
Na Vincent Mpepo, OUT
Imeelezwa kuwa elimu ya darasani pamoja na mafunzo ya ufundi yanayotolewa katika mfumo rasmi bado hayajawawezesha wahitimu kuwa wabunifu, mahiri na wenye uwezo wa kukabiliana na changamoto za maisha na ajira katika mazingira halisi.
Hayo yamebainishwa leo katika mhadhara wa wazi uliofanyika katika ukumbi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, ambapo Profesa Mara Huber kutoka University at Buffalo aliwasilisha mada kuhusu mfumo wa kukuza stadi za ufundi kwa maendeleo ya uchumi wa viwanda.
Profesa Mara alisema kuna umuhimu wa kuanzishwa kwa mfumo wa kitaifa utakaounganisha elimu, mafunzo ya ufundi stadi, tafiti, ubunifu, viwanda pamoja na mahitaji ya soko la ajira ili kujenga wataalamu wenye ujuzi wa vitendo na uwezo wa kujitegemea.
Aidha, aliwasilisha matumizi ya nyenzo yake ya PEARL, inayolenga kuwawezesha watafiti, wanafunzi wa vyuo na ufundi pamoja na wadau wa maendeleo kujifunza kwa vitendo katika kutatua changamoto halisi za maendeleo, kuongeza thamani ya bidhaa na kubaini fursa mpya za ubunifu.
“Hata wahitimu wa shahada mara nyingi hawapati uwezo wa kukidhi mahitaji ya soko la ajira na mazingira halisi ya kazi,” alisema Profesa Mara.
Aliongeza kuwa kutokana na kasi ya maendeleo ya sayansi, teknolojia na matumizi ya akili unde, kuna umuhimu mkubwa wa elimu inayotolewa nje ya darasa kupitia uzoefu wa vitendo ili kuwajengea wahitimu umahiri wa kweli katika taaluma zao.
“Kujenga uwezo katika elimu ya ufundi kutasaidia kuongeza thamani ya elimu kwa kuwapa wahitimu ujuzi wa vitendo, mfano katika fani za uchomeleaji,” alisisitiza.
Akifungua mjadala huo, Mratibu wa Kigoda cha Viwanda na Maendeleo chuoni hapo, Dkt. Christopher Awinia alisema uchumi wa kati unaenda sambamba na maendeleo ya miundombinu ya kisasa, huku sekta ya uchomeleaji ikiwa miongoni mwa maeneo yanayokua kwa kasi na yanayohitaji kupewa kipaumbele maalumu.

Alitaja maeneo mbalimbali yanayotegemea stadi za uchomeleaji, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya gesi, madini, afya pamoja na mitambo ya viwandani, akisisitiza kuwa sekta hiyo ni muhimu kwa maendeleo ya taifa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitivo cha Sanaa na Sayansi za Jamii, Dkt. Dunlop Ochieng, aliwashukuru washiriki wa mhadhara huo na kueleza kuwa kigoda hicho ni jukwaa muhimu linalowakutanisha watafiti, wanazuoni na jamii kujadili masuala yenye manufaa kwa umma.
Akizungumzia elimu ya ufundi na stadi za maisha, alisema waliopata elimu miaka 30 au 40 iliyopita wanakumbuka namna shule za msingi na sekondari zilivyotoa elimu ya kujitegemea iliyowajengea wanafunzi ujuzi wa vitendo na kuwafanya kuwa mahiri katika shughuli mbalimbali hata baada ya kuhitimu.
Naye mhadhiri wa Sayansi ya Siasa, Dkt. Emmanuel Mallya, alisema mjadala kuhusu elimu ya ufundi unapaswa kuangalia namna mifumo ya elimu ya sasa isivyoendana na mahitaji halisi ya vijana.
“Tatizo si vijana, bali ni mifumo. Haiwezekani kijana aliyesomea taaluma fulani akaambiwa aende kuzalisha parachichi au mafuta bila kuwa na uhakika wa soko na kipato,” alisema Dkt. Mallya.
Alisisitiza umuhimu wa kuwa na mfumo wa elimu unaoanzia ngazi za chini ili kujenga kizazi kitakachoendana na mahitaji ya elimu ya ufundi na uchumi wa kisasa.

















