• Na Damasi Kalembwe

    Mashindano ya michezo ya Polisi Jamii Cup katika Mkoa wa Kinondoni yamezinduliwa rasmi Julai 27, 2026, katika viwanja vya michezo vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

    Uzinduzi huo ulihudhuriwa na Mgeni Rasmi, Mkuu wa Ushirikishwaji wa Jamii Mkoa wa Kinondoni, ACP Ally Wendo, aliyeambatana na Wakuu wa Himaya za Kinondoni na Kawe pamoja na Maafisa Watendaji wa Wilaya (DCEO) wa maeneo hayo.

    Akizungumza kwa niaba ya askari na washiriki wote, Koplo Itumbi Wambura alisema mashindano hayo ni fursa muhimu ya kuwakutanisha askari polisi na wananchi wanaowahudumia, hivyo kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya pande hizo mbili.

    Alisema lengo kuu la mashindano hayo ni kupata wachezaji mahiri watakaounda timu imara ya mkoa, sambamba na kuhamasisha afya bora kupitia mazoezi na michezo.

    Aidha, mashindano hayo yanalenga kuongeza mshikamano, kufahamiana na kujenga ushirikiano wa dhati kati ya Jeshi la Polisi, jamii na wajumbe kutoka wilaya zote tano zinazoshiriki.

    Katika siku ya ufunguzi, timu mbalimbali zilishiriki katika michezo ya riadha, kuvuta kamba, mpira wa miguu na mpira wa pete. Washiriki walionyesha ushindani mkubwa katika kila mchezo wakilenga kuzipatia ushindi himaya zao.

    Matokeo ya michezo ya ufunguzi yalionesha Mkoa wa Kinondoni ukiibuka bingwa katika riadha na mpira wa pete. Kwa upande wa mchezo wa kuvuta kamba, Himaya ya Kawe iliibuka mshindi, huku mchezo wa mpira wa miguu kati ya Kinondoni na Kawe ukimalizika kwa sare ya mabao 2-2.

  • Na Jastini Bukebuke

    Walimu wa Shule ya Msingi Simbaguji, iliyopo Kata ya Kanyala, Wilaya ya Geita, wametakiwa kuimarisha usimamizi wa vilabu vya kupinga ukatili wa kijinsia shuleni ili viendelee kuwajengea wanafunzi uelewa wa haki zao, ujasiri wa kutoa taarifa, maadili mema na uwezo wa kujilinda dhidi ya ukatili pamoja na vitendo vingine vinavyohatarisha usalama wao.

    Wito huo ulitolewa jana na Polisi Kata wa Kanyala, Inspekta Said Juma, alipokuwa akitoa elimu ya kinga kwa walimu na wanafunzi wa shule hiyo.

    Akizungumza katika elimu hiyo, Inspekta Juma alisema vilabu vya kupinga ukatili wa kijinsia ni nyenzo muhimu katika kuwafundisha wanafunzi kutambua haki zao, kutoa taarifa kwa wakati wanapobaini viashiria vya ukatili na kujiepusha na mazingira yanayoweza kuhatarisha usalama wao.

    Aidha, aliwataka walimu kuhakikisha vilabu hivyo vinaendelea kufanya kazi kwa ufanisi kupitia mikutano ya mara kwa mara, utoaji wa elimu endelevu na ushirikiano wa karibu kati ya shule, wazazi na jamii ili kuimarisha ulinzi wa watoto.

    Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Simbaguji, Renatus Misago Chigunga, alilipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kutoa elimu ya kinga shuleni.

    Alisema ushirikiano huo unachangia kuongeza uelewa wa wanafunzi kuhusu masuala ya usalama, kuimarisha maadili mema na kujenga mazingira salama na rafiki ya kujifunzia.

  • Na George Gabriel

    Wananchi wa Kijiji cha Masugulu, Wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara, wameiomba Serikali kuhakikisha Mradi wa Maji wa Mto Ruvuma–Mangaka unakamilika kwa wakati ili waanze kunufaika na huduma ya maji safi na salama.

    Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Mwanahawa Juma alisema licha ya mradi huo kuanza kutekelezwa, bado wanaiomba Serikali kuongeza kasi ya utekelezaji ili kutimiza ahadi ya kuwapatia maji ya uhakika na kuondoa kero ya muda mrefu.

    “Tunaishukuru Serikali kwa kuleta mradi huu mkubwa, lakini tunaomba ukamilike haraka kwa sababu tumekuwa tukiusubiri kwa muda mrefu tangu Rais alipotuahidi,” alisema Mwanahawa.

    Naye Mzee Shaibu Lipindi alisema upatikanaji wa maji ya uhakika utapunguza adha ambayo wananchi wamekuwa wakikabiliana nayo kwa miaka mingi. Aliipongeza Serikali kwa kuendelea kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo yenye manufaa kwa wananchi.

    Kwa upande wake, mwakilishi wa mkandarasi, AFCONS Infrastructure Ltd, alisema kampuni hiyo imepokea maelekezo ya Mkuu wa Mkoa ya kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo. Aliahidi kuwa watafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha mradi unakamilika ndani ya muda uliopangwa.

    Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Donald Msengi, alimtaka mkandarasi kuongeza nguvu kazi, vifaa na rasilimali nyingine muhimu ili kuhakikisha mradi huo wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 38.1 unakamilika kwa wakati na kuanza kutoa huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Nanyumbu na maeneo ya jirani.

    Serikali imeendelea kusisitiza kuwa upatikanaji wa maji safi na salama ni miongoni mwa vipaumbele vyake katika kuboresha maisha na kuchochea maendeleo ya wananchi.

    Maoni ya wananchi pamoja na agizo la Mkuu wa Mkoa kwa mkandarasi yalitolewa wakati wa ziara ya Kanali Donald Msengi ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo.

  • Na Cosmas Msuha

    Zaidi ya shilingi bilioni 38 zimetumika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika Wilaya ya Kongwa, mkoani Dodoma, katika mwaka wa fedha 2025/2026, huku Serikali ikiahidi kuendelea kuboresha huduma za elimu, afya, maji, mawasiliano na miundombinu.

    Hayo yameelezwa hivi karibuni na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Laikala baada ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani humo, ikiwemo ujenzi wa jengo jipya la Ofisi ya Mkuu wa Wilaya pamoja na Vituo vya Afya vya Laikala na Sagara.

    Akizungumza na wananchi wa kata za Laikala na Sagara, Waziri Kairuki alisema fedha hizo zimewezesha utekelezaji wa miradi katika sekta za afya, elimu, maji, kilimo, umwagiliaji na miundombinu.

    “Hadi Juni 2026, Serikali imeelekeza shilingi bilioni 38.6 kutekeleza miradi ya afya, elimu, kilimo, umwagiliaji na miundombinu mingine ya maendeleo katika Wilaya ya Kongwa,” alisema Kairuki.

    Aliongeza kuwa Serikali imejenga zaidi ya madarasa 640, maabara za sayansi karibu 50 na kuajiri walimu wa kutosha ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.

    Aidha, aliahidi kupeleka kompyuta 44 katika shule mbili za wilaya hiyo pamoja na kuendelea kujenga madarasa ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF), kwa lengo la kuwawezesha wanafunzi kupata ujuzi wa teknolojia.

    Katika sekta ya maji, alisema upatikanaji wa huduma hiyo wilayani Kongwa umefikia asilimia 76.8, huku Serikali ikijiandaa kuchimba visima 19 katika vijiji ambavyo bado havijafikiwa na huduma ya maji safi na salama.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Saimon Mayeka, alisema wilaya hiyo imepata mafanikio makubwa katika utoaji wa huduma za jamii. Alieleza kuwa idadi ya shule za sekondari imeongezeka kutoka 26 hadi 41 baada ya kujengwa shule mpya 15, huku ongezeko la vituo vya afya likichangia kuboresha huduma za afya na kupunguza vifo vya mama na watoto.

    Kwa mujibu wa Mayeka Wilaya ya Kongwa ina jumla ya shule za sekondari 45, zikiwemo 39 za Serikali na sita za binafsi.

  • Na Jastini Bukebuke

    Mkuu wa Kituo cha Polisi Kasamwa, Inspekta Said Juma, akishirikiana na askari wa kituo hicho, wamewafariji wagonjwa wanaopatiwa matibabu katika Kituo cha Afya Kasamwa kwa kuwapa pole na kuwakabidhi mahitaji muhimu.

    Tukio hilo lilifanyika Julai 25, 2026, katika Kituo cha Afya Kasamwa, Wilaya ya Geita, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Jeshi la Polisi kuendelea kuwa karibu na wananchi na kuimarisha mahusiano mema kupitia falsafa ya Polisi Jamii.

    Akipokea msaada huo, Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Kasamwa, Dkt. Emmanuel Ziragira, alilishukuru Jeshi la Polisi kwa kuonesha moyo wa kujali na kuwafariji wagonjwa. Alisema matendo hayo yanawapa faraja na kuongeza matumaini kwa wananchi wanaopitia changamoto za kiafya.

    Kupitia tukio hilo, Jeshi la Polisi limeendelea kudhihirisha kuwa jukumu lake halijikiti katika kulinda amani na usalama pekee, bali pia kujenga mahusiano ya karibu na jamii kupitia matendo ya huruma na huduma kwa wananchi.

    Aidha, wananchi wamehimizwa kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu kwa wakati, ili kuimarisha amani, usalama na utulivu katika jamii.

  • Na Damasi Kalembwe

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni limewataka wamiliki wote wa vyombo vya moto kujitokeza kuhakiki magari yao na kuzingatia taratibu za usalama barabarani, likisisitiza kuwa kampeni ya “Nenda kwa Usalama” inalenga kupunguza ajali na kulinda maisha ya watumiaji wote wa barabara.

    Zoezi hilo linafanyika katika Kituo cha Polisi Oysterbay cha Zamani kuanzia Julai 23, 2026, chini ya usimamizi wa Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, SSP Adamson Mwangamilo.

    Sambamba na zoezi hilo, wananchi wanaendelea kupatiwa elimu kuhusu matumizi salama ya vyombo vya usafiri, ikiwemo magari na pikipiki, pamoja na namna ya kujaza taarifa katika mfumo wa ukaguzi wa magari ili kupata stika za MIMIS.

    Hatua hiyo inalenga kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma na kuimarisha usalama barabarani.

    Miongoni mwa wananchi walioshiriki katika zoezi hilo ni Shabani Omary, ambaye amelipongeza Jeshi la Polisi pamoja na Serikali kwa kuanzisha mfumo wa kisasa wa ukaguzi wa magari.

    Amesema mfumo huo umeongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa kupunguza muda wa kusubiri na kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

    Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Kipolisi Kinondoni kinaendelea na zoezi la uhakiki wa magari na utoaji wa stika za “Nenda kwa Usalama” ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kuimarisha usalama barabarani na kuhamasisha uzingatiaji wa sheria za usalama wa barabarani.

  • Na George Gabriel

    Wananchi wa Kata ya Nanyumbu wamepongeza ziara ya Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Magala, wakisema imeleta manufaa makubwa kwa jamii kupitia usikilizaji wa kero, utatuzi wa migogoro ya wakulima na wafugaji pamoja na usimamizi wa ugawaji wa pembejeo za kilimo kwa wakati.

    Wakizungumza baada ya kukamilika kwa ziara hiyo, wananchi walisema hatua ya Mkuu wa Wilaya kufika moja kwa moja katika maeneo yao imeongeza imani kwa Serikali kwa kuwapa fursa ya kueleza changamoto zao na kupata ufumbuzi wa haraka.

    Fatuma Abdalah alisema migogoro iliyokuwa ikiwakabili wakulima na wafugaji imeanza kutafutiwa ufumbuzi, jambo ambalo litasaidia kurejesha amani na kuongeza uzalishaji.

    “Tunamshukuru Mkuu wa Wilaya kwa kutusikiliza. Migogoro iliyokuwa inatukabili kati ya wakulima na wafugaji imeanza kutafutiwa ufumbuzi, jambo litakalorejesha amani na kuongeza uzalishaji,” alisema Fatuma.

    Naye Juma Shaibu alisema ziara hiyo imeonesha dhamira ya Serikali ya kuwahudumia wananchi kwa vitendo badala ya kusubiri malalamiko yafikishwe ofisini.

    “Tunafurahi kuona viongozi wanakuja vijijini kusikiliza matatizo yetu. Pia tunashukuru pembejeo za kilimo zimeanza kutolewa mapema, jambo litakalotusaidia kujiandaa vizuri kwa msimu wa kilimo,” alisema Juma.

    Kwa upande wake, Shaiki Ulenje aliipongeza Serikali kwa juhudi za kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji ambayo kwa muda mrefu imekuwa chanzo cha migongano katika kata hiyo. Alisema maamuzi yaliyotolewa wakati wa ziara hiyo yameleta matumaini mapya kwa wananchi.

    “Tunampongeza Magala kwa kusimamia haki na kuhakikisha kila upande unasikilizwa. Tunayo imani kuwa amani itaendelea kudumu na shughuli za uzalishaji zitaimarika,” alisema Ulenje.

    Awali, Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Magala, alisema ziara hiyo imelenga kusikiliza na kutatua kero za wananchi kwa wakati, kufuatilia utekelezaji wa miradi na shughuli za maendeleo, pamoja na kuhakikisha ugawaji wa pembejeo za kilimo unafanyika kwa uwazi na haki ili kuongeza tija katika uzalishaji wa kilimo.

  • Na Damasi Kalembwe

    Jeshi la Polisi Wilaya ya Kipolisi Mabwepande, Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, limetoa msaada wa mahitaji mbalimbali kwa watoto wanaolelewa katika Kituo cha Babu na Bibi Children’s Care kilichopo Madale, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirikiano na jamii na kuwajali watoto wenye mahitaji maalumu.

    Ziara hiyo ilifanyika juzi chini ya uongozi wa OCD Mabwepande, SSP Colle Mshauri, akifuatana na maofisa mbalimbali wa Jeshi la Polisi, akiwemo OCS Madale, SP Ngoso, DTO Mabwepande, ASP Joseph, DFBO Mabwepande, ASP Elizabeth, I/C CID Madale, ASP Virgiana, pamoja na askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani.

    Katika ziara hiyo, Jeshi la Polisi lilikabidhi msaada uliokuwa na fedha taslimu shilingi 100,000, unga, mchele, sukari, mafuta ya kula, pampasi na mahitaji mengine muhimu kwa ajili ya kuwasaidia watoto wanaolelewa katika kituo hicho.

    Akizungumza kwa niaba ya kituo hicho, mlezi wake, Diocres Apolnary Mutalemwa, alilishukuru Jeshi la Polisi kwa moyo wa kujitolea na kuwajali watoto wenye mahitaji maalumu.

    Alisema msaada huo ni faraja kubwa na utasaidia kupunguza baadhi ya changamoto zinazokikabili kituo katika kuhudumia watoto.

    Mutalemwa alibainisha kuwa ushirikishwaji wa jamii unaofanywa na Jeshi la Polisi unaendelea kuwa daraja muhimu la kuimarisha uhusiano kati ya polisi na wananchi, huku ukihamasisha mshikamano na uwajibikaji wa kijamii.

    Kituo cha Babu na Bibi Children’s Care kinahudumia watoto 68 wa rika mbalimbali kuanzia miaka mitatu na kuendelea huku baadhi yao wanasoma katika vyuo, shule za sekondari, msingi na chekechea.

    Msaada huo unatarajiwa kuboresha ustawi wa watoto hao na kuendeleza mshikamano kati ya Jeshi la Polisi na jamii.

  • Na Jastini Bukebuke

    Polisi Kata wa Ihanamilo, INSP Yosepha Michael, Julai 20, 2026, alitoa elimu kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Nyakahengele, Wilaya ya Geita, Mkoa wa Geita, akiwahimiza kuwa wazalendo, wenye nidhamu na bidii katika masomo ili kujijengea msingi imara wa maisha yao ya baadaye.

    Akizungumza wakati wa elimu hiyo, INSP Michael alisema elimu ni nguzo muhimu ya maendeleo ya mtu binafsi na taifa, hivyo aliwataka wanafunzi kuipenda shule, kuwaheshimu walimu na wazazi, pamoja na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuhatarisha masomo na mustakabali wao.

    Aidha, aliwakumbusha kuzingatia tahadhari za kiusalama kwa kujilinda dhidi ya vitendo vya kihalifu. Aliwashauri kutembea kwa makundi wanapokwenda na wanaporudi kutoka shuleni, kuepuka kuzungumza na watu wasiowafahamu, pamoja na kutoa taarifa kwa walimu, wazazi au Jeshi la Polisi wanapobaini viashiria vya uhalifu au mazingira yasiyo salama.

    Kwa upande wao, wanafunzi wa Shule ya Msingi Nyakahengele walilishukuru Jeshi la Polisi kwa elimu hiyo, wakisema imewaongezea uelewa kuhusu umuhimu wa elimu, uzalendo na mbinu za kujilinda dhidi ya vitendo vya kihalifu.

    Pia waliahidi kuendelea kushirikiana, kuishi kwa upendo, kuzingatia maadili mema na kufuata ushauri walioupata ili kuendelea kuwa salama wawapo shuleni na wanaporejea nyumbani.