• Na George Gabriel

    Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Edward Magala, ameyataka mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs) wilayani humo kubuni na kutekeleza miradi itakayowawezesha kujitegemea kifedha badala ya kutegemea fedha za wafadhili pekee.

    Magala alitoa wito huo hivi karibuni wakati akifungua Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu.

    Alisema ni muhimu kwa mashirika hayo kujenga uwezo wa kutekeleza miradi kwa ufanisi na weledi, huku yakizingatia maadili, misingi na vipaumbele vya jamii.

    Magala alionya kuwa utegemezi mkubwa wa fedha za wafadhili unaweza kuhatarisha mwendelezo wa miradi endapo ufadhili huo utakoma. Hivyo, alizitaka NGOs kubuni vyanzo mbadala vya mapato na kuimarisha ubunifu ili ziweze kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa uendelevu.

    Akizungumza baada ya mkutano huo, Anyesi John Mhalu alipongeza hatua ya Serikali ya kuwakutanisha wadau hao, akisema jukwaa hilo ni muhimu katika kujenga uwezo, kubadilishana uzoefu na kujadili namna bora ya kuboresha utendaji wa mashirika yasiyo ya kiserikali.

    Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Rudrick Charles, alisema Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali huratibiwa kwa kushirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum pamoja na Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NaCoNGO).

    Alisema kupitia jukwaa hilo, mashirika huwasilisha na kujadili taarifa za utekelezaji wa shughuli na miradi yao, pamoja na kubainisha changamoto na fursa zinazohusu utendaji wao.

    Jukwaa hilo lilishirikisha pia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na mashirika saba yasiyo ya kiserikali yanayotekeleza shughuli mbalimbali katika Wilaya ya Nanyumbu.

    Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa mwaka 2026 limebebwa na kaulimbiu: “Fikra Mpya Kuhusu Uendelevu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali: Ubunifu, Ubia na Upatikanaji wa Rasilimali Fedha Kupitia Vyanzo vya Ndani.”

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Kampuni ya Yas Tanzania imezindua huduma ya Yas Fiber jijini Dodoma, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa intaneti ya kasi kwa kaya, wafanyabiashara na taasisi katika mji unaoendelea kukua kwa kasi.

    Huduma hiyo ya nyuzi-optiki kwa sasa inapatikana katika maeneo ya Ilazo, Ipagala, Swaswa, Mjini Kati na Barabara za Namba, huku kampuni hiyo ikieleza kuwa itaendelea kupanua huduma katika maeneo mengine kulingana na mahitaji ya wananchi.

    Uzinduzi huo ulifanyika jijini Dodoma hivi karibuni na kuhudhuriwa na viongozi wa Serikali, wateja pamoja na wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya jiji, ukiwa sehemu ya juhudi za kuongeza miundombinu ya mawasiliano ya kisasa.

    Mkurugenzi Mtendaji wa Yas Fiber, Maxime Woimant, alisema kampuni hiyo inalenga kuchochea mabadiliko ya kidijitali Dodoma kwa kuhakikisha wakazi na wafanyabiashara wanapata muunganisho wa uhakika utakaowawezesha kufanya kazi, kujifunza na kupata huduma za kidijitali kwa ufanisi zaidi.

    “Tunajitolea kusaidia mabadiliko ya kidijitali ya Dodoma kwa kutoa muunganisho wa kuaminika ambao utawawezesha wakazi na wafanyabiashara kufanya kazi, kujifunza, kuendesha shughuli kwa ufanisi zaidi na kupata huduma za kidijitali,” alisema Woimant.

    Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, Jabir Shekimweri, aliyeshiriki katika uzinduzi huo, alisisitiza umuhimu wa kuwa na miundombinu ya kidijitali yenye uhakika wakati Dodoma ikiendelea kupanuka.

    Shekimweri alisema upanuzi wa huduma za mawasiliano unaweza kufungua fursa zaidi za kiuchumi na kijamii kupitia uchumi wa kidijitali.

    Katika uzinduzi mwingine wa huduma za Yas jijini Dodoma mwezi Machi 2026, Shekimweri alisema upanuzi wa huduma za mawasiliano unaweza kusaidia kuongeza shughuli za kiuchumi, kurahisisha upatikanaji wa huduma na kuimarisha muunganisho kwa wakazi.

    Kwa upande wake, Yas Tanzania imesema uzinduzi wa Yas Fiber unalenga pia kuongeza fursa za kujifunza mtandaoni, kuwasaidia wajasiriamali kufikia masoko mapya, kurahisisha uendeshaji wa biashara na kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali kwa kaya.

    Hatua hiyo inakuja wakati matumizi ya intaneti nchini yakiendelea kuongezeka. Kwa mujibu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), hadi Juni 2025 kulikuwa na watumiaji wa intaneti 54,078,530 nchini, huku teknolojia za 3G, 4G na 5G zikiendelea kuenea katika maeneo mbalimbali.

  • Na Juma John Elisha

    Dar es Salaam — Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, amesema atatumia haki yake ya kujitetea mwenyewe katika kesi ya uhaini inayomkabili, baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dar es Salaam, kuamua kuwa ana kesi ya kujibu.

    Uamuzi huo umetolewa leo, Agosti 21, 2026, na Jopo la Majaji watatu linaloongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru, akisaidiwa na Jaji James Karayemaha na Jaji Ferdinand Kiwonde.

    Uamuzi huo umefikiwa baada ya upande wa Jamhuri kuwasilisha ushahidi wake na Mahakama kusikiliza hoja za pande zote kuhusu iwapo ushahidi uliowasilishwa umeweka msingi wa kumtaka Lissu kuingia katika hatua ya kujitetea. Katika hatua hiyo, upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi 17.

    LISSU KUJITETEA MWENYEWE

    Baada ya Mahakama kutangaza kuwa ana kesi ya kujibu, Lissu amesema atatumia haki yake ya kisheria ya kujitetea na kutoa ushahidi wake mwenyewe kama shahidi wa upande wa utetezi.

    Hatua hiyo inaashiria kuanza kwa awamu mpya ya kesi, ambapo upande wa utetezi sasa utapata fursa ya kujibu ushahidi na hoja zilizowasilishwa na upande wa Jamhuri.

    Awali, Lissu alikuwa ameiomba Mahakama itamke kuwa hana kesi ya kujibu, akidai kuwa ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka haukufikia kiwango cha kumlazimisha kuingia katika hatua ya utetezi.

    KESI YA UHAINI INAYOMKABILI LISSU

    Lissu anakabiliwa na shtaka moja la uhaini chini ya kifungu cha 39(2)(d) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu. Shtaka hilo linahusishwa na kauli anazodaiwa kutoa kuhusu nia ya kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

    Upande wa mashtaka unadai kuwa kauli hizo zililenga kushinikiza uongozi wa Serikali na kuzuia mchakato wa uchaguzi, madai ambayo Lissu ameyapinga.

    Katika hoja zake za awali, Lissu alisisitiza kuwa ili kuthibitisha shtaka la uhaini, lazima kuwe na ushahidi unaoonyesha nia ya kutenda kitendo kinachodaiwa kuwa cha uhaini. Alidai pia kuwa ushahidi uliowasilishwa na Jamhuri haukuthibitisha msingi huo.

    HATUA INAYOFUATA

    Kwa uamuzi wa Mahakama kwamba Lissu ana kesi ya kujibu, shauri hilo sasa linaingia katika hatua ya utetezi. Lissu atapata nafasi ya kutoa ushahidi wake, huku upande wa mashtaka ukiwa na fursa ya kumuuliza maswali kwa mujibu wa taratibu za kawaida za kesi.

    Hatahivyo, uamuzi wa Mahakama kwamba Lissu ana kesi ya kujibu si hukumu ya kuwa ana hatia. Ni uamuzi kwamba ushahidi uliowasilishwa katika hatua ya mashtaka umeweka msingi wa kesi kuendelea katika hatua ya utetezi.

    Kesi hiyo imekuwa ikifuatiliwa kwa karibu kutokana na nafasi ya Lissu kama Mwenyekiti wa CHADEMA na uzito wa shtaka linalomkabili.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Wanaishi nyumba moja. Wanalala kitanda kimoja. Wanaweza hata kula chakula mezani pamoja. Lakini wakati mwingine au wakati wote, kila mmoja anaishi katika dunia yake.

    Mmoja anashika simu kuangalia WhatsApp. Mwingine anaingia Instagram, TikTok au Facebook. Dakika zinapita, saa zinapita, siku zinapita mazungumzo yanapungua na ukimya unatawala.

    Kwa nje, ndoa inaonekana na kila kitu kinachohitajika. Lakini ndani yake, mmoja au wote wawili wanaweza kuwa wanapitia hisia za upweke.

    Hapo ndipo simu inapoanza kupata nafasi nyingine katika maisha ya wanandoa. Badala ya kuwa chombo cha kuwasiliana tu, simu inaweza kuwa sehemu ya kukimbilia wakati mtu anahisi hana mtu wa kuzungumza naye. Inaweza kumpa burudani, mazungumzo na watu wengine au hisia ya kwamba kuna mtu anayemsikiliza.

    Lakini swali linabaki: Je, simu inawasaidia wanandoa kukabiliana na upweke, au wakati mwingine inazidi kuwapeleka mbali zaidi?

    UPWEKE UPO HATA KATIKA NDOA

    Tunaposema mtu yuko peke yake, mara nyingi tunafikiria mtu asiye na mwenza, familia au marafiki. Lakini upweke unaweza kuwa tofauti. Mtu anaweza kuwa na mwenza lakini akahisi hana mtu anayemsikiliza, anayemwelewa au anayeshirikiana naye kihisia.

    Katika ndoa, hususani za miongo hii, hali hii hujitokeza mawasiliano yanapopungua, wanandoa wanapokuwa na ratiba zinazowatenganisha, migogoro inapokaa muda mrefu bila kutatuliwa au kila mmoja anapojenga maisha yake bila kumshirikisha mwenzake.

    Utafiti wa Mhadhiri Msaidizi katika Idara ya Uandishi wa Habari na Masomo ya Mawasiliano, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Vincent Mpepo wa mwaka 2017, uliohusu athari za mitandao ya kijamii katika mawasiliano ya wanandoa katika Mkoa wa Dar es Salaam, ulihusisha washiriki 117 kutoka Ilala, Kinondoni na Temeke.

    Utafiti huo ulionyesha kuwa mitandao ya kijamii inaweza kuwa na mchango chanya katika mawasiliano ya wanandoa. Asilimia 80 ya washiriki walisema mawasiliano kupitia mitandao ya kijamii yalisaidia kuimarisha uhusiano wao, huku asilimia 12 wakiwa hawana uhakika na asilimia nane wakisema hayakusaidia kuimarisha uhusiano.

    Mpepo alipendekeza wanandoa kupata elimu kuhusu matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii na kuwa makini na masuala ya faragha na usiri katika matumizi ya teknolojia hiyo.

    Hapa ndipo tunapoona kwamba tatizo si simu yenyewe. Tatizo linaweza kuwa namna simu na mitandao ya kijamii vinavyotumiwa ndani ya mahusiano.

    SIMU INAPOKUWA MAHALI PA KUKIMBILIA

    Kwa mwanandoa anayehisi kupuuzwa au kutosikilizwa, simu inaweza kuwa na mvuto mkubwa.

    Anaweza kuingia kwenye mitandao ya kijamii na kuanza kuzungumza na watu wengine. Anaweza kutazama video kwa muda mrefu, kusoma maoni, kushiriki kwenye vikundi au kuwasiliana na rafiki ambaye anahisi anamwelewa zaidi.

    Hapo simu inaweza kuanza kufanya kazi kama aina ya rafiki wa kidijitali.

    Tatizo linatokea ambapo muda unaotumika kutafuta faraja kwenye simu unaanza kuchukua nafasi ya muda ambao ungeweza kutumika kujenga, kuboresha uhusiano wa wanandoa.

    Katika utafiti huo wa mwaka 2017 unaonyesha upande mmoja muhimu wa jambo hili: mitandao ya kijamii inaweza kusaidia wanandoa kuwasiliana na kuimarisha uhusiano wao, lakini matumizi yake yanahitaji mipaka na uelewa wa namna yanavyoweza kuathiri faragha na mawasiliano ya wanandoa.

    Kwa hiyo, simu inaweza kuwa daraja la mawasiliano au ikawa njia ya kukwepa mazungumzo ya ana kwa ana, kutegemea namna inavyotumiwa.

    WANANDOA WANAWEZA KUWA KARIBU KIDIJITALI LAKINI MBALI KIHISIA

    Mwanandoa anaweza kutuma ujumbe kwa mwenza wake akiwa kazini. Anaweza kumpigia simu, kumtumia picha au hata kumjibu ndani ya sekunde chache au pia asijibu huku pia mwenza anaweza kuona aina fulani ya kupuuzwa.

    Lakini mawasiliano yote hayo yanaweza kuwepo huku mazungumzo muhimu ya ndani ya ndoa yakikosekana.

    “Unaendeleaje?” inaweza kuulizwa, lakini hakuna anayefika kwenye swali la “Umeshindaje?”

    Hapo ndipo tofauti kati ya mawasiliano na ukaribu wa kihisia vinapoonekana.

    Utafiti wa Estella Alfred Mwambene wa mwaka 2019 kuhusu matumizi ya simu katika ndoa huko Iringa uliangalia namna matumizi ya teknolojia yanavyoathiri maisha ya familia na mawasiliano ya wanandoa.

    Utafiti huo ulihusisha wanandoa pamoja na viongozi wa jamii na watoto, na uliangazia namna simu zinavyoweza kusaidia mawasiliano lakini pia kuleta changamoto pale matumizi yanapokuwa ya kupita kiasi.

    Matokeo hayo yanaonyesha kuwa uwezo wa kuwasiliana kwa simu siyo lazima kubebe maana halisi ya ukaribu wa kihisia kwa wanandoa hao.

    Mwanandoa anaweza kuwa anawasiliana kila siku na mwenza wake kupitia simu, lakini bado akahisi hasikilizwi, haeleweki au anapuuzwa.

    SIMU INAPOCHUKUA NAFASI YA MWENZA….

    Kuna wakati mtu haishiki simu kwa sababu ana jambo maalumu la kufanya. Anaishika kwa sababu amezoea.

    Anaangalia ujumbe. Anafungua TikTok. Anarudi WhatsApp. Anaangalia Instagram na katika mitandao mingine au programu tumizi.

    Kwa mwanandoa anayehisi upweke, mzunguko huu unaweza kumpa hisia ya kuwa ana watu karibu naye.

    Lakini ukaribu wa kidijitali si lazima uwe sawa na ukaribu wa kihisia.

    Mtu anaweza kupata jumbe nyingi mtandaoni lakini bado akahisi hana mtu wa kumweleza kinachomsibu moyoni.

    Hili linafanya swali la matumizi ya simu ndani ya ndoa kuwa kubwa kuliko suala la muda wa kutumia skrini. Linakuwa suala la mahusiano.

    SIMU NA MIGOGORO YA NDOA…

    Mwaka 2026, Haji Ally Mkande kutoka Chuo cha Maendeleo ya Jamii ya Jamii Tengeru alichapisha utafiti uliochunguza matumizi na athari za simu katika migogoro ya ndoa mkoani Dar es Salaam.

    Utafiti huo ulihusisha washiriki 30, wakiwemo wanaume 10 waliooa, wanawake 10 walioolewa, wakwe wanne, watoto wanne na maafisa wawili wa ustawi wa jamii.

    Utafiti huo ulionyesha kuwa simu zinaweza kuwa chombo muhimu cha mawasiliano kati ya wanandoa, lakini matumizi yasiyofaa yanaweza pia kuongeza migogoro, hasa pale yanapohusisha usiri, mawasiliano ya nje ya ndoa na tuhuma za kutokuwa waaminifu.

    Hii inaonyesha kuwa simu si lazima iwe chanzo pekee cha migogoro ya ndoa. Wakati mwingine inaweza kuwa chombo kinachorahisisha au kuonyesha matatizo ambayo tayari yapo ndani ya uhusiano.

    USIRI WA SIMU UNAPOJENGA UKUTA…

    Kuna tofauti kati ya kuwa na faragha na kuwa na usiri.

    Kila mwanandoa ana haki ya kuwa na nafasi yake binafsi. Lakini pale simu inapokuwa eneo ambalo mwenza haruhusiwi kabisa kulikaribia, kila ujumbe unafichwa, kufutwa na matumizi yake yanaambatana na hofu ya kugundulika, mashaka yanaweza kuanza.

    Mwanandoa anaweza kujiuliza: “Kwa nini simu yake siku zote iko kimya?” “Kwa nini akipokea simu anatoka nje?” “Kwa nini ujumbe fulani unafutwa?” “Kwa nini muda mwingi anaonekana kuwa karibu na watu wa mtandaoni kuliko mimi?”

    Maswali haya yanaweza kuzaa mashaka hata kabla ya mtu kuwa na ushahidi wa jambo lolote.

    Utafiti wa Mkande unaonyesha umuhimu wa kuangalia namna matumizi ya simu yanavyohusiana na migogoro ya ndoa, mawasiliano na masuala ya uaminifu.

    Kwa hiyo, tatizo linaweza lisianze na usaliti wenyewe, bali linaweza kuanza na kuvunjika kwa uaminifu na mawasiliano.

    SIMU INAWEZA PIA KUWA SEHEMU YA SULUHISHO

    Pamoja na changamoto hizo, si sahihi kuifanya simu ionekane kama adui wa ndoa.

    Kwa wanandoa wanaoishi mbali kutokana na kazi, biashara au majukumu mengine, simu inaweza kuwa muhimu sana.

    Mwanandoa anaweza kumpigia mwenza wake wakati wa mapumziko kazini, kumjulisha anachofanya, kumjulia hali au kumtumia ujumbe wa kumtia moyo.

    Mitandao ya kijamii pia inaweza kuwa sehemu ya kushirikishana mambo yanayowafurahisha.

    Utafiti wa Mpepo wa mwaka 2017 unaunga mkono upande huu chanya. Asilimia 80 ya washiriki wake walisema mawasiliano kupitia mitandao ya kijamii yalisaidia kuimarisha uhusiano wao.

    Kwa hiyo, suala si kuondoa simu kwenye ndoa. Ni kuhakikisha simu haiondoi ndoa kwenye maisha ya wanandoa.

    WAKATI SIMU INAPOCHUKUA NAFASI YA MAZUNGUMZO

    Fikiria wanandoa wawili wamekaa sebuleni.

    Mume anaangalia simu. Mke anaangalia simu.

    Wote wako pamoja, lakini hakuna anayezungumza na mwenzake.

    Hii inaweza kuonekana kama jambo dogo, lakini ikiwa ni tabia ya kila siku na endelevu, inapunguza muda wa mawasiliano ya ana kwa ana.

    Utafiti wa mwaka 2019 kuhusu matumizi ya simu mahiri katika ndoa huko Iringa ulionyesha changamoto zinazoweza kujitokeza pale simu zinapotumika kupita kiasi, ikiwemo kuvurugika kwa mawasiliano ya ana kwa ana na muda wa familia.

    Hapo ndipo matumizi ya simu yanapohitaji mipaka.

    Siyo kila dakika ya mapumziko lazima ijazwe na matumizi ya simu au skrini.

    Wakati mwingine ndoa inahitaji dakika chache ambazo hakuna anayeshika simu.

    UPWEKE HAUJIBIWI KWA DATA,BANDO PEKEE

    Kuna jambo moja muhimu ambalo wanandoa wanapaswa kulifikiria.

    Kama mtu anatumia simu kila usiku kwa sababu hataki kukaa kimya na mwenza wake, huenda tatizo si simu.

    Huenda kuna mazungumzo ambayo hayajafanyika.

    Huenda kuna maumivu ambayo hayajasikilizwa.

    Huenda kuna migogoro ambayo imeachwa kwa muda mrefu.

    Huenda mmoja anahisi hapendwi, au anapuuzwa.

    Au huenda wote wawili wamekuwa wakiishi ndani ya ratiba yenye majukumu mengi kiasi kwamba wamesahau kujenga urafiki wao wenyewe.

    Katika hali kama hiyo, simu inaweza kutoa usumbufu wa muda lakini isitatue chanzo cha upweke.

    Ni dhahiri mazungumzo yanahitajika kati ya wanandoa ili kubaini chanzo cha upweke huo na kupatikana kwa suluhu isiyohusisha matumizi ya simu kama kimbilio au kichaka cha upweke.

    WANANDOA WANAHITAJI KUJENGA MUDA WAO

    Kuna umuhimu wa wanandoa kuwa na muda ambao ni wao.

    Muda wa kuzungumza, muda wa kula pamoja, muda wa kutembea. Muda wa kucheka, muda wa kuzungumzia fedha, watoto, kazi, mahusiano yao na mambo yanayowasumbua.

    Na wakati mwingine, muda wa kukaa bila simu.

    Hili si suala la teknolojia pekee. Ni suala la kuweka uhusiano mbele wakati ambapo kila mmoja anaweza kuwa na ulimwengu wake wa kidijitali.

    Utafiti wa mwaka 2024 kuhusu mahusiano ya wanandoa na mitandao ya kijamii ulionyesha kuwa matumizi ya mitandao yanaweza kuathiri namna wanandoa wanavyowasiliana na kuhusiana, jambo linaloonyesha umuhimu wa kuweka mipaka na kuwa na mawasiliano ya wazi kuhusu matumizi ya teknolojia ndani ya ndoa.

    SIMU ISIWE SEHEMU YA KUFICHA UPWEKE

    Mwanandoa anayejihisi mpweke si lazima aihitaji simu zaidi ya mwenza wake.

    Anaweza kuwa anahitaji mwenza wake zaidi.

    Anahitaji kuzungumza.

    Anahitaji kusikilizwa.

    Anahitaji kuulizwa anaendeleaje bila mazungumzo kuishia kwenye bili, watoto, chakula, kazi au majukumu ya nyumbani.

    Kwa sababu ndoa inaweza kuwa na kila kitu kinachoonekana nje lakini ikawa na upweke mkubwa ndani.

    Na wakati huo, simu inaweza kuwa rahisi zaidi kuishika kuliko kumtazama mwenza machoni na kusema:

    “Nahisi niko peke yangu.”

    Hilo ndilo jambo ambalo wanandoa wanahitaji kulifikiria.

    TEKNOLOJIA ISIJENGE UKUTA KATI YA WENZA

    Simu imebadilisha namna tunavyowasiliana. Imefanya iwe rahisi kumpata mwenza aliye mbali, kutuma ujumbe, kupiga video na kushirikishana maisha ya kila siku.

    Lakini teknolojia hiyo hiyo inaweza kuwa chanzo cha umbali ikiwa itaanza kuchukua nafasi ya mawasiliano ya kweli.

    Tafiti za Tanzania za mwaka 2017, 2019 na 2026 zinaonyesha namna tofauti kwamba simu na mitandao ya kijamii zinaweza kuwa na faida katika mahusiano, lakini matumizi yasiyo na mipaka yanaweza pia kuvuruga mawasiliano, kuongeza usiri, kuathiri uaminifu na kuleta migogoro.

    Kwa hiyo, suluhisho si kuwaambia wanandoa waache kutumia simu.

    Suluhisho ni kujenga utamaduni ambao simu inakuwa chombo cha kuimarisha ndoa, si mahali pa kukimbilia kila mmoja anapohisi mpweke.

    Kwa sababu mwisho wa siku, mtu anaweza kuwa na maelfu ya watu kwenye simu yake lakini bado akahitaji mtu mmoja tu aliyeko pembeni yake, na si mwingine ni mwenza wake.

    Na kama mtu huyo ni mwenza wake, basi labda kabla hajafungua simu kutafuta mtu wa kuzungumza naye, anapaswa kwanza kuuliza:

    “Tumepata lini muda wa kuzungumza?”

    Huenda jibu la upweke ndani ya ndoa lisianzie kwenye simu. Huenda linaanzia kwenye mazungumzo yaliyokosekana kati ya watu wawili wanaoishi chini ya paa moja.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Nyumbani kunaweza kuwa na watu wengi, lakini mazungumzo yakawa machache. Mzazi anaweza kuwa ameketi kwenye kiti akijibu ujumbe wa simu, mtoto akiwa upande mwingine akiangalia video na mwingine akicheza mchezo wa mtandaoni, huku muda ambao familia ingeutumia kuzungumza ukipita.

    Hii ndiyo hali mpya ambayo teknolojia imeleta ndani ya familia nyingi. Simu zimechukua nafasi kubwa katika kurahisisha mawasiliano, elimu, biashara na burudani. Hata hivyo, wakati huohuo zimeibua swali muhimu: Tunapokuwa karibu kimwili, je, bado tupo pamoja kihisia?

    Tanzania inaingia zaidi katika maisha ya kidijitali. Takwimu zilizowasilishwa Bungeni Juni 2026 zilionyesha kuwa asilimia 67 ya watoto wenye umri wa miaka 12 hadi 17 wanatumia simu janja, huku asilimia nne wakiwa wamewahi kukutana na aina fulani ya ukatili mtandaoni.

    Hii ina maana kwamba kwa kizazi kinachokua sasa, maisha ya mtandaoni si jambo la pembeni. Ni sehemu ya maisha yao ya kila siku.

    Na hapo ndipo jukumu la mzazi linapobadilika.

    MTOTO HAISHI TENA NDANI YA NYUMBA PEKEE

    Zamani, mzazi angeweza kujua kwa kiasi kikubwa mtoto wake yuko wapi, anaongozana na nani na anafanya nini baada ya kutoka shule.

    Leo, sehemu ya maisha ya mtoto inaweza kuwa mahali ambapo mzazi hawezi kuiona moja kwa moja.

    Mtoto anaweza kuwa chumbani kwake, lakini mazungumzo yake, marafiki zake, video anazotazama na taarifa anazopokea vinaweza kutoka sehemu mbalimbali za dunia kupitia simu yake.

    Mwanasaikolojia wa jamii, Shabani Riziki, amewahi kueleza kuwa mtoto anayejua kutumia teknolojia si lazima awe anaelewa hatari zinazoweza kuambatana nayo.

    Kwa mtazamo wake, watoto wanaweza kujua kufungua akaunti, kutumia programu tumizi na kufuta mazungumzo, lakini ujuzi huo hauwafanyi moja kwa moja kuwa salama dhidi ya hatari za mtandaoni.

    Hii ndiyo tofauti kati ya kujua kutumia simu na kujua kuishi kwa usalama katika dunia ya kidijitali.

    Mtoto anaweza kujua jinsi ya kufungua akaunti katika mitandao kama vile TikTok, Instagram au programu nyingine, lakini bado akahitaji mzazi wa kumsaidia kuelewa ni taarifa gani anapaswa kuamini, ni mtu gani anayepaswa kumkwepa na ni jambo gani anapaswa kuliripoti.

    SIMU IMEINGIA NDANI YA MALEZI

    Lakini teknolojia yenyewe si adui wa familia.

    Utafiti uliofanywa na Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa Tanzania (NIMR), kwa kushirikiana na REPSSI na Chuo Kikuu cha Stellenbosch, uliangazia namna simu janja zinavyoweza kutumiwa kuimarisha malezi na uhusiano kati ya mzazi na mtoto.

    Mradi huo ulihusisha programu ya simu yenye masomo, michezo, vitabu na shughuli za nyumbani zilizolenga kuwasaidia wazazi kutumia teknolojia kujenga mahusiano bora na watoto.

    Rahaba Mvuoni, Meneja wa Mradi kutoka REPSSI, alisema programu hiyo ilikuwa na masomo tisa yaliyolenga kuimarisha uhusiano wa mzazi na mtoto, kujenga ujuzi wa malezi na kuboresha afya ya akili ya wazazi.

    Alieleza pia kuwa mzazi angeweza kutumia dakika 10 hadi 15 kwa siku kusoma, kucheza au kujifunza pamoja na mtoto.

    Hapa ndipo tunapoona upande mwingine wa simu.

    Kifaa kilekile kinachoweza kumtenganisha mzazi na mtoto kinaweza pia kuwaunganisha, ikiwa kitatumiwa kwa kusudi hilo.

    WAZAZI NAO WANAHITAJI KUJIFUNZA

    Eva Nyella, mhudumu wa jamii kutoka Msasani, ni mmoja wa wazazi walioshiriki katika mpango huo.

    Alisema awali hakuwa na utaratibu maalumu wa kushirikiana na mtoto wake katika shughuli za kujifunza na kucheza, lakini programu hiyo ilimsaidia kubadilisha namna anavyomlea.

    Kwa upande wake, alieleza kuwa alianza kutumia muda mwingi kujifunza kuhusu malezi badala ya kutumia muda huo wote kuvinjari mitandao ya kijamii.

    Uzoefu huo unaibua jambo muhimu: tatizo si kwamba wazazi hawajali watoto wao. Wakati mwingine nao hawajui namna ya kuendana na mazingira mapya ambayo teknolojia imeyaleta katika malezi.

    Mtoto wa leo anakua katika dunia ambayo mzazi wake huenda hakuwahi kuishi akiwa mtoto.

    Mzazi alikulia katika mazingira ambayo habari ilipatikana kupitia kitabu, redio, runinga au mtu wa karibu. Mtoto wa leo anaweza kupata taarifa hiyo hiyo ndani ya sekunde chache kupitia simu.

    Pengo hilo la kizazi linahitaji mazungumzo, si lawama pekee.

    WAKATI SIMU INAPOANZA KUWA HATARI

    Pamoja na faida zake, maisha ya kidijitali yana upande mwingine ambao familia haipaswi kuupuuza.

    Mtoto anaweza kukutana na maudhui yasiyofaa, watu wasiojulikana, unyanyasaji mtandaoni, taarifa za uongo au watu wanaojenga uaminifu kwa mtoto kwa lengo la baadaye kumtumia vibaya.

    Shabani Riziki anasema ni muhimu kwa wazazi kujenga mazingira ambayo mtoto anaweza kueleza mambo anayokutana nayo mtandaoni bila kuogopa kuhukumiwa.

    Hili ni muhimu kwa sababu mtoto anayejua kwamba kila akisema jambo ataadhibiwa anaweza kuchagua kukaa kimya.

    Na ukimya huo unaweza kuwa hatari zaidi kuliko simu yenyewe.

    Mtoto anahitaji kujua kwamba akipokea ujumbe unaomtisha, akiona picha isiyofaa, akishawishiwa kukutana na mtu aliyemjua mtandaoni au akitishiwa, anaweza kumwambia mzazi bila kuogopa.

    WAZAZI WANAHITAJI KUJUA TEKNOLOJIA PIA

    Mtaalamu wa teknolojia, Dominic Dismas, anaonya kwamba wazazi hawawezi kuwalinda watoto katika mazingira ya kidijitali bila kuelewa, angalau kwa kiwango fulani, programu ambazo watoto wao wanatumia.

    Amesisitiza umuhimu wa wazazi kujifunza kutumia udhibiti wa wazazi, kuweka mipaka ya muda wa kutumia vifaa vya kidijitali na kufuatilia mazingira ya matumizi ya mtoto, siyo tu pale inapohitajika, bali iwe sehemu ya utamaduni wa familia.

    Hata hivyo, ulinzi huo haupaswi kugeuka kuwa upelelezi usioambatana na mazungumzo.

    Mtoto akihisi simu yake inachukuliwa kila mara, akaunti zake zinafunguliwa bila maelezo na kila anachofanya kinaonekana kuwa kosa, anaweza kujifunza kuficha zaidi mambo anayofanya, badala ya kujifunza namna ya kuwa salama mtandaoni.

    Ni muhimu pia kwa wazazi na walezi kuelewa namna mifumo ya kidijitali na mapendekezo ya maudhui inavyofanya kazi.

    Mtoto akitazama aina fulani ya maudhui mara kwa mara, mfumo unaweza kuendelea kumpa maudhui yanayofanana.

    Kwa hiyo, mtoto anahitaji kufundishwa kwamba si kila kitu kinachoonekana kwenye skrini ya simu au kishikwambi kimejitokeza kwa bahati.

    SERIKALI: SIMU HAIPASWI KUWA MZAZI

    Mjadala huu umefika pia katika ngazi ya Serikali.

    Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, amewahi kuwaonya wazazi dhidi ya kuwaacha watoto walelewe na simu, mitandao ya kijamii au marafiki.

    Alisisitiza kuwa mzazi ndiye mlezi wa kwanza na muhimu wa mtoto na kwamba jukumu la malezi haliwezi kukabidhiwa kwa vifaa vya kidijitali.

    Kauli hiyo inakuja wakati Serikali ikichukua hatua zaidi kuhusu usalama wa watoto mtandaoni.

    Miongoni mwa hatua zinazojadiliwa ni uwezekano wa kuanzisha laini maalumu za simu kwa watoto zitakazokuwa na mifumo ya kuchuja maudhui hatarishi.

    Hata hivyo, hatua kama hizi haziwezi kuchukua nafasi ya mzazi.

    Teknolojia inaweza kuchuja baadhi ya maudhui, lakini haiwezi kujua kila wakati mtoto anapitia hali gani kihisia, kwa nini amebadilika kitabia au kwa nini ameamua kukaa kimya.

    Hayo yanahitaji mzazi.

    FAMILIA INAPOKAA PAMOJA LAKINI HAIZUNGUMZI

    Huenda changamoto kubwa zaidi isiwe mtoto kutumia simu.

    Inaweza kuwa familia nzima kupoteza muda wa kuwa pamoja.

    Muda wa chakula unaweza kugeuka kuwa muda wa kuangalia simu. Muda wa kulala unaweza kugeuka kuwa muda wa kuendelea kuvinjari. Wazazi na watoto wanaweza kuwa sehemu moja, lakini kila mmoja akiwa katika dunia yake ya kidijitali.

    Hali kama hii inaweza kupunguza nafasi ya mazungumzo ambayo ndiyo hujenga uaminifu ndani ya familia.

    Mtoto anapokuwa na jambo linalomsumbua, mara nyingi hatamtafuta mzazi ambaye hawazungumzi naye.

    Atamtafuta mtu anayehisi anaweza kumsikiliza nje ya wazazi wake au mtandaoni.

    Ndiyo maana malezi ya kidijitali hayawezi kutenganishwa na malezi ya kawaida.

    HAITAKIWI SIMU IONDOLEWE, INATAKIWA ITUMIKE KWA UFAHAMU

    Mjadala kuhusu simu na familia unaweza kupotoshwa kama tutaweka mambo mawili tu: kumpa mtoto simu au kumpokonya simu.

    Ukweli uko katikati.

    Mtoto anaweza kutumia simu kujifunza, kusoma, kuwasiliana na familia, kupata taarifa na kujenga ujuzi.

    Lakini anahitaji pia mipaka.

    Anahitaji muda wa kulala bila skrini. Anahitaji kucheza. Anahitaji kuzungumza na wazazi. Anahitaji kukutana na watu ana kwa ana. Na anahitaji kujifunza kwamba si kila kitu anachokiona mtandaoni ni sahihi au salama.

    Mzazi naye anahitaji kujifunza kuweka mfano.

    Ni vigumu kumwambia mtoto, “Acha simu,” wakati mzazi mwenyewe hawezi kuiweka chini wakati wa chakula au mazungumzo.

    Kwa hiyo, familia inahitaji kuwa na utamaduni wa matumizi ya vifaa vya kidijitali wenye uwiano.

    SIMU IWE CHOMBO, ISIWE MBADALA WA FAMILIA

    Teknolojia haitarudi nyuma.

    Watoto wataendelea kukua katika dunia ya simu, mitandao ya kijamii, akili bandia na taarifa zinazopatikana kwa sekunde chache.

    Changamoto si kuwarudisha watoto katika dunia ambayo haipo tena. Changamoto ni kuwafundisha kuishi vizuri katika dunia hiyo.

    Mzazi anahitaji kujua mtoto wake yuko wapi mtandaoni, anazungumza na nani na anakutana na maudhui gani. Mtoto naye anahitaji kujua kwamba anaweza kutumia teknolojia bila kuruhusu teknolojia imtumie.

    Familia pia inahitaji kukumbuka kwamba kabla ya kuwa watumiaji wa simu, sisi ni wazazi, watoto, ndugu na familia.

    Simu inaweza kutuunganisha na mtu aliye maelfu ya kilomita kutoka tulipo.

    Lakini wakati mwingine, mtu tunayehitaji kuzungumza naye zaidi yupo upande mwingine wa chumba.

    Hapo ndipo swali la msingi linapobaki:

    Je, simu zetu zinatuunganisha na dunia, lakini zinatutenganisha na watu walio karibu nasi?

  • Na George Gabriel

    Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Magala, amefungua mafunzo ya siku moja kwa madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, yenye lengo la kuwajengea uwezo katika kutekeleza majukumu yao, hususan usimamizi wa fedha na rasilimali za umma.

    Akizungumza katika mafunzo hayo yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri, Magala alisema madiwani wana wajibu wa kusimamia kikamilifu maslahi ya wananchi waliowachagua kwa kuzingatia sheria, kanuni na maadili ya viongozi wa umma, pamoja na kuepuka vitendo vinavyoweza kusababisha mgongano wa maslahi.

    Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Mkoa wa Mtwara, Shedrack Mrema, alisema ni muhimu vikao na mabaraza ya madiwani kujadili kwa kina hoja zinazoibuliwa na CAG ili kuhakikisha Serikali inawajibika kutoa majibu na kuchukua hatua stahiki.

    Alisema hatua hiyo itasaidia kuimarisha uwajibikaji na kuongeza kasi ya utekelezaji wa shughuli za maendeleo kwa wananchi.

    Miongoni mwa mada zilizowasilishwa katika mafunzo hayo ni wajibu wa Baraza la Madiwani katika kusimamia rasilimali za Halmashauri, pamoja na wajibu na majukumu ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.

    Mada nyingine zilihusu mwenendo wa utekelezaji wa mapendekezo ya ukaguzi, pamoja na uchambuzi wa taarifa za fedha na miradi ya maendeleo.

    Kwa upande wao, madiwani Benjamini Masimbo na Salvatory Lyimo walipongeza kutolewa kwa mafunzo hayo, wakisema yamewasaidia kuongeza uelewa na uwezo katika kutekeleza majukumu yao ya udiwani.

    Madiwani hao waliahidi kutumia maarifa waliyoyapata kupitia mafunzo hayo kuimarisha usimamizi wa Halmashauri na rasilimali zake, ili kuhakikisha zinatumika kwa ufanisi na kuleta tija na manufaa kwa wananchi.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Mtoto wa kiume anapokua, mara nyingi huanza kufundishwa mapema kwamba siku moja atakuwa mwanaume wa familia. Anaambiwa anatakiwa kuwa jasiri, kufanya kazi, kujitegemea na kuhakikisha familia yake haikosi mahitaji muhimu.

    Lakini katika dunia inayobadilika, swali linabaki: Je, hayo ndiyo maandalizi yote anayohitaji mtoto wa kiume kabla hajawa mume na baba?

    Kuwa mwanaume si suala la kuwa na uwezo wa kupata fedha pekee. Ni pia kujua namna ya kuwasiliana, kuheshimu mwenza, kutunza familia, kufanya maamuzi, kushirikiana katika majukumu ya nyumbani na kuwa baba anayehusika katika malezi ya watoto wake.

    Kwa hiyo, malezi ya mtoto wa kiume yanahitaji kwenda zaidi ya maandalizi ya kupata kipato. Yanapaswa pia kumwandaa kwa maisha ya familia, mahusiano na jamii kwa ujumla.

    MWANAUME ANAPOFUNDISHWA KUWA MTOA MAHITAJI

    Katika jamii nyingi, moja ya alama zinazotumika kumpima mwanaume ni uwezo wake wa kuitunza familia.

    Utafiti wa Hali ya Ubaba Tanzania uliofanywa mwaka 2021 uliangalia ushiriki wa wanaume katika malezi na uangalizi wa watoto, haki za watoto, usawa wa kijinsia na kuzuia ukatili wa kijinsia.

    Utafiti huo ulifanyika katika mikoa tisa ya Tanzania Bara na ulihusisha washiriki 63, wakiwemo wazazi 52, maafisa watano wa Serikali na wawakilishi sita wa mashirika yasiyo ya kiserikali.

    Utafiti huo unaonyesha umuhimu ambao jamii inaupa wajibu wa mwanaume kama mtoa mahitaji ya familia. Hata hivyo, suala la ubaba haliishii kwenye uwezo wa kifedha.

    Mwanaume anaweza kuwa mtoa mahitaji na bado akawa baba ambaye hayupo makini katika maisha ya watoto wake.

    Hapo ndipo tunapopaswa kujiuliza: Je, kutoa mahitaji ndiyo kipimo pekee cha kuwa mume au baba bora?

    MUME SI MFUKO WA FEDHA PEKEE

    Kutoa mahitaji ya familia ni jukumu muhimu. Chakula, mavazi, makazi, elimu na mahitaji mengine ni sehemu ya msingi wa ustawi wa familia.

    Lakini familia inahitaji zaidi ya mahitaji ya kimwili.

    Mume anahitaji pia kujua namna ya kuwasiliana na mwenza wake, kusikiliza, kufanya maamuzi kwa ushirikiano na kushiriki katika malezi ya watoto. Baba naye anahitaji kuwa sehemu ya maisha ya watoto wake, si kwa kutoa fedha pekee, bali pia kwa kutoa muda, miongozo na uwepo wake kihisia.

    Hii haimaanishi kwamba kila jukumu la familia lazima ligawanywe kwa asilimia 50 kwa 50 kila siku. Familia zina mazingira tofauti, kipato tofauti na majukumu tofauti.

    Kinachohitajika ni mtoto wa kiume kukua akielewa kwamba familia ni ushirikiano. Anaweza kuwa mtoa mahitaji, lakini pia anapaswa kujua namna ya kumtunza mtoto, kusaidia kazi za nyumbani, kusikiliza mwenza wake na kushiriki katika maamuzi ya familia.

    Kwa mtazamo huo, ndoa si nafasi ya mtu mmoja kubeba kila jukumu huku mwingine akingoja kuhudumiwa. Ni uhusiano unaohitaji ushirikiano, mawasiliano na uwajibikaji kutoka kwa pande zote.

    FILIMON NKUNGU: “HATUWEZI KUZUNGUMZIA USAWA BILA KUWAHUSISHA WANAUME”

    Mfano wa umuhimu wa kuwashirikisha wanaume katika mabadiliko ya kijamii unaonekana katika kazi ya Filimon Nkungu, mkulima na kiongozi wa jamii kutoka Kijiji cha Samaka, Mkoa wa Singida.

    Katika taarifa kuhusu kazi yake kama mtetezi wa usawa wa kijinsia anayeshirikisha wanaume, Nkungu anasisitiza kwamba haiwezekani kuzungumzia usawa wa kijinsia au uwezeshaji wa wanawake bila kuwahusisha wanaume.

    Katika tafsiri ya Kiswahili ya kauli yake, anasema:

    “Hatuwezi kuzungumzia usawa wa kijinsia au uwezeshaji wa wanawake bila kuwahusisha wanaume. Tuna nafasi muhimu ya kutekeleza.”

    Kauli hiyo inaweka jukumu la mwanaume katika mtazamo mpana zaidi.

    Kwa mtoto wa kiume anayekua, ujumbe unaweza kuwa kwamba suala la uanaume si kuwa na mamlaka pekee ndani ya familia, bali pia kuwa sehemu ya kujenga mazingira ambayo kila mmoja anapata nafasi ya kushiriki na kufanikiwa.

    Nkungu pia anaeleza kwamba mabadiliko ya mitazamo hayaji mara moja. Katika tafsiri ya Kiswahili ya kauli yake, anasema:

    “Mabadiliko hayatokei katika mkutano mmoja; hutokea polepole, familia moja baada ya nyingine.”

    Hivyo, ikiwa tunataka kuwa na wanaume wanaoelewa ushirikiano katika familia za baadaye, mabadiliko hayo yanaweza kuanza wakati mtoto bado analelewa.

    MTOTO WA KIUME ANAJIFUNZA UANAUME KUTOKA KWA ANACHOKIONA

    Mtoto hujifunza kuhusu nafasi yake katika familia si kupitia maneno pekee, bali pia kupitia kile anachokiona nyumbani na katika mazingira yanayomzunguka.

    Anapokua akiona baba akifanya kazi za kutafuta kipato huku mama akifanya karibu majukumu yote ya nyumbani, anaweza kujenga picha kwamba kazi za nyumbani ni jukumu la mwanamke pekee.

    Ndiyo maana mtoto wa kiume anaweza kufundishwa kupika, kufua, kusafisha, kutunza mdogo wake na kufanya majukumu mengine ya kawaida ya nyumbani.

    Hii haipunguzi thamani yake kama mwanaume.

    Badala yake, inamfundisha kujitegemea na kumwandaa kuwa mtu anayeweza kushirikiana na wengine.

    Utafiti wa Hali ya Ubaba Tanzania uliangazia pia ushiriki wa wanaume katika malezi, haki za watoto, usawa wa kijinsia na kuzuia ukatili wa kijinsia.

    Kwa kuwa utafiti huo ulikuwa wa kimaelezo na ulihusisha washiriki 63 katika mikoa tisa ya Tanzania Bara, matokeo yake yanapaswa kutumiwa kuelewa mitazamo na uzoefu wa washiriki, badala ya kuyachukulia kama uwakilishi wa takwimu za wanaume wote nchini.

    Hilo ni muhimu katika kuzungumzia malezi ya wavulana: tunahitaji ushahidi, lakini pia tunahitaji kuangalia mazingira halisi ambayo watoto wanakulia.

    WANAUME HAWAPASWI KUFUNDISHWA KWAMBA HISIA NI UDHAIFU

    Kuna upande mwingine wa malezi ya mtoto wa kiume ambao mara nyingi haupewi nafasi kubwa: hisia.

    Mtoto wa kiume anaweza kukua akisikia kauli kama “wanaume hawalii”, “kuwa mwanaume” au “usioneshe udhaifu”.

    Kauli hizi zinaweza kuwa na nia ya kumfundisha mtoto kuwa jasiri. Lakini mtoto anahitaji pia kujua namna ya kutambua na kueleza hisia zake.

    Huzuni, hofu, kukatishwa tamaa na msongo wa mawazo ni sehemu ya maisha ya binadamu.

    Kumfundisha mtoto wa kiume kuzungumza kuhusu hisia zake hakumaanishi kumfanya awe dhaifu. Kunampa uwezo wa kuelewa anachopitia, kuwasiliana vizuri na kutafuta msaada inapohitajika.

    Uwezo huo unaweza kuwa muhimu sana anapokuwa mume, baba na mwanajamii.

    BABA WA KESHO ANAPASWA KUJIFUNZA KUWA MZAZI, SI MTOA MAHITAJI TU

    Kuwa baba kunahitaji zaidi ya kulipa gharama za familia.

    Ni kushiriki katika maisha ya mtoto, kujua anachopitia, kufuatilia maendeleo yake, kumsaidia anapokabili changamoto na kuwa sehemu ya malezi yake.

    Hapa ndipo tunapokutana na changamoto ya matarajio makubwa ya mwanaume kuwa mtoa mahitaji.

    Mwanaume anayehisi kwamba thamani yake yote kama baba inategemea kiasi cha fedha anacholeta nyumbani anaweza kujikuta akitumia muda mwingi katika shughuli za kutafuta kipato.

    Kwa upande mwingine, mtoto anahitaji pia muda na uwepo wa mzazi.

    Kwa hiyo, tunapomfundisha mtoto wa kiume kwamba mwanaume lazima awe mtoa mahitaji, tunapaswa pia kumfundisha kwamba kuwa baba kunahitaji uwepo, muda na ushiriki katika malezi.

    KUMFUNDISHA MTOTO WA KIUME KUJITEGEMEA

    Kabla ya mtoto wa kiume kuwa mume, anapaswa kwanza kujifunza kuwa mtu anayejitegemea.

    Afundishwe kupika, kufua, kusafisha mazingira yake, kupanga muda, kutunza fedha na kutatua matatizo ya kila siku.

    Ujuzi huu wakati mwingine huonekana kama mambo madogo.

    Lakini kijana anayejua kujitunza anapoingia kwenye ndoa haingii akimsubiri mwenza wake amfanyie kila kitu.

    Anaingia akiwa tayari kushirikiana.

    Na zaidi ya yote, anakuwa amejifunza kwamba kujitegemea si jukumu la jinsia moja. Ni ujuzi wa maisha.

    MAANDALIZI YA NDOA HAYANZII SIKU YA HARUSI

    Mara nyingi maandalizi ya ndoa huanza wakati kijana tayari ameamua kuoa.

    Lakini maandalizi muhimu zaidi yanaweza kuanza miaka mingi kabla.

    Yanajengwa kupitia namna mtoto anavyolelewa, elimu anayopata, mifano anayoiona nyumbani na namna anavyofundishwa kuhusu heshima, uwajibikaji na mahusiano.

    Kijana anayekulia katika mazingira yanayomfundisha kuheshimu watu wengine, kusikiliza, kushirikiana na kuwajibika ataingia kwenye utu uzima akiwa na msingi muhimu wa kujenga mahusiano yenye afya.

    Hivyo, maandalizi ya kuwa mume hayapaswi kuwa somo la siku moja. Ni mchakato unaoanza utotoni.

    NI AINA GANI YA MWANAUME JAMII INAKUSUDIA KUMJENGA?

    Swali hili linaweza kuonekana rahisi, lakini lina uzito mkubwa.

    Tunapomlea mtoto wa kiume, tunapaswa kujiuliza tunataka awe mtu wa aina gani baada ya miaka 20 au 30.

    Je, tunataka awe mwanaume anayejua kutafuta fedha pekee?

    Au tunataka awe mwanaume anayejua kufanya kazi, kusimamia fedha, kuheshimu mwenza wake, kulea watoto wake, kushiriki katika familia na kuwajibika kwa jamii?

    Kazi ya Filimon Nkungu inaonyesha umuhimu wa kuwashirikisha wanaume katika mabadiliko ya mitazamo kuhusu usawa wa kijinsia na mahusiano ndani ya familia.

    Katika tafsiri ya Kiswahili ya kauli yake, Nkungu anasema:

    “Ukweli ni kwamba wanaume wanaposimama pamoja na wanawake, maendeleo huwa hayazuiliki.”

    Ujumbe huo unaweza kutumika pia katika malezi ya wavulana: si kuwaandaa kupambana na wanawake wanapokuwa watu wazima, bali kuwaandaa kushirikiana nao katika familia na jamii.

    MWANAUME WA KESHO ANAANZA KUJENGWA LEO

    Mtoto wa kiume wa leo ndiye kijana, baba na mume wa kesho.

    Ndiyo maana malezi yake hayawezi kuishia kwenye kumfundisha kuwa na nguvu, kupata fedha au kutatua matatizo kwa kutumia mamlaka.

    Anahitaji pia kufundishwa namna ya kujenga mahusiano yenye heshima, kushirikiana, kuwasiliana na kuwa sehemu ya familia yake.

    Kumwandaa mtoto wa kiume kwa maisha ya baadaye si kumwambia tu kwamba siku moja atakuwa “kichwa cha familia”.

    Ni kumfundisha kwamba uongozi wa familia unahitaji hekima, uwajibikaji, heshima, uvumilivu na uwezo wa kusikiliza wengine.

    Kwa sababu mwanaume bora wa kesho haanzi kujengwa siku anapooa.

    Anaanza kujengwa akiwa mtoto.

  • Na Alex Msumeno

    Kamanda wa Kikosi cha Kuzuia Wizi wa Mifugo nchini, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Simon Pasua, amewataka viongozi wa kimila kuwa wasuluhishi wa migogoro katika jamii zao na kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuzuia migogoro baina ya wakulima na wafugaji.

    Wito huo umetolewa leo katika mnada wa mifugo uliopo Kata ya Kwala, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani, ambapo SACP Pasua alisema viongozi wa kimila katika jamii za wakulima na wafugaji wanapaswa kushirikiana na viongozi wa Serikali katika kutatua migogoro inayojitokeza.

    Alisema viongozi hao wanapaswa kutoa maelekezo kwa vijana wao, ikiwemo kutafuta maeneo ya malisho, mazizi na mabwawa ya maji yaliyo mbali na mashamba ya wakulima, ili kuepusha migogoro ambayo inaweza kusababisha mapigano na malumbano.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wafugaji wa Kata hiyo, Mzee Kieleni, alimshukuru Kamanda Pasua kwa kutembelea mnada huo na kusema huduma zinazotolewa na Jeshi la Polisi zimekuwa na mchango mkubwa katika kupunguza uhalifu na kuwabaini wahalifu, hususan kupitia Polisi Kata wanaoshirikiana na wananchi.

    Alisema pamoja na elimu waliyopata kuhusu namna ya kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu, wameelimishwa pia kuhusu ujenzi wa mazizi salama na njia za kutatua migogoro inayojitokeza katika shughuli zao za ufugaji.

    Aidha, aliomba Serikali itenge maeneo maalumu kwa ajili ya shughuli za kilimo na ufugaji ili kuepusha migogoro inayojitokeza mara kwa mara baina ya wakulima na wafugaji.

  • Waziri Saidi, Tabora

    Mkuu wa Polisi Jamii wa Tabora Manispaa, SP Honorata Oisso, amewaongoza maafisa na wakaguzi wa Jeshi la Polisi katika hafla ya kumuaga na kumpongeza Mkaguzi Mstaafu Hassara Mkobela.

    Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Tabora Manispaa jana katika Bwalo la Polisi, SP Novatus Nyabenda, ambaye pia ni Mkuu wa Usalama Barabarani wa Tabora Manispaa, SP Oisso alimpongeza kwa utumishi wake na mchango wake katika Jeshi la Polisi.

    Aidha, alizungumzia umuhimu wa mshikamano, ushirikiano na matendo ya huruma miongoni mwa askari, akieleza kuwa matendo hayo yanapaswa kuanzia ndani ya Jeshi la Polisi kabla ya kuifikia jamii.

    Alisema mshikamano na ushirikiano mzuri miongoni mwa askari ni sehemu muhimu ya kujenga uhusiano mzuri na jamii, jambo litakalosaidia katika kuzuia na kupunguza uhalifu pamoja na wahalifu katika Manispaa ya Tabora.

    Kwa upande wake, Happiness Mwakipesile, ambaye ni mtoto wa Mkaguzi mstaafu, aliwashukuru maafisa na askari wa Jeshi la Polisi kwa kuandaa hafla hiyo na kuendelea kudumisha ushirikiano mzuri.

    Alisema ushirikiano huo unatoa taswira nzuri kwa jamii na familia kwa ujumla, huku akieleza kuwa hafla hiyo imemfundisha mambo mengi kuhusu mshikamano na upendo miongoni mwa askari.

    “Ushirikiano huu ni mzuri na unaleta picha nzuri kwa jamii na familia kwa ujumla. Leo nimejifunza mambo mengi,” alisema Happiness.

    Katika hafla hiyo, askari walipata fursa ya kula pamoja, kupiga picha za pamoja na kumpatia Mkaguzi Mstaafu Hassara Mkobela zawadi mbalimbali kama ishara ya kumpongeza na kumtakia heri katika hatua yake mpya ya maisha.

  • Na George Gabriel

    Wananchi wa Kijiji cha Mkuula, Wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara, wameeleza kufurahishwa na mpango wa ujenzi wa mnara wa redio wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), wakisema mradi huo utawasaidia kupata taarifa mbalimbali za kitaifa na kijamii pamoja na burudani kwa wakati.

    TBC, kwa kushirikiana na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF), inatarajia kuanza ujenzi wa mnara huo katika Kijiji cha Mkuula, hatua inayolenga kuboresha usikivu wa matangazo ya TBC Taifa na Bongo FM katika maeneo ya Wilaya ya Nanyumbu.

    Akizungumza katika mkutano wa kijiji uliofanyika Agosti 13, 2026, Mkuula, Bi. Faith Munyi kutoka UCSAF alisema maandalizi ya ujenzi wa mnara huo tayari yameanza kwa hatua za awali.

    Alisema ujenzi huo unatarajiwa kutekelezwa kwa kasi ili kuhakikisha wananchi wa Wilaya ya Nanyumbu wanapata huduma bora ya redio kwa wakati, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wananchi katika kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa mafanikio.

    Katika mkutano huo, wananchi wa Kijiji cha Mkuula walionyesha utayari wa kushirikiana na utekelezaji wa mradi huo kwa kutoa eneo la ujenzi wa mnara bila malipo.

    Wananchi hao wameeleza matumaini kuwa uwepo wa mnara huo utachangia maendeleo ya kijiji kwa kuimarisha upatikanaji wa taarifa muhimu, elimu na burudani kwa jamii.

    Akizungumza na mwandishi wa habari, Mzee Juma Payao alisema wananchi wamefurahishwa sana na ujio wa mradi huo, huku akiishukuru TBC pamoja na Serikali kwa kuwakumbuka na kuwaletea huduma hiyo.

    Alisema kwa muda mrefu wananchi wa Mkuula wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya kutopata matangazo ya redio kwa urahisi, hali iliyowafanya kukosa taarifa mbalimbali muhimu zinazotolewa kupitia vyombo vya habari.

    “Tunashukuru sana TBC na Serikali kwa ujumla kwa kutuletea mradi huu. Tunaamini mnara huu utatusaidia kupata taarifa na burudani kwa wakati,” alisema Mzee Payao.

    Kwa upande wake, Zuhula Khalifani alieleza furaha yake kwa ujio wa mradi huo, akisema utakuwa mkombozi kwa wananchi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakikosa taarifa kutokana na changamoto ya usikivu wa redio.

    Alisema upatikanaji wa taarifa kupitia redio utawasaidia wananchi kufahamu mambo mbalimbali yanayoendelea ndani na nje ya eneo lao, pamoja na kupata elimu na burudani.

    Ujenzi wa mnara huo unatarajiwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha upatikanaji wa huduma za utangazaji kwa wananchi wa Nanyumbu, hususan katika maeneo ambayo yamekuwa yakikabiliwa na changamoto ya usikivu wa redio.