yameongeza matarajio makubwa kwa mwakilishi wa mwaka 2026, ambaye anatarajiwa kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania katika jukwaa la kimataifa.
Jihan Dimack sasa ataiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Miss Grand International 2026, yanayotarajiwa kufanyika nchini India.
Kwa mwaka huu, mashindano hayo yametoa jumla ya warembo tisa watakaoiwakilisha Tanzania katika majukwaa mbalimbali ya kimataifa ya urembo. Warembo hao ni Jihan Dimack – Miss Grand International, Sharon Julius – Miss Elite, Celine Edson – Miss Earth, Rose Uisso – Miss Global, Eve Godwin – Miss Africa International, Namala Patrick – Miss Tourism Africa, Prisca Lyimo – Miss Cosmo, Zulfa Yazid – Miss Africa Golden, na Janeth Anselme – Miss Intercontinental.

Kwa upande wake, Janeth Anselme, mshindi wa taji la Miss Intercontinental Tanzania 2026, alisema anamshukuru Mungu kwa hatua aliyofikia na kwamba ushindi huo ni mwanzo wa safari mpya ya kutimiza ndoto zake.
Janeth alisema anafurahia ushindi huo na anatamani kutumia taji hilo kuleta mchango chanya katika jamii.
Miongoni mwa wadau waliohudhuria fainali hizo alikuwa muigizaji Angel Mazanda, maarufu kwa jina la Chioma, ambaye alisema amefurahishwa na ushindi wa Prisca Lyimo, aliyetwaa taji la Miss Cosmo Tanzania 2026.
Angel alisema anaamini Prisca ana uwezo mkubwa wa kufanya vizuri katika majukwaa ya kimataifa.
Kwa upande wake, mama wa mrembo aliyeshinda taji la Miss Africa International Tanzania 2026, Rose Shayo, alitoa shukrani kwa uongozi wa Miss Grand Tanzania kwa kuandaa mashindano hayo na kutoa fursa kwa mabinti wa Kitanzania kuonesha vipaji na uwezo wao.
Pia aliwashauri wazazi, hususan akina mama, kuwapa ushirikiano mabinti zao wanaotamani kuingia katika tasnia ya urembo ili waweze kutimiza ndoto zao.
Mashindano ya Miss Grand Tanzania ni jukwaa la kitaifa linalolenga kumpata mrembo atakayeiwakilisha Tanzania katika mashindano ya kimataifa ya Miss Grand International.
Mbali na kuangazia uzuri wa washiriki, mashindano hayo yanasisitiza pia uongozi, mawasiliano, kujiamini na ushiriki wa wanawake vijana katika masuala ya kijamii.


























