
Na Greyson Makabe
Marekebisho ya Sheria ya Mwenendo wa Madai (Civil Procedure Code), yaliyofanyika mwaka 2023, yameendelea kuzua mjadala mpana miongoni mwa mawakili, wasomi wa sheria na wadau wa mfumo wa haki nchini.
Miongoni mwa marekebisho yanayobishaniwa zaidi ni kifungu cha 13, kinachowataka wahusika wa mgogoro wa madai kutafuta suluhu kupitia upatanisho kabla ya kufungua shauri mahakamani.
Lengo la kifungu hiki ni kuhamasisha utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala (Alternative Dispute Resolution – ADR), ili kupunguza mzigo wa mashauri mahakamani na kuwapa wahusika nafasi ya kumaliza migogoro yao kwa maelewano. Hata hivyo, utekelezaji wake umeibua changamoto mbalimbali zinazohusiana na upatikanaji wa haki kwa wakati.
Katika mahojiano na mawakili na wataalamu mbalimbali wa sheria, wengi wameeleza kuwa, ingawa dhamira ya kifungu hicho ni njema, hakikuandaliwa sambamba na utaratibu rasmi wa utekelezaji wake. Kwa sasa hakuna mfumo maalumu unaowaongoza wahusika namna ya kufanya upatanisho, nani atasimamia mchakato huo, wala namna ya kuthibitisha kuwa juhudi za usuluhishi zilifanyika na zikashindikana.
Kwa mtazamo wao, hali hiyo imeifanya sheria hiyo kuwa ngumu kutekelezeka, hasa kwa watu ambao tayari wamefikia hatua ya kushindikana kabisa kuelewana.
Wanasema ni vigumu kuwatarajia mahasimu ambao hata kuzungumza au kusalimiana ni changamoto, wakae tena mezani kutafuta suluhu bila uwepo wa chombo rasmi cha kuwaongoza.
Athari za kifungu hicho tayari zimeanza kuonekana mahakamani ambapo baadhi ya mashauri yamekuwa yakitupiliwa mbali kwa sababu wahusika hawakufuata masharti ya kifungu cha 13 kabla ya kufungua kesi.
Miongoni mwa maamuzi yanayonukuliwa mara kwa mara ni ya Jaji Beda katika shauri la A. Z. Bade Kilamala Alipinde na Mwenzake dhidi ya Saed Yeslam Saed, Kesi Na. 000032909 ya mwaka 2024.
Katika uamuzi huo, mahakama ilisisitiza kuwa shauri lolote ambalo halijafuata utaratibu uliowekwa na kifungu cha 13 haliwezi kusikilizwa na linapaswa kutupiliwa mbali kwa kuvunja matakwa ya sheria.
Kwa mujibu wa wadau wa sheria, maamuzi ya aina hiyo yamewaongezea wananchi gharama zisizo za lazima.
Mbali na ada ya kufungua kesi katika Mahakama Kuu, ambayo inaweza kufikia au kuzidi shilingi 150,000 kutegemeana na aina ya shauri, mlalamikaji hulazimika pia kugharamia wakili, maandalizi ya nyaraka na gharama nyingine za uendeshaji wa shauri. Kesi inapofutwa kwa sababu ya kutokufuata utaratibu huo, gharama hizo hupotea bila shauri kusikilizwa.
Hata hivyo, si majaji wote wamekuwa na mtazamo unaofanana kuhusu tafsiri ya kifungu hicho.
Katika shauri la Imalaseko Investment v Amer Mohamed Mbarak Company Limited & Another (Land Case No. 29281 of 2024), Jaji wa Mahakama Kuu, Mheshimiwa Hemed, alitoa mtazamo tofauti. Katika uamuzi wake alieleza kuwa kifungu cha 13 hakijaweka utaratibu mahsusi wa namna wadaawa wanavyopaswa kukutana kwa ajili ya usuluhishi kabla ya kufika mahakamani.
Alisisitiza kuwa sheria haijaeleza ni taasisi gani itasimamia mchakato huo wala mahali ambapo wahusika wanapaswa kwenda ikiwa upatanisho unahitajika.
Kwa msingi huo, aliona kuwa mahakama ina wajibu wa kuhakikisha haki inapatikana na si kuzuia wananchi kuifikia kutokana na mapungufu yaliyopo katika utekelezaji wa sheria. Alisisitiza pia kuwa moja ya majukumu ya msingi ya mahakama ni kutatua migogoro katika jamii, hivyo tafsiri ya sheria inapaswa kuzingatia haki badala ya kuangalia taratibu pekee.
Wananchi mbalimbali niliowahoji, ambao hawakutaka majina yao yachapishwe, nao wameeleza wasiwasi wao kuhusu kifungu hicho. Wamesema kingekuwa na manufaa zaidi kama Serikali ingeweka mfumo rasmi wa usuluhishi unaofanana na mifumo iliyopo katika maeneo mengine ya sheria.
Kwa mfano, katika migogoro inayosikilizwa na mabaraza ya kata, mlalamikaji hulazimika kwanza kupitia hatua ya upatanisho na hupewa cheti cha usuluhishi kabla ya kuendelea na hatua zinazofuata.
Vivyo hivyo, katika mashauri ya ndoa, wahusika hulazimika kupitia mabaraza ya usuluhishi wa ndoa kabla ya kufungua shauri la talaka mahakamani.
Kwa maoni ya wananchi hao, mfumo kama huo ungewekwa pia katika mashauri ya madai ili kila mlalamikaji apate cheti kinachoonyesha kuwa juhudi za usuluhishi zilifanyika na hazikufanikiwa. Hatua hiyo ingeondoa sintofahamu iliyopo sasa na kupunguza uwezekano wa mashauri kutupiliwa mbali kwa sababu za kiutaratibu.
Kwa ujumla, mjadala kuhusu kifungu cha 13 unaonyesha mvutano kati ya dhamira ya kuhimiza utatuzi wa migogoro nje ya mahakama na haki ya kila mwananchi kupata fursa ya kusikilizwa mahakamani bila vikwazo visivyo na utaratibu wa wazi.
Wadau wengi wanaamini kuwa ili kifungu hicho kifikie malengo yaliyokusudiwa, ni muhimu Serikali iweke mfumo wa kitaasisi wa usuluhishi wenye taratibu, mamlaka na uthibitisho rasmi. Bila kufanya hivyo, kuna hatari ya kifungu hicho kuendelea kutafsiriwa kwa namna tofauti na mahakama mbalimbali, jambo linaloweza kuathiri usawa wa haki na kuongeza gharama kwa wananchi.




















