Na Andrea Mbona, Mbulu
Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Manyara, Mrakibu wa Polisi Mikael Mwakasungura, ametembelea Wilaya ya Mbulu na kufanya kikao cha kazi na askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani wa wilaya hiyo, akiwakumbusha wajibu wao wa kusimamia sheria za usalama barabarani kwa weledi na uadilifu.
Akizungumza katika kikao hicho, Mrakibu Mwakasungura alisema askari wanapaswa kutambua dhamana waliyonayo katika kusimamia sheria za usalama barabarani ili kusaidia kupunguza ajali ambazo zimekuwa zikisababisha vifo na majeruhi nchini.
Alisisitiza kuwa utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia sheria, weledi na uadilifu ni msingi wa kuendelea kujenga imani na ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.
“Fanyeni kazi kwa kuzingatia misingi ya sheria, weledi na uadilifu ili muendelee kuaminiwa na jamii,” alisema Mrakibu Mwakasungura.
Katika ziara hiyo, Mrakibu Mwakasungura aliambatana na Mkuu wa Kitengo cha Usalama Barabarani Mkoa wa Manyara, Mrakibu Msaidizi wa Polisi ASP Mohamed Mlulu, ambaye aliwataka askari hao kufahamu na kutumia ipasavyo mifumo ya kielektroniki inayorahisisha utendaji kazi.
Alisema mifumo hiyo ni muhimu katika usajili, uhifadhi na usimamizi wa taarifa mbalimbali zinazohusu usalama barabarani, hivyo ni lazima askari waendelee kuijua na kuitumia kwa ufanisi.
Akizungumza kwa niaba ya askari wa Usalama Barabarani Wilaya ya Mbulu, Sajenti Brayan Mlawa alimshukuru Mkuu wa Kikosi kwa mafunzo na maelekezo aliyoyatoa, akiahidi kuwa askari hao wataendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kwa kuzingatia sheria.
Akihitimisha ziara hiyo, Mrakibu Mwakasungura aliwataka askari kuendelea kutoa elimu kwa wamiliki wa vyombo vya moto na madereva kuhusu ukaguzi wa magari kwa njia ya kidijitali, hususan wakati huu ambapo ‘Wiki ya Nenda kwa Usalama’ inaelekea kuhitimishwa.





















