• Na Pilastus Nyaulingo, Dodoma

    Wadau wa sekta ya kilimo na mazingira wameeleza kuwa kilimo mseto cha miti na mazao kinaweza kuwa fursa muhimu kwa vijana kujiajiri, kuongeza kipato na kuchangia kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

    Kauli hiyo imetolewa katika mkutano wa wadau uliofanyika Dodoma, pembezoni mwa maonesho ya Nane Nane, ambapo washiriki walijadili namna ya kuendeleza kilimo mseto kama njia ya kuboresha maisha ya jamii na kuongeza fursa za kiuchumi kwa vijana.

    Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi wa Nchi wa Vi Agroforestry Tanzania, Martha Olotu, alisema kilimo mseto kina fursa mbalimbali za kiuchumi kwa vijana, huku kikiendelea kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto zinazoikabili sekta ya kilimo na mazingira.

    Alisema vijana wanapaswa kupewa nafasi kubwa zaidi katika sekta hiyo kwa kuwa wanaweza kutumia maarifa, teknolojia na ubunifu kuanzisha shughuli zinazohusiana na kilimo mseto na kujenga vyanzo vya kipato.

    “Uwekezaji katika kilimo mseto utasaidia vijana kujenga ajira na biashara zinazohusiana na uzalishaji wa mazao, miti na shughuli nyingine za kilimo zinazolenga kuhifadhi mazingira,” alisema Olotu.

    Kwa upande wake, mmoja wa maafisa walioshiriki katika mjadala huo, Edna Paul, alisema kilimo mseto kina nafasi muhimu katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuboresha uzalishaji wa chakula.

    Alisema mfumo huo huwezesha kuboresha rutuba ya udongo, kuongeza uzalishaji wa chakula na kuchangia kupunguza changamoto za utapiamlo katika jamii.

    Alisema kuunganisha miti na mazao katika mifumo ya kilimo kutasaidia wakulima kutumia ardhi kwa ufanisi zaidi huku wakilinda mazingira na kujenga uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa.

    Mkurugenzi wa Civil Social Protective Foundation na mshirika wa Vi Agroforestry, Nemesi Kiliya, alisema kuna umuhimu wa ushirikiano wa wadau mbalimbali katika kukuza kilimo mseto nchini.

    Alisema mpango wa kuanzisha jukwaa la kitaifa la wadau wa kilimo mseto utasaidia kuimarisha ushirikiano, kubadilishana uzoefu na kuongeza uwekezaji katika sekta hiyo kwa njia endelevu.

    Alisema jukwaa hilo pia litasaidia kuwaunganisha vijana, wakulima, mashirika na taasisi zinazohusika na sekta za kilimo na mazingira.

    Mkazi wa Nzuguni, Dodoma, Aidani Naftari, alisema kilimo mseto ni fursa inayoweza kuwasaidia vijana kujipatia kipato huku wakishiriki katika uhifadhi wa mazingira.

    “Kwa mtazamo wangu, vijana wengi tunatafuta ajira, lakini si lazima kila mtu aajiriwe kwenye ofisi. Tukipata elimu, mtaji na teknolojia sahihi, tunaweza kutumia kilimo na upandaji miti kujiajiri na kujenga maisha yetu,” alisema Naftari.

    Alisema serikali na wadau wanapaswa kuendelea kuwawezesha vijana ili fursa hiyo isiishie kwenye mijadala pekee, bali iwe chanzo cha ajira na maendeleo kwa jamii.

  • Na Pilastus Nyaulingo, Ushetu, Shinyanga

    Halmashauri ya Ushetu kupitia Idara ya Elimu imemkabidhi Tuzo ya Heshima Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel Cherehani, kwa kutambua mchango wake katika kuimarisha sekta ya elimu na kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za elimu katika halmashauri hiyo.

    Tuzo hiyo ilikabidhiwa jana katika hafla iliyosisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya viongozi, watumishi wa umma na wadau wa elimu katika kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia, kwa lengo la kuinua kiwango cha elimu kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.

    Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Ushetu, Hadija Kabojela, alisema tangu Cherehani aingie madarakani amekuwa akitoa ushirikiano mkubwa katika kuendeleza sekta ya elimu, ikiwemo kuisemea katika ngazi mbalimbali na kutoa motisha kwa walimu na wanafunzi.

    Kabojela alisema ushirikiano huo umechangia kuimarisha juhudi za maendeleo ya elimu katika halmashauri hiyo na kuongeza hamasa kwa walimu na wanafunzi kuendelea kufanya vizuri kitaaluma.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Ushetu, Gagi Lala Gagi, alisema halmashauri hiyo inajivunia ushirikiano uliopo na mbunge huyo, akieleza kuwa amekuwa mstari wa mbele kutetea maslahi ya wananchi na kuchangia upatikanaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo miradi ya sekta ya elimu.

    Alisema uwekezaji katika elimu ni msingi wa maendeleo ya jamii, huku ushirikiano kati ya viongozi na wadau ukiendelea kuwa muhimu katika kuboresha huduma zinazowagusa moja kwa moja wanafunzi na walimu.

    Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel Cherehani, aliishukuru Idara ya Elimu pamoja na watumishi wa Halmashauri ya Ushetu kwa kutambua mchango wake katika sekta hiyo.

    Alisema tuzo hiyo imempa nguvu na motisha ya kuendelea kushirikiana na halmashauri katika kuendeleza sekta ya elimu pamoja na huduma nyingine za kijamii kwa manufaa ya wananchi wa Ushetu.

    Aidha, aliahidi kuendelea kuunga mkono juhudi za kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia, pamoja na kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha sekta ya elimu inaendelea kupata mafanikio.

    Kutolewa kwa tuzo hiyo kumeelezwa kuwa ni sehemu ya kuhamasisha ushirikiano kati ya viongozi na wadau wa maendeleo katika kuimarisha sekta ya elimu, ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu ya jamii.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Mradi wa Mabasi yaendayo Haraka (BRT) Awamu ya Pili unatarajiwa kuboresha huduma za usafiri wa umma kwa wakazi wa Dar es Salaam na kusaidia kupunguza gharama za safari kwa wananchi.

    Kauli hiyo ilitolewa jana wakati wa uzinduzi wa mradi huo jijini Dar es Salaam, ambapo viongozi walisema BRT Awamu ya Pili ni sehemu ya juhudi za kuboresha miundombinu ya usafiri na maisha ya wakazi wa jiji.

    Balozi wa Japan nchini Tanzania, Yoichi Mikami, alisema mradi huo utaboresha huduma za usafiri wa umma na kusaidia kupunguza gharama za safari kwa wakazi wa Dar es Salaam.

    “Mradi wa BRT Awamu ya Pili utaboresha huduma za usafiri wa umma kwa wakazi wa Dar es Salaam na kusaidia kupunguza gharama za safari,” alisema Balozi Mikami.

    Alisema mradi huo ni sehemu ya mpango mpana wa kuboresha mfumo wa usafiri wa jiji la Dar es Salaam, uliotengenezwa kwa msaada wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA).

    Alisema Japan inajivunia kushiriki katika utekelezaji wa mpango huo kupitia kusaidia miradi muhimu ya miundombinu, ikiwemo ujenzi wa Daraja la Gerezani, ambalo ni sehemu muhimu ya mtandao wa usafiri wa Dar es Salaam.

    Kwa mujibu wa Balozi Mikami, uboreshaji wa miundombinu ya usafiri utaongeza ufanisi wa huduma za usafiri wa umma, kurahisisha usafirishaji wa watu na bidhaa na kuchangia ukuaji wa uchumi wa jiji.

    Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, alisema uzinduzi wa mradi huo ni hatua kubwa katika maendeleo yanayomweka mwananchi mbele, kwa lengo la kuboresha maisha ya wakazi wa jiji.

    Chalamila alisema Dar es Salaam imekuwa ikikabiliwa na changamoto za miundombinu ya usafiri kwa miaka mingi, akieleza kuwa utekelezaji wa BRT Awamu ya Pili unaonesha dhamira ya Serikali ya kuleta maendeleo yanayowanufaisha wananchi na kuzingatia mahitaji yao.

    Aliipongeza Serikali kwa utekelezaji wa mradi huo na kuishukuru Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) kwa mchango wake katika kufadhili miradi ya maendeleo nchini Tanzania.

    BRT Awamu ya Pili inatarajiwa kuwa na umuhimu mkubwa kwa wakazi wa Dar es Salaam wanaotegemea usafiri wa umma katika shughuli zao za kila siku, ikiwemo kwenda kazini na shuleni, kufanya biashara na kufikia huduma mbalimbali.

    Mradi huo pia unatarajiwa kuchangia ukuaji wa shughuli za kiuchumi jijini Dar es Salaam kupitia uboreshaji wa miundombinu na huduma za usafiri.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Wadau wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) wameitaka Serikali kutambua kisheria mitandao ya jamii ya mawasiliano kama watoa huduma za kidijitali zisizo za kibiashara, wakisema hatua hiyo inaweza kusaidia kuongeza upatikanaji wa intaneti katika maeneo ya vijijini na yaliyo pembezoni.

    Wito huo umetolewa hivi karibuni jijini Dar es Salaam na wadau wa TEHAMA, wawakilishi wa Serikali na mashirika ya kiraia katika kikao kilichojadili namna ya kupanua upatikanaji wa huduma za intaneti kwa jamii ambazo bado hazijahudumiwa ipasavyo.

    Kikao hicho kiliandaliwa kwa ushirikiano wa Paradigm Initiative na Tanzania School of Community Networks, huku mjadala ukijikita katika umuhimu wa kuweka mazingira ya kisera na kisheria yatakayowezesha jamii kuanzisha na kuendesha mitandao yao ya mawasiliano.

    Mmoja wa washiriki wa kikao hicho, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Dk. Jabhera Matogoro, alisema mitandao hiyo inapaswa kutambuliwa chini ya Sera ya Taifa ya TEHAMA kama miundombinu ya kidijitali inayomilikiwa na jamii na isiyo ya kibiashara, pale inapokuwa imepewa leseni.

    Kwa mujibu wa Dk. Matogoro, utambuzi huo ungezipa jamii unyumbufu zaidi wa kifedha katika kuendesha mitandao hiyo, badala ya kusimamiwa kwa mfumo unaotumika kwa kampuni za kibiashara za mawasiliano.

    Alisema pia kuna umuhimu wa wananchi kuwa na ujuzi wa kidijitali ili uwekezaji katika miundombinu ya mtandao uweze kuleta matokeo chanya ya kiuchumi na kijamii.

    “Ikiwa Tanzania inalenga kutimiza matarajio ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, ni muhimu kuwawezesha wananchi kupata ujuzi wa kidijitali,” alisema Dk. Matogoro.

    Alieleza kuwa mitandao ya jamii ya mawasiliano inaweza kusaidia kuwafikishia wananchi huduma za intaneti, huku uelewa wa matumizi ya teknolojia ukiwa muhimu katika kuhakikisha huduma hizo zinachangia maendeleo halisi ya kijamii na kiuchumi.

    Afisa Mwandamizi wa Paradigm Initiative, Ihueze Nwobilor, alisema wanataka mitandao ya jamii itambulike katika sera na sheria za Tanzania kama huduma za jamii zisizo za kibiashara.

    Alisema bila utambuzi huo, baadhi ya vijiji vinaweza kuendelea kubaki nje ya mchakato wa mabadiliko ya kidijitali nchini, licha ya kuwepo kwa teknolojia inayoweza kuwafikishia huduma za intaneti.

    Kwa upande wake, Rose Ngunangwa, mmoja wa washiriki wa kikao hicho, alisema majadiliano hayo yamepanua uelewa wa washiriki kuhusu nafasi muhimu ambayo jamii zinaweza kuwa nayo katika kupunguza pengo la kidijitali kati ya watu wa mijini na vijijini.

    Kwa mujibu wa Ngunangwa, hapo awali watu wengi waliamini kuwa jukumu la kupanua upatikanaji wa mtandao lilikuwa la kampuni za mawasiliano pekee, lakini kikao hicho kimeonesha kuwa jamii zenyewe zinaweza kuwa sehemu ya suluhisho.

    “Mitandao ya jamii imeonesha kwamba jamii zina uwezo wa kujijengea suluhisho zao. Tunachohitaji sasa ni mazingira wezeshi ya kisheria yatakayoruhusu ubunifu huu kuwafikia Watanzania wengi zaidi,” alisema Ngunangwa.

    Wadau hao wanaamini kuwa utambuzi wa kisheria wa mitandao ya jamii ya mawasiliano utasaidia jamii kuwa na nafasi kubwa zaidi katika kujenga na kuendesha miundombinu ya mawasiliano kulingana na mahitaji yao.

    Mitandao hiyo inaweza kuwa muhimu kwa wananchi wa maeneo ambayo hayajafikiwa kikamilifu na huduma za intaneti za kibiashara, na hivyo kusaidia kuongeza upatikanaji wa huduma za elimu, biashara, mawasiliano na huduma nyingine za kijamii kupitia teknolojia.

  • Na Mohamed Zongo

    Kikosi cha Polisi Reli Tanzania kimeendelea kushirikiana na jamii inayofanya shughuli zake katika ushoroba wa reli kwa kufanya usafi wa pamoja na mafundi wa magari, wauzaji wa chakula maarufu kama mama ntilie, maafisa usafirishaji pamoja na wafanyabiashara ndogondogo katika eneo la Pentagon, Mivinjeni, Kata ya Kurasini, Wilaya ya Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam.

    Akizungumza baada ya zoezi hilo, Afisa Mnadhimu wa Kikosi cha Polisi Reli Tanzania, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Mushana Mujema, kwa niaba ya Kamanda wa Kikosi hicho, ACP Matride Kuyeto, amewataka wananchi wa maeneo hayo kuendelea kufanya usafi wa mazingira ili kuepuka magonjwa ya mlipuko.

    ACP Mujema amewataka wananchi hao kuwa mabalozi wema katika kulinda na kutunza miundombinu ya Shirika la Reli Tanzania (TRC), kwa kuwa maeneo wanayofanyia shughuli zao yamezungukwa na miundombinu hiyo.

    Amesema wananchi wanapaswa kuwa wazalendo kwa kuitunza amani ya nchi, akieleza kuwa wanaweza kufanya shughuli zao kwa utulivu kutokana na kuwepo kwa amani. Hivyo, amewataka kuendelea kuilinda amani hiyo kwa hali na mali.

    Wakati huohuo, Afisa Polisi Jamii wa Kikosi cha Polisi Reli Tanzania, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Batseba Kasanga, ametoa elimu ya usalama wa reli kwa wananchi wanaofanya shughuli zao katika eneo hilo la Mivinjeni, akiwataka kutoweka kitu cha aina yoyote kwenye njia ya reli, kwani kufanya hivyo kunaweza kuhatarisha usalama wa usafiri wa reli.

    Kwa upande wake, Kiongozi wa mafundi katika eneo hilo, Joseph Mwamanda, amelipongeza Jeshi la Polisi kwa juhudi zake za kuwa karibu na jamii na kusisitiza kuwa wataendelea kushirikiana na Jeshi hilo katika kukabiliana na uhalifu.

  • Na Mwandishi Wetu, Nachingwea—Lindi

    Mbunge wa Jimbo la Nachingwea, Fadhili Liwaka, amekabidhi gari la kubebea wagonjwa (ambulance) katika Kituo cha Afya Naipanga, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa jimbo hilo.

    Makabidhiano hayo yamefanyika wakati Mbunge huyo akiendelea na ziara yake ya kuwashukuru wananchi kwa imani waliyoonyesha kwake, sambamba na kusikiliza changamoto na kero mbalimbali zinazowakabili.

    Mbali na kukabidhi ambulance hiyo, Liwaka amesema kupitia Mfuko wa Jimbo, kiasi cha Shilingi milioni tatu kimetolewa kwa ajili ya ujenzi wa jengo la kupumzikia wagonjwa katika kituo hicho, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma za afya.

    Akizungumza katika hafla ya makabidhiano, Liwaka ameishukuru Serikali kwa kuwezesha upatikanaji wa gari hilo, huku akiipongeza Wizara ya Afya kwa mchango wake katika kufanikisha upatikanaji wa ambulance hiyo.

    Kwa upande wao, wananchi wa Naipanga wameeleza kufurahishwa na ujio wa gari hilo, wakisema litasaidia kupunguza changamoto ya usafiri wa wagonjwa na kuimarisha huduma za rufaa kwa wakati.

    Wamesema hatua hiyo itaongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za afya katika Kituo cha Afya Naipanga, hususan kwa wagonjwa wanaohitaji huduma katika vituo vya juu zaidi vya afya.

  • Na Mwandishi Wetu, Nachingwea—Lindi

    Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano ya Kazi), Deus Sangu, ameweka jiwe la msingi la Jengo la Mama na Mtoto katika Zahanati ya Kijiji cha Nditi, Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, mkoani Lindi.

    Waziri Sangu ameweka jiwe hilo la msingi ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi mkoani Lindi.

    Akizungumza katika hafla hiyo, Sangu aliwapongeza wananchi wa Kijiji cha Nditi kwa ushiriki wao katika ujenzi wa jengo hilo, akisema hatua hiyo ni mfano mzuri wa maendeleo yanayotokana na ushirikiano kati ya wananchi na Serikali.

    Aliahidi kuchangia vitanda viwili vya kujifungulia vyenye thamani ya Shilingi milioni 3.6, ili kusaidia kuboresha huduma za afya kwa mama na mtoto katika zahanati hiyo.

    Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Nachingwea, Fadhili Liwaka, alimshukuru Waziri Sangu kwa kutembelea kijiji hicho na kuweka jiwe la msingi la jengo hilo.

    Liwaka alisema sekta ya afya ni miongoni mwa vipaumbele vya maendeleo katika eneo hilo, akibainisha kuwa hatua inayofuata ni ujenzi wa Kituo cha Afya ili kuendelea kuboresha huduma kwa wananchi.

    Diwani wa Kata ya Nditi, Castory Joseph Mtonga, alisema awali zahanati hiyo ilikuwa na chumba kimoja pekee, hali iliyosababisha ukosefu wa faragha kwa akina mama wakati wa kujifungua na kupata huduma nyingine za uzazi.

    Alisema kukamilika kwa jengo hilo jipya kutawawezesha wanawake kujifungua katika mazingira salama na yenye staha, huku akiishukuru Serikali kwa mchango wake katika kufanikisha mradi huo.

    Wananchi Aisha Abdallah Hassani na Shabani Omari Juma walisema ujenzi wa Jengo la Mama na Mtoto utasaidia kumaliza changamoto ya akina mama kuchanganywa na wagonjwa wengine katika chumba kimoja, hali iliyokuwa ikikosesha faragha wakati wa kupata huduma za uzazi.

    Walisema kukamilika kwa ujenzi huo kutaongeza ubora wa huduma za afya na hadhi ya huduma za uzazi katika eneo hilo.

    Aidha, wananchi hao waliiomba Serikali kuendelea kuiboresha zahanati hiyo kwa kuipatia vifaa tiba muhimu, ili waweze kupata huduma zote za msingi katika kijiji chao badala ya kulazimika kusafiri umbali mrefu kufuata huduma katika Hospitali ya Mnero.

  • Jarida hili Maalum la Mafanikio ya Mradi wa HEET OUT limeangazia safari ya mageuzi, mafanikio makubwa, na athari chanya za uwekezaji wa Mradi wa Higher Education for Economic Transformation (HEET) katika Chuo Kikuu Huria cha Tanzania.

    Jarida hili linaonesha hatua zilizofikiwa katika ujenzi wa miundombinu ya kisasa, kuimarisha ubora wa elimu, kukuza utafiti na ubunifu.

    Karibu usome na ujionee jinsi HEET inavyoendelea kuleta mabadiliko chanya katika elimu ya juu nchini Tanzania.

    ← Back

    Thank you for your response. ✨

    Drag and drop or click to select a file.

  • Na Farida Mkumba, Dodoma

    Wananchi wa vijijini wanatarajiwa kuanza kunufaika na mfumo mpya wa mita za maji za malipo kabla (prepaid), unaolenga kuondoa kero ya bili kubwa za maji na kuwapa watumiaji uhuru wa kutumia maji kulingana na kiasi cha fedha walicholipia.

    Akizungumza wakati wa Maonesho ya Nane Nane yaliyofanyika katika Viwanja vya John Samuel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma, Afisa Habari na Masoko wa RUWASA, Haji Athumani Msovu, alisema mfumo huo unafanya kazi kwa utaratibu unaofanana na mita za umeme za LUKU, ambapo mtumiaji hulipia huduma ya maji kabla kwa kiasi anachokihitaji.

    Alisema teknolojia hiyo italeta uwazi zaidi katika utoaji wa huduma za maji, kwani kila mtumiaji atatumia maji kulingana na kiasi cha fedha alicholipa, hivyo kuondoa malalamiko yanayotokana na bili zisizoeleweka.

    Msovu alisema uwekaji wa mita hizo tayari umeanza katika baadhi ya Vyombo vya Usimamizi wa Huduma za Maji vya Kijamii (CBWSO) katika mikoa mbalimbali, na kwamba mrejesho wa awali kutoka kwa wananchi umeonyesha kuridhishwa na mfumo huo.

    Alieleza kuwa RUWASA imesaini mkataba na Chuo cha Ufundi Arusha (ATC) kwa ajili ya kutengeneza mita hizo hapa nchini. Baada ya majaribio yaliyofanyika, alisema mita zilizotengenezwa na ATC zimeonyesha ufanisi mkubwa na tayari zimeanza kusambazwa katika baadhi ya mikoa inayohudumiwa na RUWASA.

    Kwa mujibu wa Msovu, ushirikiano huo utawezesha CBWSO na Mamlaka za Maji kununua mita hizo moja kwa moja kutoka ATC kulingana na bajeti na mahitaji yao, hatua itakayorahisisha upatikanaji wa vifaa hivyo.

    Aidha, alisema mita hizo zimetengenezwa kwa plastiki maalumu isiyoshambuliwa na kutu, jambo linalozifanya zifae hata katika maeneo yenye maji yenye kiwango kikubwa cha chumvi. Aliongeza kuwa teknolojia hiyo itasaidia kupunguza uharibifu wa mita na gharama za matengenezo.

    Msovu alisema RUWASA itaendelea kupokea maoni kutoka kwa wananchi ili kuboresha zaidi mfumo huo na kuhakikisha unatoa huduma bora na yenye ufanisi katika maeneo yote utakakotekelezwa nchini.

  • Na Juma John Elisha

    Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimetangaza kuwa shauri la madai namba 14864, linalohusu mgawanyo wa mali za chama pamoja na maombi ya zuio dhidi yake, litatajwa kesho Jumatano, Agosti 5, 2026, saa 5:00 asubuhi katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, mbele ya Jaji Awamu Mbagwa.

    Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uenezi wa CHADEMA, Brenda Rupia, shauri hilo lililofunguliwa na Saidi Issa Mohammed na Ahmed Rashid Khamis linafikia hatua ya kutajwa baada ya kukamilika kwa majibizano ya kisheria kwa njia ya maandishi kati ya pande zote zinazohusika.

    Katika taarifa hiyo, CHADEMA imewahimiza wanachama wake, wafuasi, wadau wa demokrasia pamoja na waandishi wa habari kujitokeza mahakamani kufuatilia mwenendo wa shauri hilo, ikisisitiza umuhimu wa umma kushuhudia hatua za mchakato wa kesi hiyo.

    Kwa mujibu wa taratibu za mahakama, kutajwa kwa shauri ni hatua ya awali ya mchakato wa kesi ambapo mahakama hutoa maelekezo kuhusu hatua zinazofuata, ikiwemo ratiba ya usikilizwaji au masuala mengine ya kiutaratibu. Hivyo, kesho mahakama inatarajiwa kutoa maelekezo yatakayofuata kuhusu mwenendo wa shauri hilo.