
Na Vincent Mpepo
Waumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Mtaa wa Kwembe, wameungana na watu wengine duniani kuadhimisha Siku ya Wapendanao kwa namna ya kipekee, ambapo wanandoa walipatiwa mafunzo na uzoefu mbalimbali kama njia ya kukumbushana wajibu na haki zao katika ndoa taasisi inayotajwa kuwa msingi wa familia, jamii na taifa kwa ujumla.
Hafla hiyo iliyofanyika jana katika ukumbi wa kanisa hilo, iliongozwa na viongozi wa mtaa wa kanisa pamoja na wawezeshaji kutoka ndani na nje ya kanisa.
Katika mafundisho yaliyotolewa, ilibainika kuwa ukosefu wa elimu ya ndoa katika jamii ni moja ya vikwazo vikubwa vinavyosababisha ndoa kushindwa kukua, kutoeleweka na kuyumba.
Akitoa mada katika maadhimisho hayo, Mwalimu na Mwanasaikolojia, Bupe Mwabenga, alisema jamii imekuwa haijali uwekezaji wa kutosha katika elimu ya ndoa, hali inayosababisha baadhi ya wanandoa kutoitambua ndoa kwa uzito unaostahili na kuichukulia kama jambo la kawaida.

“Kumekuwa na mtazamo kuwa elimu ya ndoa ni jambo la kawaida na hivyo kutopewa kipaumbele, jambo ambalo si sahihi,” alisema Mwanasaikolojia Bupe.
Alisema athari za ukosefu wa elimu ya ndoa ni pamoja na migogoro ya kifamilia, kuvunjika kwa ndoa na kuathirika kwa afya ya akili miongoni mwa wanandoa, hali inayowaacha watoto wakikua katika mazingira yasiyo salama kihisia na kimaadili.
“Ifike wakati kila mwanandoa aache kumchukulia poa mwenza wake,” alisisitiza.
Aidha, alitaja sababu nyingine zinazosababisha changamoto katika ndoa kuwa ni pamoja na athari za utandawazi, baadhi ya wanandoa kutojua kusudi la kuingia katika ndoa, pamoja na kutoelewa haki na wajibu wao ndani ya ndoa.
Akizungumzia tabia ya wanandoa kujikita zaidi katika udhaifu wa wenza wao, Bupe alisema hali hiyo huchangia migogoro isiyo ya lazima, huku akisisitiza kuwa hakuna mwanadamu mkamilifu.
“Mbinu mojawapo ya kuishi vyema katika ndoa ni kuyatambua madhaifu na mazuri ya mwenza wako, na zaidi kujikita katika kuyakuza mazuri yake badala ya kuganda na madhaifu,” alisema.
Kuhusu changamoto za utandawazi, Bupe alisema jamii imejikita mno katika utafutaji wa mali na vyeo kana kwamba pesa ndiyo suluhisho la kila changamoto, hali inayochochea kiburi na kuathiri mahusiano ya ndoa.
“Baadhi ya athari za pesa au cheo, hususan kwa wanawake, zimesababisha wanaume kujenga ukuta wa kujihami, jambo linalodhoofisha ustawi wa ndoa,” alifafanua.
Kwa upande wake, mwezeshaji mwingine wa mada, James Betram, alisisitiza umuhimu wa kila mwanandoa kujijengea sababu ya kupendwa na mwenza wake, licha ya mafundisho ya kibiblia yanayoeleza kuwa upendo haujivuni wala haufanyi ubaguzi.

Aliongeza kuwa baadhi ya mabadiliko ya kisasa yamesababisha wanandoa kutochukulia ndoa kwa uzito unaostahili, hali inayofanya ndoa kuonekana kama jambo la mazoea.
“Ni muhimu kwa wanandoa kudumisha mawasiliano, kujali hisia za wenza wao na kuwa na moyo wa kusameheana ili kujenga mahusiano yenye afya na ustawi wa familia,” alisema Betram.
Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Malezi na Uinjilisti ya kanisa hilo, Mratibu wa shughuli hiyo, Michael Mwambage, alisema ni wajibu wa kanisa kuendelea kuimarisha taasisi ya ndoa kwa kutoa elimu na jukwaa la kubadilishana uzoefu.
“Ni vyema wanandoa kukutana kanisani, kujifunza na kubadilishana uzoefu badala ya kusherehekea Siku ya Wapendanao kwa namna nyingine zisizo na tija ya kudumu,” alisema Mwambage.























