• Na George Gabriel

    Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, amekipongeza Kikundi cha Vijana Kazi Imara cha Kata ya Nanyumbu, Wilaya ya Nanyumbu, kwa uaminifu katika marejesho ya mikopo, ubunifu na ubora wa bidhaa wanazozalisha.

    Kapinga alitoa pongezi hizo jana wakati wa ziara yake wilayani Nanyumbu, ambapo alikagua shughuli mbalimbali zinazofanywa na vijana hao, ikiwemo useremala, ushonaji wa nguo kwa kutumia cherehani pamoja na biashara ya mama ntilie.

    Katika ukaguzi huo, Kapinga alivutiwa na ubunifu wa kikundi hicho katika utengenezaji wa vitanda, akieleza kuwa hatua hiyo ni mfano mzuri wa namna vijana wanavyoweza kutumia fursa zinazotolewa na Serikali kuongeza kipato na kujiajiri.

    Aidha, alipongeza uaminifu wa kikundi hicho katika kurejesha mkopo wa Shilingi milioni 14.5, ambapo hadi sasa kimefanikiwa kurejesha Shilingi milioni 2.112, hatua aliyosema inaonesha uwajibikaji wa wanakikundi.

    Katika kuwatia moyo vijana hao, Kapinga alikabidhi Shilingi milioni moja (TSh 1,000,000), huku akiwataka kuendelea kudumisha uaminifu, kuimarisha ubunifu na kuongeza ubora wa bidhaa zao ili ziweze kushindana katika soko.

    Aidha, katika ziara hiyo, Kapinga alitoa mitungi ya gesi kwa wajasiriamali, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuhamasisha matumizi ya nishati safi na salama katika shughuli za uzalishaji na matumizi ya kila siku.

    Akizungumza na mwandishi baada ya kupokea mtungi wa gesi, Mwajuma Mchakama aliipongeza Serikali kwa kuwajali wananchi na kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi, akisema hatua hiyo itasaidia kupunguza matumizi ya kuni na mkaa, pamoja na kuboresha mazingira ya kufanyia shughuli zao.

    Naye Zamda Ally, mmoja wa wanufaika wa mitungi hiyo ya gesi, aliishukuru Serikali kwa msaada huo, akieleza kuwa ni hatua muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata fursa ya kutumia nishati safi, salama na rafiki kwa mazingira.

    Wananchi hao kwa pamoja waliipongeza Serikali kwa kuendelea kusogeza huduma na fursa mbalimbali kwa wananchi, wakisema matumizi ya nishati safi yatasaidia kupunguza athari za matumizi ya nishati zinazoharibu mazingira, pamoja na kuboresha afya na maisha ya familia.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Wataalamu wa teknolojia ya habari na mawasiliano wameitaka Tanzania kuimarisha imani ya wananchi katika huduma za kidijitali, ikiwemo usalama wa mtandao, ulinzi wa taarifa binafsi na ujuzi wa kidijitali, ili nchi iweze kunufaika zaidi na teknolojia ya akili bandia (AI) na uchumi wa kidijitali.

    Wito huo umetolewa katika Jukwaa la Tanzania Digital Trust Initiative, lililowakutanisha maofisa wa serikali, wadhibiti, wataalamu wa teknolojia, viongozi wa sekta na wadau wengine kujadili namna ya kujenga mazingira salama na ya kuaminika katika matumizi ya teknolojia nchini.

    Akizungumza katika jukwaa hilo, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya TEHAMA, Dkt. Nkundwe Mwasaga, alisema Tanzania imepiga hatua kubwa tangu kupitishwa kwa Sera ya Taifa ya TEHAMA ya mwaka 2003, na kwamba miundombinu iliyojengwa inapaswa kutafsiriwa kuwa manufaa ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi.

    Alisema Sera ya Taifa ya TEHAMA ya mwaka 2003 iliweka mkazo katika uanzishaji wa taasisi, miundombinu ya taifa ya TEHAMA na ujuzi wa TEHAMA, huku sera ya mwaka 2016 ikiongeza msisitizo katika mifumo na majukwaa ya kidijitali.

    “Tanzania imeingia katika uchumi wa kidijitali na hatua inayofuata ni kujenga miundombinu ya uaminifu itakayowawezesha wananchi kutumia huduma za kidijitali kwa usalama na uhakika,” alisema Dkt. Mwasaga.

    Alisema suala la uaminifu ni muhimu zaidi katika biashara za mtandaoni na huduma za kifedha za kidijitali, ambako wananchi wanahitaji kuwa na uhakika kwamba malipo wanayofanya ni salama, taarifa zao binafsi zinalindwa na bidhaa wanazonunua mtandaoni zitawafikia.

    “Biashara za mtandaoni zinategemea uaminifu. Bila uaminifu, uchumi wa kidijitali hauwezi kustawi,” alisema Dkt. Mwasaga.

    Akizungumzia matumizi ya akili bandia, Dkt. Mwasaga alisema Tanzania haipaswi kutumia teknolojia hiyo kwa kufuata mwenendo wa dunia pekee, bali inapaswa kuangalia namna inavyoweza kutumika kutatua changamoto na kuendana na vipaumbele vya maendeleo ya nchi.

    Alitaja sekta za viwanda, kilimo na maendeleo ya uchumi kuwa miongoni mwa maeneo ambayo matumizi sahihi ya AI yanaweza kutoa mchango mkubwa.

    Kwa mujibu wa Dkt. Mwasaga, manufaa ya AI yatategemea uwekezaji katika elimu na ujuzi, akitanabaisha kuwa maandalizi duni yanaweza kusababisha teknolojia hiyo kuongeza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana kutokana na baadhi ya kazi kuchukuliwa na mifumo inayotumia akili bandia.

    Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Privacy Professionals Association (TPPA), Tumwesigye Evans, alisema taasisi hiyo ina jukumu la kulinda taarifa binafsi za watumiaji kadri matumizi ya AI na uchumi wa kidijitali yanavyopanuka.

    Alisema TPPA imesaini Mkataba wa Makubaliano (MoU) na Sandbox Security ya India, pamoja na TAFINA, kwa lengo la kuimarisha uaminifu katika huduma za kidijitali nchini.

    “Kadri mabadiliko haya yanavyoendelea, ni muhimu kuimarisha imani ya wananchi katika huduma na teknolojia za kidijitali,” alisema Evans.

    Alisema ushirikiano huo unalenga kuunganisha ulinzi wa kisheria na hatua za kiufundi na kiusalama ili kulinda watumiaji wa huduma za kidijitali.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Kanda wa Mauzo na Masoko wa Sandbox, Amrita Choudhury, alisema ujenzi wa uaminifu katika matumizi ya teknolojia hauwezi kufanywa na taasisi au sekta moja pekee, bali unahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali.

    Wadau hao walisema kuimarisha uaminifu wa wananchi katika mazingira ya kidijitali ni muhimu wakati Tanzania ikiendelea kupanua matumizi ya huduma za mtandaoni, biashara za kidijitali na teknolojia mpya kama akili bandia.

    Kwa Tanzania, wataalamu wanaamini kuwa kujenga mazingira ya kidijitali yanayoaminika kutasaidia kuongeza matumizi ya huduma za mtandaoni, kulinda watumiaji dhidi ya hatari za kidijitali na kuwezesha teknolojia kuchangia zaidi katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

  • Na Yusra Temba

    Mlimbwende Jihan Dimack ameibuka mshindi wa taji la Miss Grand Tanzania 2026, baada ya kuwashinda washiriki wengine kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania katika shindano lililojumuisha vipengele vya mahojiano, mawasilisho, matembezi ya jukwaani na uwezo wa kujieleza mbele ya majaji na hadhira.

    Ushindi huo ulishuhudiwa na wadau mbalimbali wa tasnia ya burudani, urembo na ulimwengu wa mitindo katika fainali zilizofanyika usiku wa Jumamosi katika Ukumbi wa The Super Dome, Masaki, Dar es Salaam.

    Ushindi wa Jihan Dimack unaendelea kuimarisha safari ya Tanzania katika mashindano ya Miss Grand International, baada ya mwakilishi wa mwaka 2025, Beatrice Alex, kuweka rekodi ya kuwa Mtanzania aliyefika mbali zaidi katika historia ya mashindano hayo.

    Matokeo hayo yameongeza matarajio makubwa kwa mwakilishi wa mwaka 2026, ambaye anatarajiwa kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania katika jukwaa la kimataifa.

    Jihan Dimack sasa ataiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Miss Grand International 2026, yanayotarajiwa kufanyika nchini India.

    Kwa mwaka huu, mashindano hayo yametoa jumla ya warembo tisa watakaoiwakilisha Tanzania katika majukwaa mbalimbali ya kimataifa ya urembo. Warembo hao ni Jihan Dimack – Miss Grand International, Sharon Julius – Miss Elite, Celine Edson – Miss Earth, Rose Uisso – Miss Global, Eve Godwin – Miss Africa International, Namala Patrick – Miss Tourism Africa, Prisca Lyimo – Miss Cosmo, Zulfa Yazid – Miss Africa Golden, na Janeth Anselme – Miss Intercontinental.

    Kwa upande wake, Janeth Anselme, mshindi wa taji la Miss Intercontinental Tanzania 2026, alisema anamshukuru Mungu kwa hatua aliyofikia na kwamba ushindi huo ni mwanzo wa safari mpya ya kutimiza ndoto zake.

    Janeth alisema anafurahia ushindi huo na anatamani kutumia taji hilo kuleta mchango chanya katika jamii.

    Miongoni mwa wadau waliohudhuria fainali hizo alikuwa muigizaji Angel Mazanda, maarufu kwa jina la Chioma, ambaye alisema amefurahishwa na ushindi wa Prisca Lyimo, aliyetwaa taji la Miss Cosmo Tanzania 2026.

    Angel alisema anaamini Prisca ana uwezo mkubwa wa kufanya vizuri katika majukwaa ya kimataifa.

    Kwa upande wake, mama wa mrembo aliyeshinda taji la Miss Africa International Tanzania 2026, Rose Shayo, alitoa shukrani kwa uongozi wa Miss Grand Tanzania kwa kuandaa mashindano hayo na kutoa fursa kwa mabinti wa Kitanzania kuonesha vipaji na uwezo wao.

    Pia aliwashauri wazazi, hususan akina mama, kuwapa ushirikiano mabinti zao wanaotamani kuingia katika tasnia ya urembo ili waweze kutimiza ndoto zao.

    Mashindano ya Miss Grand Tanzania ni jukwaa la kitaifa linalolenga kumpata mrembo atakayeiwakilisha Tanzania katika mashindano ya kimataifa ya Miss Grand International.

    Mbali na kuangazia uzuri wa washiriki, mashindano hayo yanasisitiza pia uongozi, mawasiliano, kujiamini na ushiriki wa wanawake vijana katika masuala ya kijamii.

  • Na Juma John Elisha

    Usajili wa mshambuliaji wa Kitanzania, Selemani Mwalimu “Gomez”, kwenda Yanga SC umegeuka kuwa moja ya habari kubwa katika dirisha la usajili kuelekea msimu wa 2026/27, hasa kutokana na namna ulivyokuja baada ya Simba SC kuwahakikishia mashabiki wake kuwa mchezaji huyo angeendelea kuitumikia klabu hiyo.

    Yanga imemtambulisha rasmi Mwalimu kuwa mchezaji wake mpya, hatua inayofungua ukurasa mpya katika safari ya mshambuliaji huyo na kuongeza ushindani wa moja kwa moja kati ya vigogo hao wawili wa soka la Tanzania.

    Mwalimu alianza wapi?

    Mwalimu, ambaye ni mshambuliaji wa Tanzania, alijiunga na Simba msimu wa 2025/26 akitokea Wydad AC ya Morocco kwa mkopo wa msimu mmoja.

    Kabla ya safari yake kwenda Morocco, tayari alikuwa amejijengea jina katika soka la Tanzania, ikiwemo kipindi chake akiwa Fountain Gate, ambako alionyesha uwezo wa kufunga na kuleta tofauti katika eneo la ushambuliaji.

    Akiwa Simba, Mwalimu aliendelea kuonyesha uwezo wa kuamua michezo yenye presha. Miongoni mwa matukio yaliyomuweka zaidi kwenye ramani ni bao alilofunga katika fainali ya Kombe la Muungano dhidi ya Yanga, ambapo Simba ilishinda 1-0 baada ya muda wa nyongeza.

    Simba iliamini Mwalimu angebaki Msimbazi

    Baada ya msimu wa 2025/26 kumalizika, hatma ya Mwalimu ilibaki kuwa kitendawili.

    Simba ilitangaza kuwa imefikia makubaliano ya kuendelea na mshambuliaji huyo kwa msimu wa 2026/27. Hata hivyo, suala hilo liliendelea kuwa na sintofahamu kutokana na msimamo wa Wydad, huku Mwalimu akirejea Morocco.

    Hali hiyo iliibua maswali kuhusu iwapo angeendelea na Simba au angehamia klabu nyingine.

    Kilele cha sakata hilo kilifika Agosti 8, 2026, wakati Mwalimu alipoonekana kupitia ujumbe uliowasilishwa katika hafla ya Simba Day, akithibitisha kuwa angeendelea kuwa sehemu ya Simba.

    Ofisa Habari wa Simba, Ahmed Ally, pia alisema klabu hiyo ilikuwa imefikia makubaliano na Wydad kwa ajili ya kumrudisha mchezaji huyo Msimbazi.

    Taarifa zilizotangulia zilieleza pia kuwa Simba ilikuwa imeongeza muda wa mkopo wa Mwalimu kutoka Wydad kwa msimu wa 2026/27.

    Yanga yaingia dakika za mwisho

    Hata hivyo, katika mgeuko ambao huenda ukawa miongoni mwa matukio yaliyoshangaza zaidi kwenye dirisha hili la usajili, Yanga imeibuka na kumtambulisha Mwalimu leo, Agosti 11, 2026.

    Hatua hiyo imekuja siku chache tu baada ya Simba kuwahakikishia mashabiki wake kuwa mshambuliaji huyo angeendelea kuichezea klabu hiyo.

    Taarifa mbalimbali za leo zinaeleza kuwa Yanga imefikia makubaliano ya kumleta Mwalimu kutoka Wydad, huku baadhi ya taarifa zikieleza kuwa usajili huo umefanyika kwa mfumo wa mkopo.

    Hata hivyo, masharti yote ya makubaliano hayo bado hayajawekwa wazi, hivyo maelezo ya mwisho kuhusu muda na aina ya mkataba yanasubiri uthibitisho rasmi wa klabu.

    Kwa nini usajili huu ni pigo kwa Simba?

    Uzito wa usajili huu haupo tu katika Yanga kumpata Mwalimu, bali zaidi katika namna alivyotoka kwenye mipango ya Simba na kuhamia kwa watani wao wakubwa.

    Simba tayari ilikuwa imemjumuisha mshambuliaji huyo katika mipango yake ya msimu mpya. Zaidi ya hapo, Mwalimu alikuwa sehemu ya kikosi kilichoshinda Kombe la Muungano na alishawahi kuonyesha uwezo wa kufanya vizuri katika michezo yenye presha kubwa.

    Kwa Yanga, usajili huu unaongeza chaguo katika safu ya ushambuliaji kwa kumpata mchezaji ambaye tayari anaifahamu ligi ya Tanzania na amepata pia uzoefu wa kucheza nje ya nchi akiwa na Wydad.

    Kwa mtazamo mpana, usajili huu hauwezi kutazamwa kama uhamisho wa kawaida wa mchezaji pekee. Ni hatua inayoongeza joto katika ushindani wa usajili kati ya Simba na Yanga, hasa baada ya timu hizo mbili kuendelea kupambana kwa nguvu katika kuvutia wachezaji bora.

    Kutoka Msimbazi hadi Jangwani

    Safari ya Mwalimu katika miezi ya hivi karibuni imekuwa na misukosuko.

    Wydad → Simba kwa mkopo → sintofahamu kuhusu hatma yake → kurejea Morocco → kuhusishwa tena na Simba → hatimaye Yanga.

    Mlolongo huo umeifanya kadhia ya Mwalimu kuwa moja ya simulizi zinazovuta zaidi kwenye dirisha la usajili la msimu wa 2026/27.

    Sasa mshambuliaji huyo anaingia katika changamoto mpya akiwa upande wa pili wa vita ya jadi ya Simba na Yanga.

    Na swali linalosubiriwa kwa hamu ni moja:

    Atakutana vipi na Simba siku Yanga itakapokutana na Wekundu wa Msimbazi?

    Jibu la swali hilo linaweza kuifanya mechi ya Simba na Yanga msimu wa 2026/27 kuwa na mvuto wa ziada, hasa iwapo Mwalimu atakuwa sehemu ya kikosi cha Yanga kitakachokabiliana na klabu yake ya zamani.

  • Na Pilastus Nyaulingo, Tanga

    Wito umetolewa kwa madereva wa bodaboda nchini kuongeza tahadhari wanapopokea abiria, hasa wanaowaomba safari za umbali mrefu, kufuatia kifo cha dereva mwenye umri wa miaka 18, Rajab Arufan, aliyefariki baada ya kwenda katika safari ya Lukozi, Wilaya ya Lushoto.

    Rajab, aliyekuwa akifanya kazi katika kituo cha bodaboda Mabanda ya Papa jijini Tanga, aliondoka kwa safari hiyo akiamini ni ya kawaida, lakini baadaye mwili wake uligundulika katika eneo la Magamba, Lushoto.

    Kwa mujibu wa watu waliokuwa karibu naye, Rajab alikuwa amemfahamu abiria aliyempa safari hiyo kwa takribani wiki mbili na awali alikuwa amewahi kumsafirisha katika maeneo ya Pangani na Horohoro.

    Rafiki yake, Hemed Said, alisema Rajab alikuwa kijana mwenye bidii aliyejiajiri kupitia kazi ya bodaboda na siku ya safari alimweleza kuwa alikuwa amepata safari ya kwenda Lushoto.

    Said alisema baada ya Rajab kutorejea na simu yake kutopatikana, walitoa taarifa kwa familia yake na baadaye walipata taarifa za kifo chake baada ya mwili kugundulika Magamba.

    Dereva mwenzake, Karim Abdallah, alisema abiria huyo hakufahamika katika kituo cha Mabanda ya Papa, huku Rajab akiwa amewaeleza wenzake kuwa alikuwa akimpa safari ndefu na malipo mazuri.

    Naye Salum Bakari, aliyewahi kufanya biashara pamoja na Rajab, alisema alimshauri kutosafiri peke yake baada ya kumweleza kuhusu safari hiyo, akisisitiza kuwa si rahisi kumwamini kila mteja.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Madereva Bodaboda Mkoa wa Tanga, Mohamed Chande, alisema madereva wanapaswa kuwa makini zaidi wanapochukua abiria wasiowafahamu, hasa wanaowaomba safari ndefu.

    Chande alisema ingawa matukio ya mauaji ya madereva yamepungua ikilinganishwa na kipindi kilichopita, bado kuna haja ya madereva kutoa taarifa mapema wanapokuwa na mashaka kuhusu abiria au safari wanazopewa.

    Alisema chama hicho kinaendelea kuhimiza ushirikiano kati ya madereva na vyombo vya usalama ili kuzuia matukio kama hayo.

    Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Almachius Mchunguzi, alisema Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi kuhusu tukio hilo na kuwataka wananchi kushirikiana na vyombo vya usalama kuwabaini wahusika wa vitendo vya uhalifu.

    Kifo cha Rajab kimeongeza wito wa kuimarishwa kwa usalama wa madereva wa bodaboda, huku wadau wakisisitiza umuhimu wa madereva kuchukua tahadhari kabla ya kukubali safari za umbali mrefu au kwenda maeneo wasiyoyafahamu.

  • Na Pilastus Nyaulingo, Dodoma

    Wadau wa sekta ya kilimo na mazingira wameeleza kuwa kilimo mseto cha miti na mazao kinaweza kuwa fursa muhimu kwa vijana kujiajiri, kuongeza kipato na kuchangia kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

    Kauli hiyo imetolewa katika mkutano wa wadau uliofanyika Dodoma, pembezoni mwa maonesho ya Nane Nane, ambapo washiriki walijadili namna ya kuendeleza kilimo mseto kama njia ya kuboresha maisha ya jamii na kuongeza fursa za kiuchumi kwa vijana.

    Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi wa Nchi wa Vi Agroforestry Tanzania, Martha Olotu, alisema kilimo mseto kina fursa mbalimbali za kiuchumi kwa vijana, huku kikiendelea kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto zinazoikabili sekta ya kilimo na mazingira.

    Alisema vijana wanapaswa kupewa nafasi kubwa zaidi katika sekta hiyo kwa kuwa wanaweza kutumia maarifa, teknolojia na ubunifu kuanzisha shughuli zinazohusiana na kilimo mseto na kujenga vyanzo vya kipato.

    “Uwekezaji katika kilimo mseto utasaidia vijana kujenga ajira na biashara zinazohusiana na uzalishaji wa mazao, miti na shughuli nyingine za kilimo zinazolenga kuhifadhi mazingira,” alisema Olotu.

    Kwa upande wake, mmoja wa maafisa walioshiriki katika mjadala huo, Edna Paul, alisema kilimo mseto kina nafasi muhimu katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuboresha uzalishaji wa chakula.

    Alisema mfumo huo huwezesha kuboresha rutuba ya udongo, kuongeza uzalishaji wa chakula na kuchangia kupunguza changamoto za utapiamlo katika jamii.

    Alisema kuunganisha miti na mazao katika mifumo ya kilimo kutasaidia wakulima kutumia ardhi kwa ufanisi zaidi huku wakilinda mazingira na kujenga uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa.

    Mkurugenzi wa Civil Social Protective Foundation na mshirika wa Vi Agroforestry, Nemesi Kiliya, alisema kuna umuhimu wa ushirikiano wa wadau mbalimbali katika kukuza kilimo mseto nchini.

    Alisema mpango wa kuanzisha jukwaa la kitaifa la wadau wa kilimo mseto utasaidia kuimarisha ushirikiano, kubadilishana uzoefu na kuongeza uwekezaji katika sekta hiyo kwa njia endelevu.

    Alisema jukwaa hilo pia litasaidia kuwaunganisha vijana, wakulima, mashirika na taasisi zinazohusika na sekta za kilimo na mazingira.

    Mkazi wa Nzuguni, Dodoma, Aidani Naftari, alisema kilimo mseto ni fursa inayoweza kuwasaidia vijana kujipatia kipato huku wakishiriki katika uhifadhi wa mazingira.

    “Kwa mtazamo wangu, vijana wengi tunatafuta ajira, lakini si lazima kila mtu aajiriwe kwenye ofisi. Tukipata elimu, mtaji na teknolojia sahihi, tunaweza kutumia kilimo na upandaji miti kujiajiri na kujenga maisha yetu,” alisema Naftari.

    Alisema serikali na wadau wanapaswa kuendelea kuwawezesha vijana ili fursa hiyo isiishie kwenye mijadala pekee, bali iwe chanzo cha ajira na maendeleo kwa jamii.

  • Na Pilastus Nyaulingo, Ushetu, Shinyanga

    Halmashauri ya Ushetu kupitia Idara ya Elimu imemkabidhi Tuzo ya Heshima Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel Cherehani, kwa kutambua mchango wake katika kuimarisha sekta ya elimu na kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za elimu katika halmashauri hiyo.

    Tuzo hiyo ilikabidhiwa jana katika hafla iliyosisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya viongozi, watumishi wa umma na wadau wa elimu katika kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia, kwa lengo la kuinua kiwango cha elimu kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.

    Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Ushetu, Hadija Kabojela, alisema tangu Cherehani aingie madarakani amekuwa akitoa ushirikiano mkubwa katika kuendeleza sekta ya elimu, ikiwemo kuisemea katika ngazi mbalimbali na kutoa motisha kwa walimu na wanafunzi.

    Kabojela alisema ushirikiano huo umechangia kuimarisha juhudi za maendeleo ya elimu katika halmashauri hiyo na kuongeza hamasa kwa walimu na wanafunzi kuendelea kufanya vizuri kitaaluma.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Ushetu, Gagi Lala Gagi, alisema halmashauri hiyo inajivunia ushirikiano uliopo na mbunge huyo, akieleza kuwa amekuwa mstari wa mbele kutetea maslahi ya wananchi na kuchangia upatikanaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo miradi ya sekta ya elimu.

    Alisema uwekezaji katika elimu ni msingi wa maendeleo ya jamii, huku ushirikiano kati ya viongozi na wadau ukiendelea kuwa muhimu katika kuboresha huduma zinazowagusa moja kwa moja wanafunzi na walimu.

    Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel Cherehani, aliishukuru Idara ya Elimu pamoja na watumishi wa Halmashauri ya Ushetu kwa kutambua mchango wake katika sekta hiyo.

    Alisema tuzo hiyo imempa nguvu na motisha ya kuendelea kushirikiana na halmashauri katika kuendeleza sekta ya elimu pamoja na huduma nyingine za kijamii kwa manufaa ya wananchi wa Ushetu.

    Aidha, aliahidi kuendelea kuunga mkono juhudi za kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia, pamoja na kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha sekta ya elimu inaendelea kupata mafanikio.

    Kutolewa kwa tuzo hiyo kumeelezwa kuwa ni sehemu ya kuhamasisha ushirikiano kati ya viongozi na wadau wa maendeleo katika kuimarisha sekta ya elimu, ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu ya jamii.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Mradi wa Mabasi yaendayo Haraka (BRT) Awamu ya Pili unatarajiwa kuboresha huduma za usafiri wa umma kwa wakazi wa Dar es Salaam na kusaidia kupunguza gharama za safari kwa wananchi.

    Kauli hiyo ilitolewa jana wakati wa uzinduzi wa mradi huo jijini Dar es Salaam, ambapo viongozi walisema BRT Awamu ya Pili ni sehemu ya juhudi za kuboresha miundombinu ya usafiri na maisha ya wakazi wa jiji.

    Balozi wa Japan nchini Tanzania, Yoichi Mikami, alisema mradi huo utaboresha huduma za usafiri wa umma na kusaidia kupunguza gharama za safari kwa wakazi wa Dar es Salaam.

    “Mradi wa BRT Awamu ya Pili utaboresha huduma za usafiri wa umma kwa wakazi wa Dar es Salaam na kusaidia kupunguza gharama za safari,” alisema Balozi Mikami.

    Alisema mradi huo ni sehemu ya mpango mpana wa kuboresha mfumo wa usafiri wa jiji la Dar es Salaam, uliotengenezwa kwa msaada wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA).

    Alisema Japan inajivunia kushiriki katika utekelezaji wa mpango huo kupitia kusaidia miradi muhimu ya miundombinu, ikiwemo ujenzi wa Daraja la Gerezani, ambalo ni sehemu muhimu ya mtandao wa usafiri wa Dar es Salaam.

    Kwa mujibu wa Balozi Mikami, uboreshaji wa miundombinu ya usafiri utaongeza ufanisi wa huduma za usafiri wa umma, kurahisisha usafirishaji wa watu na bidhaa na kuchangia ukuaji wa uchumi wa jiji.

    Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, alisema uzinduzi wa mradi huo ni hatua kubwa katika maendeleo yanayomweka mwananchi mbele, kwa lengo la kuboresha maisha ya wakazi wa jiji.

    Chalamila alisema Dar es Salaam imekuwa ikikabiliwa na changamoto za miundombinu ya usafiri kwa miaka mingi, akieleza kuwa utekelezaji wa BRT Awamu ya Pili unaonesha dhamira ya Serikali ya kuleta maendeleo yanayowanufaisha wananchi na kuzingatia mahitaji yao.

    Aliipongeza Serikali kwa utekelezaji wa mradi huo na kuishukuru Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) kwa mchango wake katika kufadhili miradi ya maendeleo nchini Tanzania.

    BRT Awamu ya Pili inatarajiwa kuwa na umuhimu mkubwa kwa wakazi wa Dar es Salaam wanaotegemea usafiri wa umma katika shughuli zao za kila siku, ikiwemo kwenda kazini na shuleni, kufanya biashara na kufikia huduma mbalimbali.

    Mradi huo pia unatarajiwa kuchangia ukuaji wa shughuli za kiuchumi jijini Dar es Salaam kupitia uboreshaji wa miundombinu na huduma za usafiri.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Wadau wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) wameitaka Serikali kutambua kisheria mitandao ya jamii ya mawasiliano kama watoa huduma za kidijitali zisizo za kibiashara, wakisema hatua hiyo inaweza kusaidia kuongeza upatikanaji wa intaneti katika maeneo ya vijijini na yaliyo pembezoni.

    Wito huo umetolewa hivi karibuni jijini Dar es Salaam na wadau wa TEHAMA, wawakilishi wa Serikali na mashirika ya kiraia katika kikao kilichojadili namna ya kupanua upatikanaji wa huduma za intaneti kwa jamii ambazo bado hazijahudumiwa ipasavyo.

    Kikao hicho kiliandaliwa kwa ushirikiano wa Paradigm Initiative na Tanzania School of Community Networks, huku mjadala ukijikita katika umuhimu wa kuweka mazingira ya kisera na kisheria yatakayowezesha jamii kuanzisha na kuendesha mitandao yao ya mawasiliano.

    Mmoja wa washiriki wa kikao hicho, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Dk. Jabhera Matogoro, alisema mitandao hiyo inapaswa kutambuliwa chini ya Sera ya Taifa ya TEHAMA kama miundombinu ya kidijitali inayomilikiwa na jamii na isiyo ya kibiashara, pale inapokuwa imepewa leseni.

    Kwa mujibu wa Dk. Matogoro, utambuzi huo ungezipa jamii unyumbufu zaidi wa kifedha katika kuendesha mitandao hiyo, badala ya kusimamiwa kwa mfumo unaotumika kwa kampuni za kibiashara za mawasiliano.

    Alisema pia kuna umuhimu wa wananchi kuwa na ujuzi wa kidijitali ili uwekezaji katika miundombinu ya mtandao uweze kuleta matokeo chanya ya kiuchumi na kijamii.

    “Ikiwa Tanzania inalenga kutimiza matarajio ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, ni muhimu kuwawezesha wananchi kupata ujuzi wa kidijitali,” alisema Dk. Matogoro.

    Alieleza kuwa mitandao ya jamii ya mawasiliano inaweza kusaidia kuwafikishia wananchi huduma za intaneti, huku uelewa wa matumizi ya teknolojia ukiwa muhimu katika kuhakikisha huduma hizo zinachangia maendeleo halisi ya kijamii na kiuchumi.

    Afisa Mwandamizi wa Paradigm Initiative, Ihueze Nwobilor, alisema wanataka mitandao ya jamii itambulike katika sera na sheria za Tanzania kama huduma za jamii zisizo za kibiashara.

    Alisema bila utambuzi huo, baadhi ya vijiji vinaweza kuendelea kubaki nje ya mchakato wa mabadiliko ya kidijitali nchini, licha ya kuwepo kwa teknolojia inayoweza kuwafikishia huduma za intaneti.

    Kwa upande wake, Rose Ngunangwa, mmoja wa washiriki wa kikao hicho, alisema majadiliano hayo yamepanua uelewa wa washiriki kuhusu nafasi muhimu ambayo jamii zinaweza kuwa nayo katika kupunguza pengo la kidijitali kati ya watu wa mijini na vijijini.

    Kwa mujibu wa Ngunangwa, hapo awali watu wengi waliamini kuwa jukumu la kupanua upatikanaji wa mtandao lilikuwa la kampuni za mawasiliano pekee, lakini kikao hicho kimeonesha kuwa jamii zenyewe zinaweza kuwa sehemu ya suluhisho.

    “Mitandao ya jamii imeonesha kwamba jamii zina uwezo wa kujijengea suluhisho zao. Tunachohitaji sasa ni mazingira wezeshi ya kisheria yatakayoruhusu ubunifu huu kuwafikia Watanzania wengi zaidi,” alisema Ngunangwa.

    Wadau hao wanaamini kuwa utambuzi wa kisheria wa mitandao ya jamii ya mawasiliano utasaidia jamii kuwa na nafasi kubwa zaidi katika kujenga na kuendesha miundombinu ya mawasiliano kulingana na mahitaji yao.

    Mitandao hiyo inaweza kuwa muhimu kwa wananchi wa maeneo ambayo hayajafikiwa kikamilifu na huduma za intaneti za kibiashara, na hivyo kusaidia kuongeza upatikanaji wa huduma za elimu, biashara, mawasiliano na huduma nyingine za kijamii kupitia teknolojia.

  • Na Mohamed Zongo

    Kikosi cha Polisi Reli Tanzania kimeendelea kushirikiana na jamii inayofanya shughuli zake katika ushoroba wa reli kwa kufanya usafi wa pamoja na mafundi wa magari, wauzaji wa chakula maarufu kama mama ntilie, maafisa usafirishaji pamoja na wafanyabiashara ndogondogo katika eneo la Pentagon, Mivinjeni, Kata ya Kurasini, Wilaya ya Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam.

    Akizungumza baada ya zoezi hilo, Afisa Mnadhimu wa Kikosi cha Polisi Reli Tanzania, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Mushana Mujema, kwa niaba ya Kamanda wa Kikosi hicho, ACP Matride Kuyeto, amewataka wananchi wa maeneo hayo kuendelea kufanya usafi wa mazingira ili kuepuka magonjwa ya mlipuko.

    ACP Mujema amewataka wananchi hao kuwa mabalozi wema katika kulinda na kutunza miundombinu ya Shirika la Reli Tanzania (TRC), kwa kuwa maeneo wanayofanyia shughuli zao yamezungukwa na miundombinu hiyo.

    Amesema wananchi wanapaswa kuwa wazalendo kwa kuitunza amani ya nchi, akieleza kuwa wanaweza kufanya shughuli zao kwa utulivu kutokana na kuwepo kwa amani. Hivyo, amewataka kuendelea kuilinda amani hiyo kwa hali na mali.

    Wakati huohuo, Afisa Polisi Jamii wa Kikosi cha Polisi Reli Tanzania, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Batseba Kasanga, ametoa elimu ya usalama wa reli kwa wananchi wanaofanya shughuli zao katika eneo hilo la Mivinjeni, akiwataka kutoweka kitu cha aina yoyote kwenye njia ya reli, kwani kufanya hivyo kunaweza kuhatarisha usalama wa usafiri wa reli.

    Kwa upande wake, Kiongozi wa mafundi katika eneo hilo, Joseph Mwamanda, amelipongeza Jeshi la Polisi kwa juhudi zake za kuwa karibu na jamii na kusisitiza kuwa wataendelea kushirikiana na Jeshi hilo katika kukabiliana na uhalifu.