• Na Cosmas Msuha

    Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, TAKUKURU Mkoani Rukwa imefanikiwa kudhibiti vitendo vya rushwa katika miradi ya maendeleo yenye thamani ya shilingi bilioni 1.7 kwa kipindi cha Oktoba hadi Disemba mwaka 2025.

    Mkuu waTAKUKURU Mkoa wa Rukwa,  Mzalendo Widege  aliyasema hayo katika taarifa yake kwa umma ambapo inaonesha kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2026, TAKUKURU Mkoani humo imepanga  kufuatilia matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo pamoja na mali za watuhumiwa ili kufidia hasara zinazotokana na vitendo vya rushwa.

    Alisema katika kuboresha utekelezaji wa miradi, TAKUKURU ilitoa mapendekezo kadhaa ikiwemo matumizi ya wahandisi waliosajiliwa, matumizi ya vifaa vya kujikinga kwa mafundi, kutangaza zabuni mapema kupitia mfumo wa NeST pamoja na kuimarisha vikao katika eneo la mradi na utunzaji wa nyaraka.

     Katika hatua nyingine, alisema TAKUKURU ilifanikiwa kumrejesha mkandarasi aliyekuwa ameacha ujenzi wa bweni na madarasa katika Shule ya Sekondari Mzindakaya.

    “Mradi huo wenye thamani ya shilingi milioni 380 ulisimama kwa miezi miwili kuanzia Oktoba hadi Novemba 2025 kutokana na mkandarasi huyo kuwa na zabuni nyingi, alisema Widege.

    Sanjali na hayo alitoa taarifa ya kuhusu uchambuzi wa mifumo ambapo taasisi hiyo imefanya tathmini ya ukusanyaji mapato katika Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo na usimamizi wa Jumuiya za Maji ngazi ya Jamii katika Wilaya ya Sumbawanga, ambapo mapendekezo yametolewa na ufuatiliaji unaendelea.

    Katika taarifa yake alibainisha jumla ya malalamiko 64 yalipokelewa katika kipindi hicho ambapo kati ya hayo, malalamiko 35 sawa na asilimia 55 yalihusu rushwa, huku 29 sawa na asilimia 45 hayakuhusu rushwa.

    “Malalamiko yasiyohusu rushwa yalifungwa baada ya ushauri, wakati yale yanayohusu rushwa uchunguzi unaendelea”, alisema Widege.

    Akizungumzia suala la elimu kwa umma, TAKUKURU imeendesha semina 19, mikutano ya hadhara 15, maonesho matano, kuimarisha klabu 10 za wapinga rushwa na kufungua klabu moja mpya na kudai kuwa hatua hiyo imeongeza mwitikio wa wananchi kutoa taarifa za vitendo vya rushwa.

    Widege aliwataka wananchi kuepuka vitendo vya  rushwa na kuendelea kutoa taarifa kupitia simu ya bure 113 au namba ya Mkuu wa TAKUKURU Mkoa 0738150186.

  • Na Cosmas Msuha

    Waziri wa Mifugo na Uvuvi Balozi Dkt. Bashiru Ally amefanya ziara mkoani Geita na kugagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya Soko la Kimataifa Samaki la Chato na kumtaka mkandarasi kukamilisha ujenzi wa mtambo wa kukaushia dagaa kabla ya mwezi April mwaka huu.

    Dkt. Bashiru alitoa maagizo hayo Februari 28, 2026 baada ya kukagua ujenzi wa miundombinu ya soko hilo ambapo ameonesha kutoridhishwa na kasi ya kazi zinazofanywa na mkandarasi huyo licha ya changamoto za malipo zinazomkabiri.A

    Aliagiza kufanyika tathmini mpya ya gharama za mtambo huo ili upatikane kwa haraka  ambapo kukamilika kwa ujenzi huo kutachangia upatikanaji wa ajira kwa makundi mbali mbali ya vijana katika soko hilo.

    “Nataka kazi ifanyike kwa kasi na Jumatatu barua iwe imejibiwa na mpaka Jumatano mkandarasi awe ameipata na mimi nipate nakala”, alisema Dkt. Bashiru

    Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Miundombinu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Mhandisi George Kwandu alisema kuchelewa kwa malipo kwa mkandarasi kulitokana na changamoto kadhaa ambazo zilisababisha mkandarasi kushindwa kununua mtambo kwa wakati hatahivyo wamejipanga kujadiliana na kuzifanyia kazi ili kuharakisha malipo hayo.

    Sanjali na maagizo hayo, Dkt. Bashiru amemtaka mkandarasi huyo kushirikiana na taasisi nyingine katika uimarishaji wa miundombinu na huduma za kijamii ikiwemo miundombinu ya maji, umeme, barabara ili soko hilo litambuliwe kimataifa na kuanza kufanya kazi kwa manufaa ya wananchi.

  • Na Mwandishi Wetu, Nachingwea – Lindi

    Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea, Mohamed Hassan Moyo ameongoza zoezi la ugawaji wa miche zaidi ya elfu sabini ya mikorosho kwa wananchi, ikiwa ni juhudi za kuongeza uzalishaji wa zao la korosho wilayani humo.

    Akizungumza wakati wa zoezi hilo tarehe 23/02/2026, Moyo alisema serikali imeamua kuwapatia wakulima miche hiyo bila malipo ili kupunguza gharama za uzalishaji na kuwawezesha kuongeza kipato chao.

    Ameeleza kuwa mpango huo unatekelezwa kwa lengo la kuimarisha sekta ya kilimo na kuinua uchumi wa wananchi.

    Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Adinan Mpyagila, ambaye ameshiriki katika zoezi hilo, amesema ugawaji wa miche hiyo ya mikorosho utachochea ongezeko la uzalishaji na kuboresha ubora wa zao la korosho wilayani hapo.

    Kwa upande wao, wakulima walishukuru kupata miche hiyo, walisema hapo awali walikuwa wakisubiri kwa muda mrefu kupata mavuno walipopanda miche ya zamani tofauti ni miche mipya waliyopewa ambayo itawawezesha kupata mavuno kwa muda mfupi zaidi.

    Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa serikali wa kuendeleza mazao ya kimkakati, ikiwemo korosho, kwa lengo la kuongeza mapato ya wakulima na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

  • Na Vincent Mpepo

    Waumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Mtaa wa Kwembe, wameungana na watu wengine duniani kuadhimisha Siku ya Wapendanao kwa namna ya kipekee, ambapo wanandoa walipatiwa mafunzo na uzoefu mbalimbali kama njia ya kukumbushana wajibu na haki zao katika ndoa taasisi inayotajwa kuwa msingi wa familia, jamii na taifa kwa ujumla.

    Hafla hiyo iliyofanyika jana katika ukumbi wa kanisa hilo, iliongozwa na viongozi wa mtaa wa kanisa pamoja na wawezeshaji kutoka ndani na nje ya kanisa.

    Katika mafundisho yaliyotolewa, ilibainika kuwa ukosefu wa elimu ya ndoa katika jamii ni moja ya vikwazo vikubwa vinavyosababisha ndoa kushindwa kukua, kutoeleweka na kuyumba.

    Akitoa mada katika maadhimisho hayo, Mwalimu na Mwanasaikolojia, Bupe Mwabenga, alisema jamii imekuwa haijali uwekezaji wa kutosha katika elimu ya ndoa, hali inayosababisha baadhi ya wanandoa kutoitambua ndoa kwa uzito unaostahili na kuichukulia kama jambo la kawaida.

    “Kumekuwa na mtazamo kuwa elimu ya ndoa ni jambo la kawaida na hivyo kutopewa kipaumbele, jambo ambalo si sahihi,” alisema Mwanasaikolojia Bupe.

    Alisema athari za ukosefu wa elimu ya ndoa ni pamoja na migogoro ya kifamilia, kuvunjika kwa ndoa na kuathirika kwa afya ya akili miongoni mwa wanandoa, hali inayowaacha watoto wakikua katika mazingira yasiyo salama kihisia na kimaadili.

    “Ifike wakati kila mwanandoa aache kumchukulia poa mwenza wake,” alisisitiza.

    Aidha, alitaja sababu nyingine zinazosababisha changamoto katika ndoa kuwa ni pamoja na athari za utandawazi, baadhi ya wanandoa kutojua kusudi la kuingia katika ndoa, pamoja na kutoelewa haki na wajibu wao ndani ya ndoa.

    Akizungumzia tabia ya wanandoa kujikita zaidi katika udhaifu wa wenza wao, Bupe alisema hali hiyo huchangia migogoro isiyo ya lazima, huku akisisitiza kuwa hakuna mwanadamu mkamilifu.

    “Mbinu mojawapo ya kuishi vyema katika ndoa ni kuyatambua madhaifu na mazuri ya mwenza wako, na zaidi kujikita katika kuyakuza mazuri yake badala ya kuganda na madhaifu,” alisema.

    Kuhusu changamoto za utandawazi, Bupe alisema jamii imejikita mno katika utafutaji wa mali na vyeo kana kwamba pesa ndiyo suluhisho la kila changamoto, hali inayochochea kiburi na kuathiri mahusiano ya ndoa.

    “Baadhi ya athari za pesa au cheo, hususan kwa wanawake, zimesababisha wanaume kujenga ukuta wa kujihami, jambo linalodhoofisha ustawi wa ndoa,” alifafanua.

    Kwa upande wake, mwezeshaji mwingine wa mada, James Betram, alisisitiza umuhimu wa kila mwanandoa kujijengea sababu ya kupendwa na mwenza wake, licha ya mafundisho ya kibiblia yanayoeleza kuwa upendo haujivuni wala haufanyi ubaguzi.

    Aliongeza kuwa baadhi ya mabadiliko ya kisasa yamesababisha wanandoa kutochukulia ndoa kwa uzito unaostahili, hali inayofanya ndoa kuonekana kama jambo la mazoea.

    “Ni muhimu kwa wanandoa kudumisha mawasiliano, kujali hisia za wenza wao na kuwa na moyo wa kusameheana ili kujenga mahusiano yenye afya na ustawi wa familia,” alisema Betram.

    Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Malezi na Uinjilisti ya kanisa hilo, Mratibu wa shughuli hiyo, Michael Mwambage, alisema ni wajibu wa kanisa kuendelea kuimarisha taasisi ya ndoa kwa kutoa elimu na jukwaa la kubadilishana uzoefu.

    “Ni vyema wanandoa kukutana kanisani, kujifunza na kubadilishana uzoefu badala ya kusherehekea Siku ya Wapendanao kwa namna nyingine zisizo na tija ya kudumu,” alisema Mwambage.

  • Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

    Katika mwendelezo wa utoaji wa elimu kwa umma, Jeshi la polisi limeendelea na kazi hiyo ambapo jana, Mratibu wa Program ya Usalama Wetu Kwanza Wilaya ya Kati na Kariakoo Mkaguzi Msaidizi wa Polisi (Insp) Martin Shila alifika katika Shule ya Msingi Olympio Iliyopo Upanga Dar es salaam na kuzungumza na wanafunzi wa Shule hiyo.

    Katika tukio hilo Insp Shilla aliwaeleza watoto hao kuwa kila mtu ana mchango katika kuzuia ukatili hivyo kuwataka kuwajibika katika kupambana na changamoto hiyo katika katika jamii.

    Aidha katika hatua nyingine Insp Shilla alibainisha mazingira hatarishi yanayoweza kusababisha ukatili kutokea na kuwaasa kutoa taarifa katika vituo vya polisi, ofisi za serikali za mitaa na mamlaka nyingine za kisheria.

  • Na Mwandishi Wetu, Dar es salaam

    Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Kariakoo Mrakibu wa Polisi (SP) Rosemary Kitwara amewataka wananchi kujiepusha na taarifa za upotoshaji zinazotolewa na watu mbalimbali wasio na mamlaka ya kutoa taarifa kwa jamii.

    SP Kitwara aliyasema hayo jana wakati wakati akizungumza na wafanyabiashara wa Kariakoo Dar es salaam ambapo amewaasa kupuuza taarifa za uongo zinazosambazwa katika mitandao ya kijamii ambazo vyanzo vyake si sahahi na hivyo kusababisha taharuki katika jamii.

    Pia amewaasa wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla kutojihusisha na  uhalifu na kuwaomba kutoa taarifa za wahalifu uharifu ili kuzuia vitendo hivyo katika eneo hilo la biashara na sehemu zingine.

  • Na Issa Mwadangala

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe limetoa taarifa ya matukio mawili ambapo katika tukio moja limeripoti kifo cha Feriki Kareai (54) Mkulima, Mkazi wa Kijiji cha Lukululu Wilaya ya Mbozi Mkoani Songwe, amabaye alikutwa amefariki dunia huku mwili wake ukiwa umefukiwa na kifusi pembeni mwa Mto Itemba.

    Kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la Polisi Mkoni humo, kifo hicho kilichotokea tarehe 01 Februari, 2026 saa 07:00 mchana katika maeneo ya Mto Itemba, Kijiji cha Lukululu, Kata ya Mlangali, Tarafa ya Iyula, Wilaya ya Mbozi, Mkoa wa Songwe.


    Uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa chanzo cha kifo ni marehemu kufukiwa na kifusi alipokuwa  anachimba madini aina ya dhahabu, hali iliyopelekea kifusi hicho kuporomoka na kumfukia  Hivyo kusababisha kifo chake.

    Na katika hatua nyingine, jeshi  hilo limetoa taarifa ya tukio la uhalifu lililotokea tarehe 04 Februari, 2026 saa 04:00 asubuhi, katika eneo la Kisimani, Mtaa wa Unyamwanga, Kata ya Tunduma, Wilaya ya Momba, Mkoa wa Songwe.

    Katika tukio hilo, Yengo Mwapina Mkazi wa Sogea Wilaya ya Momba Mkoani Songwe, alishambuliwa na watu watatu wasiojulikana akiwa njiani akitoka Benki ya NBC Tunduma.

    Kwa mujibu wa taarifa hiyo, washambuliaji hao walimfyatulia risasi na kumsababishia jeraha kiunoni upande wa kushoto na kumnyang’anya fedha taslimu kiasi cha Shilingi Milioni Hamsini na Nne (54,000,000) za kitanzania.

    Muhanga alikimbizwa katika Kituo cha Afya Tunduma ambapo alipatiwa matibabu ya awali na baadaye alihamishiwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe kwa ajili ya matibabu zaidi.

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe linaendelea na uchunguzi wa kina sambamba na msako mkali ili kuwabaini na kuwakamata watuhumiwa wa tukio hilo na kuwafikisha Mahakamani kwa hatua zaidi.

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe linatoa wito kwa wananchi kutojihusisha na shughuli za uchimbaji wa madini kiholela na bila kufuata taratibu za usalama na linawaomba wananchi kutoa taarifa zitakazosaidia kufanikisha kuwakamata watuhumiwa waliohusika katika tukio la unyang’anyi kwa kutumia silaha.