• Na Juma John Elisha

    Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimetangaza kuwa shauri la madai namba 14864, linalohusu mgawanyo wa mali za chama pamoja na maombi ya zuio dhidi yake, litatajwa kesho Jumatano, Agosti 5, 2026, saa 5:00 asubuhi katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, mbele ya Jaji Awamu Mbagwa.

    Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uenezi wa CHADEMA, Brenda Rupia, shauri hilo lililofunguliwa na Saidi Issa Mohammed na Ahmed Rashid Khamis linafikia hatua ya kutajwa baada ya kukamilika kwa majibizano ya kisheria kwa njia ya maandishi kati ya pande zote zinazohusika.

    Katika taarifa hiyo, CHADEMA imewahimiza wanachama wake, wafuasi, wadau wa demokrasia pamoja na waandishi wa habari kujitokeza mahakamani kufuatilia mwenendo wa shauri hilo, ikisisitiza umuhimu wa umma kushuhudia hatua za mchakato wa kesi hiyo.

    Kwa mujibu wa taratibu za mahakama, kutajwa kwa shauri ni hatua ya awali ya mchakato wa kesi ambapo mahakama hutoa maelekezo kuhusu hatua zinazofuata, ikiwemo ratiba ya usikilizwaji au masuala mengine ya kiutaratibu. Hivyo, kesho mahakama inatarajiwa kutoa maelekezo yatakayofuata kuhusu mwenendo wa shauri hilo.

  • Na George Gabriel

    Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu kupitia Kitengo cha Sheria imeendelea kutekeleza mpango wa kuwajengea uwezo wajumbe wa Mabaraza ya Kata kwa kutoa mafunzo ya uendeshaji wa mabaraza katika kata za Mikang’aula, Kamundi, Nangomba, Chipuputa, Masuguru, Nanyumbu na Mkonona.

    Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Sheria, Byera Nilo, alisema Mabaraza ya Kata ni nguzo muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata haki kupitia usuluhishi wa migogoro mbalimbali katika jamii.

    Alieleza kuwa migogoro ya ndoa inaweza kusuluhishwa katika Baraza la Kata kwa lengo la kufikia maridhiano kati ya pande husika na alisisitiza kuwa mamlaka ya kutoa talaka au kugawa mali za wanandoa yako chini ya vyombo vinavyotambuliwa kisheria.

    Kwa upande wake, Afisa Sheria, Dora Kapinga, alisema katika migogoro ya ardhi, Baraza la Kata hutoa usuluhishi wa awali, na pale usuluhishi unaposhindikana, shauri hupelekwa katika Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya kwa hatua zaidi za kisheria.

    Akizungumza kwa niaba ya washiriki baada ya mafunzo hayo, mmoja wa wajumbe wa Baraza la Kata, Fatuma Hussain, aliishukuru Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu pamoja na Serikali kwa kuandaa mafunzo hayo yaliyowaongezea uwezo, maarifa na uelewa wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

    Alisema elimu waliyoipata itawasaidia kushughulikia migogoro kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa, jambo litakalochangia kupunguza migogoro isiyo ya lazima na kuimarisha amani, umoja na haki katika jamii.

    Mafunzo hayo yamelenga kuongeza uelewa wa wajumbe wa Mabaraza ya Kata katika kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu, ili kuboresha utoaji wa haki na usuluhishi wa migogoro katika jamii.

    Washiriki walipatiwa elimu kuhusu majukumu ya Mabaraza ya Kata, taratibu za kupokea na kusikiliza mashauri, uandishi wa kumbukumbu na maamuzi ya mabaraza, pamoja na mipaka ya mamlaka yao kwa mujibu wa sheria.

    Aidha, walipata mafunzo kuhusu usuluhishi wa migogoro ya ndoa na ardhi, huku wakisisitizwa kutenda haki kwa uadilifu, weledi na kuzingatia misingi ya sheria katika utekelezaji wa majukumu yao.

  • Na Yusra Temba

    Imeelezwa kuwa matumizi ya teknolojia ya kidijitali katika ununuzi wa umma yanaendelea kupewa kipaumbele nchini kufuatia hitimisho la Kongamano la 10 la Ununuzi wa Umma lililofanyika jijini Arusha mwishoni mwa mweziu Julai. Kongamano hilo liliwakutanisha wadau kutoka sekta za umma na binafsi kujadili namna ya kuimarisha ufanisi, uwazi na ushindani katika michakato ya ununuzi wa umma kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

    Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Alnason Nguvila, alisema matumizi ya teknolojia ni muhimu katika kuimarisha mfumo wa ununuzi wa umma, akieleza kuwa mifumo ya kidijitali inaweza kuongeza uwazi, ushindani na ufanisi katika utekelezaji wa miradi na utoaji wa huduma za umma.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), Denis Simba, alisema dhima kuu ya kongamano hilo ilikuwa kutumia fursa zinazotokana na ununuzi wa umma kidijitali ili kufikia uchumi endelevu, shirikishi, jumuishi na wenye ushindani kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

    Alisema matumizi ya mifumo ya kidijitali yanaendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuongeza uwazi, kuimarisha ushindani wa haki na kuhakikisha thamani ya fedha katika utekelezaji wa shughuli za ununuzi wa umma.

    Naye Afisa Masoko wa Kampuni ya Blueberry Travel, Laylati Twaha, ambaye alipokea tuzo ya Mdhamini Bora katika kongamano hilo, alisema tukio hilo limewasaidia kujifunza zaidi kuhusu mfumo wa ununuzi wa umma na kuwapatia fursa za kupanua biashara zao kwa kushirikiana na serikali.

    Kongamano hilo liliwakutanisha maafisa manunuzi, maafisa sheria, wafanya maamuzi kutoka idara mbalimbali, wazabuni, wakandarasi pamoja na wataalamu wa sekta ya ununuzi wa umma, ambapo walijadili kwa kina matumizi ya teknolojia na uzingatiaji wa sheria katika hatua mbalimbali za ununuzi wa umma.

    Aidha, PPRA ilitambua mchango wa wadau mbalimbali kwa kutoa tuzo kwa taasisi na washiriki waliofanya vizuri katika nyanja tofauti za ununuzi wa umma. Hatua hiyo imelenga kuhamasisha ubora, uwajibikaji na uzingatiaji wa sheria ili kuongeza ufanisi katika sekta hiyo.

  • Na George Gabriel

    Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Benjamin Masimbo, ameongoza Mkutano wa Baraza la Madiwani ambapo baraza lilipokea na kujadili taarifa za maendeleo ya kata pamoja na taarifa za Kamati za Kudumu za Halmashauri kwa robo ya nne ya mwaka wa fedha 2025/2026.

    Mkutano huo ulifanyika katika Ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, ambapo pamoja na ajenda nyingine, Mwenyekiti Masimbo alijibu maswali mbalimbali ya papo kwa papo yaliyoulizwa na wajumbe wa Baraza.

    Wajumbe walieleza kuridhishwa na ufafanuzi na majibu aliyoyatoa kuhusu masuala mbalimbali yaliyowasilishwa.

    Katika mkutano huo, Masimbo alieleza kutoridhishwa na mwenendo wa malipo ya zao la ufuta kwa wakulima katika msimu wa mwaka huu na kuagiza mamlaka husika kuhakikisha wakulima wote ambao bado hawajapokea malipo yao wanalipwa kwa wakati.

    Pia alizitaka mamlaka zinazohusika kushughulikia changamoto zilizojitokeza katika ununuzi wa zao hilo na kusisitiza kuwa kasoro hizo zisijirudie katika msimu ujao wa ununuzi wa korosho.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Nanyumbu, Rashid Mrope, alisisitiza umuhimu wa kuboresha huduma za bima ya afya ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma hizo kwa wananchi.

    Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Katibu Tawala wa Wilaya, Juma Kanyinda, aliwataka viongozi na watendaji kusimamia kikamilifu utekelezaji wa majukumu yao. Aliwataka kuongeza juhudi katika kudhibiti utoro shuleni, kuimarisha usafi wa mazingira na kuhakikisha ujenzi wa vyoo unaendelea kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.

    Mkutano huo ulihitimishwa kwa wito kwa viongozi na watendaji kuendelea kushirikiana katika kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo na kuboresha huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Nanyumbu.

  • Na George Gabriel

    Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Donald Msengi, ameridhishwa na maandalizi yanayofanywa na Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu kuelekea Maonesho ya Nanenane 2026, huku akisisitiza kuwa kazi zilizobaki zikamilishwe kwa wakati na kwa ubora unaostahili.

    Kanali Msengi alitoa kauli hiyo jana baada ya kukagua banda la Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, ambapo alipongeza hatua zilizofikiwa katika maandalizi ya maonesho hayo.

    Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Ibrahim Mwanauta, alisema halmashauri imejipanga kikamilifu kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na Mkuu wa Mkoa ili kuhakikisha banda la Nanyumbu linakuwa miongoni mwa mabanda bora katika Maonesho ya Nanenane 2026.

    Mwanauta aliwataka wakuu wote wa idara na vitengo kushiriki kikamilifu katika maandalizi hayo, hususan maafisa wa kilimo, mifugo na biashara, kwa kuandaa maonesho yatakayoonesha ubunifu, matumizi ya teknolojia na mafanikio yaliyopatikana kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

    Alisema maonesho hayo ni fursa muhimu ya kuitangaza Wilaya ya Nanyumbu, kuvutia wawekezaji, kutoa elimu kwa wananchi na kuonesha huduma mbalimbali zinazotolewa na halmashauri.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Magala, amewasihi wananchi wa wilaya hiyo na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi kutembelea Maonesho ya Nanenane 2026 yatakayofanyika katika Viwanja vya Ngongo, mkoani Lindi.

    Alisema maonesho hayo ni jukwaa muhimu la kujifunza teknolojia za kisasa katika sekta za kilimo, mifugo, uvuvi na biashara, pamoja na kupata fursa za masoko na uwekezaji zitakazochangia kukuza uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla.

    Maonesho ya Nanenane 2026 Kanda ya Kusini yanatarajiwa kufanyika kuanzia Agosti 1 hadi 8, 2026, katika Viwanja vya Ngongo mkoani Lindi, yakiwa na kaulimbiu isemayo: “Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.”

    Serikali imeendelea kuwahimiza wananchi kutumia maonesho hayo kama fursa ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuhamasisha matumizi ya teknolojia mpya ili kuongeza tija katika uzalishaji na kuchochea maendeleo ya uchumi.

  • Na Andrea Mbona, Mbulu

    Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Manyara, Mrakibu wa Polisi Mikael Mwakasungura, ametembelea Wilaya ya Mbulu na kufanya kikao cha kazi na askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani wa wilaya hiyo, akiwakumbusha wajibu wao wa kusimamia sheria za usalama barabarani kwa weledi na uadilifu.

    Akizungumza katika kikao hicho, Mrakibu Mwakasungura alisema askari wanapaswa kutambua dhamana waliyonayo katika kusimamia sheria za usalama barabarani ili kusaidia kupunguza ajali ambazo zimekuwa zikisababisha vifo na majeruhi nchini.

    Alisisitiza kuwa utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia sheria, weledi na uadilifu ni msingi wa kuendelea kujenga imani na ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.

    “Fanyeni kazi kwa kuzingatia misingi ya sheria, weledi na uadilifu ili muendelee kuaminiwa na jamii,” alisema Mrakibu Mwakasungura.

    Katika ziara hiyo, Mrakibu Mwakasungura aliambatana na Mkuu wa Kitengo cha Usalama Barabarani Mkoa wa Manyara, Mrakibu Msaidizi wa Polisi ASP Mohamed Mlulu, ambaye aliwataka askari hao kufahamu na kutumia ipasavyo mifumo ya kielektroniki inayorahisisha utendaji kazi.

    Alisema mifumo hiyo ni muhimu katika usajili, uhifadhi na usimamizi wa taarifa mbalimbali zinazohusu usalama barabarani, hivyo ni lazima askari waendelee kuijua na kuitumia kwa ufanisi.

    Akizungumza kwa niaba ya askari wa Usalama Barabarani Wilaya ya Mbulu, Sajenti Brayan Mlawa alimshukuru Mkuu wa Kikosi kwa mafunzo na maelekezo aliyoyatoa, akiahidi kuwa askari hao wataendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kwa kuzingatia sheria.

    Akihitimisha ziara hiyo, Mrakibu Mwakasungura aliwataka askari kuendelea kutoa elimu kwa wamiliki wa vyombo vya moto na madereva kuhusu ukaguzi wa magari kwa njia ya kidijitali, hususan wakati huu ambapo ‘Wiki ya Nenda kwa Usalama’ inaelekea kuhitimishwa.

  • Na Damasi Kalembwe

    Jeshi la Polisi, kupitia Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Kinondoni, SP Edna Maro, limetoa elimu ya usalama kwa wafanyakazi wa Hoteli ya Golden Tulip iliyopo Masaki, Dar es Salaam, likiwataka kutambua kuwa kila mmoja ana wajibu wa kulinda mali za hoteli na kutekeleza majukumu yake kwa weledi huku akiepuka kujihusisha na vitendo vya uhalifu vinavyoweza kuharibu taswira ya hoteli na nchi kwa ujumla.

    Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, SP Maro alisema wizi ni kosa la jinai na kuwahimiza wafanyakazi kutoa taarifa kwa uongozi wa hoteli pamoja na Jeshi la Polisi wanapobaini viashiria vya uhalifu.

    Aidha, aliwataka kuwa walinzi wa wenzao, kuwapokea wageni na viongozi kwa heshima, kudumisha umoja mahali pa kazi na kufahamu adhabu zinazotokana na makosa ya wizi kwa mujibu wa sheria.

    Kwa upande wake, Mkaguzi wa Polisi wa Kata ya Msasani, Mkaguzi Joel Kaaya, aliwakumbusha umuhimu wa huduma bora kwa wateja wanaoingia na kutoka hotelini kwa kuwa huchangia kuimarisha usalama, kuongeza imani ya wageni na kukuza sekta ya utalii nchini.

    Akizungumza kwa niaba ya uongozi wa hoteli, Bi. Grace Karsan alilishukuru Jeshi la Polisi kwa kutoa mafunzo hayo, akisema yameongeza uelewa wa wafanyakazi kuhusu masuala ya usalama.

    Naye Miraji Juma, akizungumza kwa niaba ya wafanyakazi, aliomba mafunzo kama hayo yaendelee kutolewa mara kwa mara katika hoteli mbalimbali ili kuongeza uelewa wa masuala ya usalama na kuwajengea wafanyakazi uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

  • Na Damasi Kalembwe

    Mashindano ya michezo ya Polisi Jamii Cup katika Mkoa wa Kinondoni yamezinduliwa rasmi Julai 27, 2026, katika viwanja vya michezo vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

    Uzinduzi huo ulihudhuriwa na Mgeni Rasmi, Mkuu wa Ushirikishwaji wa Jamii Mkoa wa Kinondoni, ACP Ally Wendo, aliyeambatana na Wakuu wa Himaya za Kinondoni na Kawe pamoja na Maafisa Watendaji wa Wilaya (DCEO) wa maeneo hayo.

    Akizungumza kwa niaba ya askari na washiriki wote, Koplo Itumbi Wambura alisema mashindano hayo ni fursa muhimu ya kuwakutanisha askari polisi na wananchi wanaowahudumia, hivyo kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya pande hizo mbili.

    Alisema lengo kuu la mashindano hayo ni kupata wachezaji mahiri watakaounda timu imara ya mkoa, sambamba na kuhamasisha afya bora kupitia mazoezi na michezo.

    Aidha, mashindano hayo yanalenga kuongeza mshikamano, kufahamiana na kujenga ushirikiano wa dhati kati ya Jeshi la Polisi, jamii na wajumbe kutoka wilaya zote tano zinazoshiriki.

    Katika siku ya ufunguzi, timu mbalimbali zilishiriki katika michezo ya riadha, kuvuta kamba, mpira wa miguu na mpira wa pete. Washiriki walionyesha ushindani mkubwa katika kila mchezo wakilenga kuzipatia ushindi himaya zao.

    Matokeo ya michezo ya ufunguzi yalionesha Mkoa wa Kinondoni ukiibuka bingwa katika riadha na mpira wa pete. Kwa upande wa mchezo wa kuvuta kamba, Himaya ya Kawe iliibuka mshindi, huku mchezo wa mpira wa miguu kati ya Kinondoni na Kawe ukimalizika kwa sare ya mabao 2-2.

  • Na Jastini Bukebuke

    Walimu wa Shule ya Msingi Simbaguji, iliyopo Kata ya Kanyala, Wilaya ya Geita, wametakiwa kuimarisha usimamizi wa vilabu vya kupinga ukatili wa kijinsia shuleni ili viendelee kuwajengea wanafunzi uelewa wa haki zao, ujasiri wa kutoa taarifa, maadili mema na uwezo wa kujilinda dhidi ya ukatili pamoja na vitendo vingine vinavyohatarisha usalama wao.

    Wito huo ulitolewa jana na Polisi Kata wa Kanyala, Inspekta Said Juma, alipokuwa akitoa elimu ya kinga kwa walimu na wanafunzi wa shule hiyo.

    Akizungumza katika elimu hiyo, Inspekta Juma alisema vilabu vya kupinga ukatili wa kijinsia ni nyenzo muhimu katika kuwafundisha wanafunzi kutambua haki zao, kutoa taarifa kwa wakati wanapobaini viashiria vya ukatili na kujiepusha na mazingira yanayoweza kuhatarisha usalama wao.

    Aidha, aliwataka walimu kuhakikisha vilabu hivyo vinaendelea kufanya kazi kwa ufanisi kupitia mikutano ya mara kwa mara, utoaji wa elimu endelevu na ushirikiano wa karibu kati ya shule, wazazi na jamii ili kuimarisha ulinzi wa watoto.

    Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Simbaguji, Renatus Misago Chigunga, alilipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kutoa elimu ya kinga shuleni.

    Alisema ushirikiano huo unachangia kuongeza uelewa wa wanafunzi kuhusu masuala ya usalama, kuimarisha maadili mema na kujenga mazingira salama na rafiki ya kujifunzia.

  • Na George Gabriel

    Wananchi wa Kijiji cha Masugulu, Wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara, wameiomba Serikali kuhakikisha Mradi wa Maji wa Mto Ruvuma–Mangaka unakamilika kwa wakati ili waanze kunufaika na huduma ya maji safi na salama.

    Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Mwanahawa Juma alisema licha ya mradi huo kuanza kutekelezwa, bado wanaiomba Serikali kuongeza kasi ya utekelezaji ili kutimiza ahadi ya kuwapatia maji ya uhakika na kuondoa kero ya muda mrefu.

    “Tunaishukuru Serikali kwa kuleta mradi huu mkubwa, lakini tunaomba ukamilike haraka kwa sababu tumekuwa tukiusubiri kwa muda mrefu tangu Rais alipotuahidi,” alisema Mwanahawa.

    Naye Mzee Shaibu Lipindi alisema upatikanaji wa maji ya uhakika utapunguza adha ambayo wananchi wamekuwa wakikabiliana nayo kwa miaka mingi. Aliipongeza Serikali kwa kuendelea kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo yenye manufaa kwa wananchi.

    Kwa upande wake, mwakilishi wa mkandarasi, AFCONS Infrastructure Ltd, alisema kampuni hiyo imepokea maelekezo ya Mkuu wa Mkoa ya kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo. Aliahidi kuwa watafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha mradi unakamilika ndani ya muda uliopangwa.

    Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Donald Msengi, alimtaka mkandarasi kuongeza nguvu kazi, vifaa na rasilimali nyingine muhimu ili kuhakikisha mradi huo wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 38.1 unakamilika kwa wakati na kuanza kutoa huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Nanyumbu na maeneo ya jirani.

    Serikali imeendelea kusisitiza kuwa upatikanaji wa maji safi na salama ni miongoni mwa vipaumbele vyake katika kuboresha maisha na kuchochea maendeleo ya wananchi.

    Maoni ya wananchi pamoja na agizo la Mkuu wa Mkoa kwa mkandarasi yalitolewa wakati wa ziara ya Kanali Donald Msengi ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo.