• Na Andrea Mlwafu

    Maji yanapoanza kuongezeka katika mito inayopita wilayani Kilosa mkoani Morogoro, hali ya kawaida ya maisha hubadilika taratibu. Hofu huanza kutawala miongoni mwa wakazi, hasa wale wanaoishi karibu na maeneo yanayokumbwa na mafuriko.

    Familia huanza kuhamisha vitu muhimu, wakulima hutazama mashamba yao kwa wasiwasi, huku wengine wakianza kutafuta maeneo salama ya kukimbilia kabla maji hayajafika kwenye nyumba zao.

    Kwa baadhi ya wananchi, hali hii si jambo jipya tena, bali ni maisha ambayo yamekuwa yakijirudia kila msimu wa mvua unapofika.

    Mwishoni mwa Desemba 2025, mvua kubwa ilisababisha mafuriko katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Kilosa, yakiwemo Kijiji cha Tindiga. Taarifa za tathmini ya athari za mafuriko zinaonesha kuwa maelfu ya wananchi waliathirika, huku nyumba, mashamba, barabara na vyanzo vya kipato vikikumbwa na uharibifu.

    Kwa mujibu wa taarifa ya Shirikisho la Kimataifa la Msalaba Mwekundu na Hilali Nyekundu, watu 5,045 kutoka kaya 1,009 waliathirika katika tukio hilo, hali iliyosababisha usumbufu mkubwa wa maisha na huduma muhimu.

    Lakini nyuma ya takwimu hizo kuna maisha ya watu ambao kila siku wanajaribu kujenga kesho yao. Kuna mkulima aliyepoteza mazao aliyokuwa akitegemea kwa ajili ya chakula na kipato, kijana aliyepoteza zana za kilimo, mfanyabiashara ambaye biashara yake ilisimama kutokana na kuharibika kwa barabara na familia iliyolazimika kuondoka katika makazi yake.

    Kwa mtazamo huo, mafuriko ya Kilosa hayawezi kuangaliwa kama tukio la maji kujaa pekee, bali ni changamoto inayogusa moja kwa moja maisha, uchumi, afya na matumaini ya wananchi.

    Mafuriko Yanapogusa Chanzo cha Maisha

    Kwa wakazi wengi wa Kilosa, kilimo ni sehemu muhimu ya maisha. Ni chanzo cha chakula, kipato na uwezo wa familia kugharamia mahitaji mbalimbali. Mvua inapokuwa kubwa na mito kufurika, athari zake huingia moja kwa moja katika mfumo huo wa maisha kwa sababu mashamba yanaweza kujaa maji, mazao kuharibika na zana za kilimo kusombwa.

    Hata baada ya maji kupungua, mkulima anaweza kubaki na ardhi ambayo haiwezi kuzalisha mara moja na familia ambayo haina uhakika wa chakula au kipato cha kuanzia upya.

    Ripoti iliyotolewa na ENHANCE Tanzania baada ya mazungumzo na vijana wa Tindiga inaonyesha kuwa mafuriko yaliyotokea Desemba 2025 yaliathiri mazao, mifugo, zana za kilimo na vyanzo vingine vya kipato.

    Uharibifu wa barabara nao ulifanya upatikanaji wa masoko kuwa mgumu, jambo lililoongeza changamoto kwa wananchi ambao tayari walikuwa wamepoteza sehemu ya mali na uzalishaji wao.

    Hali hii inaonyesha kwamba madhara ya mafuriko hayaishii wakati maji yanapokuwa juu. Maji yanaposhuka, ndipo baadhi ya familia huanza kukabiliana na gharama halisi za janga.

    Mkulima anaanza kuhesabu mazao aliyopoteza, mfanyabiashara anatafuta mtaji wa kuanza tena na familia iliyohama inaanza kutafuta namna ya kujenga upya maisha katika eneo salama.

    Kwa hiyo, mafuriko yanapogeuka kuwa tukio linalojirudia, swali kubwa linakuwa si namna ya kuwaokoa wananchi siku ya janga pekee, bali namna ya kuwasaidia wasirudi katika mazingira yale yale yanayowafanya waathirike tena.

    Vijana: Tunataka Kujenga Upya Maisha

    Miongoni mwa watu wanaobeba sehemu kubwa ya athari za mafuriko ni vijana ambao tayari wanakabiliwa na changamoto za ajira, kipato na kujenga maisha yao.

    Vijana wa Tindiga walieleza kuwa mafuriko hayakuathiri tu mali na shughuli zao za kiuchumi, bali pia yaliathiri afya, ustawi wa akili, matarajio yao na uwezo wao wa kusaidia familia zao.

    Baadhi yao walikabiliwa na kupoteza vyanzo vya kipato wakati bado wanajaribu kujijenga kiuchumi.

    Katika mazungumzo hayo, vijana waliweka wazi hitaji lao la kupata mazingira salama ya kuanzia upya. Kwa tafsiri ya kauli yao kutoka katika chanzo cha awali, walisema: “Tunataka kujenga upya maisha yetu, lakini tunahitaji ardhi salama na mahali ambapo tunaweza kuanza tena.”

    Kauli hii inaonyesha kwamba kwa waathirika wa mafuriko, msaada wa muda mfupi pekee hauwezi kumaliza changamoto zinazobaki baada ya janga.

    Mtu anaweza kupewa chakula au mahali pa kulala kwa siku chache, lakini bado akawa hana shamba, mtaji, zana za kazi au mazingira salama ya kujenga maisha ya muda mrefu.

    Ndiyo maana vijana hao wameeleza umuhimu wa kupata makazi na maeneo ya kilimo yaliyo salama, fursa za kujipatia kipato, mafunzo ya ujuzi na kushirikishwa katika maamuzi yanayohusu maendeleo ya jamii zao.

    Hapa ndipo suala la vijana linapounganishwa na mjadala mpana wa kukabiliana na majanga. Vijana si waathirika pekee wanaohitaji msaada, bali wanaweza pia kuwa sehemu ya suluhisho endapo watapewa maarifa, ujuzi, nafasi ya kushiriki na rasilimali za kujenga upya maisha yao.

    Tahadhari Ya Mapema Inaweza Kuokoa Maisha

    Mafuriko hayawezi kuondolewa kabisa, lakini madhara yake yanaweza kupunguzwa ikiwa jamii itapata taarifa sahihi kabla hatari haijafika. Utafiti uliofanywa kuhusu hali ya mwitikio wa tahadhari za mapema za mafuriko katika Wilaya ya Kilosa unaonyesha kuwa taarifa za mapema zina nafasi muhimu katika kuwasaidia wananchi kuchukua hatua kabla hali haijawa mbaya.

    Utafiti huo ulihusisha wakuu wa kaya 375 pamoja na wadau na washiriki wa mijadala ya vikundi kutoka katika jamii.

    Matokeo ya utafiti huo yanaonesha kuwa wananchi hutumia taarifa wanazopata kuhusu mafuriko kufanya maamuzi mbalimbali, ikiwemo kuwatahadharisha wanafamilia, kuhamia maeneo salama na kuandaa namna ya kulinda mali.

    Kwa tafsiri ya kauli ya mshiriki mmoja wa utafiti huo, alieleza kwamba kutokana na uzoefu wake wa kuitikia tahadhari za mafuriko, kuwafahamisha wanafamilia kuhusu ujio wa mafuriko ni jambo muhimu kwa sababu jamii huishi pamoja na kushirikiana katika nyakati za furaha na matatizo.

    Hii inaonyesha kwamba taarifa ya tahadhari inapofika kwa wakati inaweza kuwa na thamani kubwa kuliko inavyoonekana. Familia inaweza kupata muda wa kuwahamisha watoto, wazee na watu wenye mahitaji maalumu, kupeleka mifugo sehemu salama na kuhamisha mali ambazo zinaweza kuokolewa.

    Lakini ili mfumo huo ufanye kazi vizuri, taarifa inapaswa kufika kwa wakati, kueleweka na kuambatana na hatua ambazo wananchi wanapaswa kuchukua.

    Uzoefu wa Kilosa Unavyoonyesha Umuhimu wa Maandalizi

    Utafiti huo pia unaonyesha mabadiliko katika namna jamii ya Kilosa inavyokabiliana na mafuriko ikilinganishwa na vipindi vya nyuma.

    Kwa mujibu wa kauli ya Mratibu wa Maafa wa Wilaya ya Kilosa iliyonukuliwa katika utafiti huo, katika mafuriko ya mwaka 2010 na 2012 idadi ya vifo ilikuwa kubwa kwa sehemu kutokana na udhaifu wa tahadhari za mapema.

    Hata hivyo, alieleza kuwa katika mafuriko ya miaka ya karibuni idadi ya vifo imepungua ikilinganishwa na kipindi ambacho mfumo wa tahadhari haukuwepo kwa kiwango cha kutosha. Kauli hiyo inaonyesha umuhimu wa kuwekeza katika mifumo inayowawezesha wananchi kujua hatari kabla haijafika.

    Changamoto iliyopo ni kwamba tahadhari pekee haitoshi kama wananchi hawana uwezo wa kuitikia. Mwananchi anapoambiwa kuwa mto umejaa au maji yanaelekea katika makazi yake anahitaji pia kujua anakokwenda, njia salama ya kutumia na namna ya kulinda familia yake.

    Hivyo, maandalizi ya mafuriko yanahitaji zaidi ya ujumbe wa tahadhari; yanahitaji mipango ya uokoaji, maeneo salama, mafunzo kwa jamii na ushirikiano kati ya wananchi na mamlaka za eneo.

    Serikali: Mazingira ni Sehemu ya Suluhisho

    Wakati wataalamu wakisisitiza umuhimu wa tahadhari za mapema, Serikali inaangalia namna mazingira yanavyohusiana na changamoto ya mafuriko.

    Januari 2, 2026, Naibu Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Festo Dugange, alifika Tindiga wilayani Kilosa baada ya mafuriko na kuzungumzia umuhimu wa kuimarisha usimamizi wa mazingira pamoja na kuongeza kasi ya upandaji miti.

    “Ukweli ni kwamba bado kasi ya upandaji wa miti inahitajika,” alisema Dkt. Dugange: akieleza pia kuwa kina kifupi cha mito ni miongoni mwa sababu zilizochangia maji kuingia katika makazi ya wananchi wakati wa mvua kubwa.

    Alieleza kuwa mafuriko yamesababisha madhara katika maisha ya watu, miundombinu, kilimo, vituo vya huduma na makazi.

    Kauli hiyo inaongeza upande mwingine katika mjadala wa mafuriko ya Kilosa. Mvua inaponyesha kwa wingi, uwezo wa mito na mazingira yanayozunguka mito kubeba na kuelekeza maji unakuwa muhimu.

    Hivyo, kukabiliana na mafuriko kunahitaji kuangalia si tukio la siku hiyo pekee, bali pia namna ardhi inavyotumika, hali ya misitu na vyanzo vya maji, pamoja na usimamizi wa maeneo ambayo yanaweza kuwa hatarini wakati wa mvua kubwa.

    Baada ya Maji Kushuka, Kazi Ndiyo Inaanza

    Mara nyingi mafuriko huonekana zaidi wakati maji yakiwa yamejaa katika nyumba, barabara na mashamba. Kamera huonyesha maji yaliyofunika maeneo ya makazi na magari yakishindwa kupita.

    Lakini baada ya maji kushuka, kamera hizo huwa hazionyeshi kila kitu. Hapo ndipo familia huanza kuhesabu hasara, kuondoa matope ndani ya nyumba, kutafuta chakula, kurekebisha makazi na kufikiria namna ya kupata kipato tena.

    Kwa kijana ambaye amepoteza zana za kilimo, biashara au mali aliyokuwa akitegemea, kurejea katika hali ya kawaida kunaweza kuchukua muda mrefu. ENHANCE Tanzania ilibaini kuwa baadhi ya vijana wa Tindiga walieleza athari za mafuriko katika ustawi wao wa akili, matarajio yao na uwezo wao wa kuendelea na shughuli za maisha.

    Hii inaonyesha kuwa kurejesha maisha baada ya janga kunahitaji kuangalia pia mahitaji yasiyoonekana kwa macho, yakiwemo ustawi wa kisaikolojia, fursa za kipato na matumaini la baadaye.

    Kwa mantiki hiyo, msaada wa baada ya mafuriko unapaswa kwenda zaidi ya chakula, maji na vifaa vya dharura. Msaada huo unaweza kuwa na nguvu zaidi unapounganishwa na zana za kilimo, mafunzo ya ujuzi, mitaji midogo, maeneo salama ya makazi na fursa ambazo zinaweza kumsaidia mtu kurejesha chanzo chake cha kipato.

    Hapo ndipo tofauti kati ya kumsaidia mtu kuishi baada ya janga na kumsaidia kujenga upya maisha yake inapojitokeza.

    Kilosa Inahitaji Suluhisho Linalotangulia Mafuriko

    Tukio la mafuriko linapotokea mara moja, jamii inaweza kulichukulia kama janga lisilotarajiwa. Lakini linapojirudia, linapaswa pia kuwa somo la kupanga. Utafiti wa Kilosa unaonyesha umuhimu wa kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema, kuweka vifaa vya kufuatilia hali ya mito, kujenga uwezo wa jamii na kufanya mazoezi ya uokoaji.

    Pia unapendekeza nyumba kujengwa katika maeneo salama na wananchi kupewa elimu kuhusu hatua wanazopaswa kuchukua wanapopata tahadhari.

    Hapa ndipo mjadala wa suluhisho la muda mrefu unapopata maana. Ikiwa familia zinaendelea kuishi katika maeneo hatarishi, mashamba yanaendelea kuwa katika maeneo yanayoweza kufikiwa na maji na miundombinu ya tahadhari haijaenea vya kutosha, kila msimu wa mvua unaweza kuanza kama ukurasa mpya wa tatizo lilelile.

    Badala ya kusubiri mafuriko yatokee ndipo hatua zichukuliwe, maandalizi yanapaswa kuanza wakati maji bado hayajafika.

    Jamii nayo ina nafasi muhimu katika mchakato huo. Wananchi ndio wanaojua maeneo ambayo maji huanza kuingia, njia ambazo huwa hatarishi na watu wanaohitaji msaada wa haraka.

    Ushirikishwaji wao katika mipango ya maafa unaweza kusaidia kufanya mikakati iwe sehemu ya maisha ya kila siku badala ya kubaki kwenye makaratasi ya taasisi.

    Maji Yanaposhuka, Maisha Yasianze Upya Kila Mara

    Kilosa inatukumbusha kwamba mafuriko si suala la maji pekee. Ni suala la makazi, kilimo, afya, kipato, elimu, mazingira na mustakabali wa jamii.

    Ni suala linalomgusa kijana anayepoteza zana zake za kazi, mkulima anayepoteza mavuno, mzazi anayehangaika kurejesha maisha ya familia na mfanyabiashara anayekosa soko baada ya barabara kuharibika.

    Ndiyo maana maandalizi yanapaswa kwenda sambamba na uokoaji. Tahadhari za mapema zinapaswa kuwafikia wananchi kwa wakati, mazingira na vyanzo vya maji vilindwe, maeneo hatarishi yatambuliwe na jamii ipewe uwezo wa kuchukua hatua.

    Wakati huohuo, baada ya mafuriko, waathirika wanahitaji msaada unaowawezesha kurejesha maisha yao na si msaada wa muda mfupi unaomalizika kabla hawajapata nafasi ya kusimama tena.

    Kwa vijana wa Kilosa, ujumbe ni wazi: hawataki kuendelea kuwa watu wanaosubiri maji yapungue kila mwaka ili waanze tena.

    Wanataka ardhi salama, fursa za kipato, ujuzi na nafasi ya kushiriki katika maamuzi yanayohusu maisha yao. Sauti hiyo inafanya mafuriko kuwa mjadala mpana zaidi kuhusu aina ya jamii ambayo inaweza kuishi na hatari bila kupoteza kabisa uwezo wa kujijenga.

    Kwa sababu maji yanaposhuka haimaanishi kwamba tatizo limekwisha. Kwa familia iliyopoteza nyumba, mkulima aliyepoteza mazao au kijana aliyepoteza chanzo cha kipato, hapo ndipo safari ya kuanza upya inaanza.

    Kilosa haihitaji tu kujua namna ya kuokoa watu wakati maji yanapanda; inahitaji pia kuhakikisha kwamba maji yanaposhuka, wananchi wana nafasi ya kusimama tena, kujenga maisha yao na kutazama kesho bila hofu ya kurudia kila kitu walichopoteza.

    Mafuriko yanaweza kuwa sehemu ya changamoto ya mazingira, lakini namna jamii inavyojiandaa, inavyoitikia na inavyorejesha maisha baada ya janga ndiyo inayoweza kuamua kama kila msimu wa mvua utakuwa mwanzo wa hasara nyingine au mwanzo wa jamii yenye uwezo mkubwa zaidi wa kustahimili.

  • Na George Gabriel

    Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Edward Magala, amemtaka mkandarasi anayetekeleza mradi wa ujenzi wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu kuongeza kasi ya ujenzi ili kuhakikisha mradi huo unakamilika ndani ya muda uliowekwa katika mkataba.

    Magala alitoa agizo hilo hivi karibuni wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo katika ziara iliyohudhuriwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri pamoja na Timu ya Menejimenti ya Halmashauri.

    Alisema Serikali imetenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo, hivyo mkandarasi anapaswa kuongeza nguvu kazi, vifaa na muda wa kufanya kazi ili kuongeza kasi ya ujenzi na kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.

    Magala aliiagiza kampuni ya SARO Builders Limited, inayotekeleza awamu ya kwanza ya mradi huo, kuzingatia masharti ya mkataba uliosainiwa Aprili 27, 2026, pamoja na kuhakikisha kazi zote zinatekelezwa kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.

    Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Ibrahimu Mwanauta, alisema Halmashauri itaendelea kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa mradi huo ili kuhakikisha mkandarasi anazingatia masharti ya mkataba, ubora wa kazi na muda uliopangwa.

    Alisema uongozi wa Halmashauri umejipanga kuhakikisha changamoto zinazoweza kujitokeza katika utekelezaji wa mradi zinatatuliwa kwa wakati, akisisitiza kuwa ujenzi wa jengo hilo ni muhimu katika kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma za kiutawala kwa wananchi wa Nanyumbu.

    Mradi wa ujenzi wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu una thamani ya Shilingi bilioni 3.6, ambapo Serikali Kuu tayari imetoa Sh bilioni moja kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya kwanza ya mradi huo.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Saa nne usiku, wakati familia nyingi jijini Dar es Salaam zimejisitiri majumbani baada ya shughuli za siku, kwa wengine ndipo siku ya kazi inaanza.

    Taa za vibanda vya chakula zinawaka. Bodaboda na magari ya usafiri wa mtandaoni yanaendelea kuzunguka. Wafanyakazi wa hoteli wanaingia au kuendelea na zamu zao, walinzi wanakesha kwenye malango, huku wafanyabiashara wadogo wakiwahudumia wateja.

    Kwa baadhi ya watu, mji unapokuwa kimya, kwa wengine ndipo unapokuwa hai zaidi.

    Hawa ni miongoni mwa vijana wanaotumia saa za usiku kutafuta kipato, kulipa kodi, kusaidia familia na kujijengea maisha katika mazingira ambayo ajira rasmi si rahisi kupatikana.

    Kwao, usiku si muda wa kusubiri kesho. Ni sehemu ya mapambano ya kuhakikisha kesho inakuwa bora.

    Usiku Unapogeuzwa kuwa Fursa ya Kipato

    Uchumi wa usiku unapozungumziwa, wengi hufikiria baa, kumbi za burudani na muziki. Lakini nyuma ya taswira hiyo kuna shughuli nyingi zinazowawezesha watu kupata kipato.

    Kuna wauzaji wa chakula wanaofungua biashara zao jioni kwa sababu ndipo wanapopata wateja wengi. Kuna madereva wa bodaboda na usafiri wa mtandaoni wanaosubiri abiria wanaotoka kazini au kwenye maeneo ya burudani.

    Kuna walinzi wanaoanza zamu wakati wengine wanarudi majumbani. Wapo pia wafanyakazi wa hoteli, hospitali na huduma nyingine muhimu wanaoendelea kufanya kazi wakati wengi wamekwisha pumzika.

    Uchumi huu huunda mnyororo mpana wa kipato. Mteja anayenunua chakula anamwingizia muuzaji fedha. Muuzaji huyo hununua bidhaa kutoka kwa wasambazaji, huku dereva anayempeleka mteja nyumbani naye akipata kipato.

    Kwa hiyo, kadiri shughuli za usiku zinavyoongezeka, ndivyo fedha zinavyoendelea kuzunguka katika mikono ya watu mbalimbali.

    Ripoti mbalimbali kuhusu shughuli za usiku jijini Dar es Salaam zimewahi kuonesha kuwa biashara za chakula, usafiri na huduma nyingine huendelea kuwa chanzo muhimu cha kipato kwa wafanyabiashara na wafanyakazi wengi, licha ya changamoto za usalama na miundombinu.

    Kwa Vijana, Usiku Si Burudani Pekee

    Kwa vijana wengi wanaokabiliana na ushindani mkubwa katika soko la ajira, kufanya kazi usiku kunaweza kuwa njia ya kujiajiri na kujitengenezea kipato.

    Kijana asiye na ajira rasmi anaweza kuamua kuendesha bodaboda, kufanya usafiri wa mtandaoni, kuuza chakula au kujihusisha na shughuli nyingine zinazoweza kumwingizia kipato.

    Huenda kazi hiyo isiwe na ofisi, sare wala muda maalumu wa kuingia na kutoka, lakini kwa mhusika inaweza kuwa chanzo kikuu cha maisha.

    Baadhi ya madereva huchagua kufanya kazi zaidi wakati wa usiku kutokana na uwepo wa abiria wanaotoka kwenye maeneo ya biashara na burudani. Vivyo hivyo, wauzaji wa chakula huona muda wa jioni na usiku kama sehemu muhimu ya biashara zao.

    Dereva wa usafiri wa mtandaoni, Jumanne Abdallah, anaeleza kuwa maeneo yenye shughuli nyingi za burudani ni miongoni mwa sehemu zinazoweza kuwapatia madereva abiria.

    Kwa mtazamo wake, hatua zinazopunguza shughuli katika maeneo hayo zinaweza pia kuwa na athari kwa watu wengine wanaotegemea wateja wanaozalishwa na biashara hizo.

    Hii inaonesha kuwa biashara ya usiku hainufaishi mwenye biashara pekee. Inaweza kumgusa dereva, mhudumu, mlinzi, mpishi, muuzaji wa bidhaa na watu wengine wengi wanaohudumia shughuli hizo.

    Uchumi wa Usiku Unapogongana na Maisha ya Wakazi

    Pamoja na fursa zinazotokana na shughuli za usiku, kuna upande mwingine ambao hauwezi kupuuzwa.

    Kadiri biashara zinavyoongezeka na kuendelea hadi usiku wa manane, malalamiko kuhusu kelele, usalama na usumbufu kwa wakazi nayo yanaweza kuongezeka katika baadhi ya maeneo.

    Hapo ndipo changamoto kubwa inapojitokeza: jinsi ya kuendeleza shughuli za kiuchumi bila kuharibu utulivu wa watu wanaoishi karibu na maeneo hayo.

    Mjadala kuhusu biashara zinazofanyika kwa muda mrefu jijini Dar es Salaam umekuwa ukiutaja umuhimu wa kupanga maeneo, kuboresha miundombinu na kuweka kanuni zinazoweza kuruhusu shughuli za kiuchumi kuendelea bila kuhatarisha usalama na maisha ya wakazi.

    Hivyo, swali kubwa linabaki:

    Je, inawezekana kuwa na uchumi wenye nguvu wa usiku bila kuvuruga usingizi na maisha ya wakazi?

    Jibu lake haliwezi kuwa kufunga kila biashara, wala kuacha kila shughuli iendelee bila mipaka.

    Kinachohitajika ni mipango.

    Kelele: Bei Ambayo Wakazi Wanaweza Kulipa

    Kwa watu wanaoishi karibu na maeneo yenye shughuli nyingi za usiku, kelele si jambo dogo.

    Muziki mkubwa, magari, watu na shughuli nyingine zinaweza kuendelea wakati ambapo wengine wanahitaji kupumzika. Tatizo linapokuwa la kila siku, linaweza kuathiri ubora wa maisha ya wakazi.

    Hii ndiyo sababu afya na utulivu wa jamii vinapaswa kuwa sehemu ya mjadala wa uchumi wa usiku.

    Si kila kelele ni ishara ya biashara yenye mafanikio, na si kila biashara inayofanyika usiku inapaswa kuonekana kama tatizo.

    Changamoto ni kuhakikisha shughuli hizo zinaendeshwa kwa kuzingatia sheria, viwango vinavyokubalika na haki za watu wengine.

    Mji Unaofanya Kazi Usiku Unahitaji Usalama

    Uchumi wa usiku hauwezi kukua bila usalama.

    Mfanyakazi anayemaliza kazi saa saba usiku anahitaji kuwa na uhakika kwamba anaweza kufika nyumbani salama. Dereva anayesafirisha abiria anahitaji kufanya kazi katika mazingira salama.

    Mfanyabiashara anayefunga kibanda chake alfajiri anahitaji kujua kuwa anaweza kubeba fedha na bidhaa zake bila kuwa shabaha ya wahalifu.

    Kwa hiyo, kuzungumzia uchumi wa usiku ni pia kuzungumzia uwepo wa ulinzi, mwanga wa kutosha na mazingira yanayowapa watu ujasiri wa kufanya kazi hata baada ya jua kuzama.

    Changamoto za giza, uhalifu na uhaba wa miundombinu zimewahi kutajwa miongoni mwa vikwazo vinavyoweza kudhoofisha shughuli za kiuchumi za usiku jijini Dar es Salaam.

    Miundombinu Nayo Ina Nafasi Kubwa

    Barabara zenye mwanga hafifu, maeneo yasiyo na usafiri wa uhakika na vituo vya biashara visivyopangiliwa vinaweza kuwafanya watu wengi kuogopa kufanya kazi usiku.

    Kwa hiyo, kuzungumzia uchumi wa usiku ni pia kuzungumzia taa za barabarani, usafiri, ulinzi, usafi wa mazingira na mipango ya miji.

    Mjadala wa kuifanya Dar es Salaam kuwa jiji lenye shughuli za saa 24 umewahi kuhusisha mahitaji ya kuboresha miundombinu, usafiri wa umma, huduma za fedha na usalama.

    Bila maandalizi hayo, wazo la jiji linalofanya kazi usiku na mchana linaweza kubaki kuwa zuri kwenye karatasi, lakini gumu kutekelezeka kwa vitendo.

    Je, Dar es Salaam Inaweza Kuwa Jiji la Saa 24?

    Dhana ya jiji linalofanya kazi saa 24 imejadiliwa kwa muda mrefu, hasa kutokana na mahitaji ya kuongeza shughuli za kiuchumi na kutoa nafasi zaidi kwa watu kufanya biashara na kupata huduma.

    Lakini wazo la jiji la saa 24 halimaanishi kwamba kila biashara lazima ifunguliwe usiku na mchana.

    Badala yake, linaweza kumaanisha kuweka mazingira wezeshi yatakayoruhusu huduma muhimu na biashara zinazohitaji kufanya kazi kwa muda mrefu kuendelea kwa usalama na kwa kuzingatia sheria.

    Maeneo ya biashara kama Kariakoo yamekuwa sehemu ya mjadala kuhusu uwezekano wa kuongeza muda wa shughuli za kibiashara.

    Wafuasi wa wazo hilo wanaamini kuwa kuongeza muda wa biashara kunaweza kupanua fursa za kiuchumi na kupunguza msongamano wa shughuli zinazolundikana wakati wa mchana.

    Hata hivyo, hilo haliwezi kufanikiwa bila maandalizi ya kutosha.

    Jiji linalokusudia kuwa na shughuli nyingi usiku linahitaji usafiri wa uhakika, mwanga wa kutosha, usalama, huduma za afya, usafi wa mazingira na kanuni zinazoeleweka kwa wafanyabiashara na wakazi.

    Nyuma ya Biashara Kuna Familia

    Kuna jambo ambalo mara nyingi hupotea katika mjadala huu: nyuma ya kila biashara kuna maisha ya mtu.

    Muuza chipsi anayefanya kazi hadi usiku wa manane huenda ana watoto wanaohitaji ada. Dereva anayefanya safari za usiku anaweza kuwa anatafuta fedha za kodi. Mlinzi anayekesha kwenye lango hadi asubuhi huenda ndiye tegemeo kuu la familia yake.

    Kwao, kazi ya usiku si starehe.

    Ni sehemu ya mapambano ya kuhakikisha mahitaji ya familia yanapatikana.

    Na kwa vijana ambao bado hawajapata nafasi katika ajira rasmi, shughuli hizi zinaweza kuwa daraja la kuanza maisha.

    Ndiyo maana suluhisho si kuutazama uchumi wa usiku kama tatizo linalopaswa kuondolewa, wala kuuruhusu ukue bila mipaka.

    Kinachohitajika ni kuutambua, kuupanga na kuuweka katika mazingira yatakayoweza kunufaisha jamii kwa ujumla.

    Kati ya Fursa na Wajibu

    Dar es Salaam inavyoendelea kukua, uchumi wake wa usiku nao unaweza kuendelea kupanuka.

    Lakini ukuaji huo lazima uende sambamba na uwajibikaji.

    Serikali na mamlaka husika zina wajibu wa kuhakikisha maeneo ya biashara yanapangwa vizuri, sheria zinatekelezwa, usalama unaimarishwa na wakazi wanalindwa dhidi ya usumbufu usio wa lazima.

    Wafanyabiashara nao wana wajibu wa kuheshimu sheria, kudhibiti kelele na kuhakikisha shughuli zao haziweki maisha ya wengine hatarini.

    Kwa upande mwingine, watu wanaofanya kazi usiku wanahitaji kutambuliwa kama sehemu muhimu ya nguvu kazi inayochangia uchumi wa jiji.

    Kwa sababu ukweli ni kwamba Dar es Salaam tayari haifanyi kazi mchana pekee.

    Wakati wengine wamelala, wengine wanaendesha bodaboda.

    Wakati baadhi ya wafanyabiashara wamefunga milango, wengine wanafungua vibanda vyao.

    Wakati familia nyingi zimezima taa, kuna mlinzi anayekesha.

    Huo ndio uso mwingine wa Dar es Salaam.

    Jiji ambalo usiku hauashirii mwisho wa shughuli, bali mwanzo wa siku nyingine kwa watu wanaotafuta maisha.

    Usiku si Mwisho, ni Mwanzo wa Kesho

    Kwa maelfu ya vijana wanaofanya kazi usiku, giza linaposhuka si ishara ya kufunga siku, bali mwanzo wa safari nyingine ya kutafuta kipato, kuhudumia familia na kujenga maisha.

    Wakati wengine wakiwa majumbani wakipumzika, wao huingia barabarani, sokoni, kwenye migahawa, hoteli, vituo vya usafiri na maeneo mengine ya biashara wakisaka fursa ambazo huenda wasingeweza kuzipata mchana.

    Lakini uchumi wa usiku hauwezi kukua kwa nguvu ya watu wanaofanya kazi pekee.

    Unahitaji mazingira yenye ulinzi na usalama, usafiri wa uhakika, mwanga wa barabarani, miundombinu bora, kanuni zinazoeleweka na utekelezaji unaozingatia maslahi ya wafanyabiashara, wafanyakazi na wakazi kwa pamoja.

    Maana yake ni kwamba mjadala wa kuifanya Dar es Salaam kuwa jiji lenye shughuli za saa 24 haupaswi kuishia kwenye burudani.

    Unapaswa pia kuangalia maisha ya wale ambao usiku ndiyo muda wao wa kuzalisha.

    Dar es Salaam inapokua, swali si kama watu wataendelea kufanya kazi usiku, kwa sababu tayari wanafanya hivyo.

    Swali kubwa ni kama jiji litaweka mazingira yatakayofanya uchumi huo uwe salama, wenye tija na wenye manufaa kwa wote.

    Kwao, usiku si mwisho wa siku.

    Ni muda wa kutafuta kesho

    Na kama usiku ni mchana wa maisha yao, basi ni wakati wa jiji kuanza kuutambua, kuupanga na kuuwekeza kama sehemu muhimu ya uchumi wake.

  • Na Mwandishi Wetu, China

    Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Dkt. Pius Chaya, amewataka wawekezaji kutoka China kuja kuwekeza nchini Tanzania katika uzalishaji wa dawa na vifaa tiba.

    Dkt. Chaya alitoa wito huo jana nchini China, ambako yupo katika ziara ya kutangaza fursa za uwekezaji zinazopatikana nchini Tanzania.

    Katika ziara hiyo, aliambatana na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, na walitembelea kiwanda cha Yiling Pharmaceutical Company Limited, ambako walijionea teknolojia na mifumo mbalimbali ya kisasa inayotumika katika uzalishaji wa dawa.

    Dkt. Chaya alisema Tanzania ina mazingira wezeshi na rafiki kwa uwekezaji wa muda mrefu, huku Serikali ikiendelea kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini.

    Alisema uwekezaji katika uzalishaji wa dawa nchini utaimarisha upatikanaji wa bidhaa za afya, sambamba na kuongeza ajira, ujuzi, teknolojia na fursa za biashara kwa Watanzania.

    Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za Tanzania kutumia diplomasia ya uwekezaji kuvutia mitaji na teknolojia kutoka China, ikiwa ni hatua inayolenga kukuza uzalishaji wa ndani na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

  • Na Andrea Mbona, Haydom, Mbulu

    Wahitimu wa darasa la saba katika Shule ya Msingi Haydom, mkoani Manyara, wametakiwa kutojiunga na makundi ya kihalifu na makundi rika ya mitaani yanayojihusisha na vitendo vya kihalifu kwa kuwa yatasababisha kuathiri ndoto zao za maisha.

    Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Kituo cha Polisi Msaidizi cha Haydom, Mkaguzi Alex Malimbwi, wakati akitoa nasaha kwa wahitimu hao baada ya kuhitimu elimu ya msingi.

    Malimbwi alisema makundi rika ya mitaani yanaweza kuwa chanzo cha matukio mbalimbali ya kihalifu katika jamii, hivyo kuwasa wahitimu hao kuwa makini na marafiki wanaochagua ili kuepuka mazingira yanayoweza kuwapeleka kwenye vitendo vya uhalifu.

    “Ninatamani mtambue kuwa uhalifu hauna nafasi katika jamii na endapo mtajiingiza katika vitendo hivyo mtaua ndoto zenu, ikiwemo kutoendelea na masomo,” alisema Malimbwi.

    Aidha, alisema wazazi na walezi wana wajibu wa kuwafundisha, kuwaongoza na kuwalinda watoto wanaporejea majumbani, huku akiwataka kuwashirikisha katika shughuli mbalimbali za kijamii na uzalishaji, ikiwemo kilimo na ufugaji.

    Alisema ushiriki wa watoto katika shughuli hizo unaweza kuwajenga katika misingi ya uwajibikaji hivyo kupunguza muda wa kujihusisha na makundi au matukio ya kihalifu.

    Akizungumza kwa niaba ya wahitimu wenzake, Marselina Bahha alishukuru kwa nasaha hizo, akisema zitawasaidia kutambua wajibu wao katika jamii na kuendelea kufuata njia sahihi wanapoanza hatua nyingine ya maisha.

    “Tunashukuru kwa nasaha zako, tunaamini zitatukumbusha wajibu wetu katika jamii ili kuhakikisha tunakuwa raia wema na wanaokubalika baada ya kuhitimu masomo ya elimu ya msingi,” alisema Marselina.

    Kwa upande wake, mzazi Paskali Lohay alilishukuru Jeshi la Polisi kwa kutoa elimu kwa jamii na kuomba liendelee kutoa elimu kuhusu madhara ya uhalifu kwa makundi mbalimbali, hususan watoto na vijana.

    Alisema elimu hiyo ni muhimu katika kusaidia kujenga jamii inayozingatia amani, upendo, uwajibikaji na maendeleo.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Katika jamii nyingi, mwanaume hukua akifundishwa kuwa imara, kuvumilia changamoto na kutokuonyesha udhaifu mbele ya wengine. Kauli kama “Wewe ni mwanaume,” “Usilie,” au “Vumilia tu” zimekuwa sehemu ya malezi ya wavulana na wanaume.

    Lakini nyuma ya maneno hayo kuna swali ambalo mara nyingi halizungumzwi: Mwanaume anapokuwa na maumivu, msongo au matatizo, anamweleza nani?

    Matarajio hayo yanaweza kumfanya mwanaume aamini kuwa kuomba msaada ni ishara ya udhaifu, hivyo kuchagua kubeba matatizo yake kimyakimya.

    Hali hiyo imeendelea kuibua mjadala kuhusu namna jamii inavyomfundisha mwanaume maana ya kuwa “mwanaume halisi” na madhara yanayoweza kujitokeza pale hisia zinapofichwa kwa muda mrefu.

    Utafiti uliofanyika Tanzania kuhusu afya ya akili ya akina baba mjini Mwanza umebaini kuwa takribani akina baba wote waliohusishwa katika utafiti huo walieleza kuwa jukumu lao kuu ni kuwa watoa mahitaji ya familia. Hata hivyo, ukosefu wa ajira na kipato kidogo ulihusishwa na msongo wa kiuchumi, huku baadhi ya wanaume wakihusisha uwezo wa kuitunza familia na uthibitisho wa uanaume wao.

    MWANAUME ANAPOFUNDISHWA KUTOKUONESHA HISIA

    Michael Baruti, mwandishi wa habari wa Tanzania ambaye ameendesha mazungumzo kuhusu afya ya akili ya wanaume kupitia vipindi vyake mtandaoni, amesema jamii imekuwa ikiwafundisha wanaume kwamba hawapaswi kulia wala kuonyesha hisia.

    “Jamii yetu inatuambia kwamba wanaume hawapaswi kulia. Hawapaswi kufunguka na kuwa na hisia,” alisema Baruti.

    Baruti alisema changamoto hiyo ilimfanya aanzishe mazungumzo kuhusu afya ya akili ya wanaume baada ya kupitia mwenyewe kipindi kigumu kilichoathiri kazi, familia na mahusiano yake.

    Baada ya kupata msaada wa kitaalamu, anasema alianza kuwaeleza marafiki zake kuhusu kile alichokuwa akipitia na kugundua kuwa wanaume wengi walikuwa wakikabili changamoto kama hizo, lakini walikuwa wamezoea kuzichukulia kama sehemu ya maisha kwa sababu tu ni wanaume.

    Anasema baadhi ya wanaume wamefundishwa tangu utotoni kwamba wanapaswa kukabiliana na matatizo yao wenyewe na kwamba kushindwa ni jambo lisilokubalika kwa mwanaume. Hata hivyo, anasema mtazamo huo unaweza kuwa sahihi au usiwe sahihi, kutegemea aina na muktadha wa changamoto anayokabiliana nayo mtu.

    MTAALAMU: HISIA SI ZA WANAWAKE PEKEE

    Nadia Ahmed, mshauri na mwanasaikolojia anayeshiriki katika mijadala kuhusu afya ya akili ya wanaume, amesema hakuna sababu ya kuwazuia wanaume kuonyesha hisia zao kwa sababu hisia ni sehemu ya asili ya binadamu.

    “Kibaiolojia, wanaume na wanawake wana mabadiliko ya kikemikali yanayofanana. Wanaume wanaweza kuhisi hisia zote sawa na wanawake, na hilo linadhihirisha kuwa si suala la jinsia, bali ni hisia za kawaida ambazo zinapaswa kushughulikiwa kwa njia yenye afya,” anasema Ahmed.

    Ahmed anashauri watu kukubali hisia za huzuni badala ya kuzikataa, akieleza kuwa kufanya hivyo kunaweza kumsaidia mtu kujenga njia bora za kukabiliana na changamoto.

    Mtazamo huo unatoa picha tofauti na dhana kwamba mwanaume anapaswa kuwa mtu asiyeathirika na matatizo. Mwanaume anaweza kuwa mwenye nguvu, mwenye wajibu wa familia na bado akawa na huzuni, hofu au msongo unaohitaji kuzungumziwa.

    MAJUKUMU YA KUWA MTOAJI WA FAMILIA

    Kwa wanaume wengi, jukumu la kuwa mtoaji wa mahitaji ya familia limekuwa sehemu kubwa ya utambulisho wao. Chakula, kodi, ada za watoto, matibabu na mahitaji mengine yanaweza kuonekana kuwa wajibu ambao mwanaume anapaswa kuhakikisha unapatikana bila kujali hali yake.

    Utafiti wa akina baba mjini Mwanza umeonesha kuwa matarajio hayo yanaweza kuhusishwa na msongo wa kiuchumi, hasa pale ambapo mwanaume hana ajira au kipato cha kutosha.

    Watafiti walibaini pia kuwa baadhi ya akina baba walihusisha uwezo wa kuwa mtoaji wa familia na maana ya kuwa mwanaume.

    Hii ina maana kwamba mwanaume anayeshindwa kutimiza mahitaji yote ya familia anaweza asiwe anakabiliana na tatizo la fedha pekee, bali pia hisia za kushindwa kutimiza kile ambacho jamii imemfundisha kuwa ni wajibu wake.

    Changamoto hiyo inaweza kuwa kubwa zaidi wakati mwanaume hana mtu wa kuzungumza naye kwa sababu anaogopa kuonekana dhaifu au kushindwa.

    UKIMYA UNAPOBADILIKA KUWA NJIA YA KUKABILIANA NA MATATIZO

    Baruti anasema baadhi ya wanaume wanapokabiliwa na matatizo huamua kuyaficha badala ya kuzungumza, hali ambayo wakati mwingine inaweza kuwafanya kujiingiza katika matumizi ya pombe au dawa za kulevya na tabia nyingine hatarishi zisizosaidia kutatua tatizo lililopo.

    Utafiti wa mwaka 2026 uliofanywa na watafiti wanaohusishwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi cha Muhimbili (MUHAS), Chuo Kikuu cha Oslo, pamoja na taasisi nyingine, uliangalia msongo wa akili miongoni mwa wanaume nchini Tanzania.

    Utafiti huo ulibaini uhusiano kati ya changamoto za kijamii, unyanyapaa, ukosefu wa msaada wa kijamii na afya ya akili.

    Tafiti kama hizi zinaonesha umuhimu wa kulitazama suala la afya ya akili kwa wanaume kwa upana zaidi, badala ya kusubiri tatizo liwe kubwa ndipo msaada utafutwe.

    UANAUME SI LAZIMA UJENGWE JUU YA UKIMYA

    Ongezeko la mijadala kuhusu afya ya akili ya wanaume linaonyesha kuwa kuna haja ya kuangalia upya baadhi ya mitazamo iliyorithishwa kutoka vizazi vilivyopita.

    Mwanaume anaweza kuwa jasiri bila kuficha hisia zake. Anaweza kuwa baba anayewajibika na bado akahitaji msaada. Anaweza kuwa mume anayelinda familia yake na bado akahitaji mtu wa kumsikiliza.

    Baruti anasema ni muhimu kuanza mabadiliko hayo tangu utotoni kwa kuacha kuwafundisha wavulana kwamba kulia ni ishara ya kutokuwa mwanaume.

    Amesema wazazi wanapaswa kuwauliza watoto wao wanavyojisikia na kuwapa nafasi ya kueleza hisia zao badala ya kuwafundisha kuzificha.

    Hili linaweka familia katika nafasi muhimu ya kusaidia kubadilisha mtazamo kuhusu uanaume. Mwanaume anayejua kuwa anaweza kuzungumza na mke wake, mzazi, rafiki au mtaalamu bila kuhukumiwa anaweza kuwa katika nafasi nzuri zaidi ya kukabiliana na changamoto.

    MSAADA HAUMFANYI MWANAUME KUWA DHAIFU

    Mjadala huu hauhusu kuondoa wajibu wa mwanaume katika familia wala kumfanya asiwe mwajibikaji. Badala yake, unahusu kutambua kwamba wajibu huo unaweza kuwa rahisi zaidi kutekelezwa pale anapokuwa na afya njema ya mwili na akili, akiwa pia na watu anaoweza kuwategemea.

    Mwanaume anayesema “Siko sawa” anapokuwa katika hali ngumu si lazima awe ameshindwa. Anaweza kuwa ametambua tatizo mapema na kuchukua hatua ya kutafuta suluhisho.

    Kwa mujibu wa Nadia Ahmed, hisia zinapaswa kushughulikiwa kwa njia yenye afya, jambo linalomaanisha kuwa kuzificha si lazima kuwe ishara ya nguvu.

    MWISHO WA UKIMYA

    Mwanaume si mashine inayotakiwa kufanya kazi bila kuchoka, kulipa gharama bila kulalamika na kukabiliana na kila tatizo bila kuhitaji msaada.

    Nyuma ya mwanaume anayeonekana imara kuna mtu mwenye hisia, hofu, matumaini, kushindwa na mafanikio. Kumruhusu mwanaume kuzungumza kuhusu anachopitia hakumvui uanaume; kunampa nafasi ya kuwa binadamu.

    Kwa hiyo, huenda wakati umefika wa kuacha kumuuliza mwanaume, “Kwa nini unalia?” na kuanza kumuuliza, “Nini kinakufanya uumie?”

    Kwa sababu wakati mwingine, kumsaidia mwanaume hakuanzi kwa kumpa suluhisho. Kunaweza kuanza kwa kumpa nafasi ya kusema ukweli kwamba hayuko sawa.

  • Na Mwandishi Wetu, Nachingwea – Lindi

    Wajasiriamali wa Wilaya ya Nachingwea, mkoani Lindi, wametakiwa kutumia kwa ufanisi mitaji wanayopewa na Halmashauri ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na kukuza shughuli zao za kiuchumi.

    Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Bi. Stella Kategile, wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wajasiriamali kutoka vikundi mbalimbali yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mondulane Messi.

    Kategile alisema matumizi sahihi ya mitaji yatawawezesha wajasiriamali kufikia malengo waliyojiwekea na kukuza biashara na shughuli zao za kiuchumi, badala ya kutumia fedha hizo kwa mambo tofauti na mpango waliouwasilisha na kuidhinishiwa.

    Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Jamii, James Mbakile, alisema wajasiriamali wanakabiliwa na changamoto mbalimbali katika uendeshaji wa shughuli zao, zikiwemo utoaji na usimamizi wa mitaji, usimamizi wa mapato na matumizi, ukosefu wa masoko, teknolojia pamoja na mabadiliko ya mazingira ya kibiashara.

    Naye Mkaguzi wa Ndani, Mesia Mlay, aliwataka wanachama wa vikundi kutunza kumbukumbu sahihi za fedha ili kuhakikisha uwazi na ufanisi katika uendeshaji wa shughuli zao.

    Alisema kutokuwepo kwa kumbukumbu sahihi kunasababisha changamoto mbalimbali, ikiwemo wanakikundi kushindwa kufahamu kiwango halisi cha fedha kinachoingia, kupotea kwa uaminifu miongoni mwa wanachama, pamoja na kushindwa kubaini kiasi cha fedha kinachodaiwa na kinachodaiwa na wengine.

    Aidha, Afisa Biashara wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Aurelia Haule, alieleza umuhimu wa vikundi vya wajasiriamali kujenga utamaduni wa kuweka akiba.

    Alisema akiba husaidia vikundi kukabiliana na dharura, kuwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuongeza uwekezaji, kujenga umoja na ushirika miongoni mwa wanachama, kutumia fursa za biashara kwa wakati na kuimarisha nidhamu ya matumizi ya fedha.

    Kwa upande wake, Afisa Sheria, Diana Mmary, alisema ukosefu wa mawasiliano thabiti miongoni mwa wanakikundi ni miongoni mwa vyanzo vikuu vya migogoro inayoweza kudhoofisha maendeleo ya vikundi.

    Alisema hali hiyo inaweza kusababisha baadhi ya wanachama kujiondoa katika vikundi na hivyo kuchelewesha utekelezaji wa malengo na mipango ya maendeleo.

    Mafunzo hayo yamehusisha zaidi ya vikundi 20 vya wajasiriamali pamoja na maafisa kutoka idara mbalimbali za Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, kwa lengo la kuwajengea uwezo katika usimamizi wa mitaji, fedha, kumbukumbu za kifedha, biashara na utatuzi wa changamoto zinazoweza kujitokeza katika uendeshaji wa vikundi.

  • Na Juma John Elisha

    Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Deogratius Ndejembi, ameapishwa rasmi kushika wadhifa huo katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino, Dodoma.

    Ndejembi ameapa mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, na hivyo kuanza rasmi majukumu yake mapya kama Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

    Uteuzi wa Ndejembi umefuatia kuondoka kwa aliyekuwa Makamu wa Rais, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ambaye alijiuzulu nafasi hiyo Agosti 25, 2026. Hatua hiyo ilisababisha kuwepo kwa nafasi wazi na kufungua mchakato wa kumpata Makamu wa Rais mpya.

    Hafla ya kuapishwa kwa Ndejembi imefanyika katika Ikulu ya Chamwino, Dodoma, ikiashiria mwanzo rasmi wa utekelezaji wa majukumu yake katika nafasi hiyo muhimu ya uongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

    Ndejembi anatarajiwa kushirikiana kwa karibu na Rais Samia Suluhu Hassan katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali, ikiwemo kusimamia maeneo atakayokabidhiwa kwa mujibu wa Katiba na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amezitaka taasisi za elimu kuhakikisha ubora wa elimu nchini unaendelea kuzingatiwa, akionya dhidi ya mfumo unaoweza kuwafanya wanafunzi kupata alama kubwa bila kuwa na uwezo na ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira.

    Dkt. Nchemba alitoa kauli hiyo leo wakati akifunga Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu mkoani Tanga, ambapo alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha wahitimu wanakuwa na uwezo halisi wa kutekeleza majukumu yao katika maeneo waliyosomea.

    Alisema taasisi zinazohusika na uhakiki wa ubora wa elimu zinapaswa kuhakikisha viwango vinaendelea kuzingatiwa ili elimu inayotolewa nchini iwe na tija kwa mwanafunzi na Taifa kwa ujumla.

    “Tusitengeneze mazingira ambayo kusoma kunakuwa rahisi na alama zinakuwa kubwa sana, halafu wahitimu wanapofika kazini wanapata sifuri kubwa. Hilo halikubaliki,” alisema Waziri Mkuu.

    Alisema ubora wa mafunzo ni muhimu zaidi katika sekta zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja, zikiwemo afya, uhandisi na elimu, kwa kuwa Taifa linahitaji wataalamu wenye uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa usahihi.

    “Hatuwezi kucheza kamari na afya za Watanzania kwa kuwafundisha wataalamu vibaya halafu tukatarajia matokeo mazuri. Tunahitaji walimu na wahandisi wenye uwezo; wanapojenga daraja au jengo, ni lazima liwe salama na lenye ubora,” alisema Dkt. Nchemba.

    Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, alisema Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu imekuwa sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Serikali katika kuimarisha elimu inayounganisha nadharia na ujuzi wa vitendo.

    Alisema hatua hiyo inalenga kuhakikisha wahitimu wanapata ujuzi na umahiri unaowawezesha kujiajiri na pia kukidhi mahitaji ya soko la ajira.

    Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameiagiza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na taasisi zake kuhakikisha ubunifu unaofanywa na Watanzania hauishii kwenye maonesho, bali unaendelezwa hadi kufikia uzalishaji na kuuzwa sokoni.

    Alisema Tanzania ina wabunifu wenye uwezo wa kutatua changamoto mbalimbali, lakini changamoto iliyopo ni kuhakikisha mawazo na bidhaa zao zinalindwa, zinaendelezwa na hatimaye kutumika katika maisha halisi.

    “Ni lazima tuondoke kwenye maonesho na kwenda kwenye maisha halisi, kuhakikisha kinachooneshwa kwenye matukio kama haya kinakuwa sehemu ya maisha ya kila siku na kinaingia sokoni,” alisema Waziri Mkuu.

    Alisema Serikali itaendelea kuwekeza katika sayansi, ujuzi na ubunifu kwa kuwa maeneo hayo ni muhimu katika kuibadilisha uchumi wa Taifa na kuongeza kasi ya maendeleo kupitia matumizi ya tafiti na teknolojia.

    “Hatutaweza kuendelea bila sayansi, teknolojia na utafiti na bila kutumia matokeo ya tafiti hizo. Hatuwezi kuongeza uzalishaji bila kutumia matokeo ya utafiti,” alisema.

    Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameitaka mipango ya maendeleo ya Uwanja wa Ndege wa Tanga kuzingatia mahitaji ya kiuchumi na kijamii ya mkoa huo kwa kipindi cha miaka 25 ijayo.

    Alisema miundombinu inayojengwa sasa inapaswa kuandaliwa kwa kuzingatia ongezeko la biashara, uwekezaji na usafiri wa anga katika siku zijazo, akieleza kuwa Tanga ina nafasi muhimu kama lango la kiuchumi kutokana na miradi mikubwa inayotekelezwa mkoani humo.