• Na Cosmas Msuha

    Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi imesema katika mwaka wa fedha 2026/27 inatarajia kuajiri watumishi wapya 10,919 pamoja na kutekeleza vipaumbele vinane vinavyolenga kuimarisha usalama, huduma za uraia na matumizi ya teknolojia nchini.

    Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo bungeni jijini Dodoma Mei 25, 2026, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi alisema ajira hizo ni sehemu ya mkakati wa kuongeza ufanisi katika vyombo vya usalama vilivyo chini ya wizara hiyo.

    Aidha, Idara ya Uhamiaji Tanzania inatarajia kuajiri watumishi 1,000 huku Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) ikipanga kuajiri watumishi 84 ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

    Katika bajeti hiyo, Waziri Katambi alisema wizara itaendelea kuboresha miundombinu ya vyombo vya usalama ikiwemo makazi ya maofisa, wakaguzi, askari pamoja na watumishi wasio askari ili kuongeza mazingira bora ya kazi na ufanisi wa utendaji.

    Pia wizara imepanga kuimarisha upatikanaji wa vitendea kazi, ikiwemo vyombo vya usafiri na usafirishaji kwa taasisi zote zilizo chini yake, hatua inayolenga kuongeza kasi ya utekelezaji wa majukumu ya kiusalama nchini.

    Mheshimiwa Katambi alisema wizara itaendelea kufanya tafiti mbalimbali kubaini sababu za kuongezeka kwa makosa mapya pamoja na kuweka mikakati madhubuti ya kuyadhibiti. Aliongeza kuwa matumizi ya TEHAMA yataendelea kupewa kipaumbele katika utoaji wa huduma na usimamizi wa shughuli za wizara hiyo.

    Katika miradi ya maendeleo, wizara itaanza ujenzi wa makao makuu ya NIDA jijini Dodoma, pamoja na ofisi 31 za usajili katika wilaya mbalimbali na kituo cha mafunzo na matengenezo ya vifaa vya TEHAMA mjini Kibaha.

    Mbali na hilo, wizara imesema itaendelea kuimarisha shughuli za uzalishaji mali kupitia sekta za kilimo, mifugo, viwanda pamoja na utunzaji wa mazingira.

  • Na Cosmas Msuha

    Shughuli za uchimbaji madini katika Mgodi wa Namungo uliopo Wilaya ya Ruangwa zimeendelea kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa eneo hilo, huku wachimbaji waliokuwa wakihangaika kimaisha wakianza kunufaika na maendeleo kupitia sekta ya madini.

    Akizungumza kwa niaba ya Afisa Madini Mkazi wa Lindi, Dickson Joram alisema shughuli za uchimbaji katika mgodi huo zimechangia kuboresha huduma za maji, elimu, afya pamoja na miundombinu huku zikifungua fursa za ajira na kukuza biashara kwa wananchi wa maeneo yanayouzunguka mgodi huo.

    Alieleza kuwa hali ya maisha ya wachimbaji na wananchi wa Namungo imebadilika kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na mwaka 2019, ambapo wachimbaji wengi walikuwa wakitumia njia duni za uzalishaji na kushindwa kumudu mahitaji muhimu ya kila siku.

    “Leo Namungo imebadilika kwa kiasi kikubwa, wananchi wanajitegemea na wanaendesha shughuli kubwa kupitia sekta ya madini,” alisema Mhandisi Joram.

    Kwa upande wake, Afisa Uhusiano wa kampuni ya Elianje Limited, Joseph Shayo alisema kampuni hiyo ilianza shughuli za utafiti na uchimbaji mwaka 2020 na imekuwa ikihakikisha jamii inayozunguka mgodi inanufaika kupitia miradi mbalimbali ya kijamii.

    Alisema kampuni hiyo imechimba visima na kusambaza maji katika Kijiji cha Tongwe pamoja na Kitongoji cha Namungo, huku ikiendelea kuboresha huduma ya maji safi na salama katika maeneo yenye changamoto ya upatikanaji wa maji.

    Katika sekta ya elimu, kampuni hiyo imejenga shule ya awali, kuboresha madarasa, kujenga vyoo vya kisasa na kushiriki katika ujenzi wa shule ya msingi katika Kitongoji cha Namungo ili kupunguza umbali wa wanafunzi kufuata elimu.

    Aidha, mgodi huo umechangia uboreshaji wa barabara zinazounganisha vijiji na kata jirani pamoja na kusaidia shule mbalimbali kwa vifaa vya elimu ikiwemo kompyuta na mashine za uchapishaji.

    Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Chingumbwa, Kata ya Mbekenyela Wilaya ya Ruangwa, Abdallah Manjakali alisema uwepo wa mgodi huo umefungua fursa nyingi za ajira, biashara na huduma za kijamii ambazo hapo awali zilikuwa changamoto kubwa kwa wananchi.

    “Leo wananchi wanapata kipato na maisha yameimarika, pia kampuni imenunua gari la wagonjwa linalowahudumia wananchi bure wakati wa dharura bila kuchangishwa fedha yoyote,” alisema Manjakali.

    Aidha, alisisitiza kuwa ushirikiano kati ya mgodi na jamii inayouzunguka unapaswa kuwa mfano kwa wawekezaji wengine wa sekta ya madini, huku akizitaka kampuni zenye leseni ambazo bado hazijaanza uzalishaji kuharakisha uwekezaji ili wananchi wanufaike zaidi na rasilimali zilizopo katika maeneo yao.

  • Na Cosmas Msuha

    Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imeridhishwa na maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa Msalato Satellite City unaotekelezwa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia programu ya Kupanga, Kupima na Kumilikisha Ardhi (KKK) katika eneo la Msalato jijini Dodoma.

    Ziara hiyo ya ukaguzi ililenga kujionea maendeleo ya mradi huo wenye ukubwa wa takribani ekari 971, unaotarajiwa kutumika kwa shughuli mbalimbali za maendeleo na unatarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa na maeneo yanayozunguka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato.

    Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Timotheo Mnzava, amepongeza juhudi zinazofanywa na wizara katika usimamizi wa sekta ya ardhi na kusisitiza kuwa utekelezaji wa mradi huo unaendana na mipango ya serikali ya upimaji na upangaji bora wa ardhi.

    Kwa upande wake, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapo, aliishukuru kamati hiyo kwa kutembelea mradi na kupokea taarifa ya utekelezaji wake. Pia aliahidi kuyafanyia kazi maelekezo yaliyotolewa ili kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa ufanisi, tija na kwa kuzingatia masilahi ya Taifa.

    Aidha, Dkt. Akwilapo alisema mradi huo utasaidia kuongeza thamani ya ardhi, kuboresha mipango ya matumizi ya ardhi, kuvutia wawekezaji na kufungua fursa mpya za kiuchumi katika maeneo yanayozunguka Uwanja wa Ndege wa Msalato.

    Katika ziara hiyo, Waziri Akwilapo aliambatana na Naibu Waziri wa wizara hiyo Kaspar Mmuya, Katibu Mkuu Anthony Sanga pamoja na wajumbe wa menejimenti na wataalamu mbalimbali wa wizara hiyo.

  • Na Mwandishi Wetu, Songea

    Jeshi la Polisi kupitia Kitengo cha Usalama Barabarani Mkoa wa Ruvuma limeendelea kutoa elimu ya usalama barabarani kwa wanafunzi wa Shule ya Awali na Msingi ya Good Shepherd Montessori iliyopo Mjimwema, Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma.

    Elimu hiyo ilitolewa na watendaji wa Dawati la Elimu kutoka Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Ruvuma ikiwa ni sehemu ya juhudi za Jeshi la Polisi za kujenga uelewa kwa jamii, hususan watoto, kuhusu matumizi sahihi na salama ya barabara.

    Akizungumza wakati wa utoaji wa elimu hiyo, Mkaguzi wa Polisi (Insp.) Nelson Mwambashi aliwataka wanafunzi kuzingatia kanuni za matumizi salama ya barabara wanapokuwa barabarani ili kujiepusha na ajali.

    Alisema wanafunzi wanapaswa kujenga utamaduni wa kutembea pembeni mwa barabara na kutumia vivuko maalum pamoja na taa za barabarani wakati wa kuvuka.

    Naye Mkaguzi wa Polisi (Insp.) Bahati Festo aliwakumbusha wanafunzi namna sahihi ya kutembea barabarani, kuvuka kwa usalama pamoja na kutambua alama muhimu za usalama barabarani zinazowaongoza watembea kwa miguu.

    Kwa upande wake, Koplo Samwel Saguli aliwataka wanafunzi kuwa mabalozi wa elimu hiyo kwa wenzao na jamii zinazowazunguka kwa kuelekeza matumizi sahihi ya alama za barabarani na kuonya dhidi ya kucheza barabarani.

    Alisema tabia ya kucheza barabarani inaweza kusababisha ajali zisizo za lazima zinazopelekea majeraha, ulemavu au hata vifo.

    Naye Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Joshua Sonsoge, alilishukuru Jeshi la Polisi Mkoa wa Ruvuma kwa kuendelea kutoa elimu ya kinga kwa wanafunzi, akisema hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa na nidhamu ya matumizi ya barabara kwa watoto wakiwa shuleni na hata wanapokuwa nyumbani.

  • Na Cartace Ngajiro, Tanga

    Serikali ya Jamhuri ya Rwanda imesema itaendelea kuimarisha uhusiano wa kibiashara na Bandari ya Tanga pamoja na kuendelea kutumia bandari hiyo kupitishia mizigo yake.

    Kauli hiyo imetolewa na Balozi wa Rwanda nchini Tanzania, Mhe. Jenerali Patrick Nyamvumba, alipofanya ziara katika Bandari ya Tanga kwa lengo la kujionea utendaji kazi wa bandari hiyo na kutathmini fursa mbalimbali zinazopatikana.

    Balozi Nyamvumba alisema Bandari ya Tanga ni kiunganishi muhimu katika usafirishaji wa mizigo ya kibiashara kwenda na kutoka Rwanda, hivyo kuna umuhimu wa kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kibiashara kati ya pande hizo mbili.

    Aidha, aliipongeza Bandari ya Tanga kwa huduma bora zinazotolewa katika kuhudumia mizigo ya Rwanda, jambo ambalo linaifanya nchi hiyo kuendelea kutumia bandari hiyo.

    Awali, Kaimu Meneja wa Bandari ya Tanga, Bw. Peter Millanzi, alisema Rwanda ni miongoni mwa nchi zinazotumia Bandari ya Tanga kupitishia mizigo yake.

    “Miongoni mwa bidhaa za Rwanda zinazopita katika Bandari ya Tanga ni pamoja na coil, magari, mitambo mbalimbali na mafuta,” alisema Millanzi.

    Aliongeza kuwa Bandari ya Tanga imejipanga kuendelea kuboresha huduma kwa wateja wake ili kuvutia mataifa na wafanyabiashara wengi zaidi kutumia bandari hiyo.

  • ← Back

    Thank you for your response. ✨

    Drag and drop or click to select a file.

    Na Cosmas Msuha

    WOMESA imewataka wanawake kutumia fursa mbalimbali za ajira zinazopatikana katika sekta ya bahari, ambazo zinagusa nyanja tofauti za kijamii na kiuchumi.

    Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani wa TASAC, Mwatano Maganga, wakati wa kongamano la maadhimisho ya umoja huo lililofanyika Bagamoyo, mkoani Pwani.

    Maganga alisema sekta ya bahari ni miongoni mwa sekta zinazotoa fursa nyingi za kiuchumi duniani kutokana na uwepo wa mnyororo mpana wa thamani unaowezesha shughuli mbalimbali za uchumi kufanyika kutoka eneo moja hadi jingine.

    Aidha, mdau wa sekta ya bahari, Dkt. Judith Mhina, aliwataka wanawake nchini na barani Afrika kujikita katika ajira zinazotokana na sekta hiyo ili kuchangia ukuaji wa uchumi binafsi na taifa kwa ujumla.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa WOMESA, Fatma Masenene, alisema maadhimisho hayo hufanyika kila mwaka katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kutoa nafasi ya wanawake wanaofanya kazi katika sekta ya bahari kukutana, kubadilishana uzoefu, na kuelimishana kuhusu fursa zilizopo.

    Aliongeza kuwa mwaka huu maadhimisho hayo yamefanyika Bagamoyo mkoani Pwani, ambapo washiriki walitembelea Chuo cha Uvuvi cha Mbegani pamoja na shule za sekondari za Asanari Damji, Zinga, Makurunge Coast na Kongo kwa ajili ya kuwaelimisha wanafunzi kuhusu fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya bahari.

    Washiriki wa kongamano hilo kutoka taasisi mbalimbali walishauri mamlaka zinazohusika na usimamizi wa sekta ya bahari nchini kuongeza juhudi katika utoaji wa fursa za ajira kwa wanawake ili kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya sekta hiyo.

  • Na Mwandishi Wetu, Ruvuma

    Wananchi wa Kijiji cha Maposeni wametakiwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za wahalifu na wageni wanaowatia shaka katika maeneo yao ili kudhibiti matukio ya uhalifu.

    Kauli hiyo ilitolewa na Polisi Kata wa Maposeni, Mkaguzi wa Polisi (Insp.) Ramadhani Duru, alipokuwa akizungumza na wananchi hao huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano katika masuala ya ulinzi na usalama.

    Aidha, aliwataka wananchi kushiriki kikamilifu katika ulinzi shirikishi, kulinda amani na kuepuka vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama wa jamii ili kuhakikisha mazingira salama kwa maendeleo ya wananchi.

    Katika hatua nyingine, wanafunzi wa Shule ya Msingi Lulimbo, Kata ya Tingi, Tarafa ya Mpepo, Wilaya ya Nyasa, wametakiwa kujiepusha na makundi mabaya yanayoweza kudhoofisha maendeleo yao ya kitaaluma na kuharibu mustakabali wao.

    Wito huo ulitolewa jana na Polisi Kata ya Tingi, Mkaguzi wa Polisi (Insp.) Juma Mbwana, alipotembelea shule hiyo kwa ajili ya kutoa elimu kuhusu maadili, usalama na maendeleo ya kijamii kwa wanafunzi.

    Aidha, wanafunzi hao walipata ufafanuzi kuhusu masuala ya ukatili wa kijinsia na madhara yake kwa watoto pamoja na jamii. Pia walielekezwa sehemu sahihi za kuripoti matukio ya uhalifu na namna bora ya kutoa taarifa hizo ili hatua za kisheria zichukuliwe kwa wakati.

    Sambamba na hayo, Insp. Mbwana aliwakumbusha madhara ya mimba za utotoni na umuhimu wa kuzingatia maadili mema huku akisisitiza nidhamu shuleni na katika jamii ili waweze kufikia malengo yao ya elimu na maisha kwa ujumla.

  • Na Mwandishi Wetu, Ruvuma

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Ruvuma limeendelea kusisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wananchi na vyombo vya usalama pamoja na matumizi sahihi ya elimu, vipaji na ubunifu wa vijana katika kudumisha amani, mshikamano na maendeleo ya jamii.

    Wito huo umetolewa Mei 8, 2026 na Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa wa Ruvuma, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Ramia Mganga wakati wa kikao kazi na Polisi Kata wa mkoa huo kilicholenga kujadili masuala mbalimbali ya kiutendaji na kuweka mikakati ya kuboresha utoaji wa huduma bora kwa wananchi. Kikao hicho kilifanyika katika ukumbi wa mikutano wa Polisi Mkoa wa Ruvuma.

    ACP Mganga aliwataka Polisi Kata kuongeza ushirikiano wa karibu na viongozi wa mitaa, vitongoji, kata pamoja na wananchi ili kusaidia kubaini changamoto mbalimbali zilizopo katika maeneo yao na kuzitatua kwa wakati, hatua itakayosaidia kuhakikisha jamii zinaendelea kuwa salama muda wote.

    Aidha, aliwasisitiza kuhakikisha wanafikia makundi yote katika jamii kwa kutoa elimu ya ushirikishwaji wa wananchi katika masuala ya usalama, ili kuongeza uelewa kuhusu madhara ya vitendo vya uhalifu pamoja na umuhimu wa kushirikiana na Jeshi la Polisi. Pia aliwataka kuendelea kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii ili kuimarisha mshikamano kati ya Polisi na wananchi.

    Katika hatua nyingine, Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Tunduru, Mkaguzi wa Polisi Sonda Mkoyi, amewataka vijana kutumia elimu, vipaji na fani walizonazo kama nyenzo ya kujiletea maendeleo binafsi na ya jamii kwa ujumla.

    Akizungumza Mei 8, 2026 wakati wa kongamano la vijana lililofanyika katika Ukumbi wa Skyway wilayani Tunduru, Insp. Mkoyi aliwahimiza vijana kuendelea kuwa mabalozi wa amani, uzalendo na utii wa sheria za nchi, pamoja na kujiepusha na vitendo vya uhalifu, matumizi ya dawa za kulevya, vurugu na ushawishi wa makundi yasiyo na maadili mema.

    “Jeshi la Polisi linaamini vijana ni nguvu kazi muhimu ya taifa, hivyo ushirikiano wao katika kudumisha usalama na utulivu wa nchi ni jambo la msingi”, alisema Insp. Mkoyi.

  • Na Mwandishi Wetu, Songea

    Wamiliki wa kampuni za ulinzi mkoani Ruvuma wametakiwa kuhakikisha wanasimamia ipasavyo na kulipa stahiki za askari wao kwa wakati, ili kuwaepusha na vitendo vya uhalifu kama vile wizi wa mali za wananchi pamoja na kuchukua mikopo yenye riba kubwa inayosababisha kukosa uadilifu kazini.

    Hayo yamesemwa leo na Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa wa Ruvuma, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Ramia B. Mganga, wakati alipokutana na wamiliki, viongozi wa makampuni binafsi pamoja na askari wao katika Bwalo la Polisi Wilaya ya Songea.

    ACP Mganga amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wamiliki wa makampuni ya ulinzi, akiwataka kuweka viwango vinavyofanana vya malipo kwa huduma wanazotoa kwa jamii hatua itakayosdaidia kuongeza mapato ya kampuni na hivyo kuwawezesha kuwalipa askari wao vizuri, na kuepuka upungufu wa wafanyakazi unaotokana na malipo duni.

    Aidha, amekemea baadhi ya kampuni zinazofanya kazi bila kuzingatia sheria na kanuni za usajili pamoja na umiliki wa silaha akitaja tabia ya kuazimana silaha kuwa ni kinyume cha sheria, na kuwataka kufuata taratibu zote ili kuepuka kuchukuliwa hatua za kisheria.

    Kwa upande wao, askari wa kampuni hizo wameahidi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kuhakikisha usalama katika maeneo yao ya kazi wameonesha utayari wao wa kutoa taarifa za matukio ya uvunjifu wa sheria watakayobaini ili wahusika wachukuliwe hatua stahiki.

    Madhumnuni ya mkutano huo yalikuwa ni pamoja na kujadili masuala mbalimbali ya kiutendaji ndani ya kampuni hizo.

  • Na Cosmas Msuha

    Tume ya Madini, kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), inaendelea kutoa mafunzo kwa wachimbaji wadogo nchini ili kuboresha ujuzi wao na kuongeza tija katika sekta ya madini na uendelezaji wa Taasisi ya Uchimbaji Mdogo wa Madini (FADev).

    Akizungumza na wananchi Aprili 19, 2026 mkoani Morogoro, mwakilishi wa FADev, Bi. Rehema Mkuli, alisema mkakati wa serikali unalenga kuwasaidia wachimbaji wadogo kwa kuwajengea uwezo wa kitaalamu na kuwahamasisha kutumia mbinu salama na zenye tija katika uchimbaji.

    Alisema kupitia mradi huo unaofadhiliwa na UNDP, wachimbaji watapata mafunzo ya msingi ikiwemo uchoraji wa ramani za kijiolojia pamoja na usanifu salama na bora wa mashimo ya uchimbaji.

    “Tunashukuru UNDP kwa kuwasaidia wachimbaji wadogo hususani wa madini ya ujenzi na viwanda ambao mara nyingi hawapati fursa ya kufadhiliwa kwani wafadhili wengi huelekeza nguvu kwenye sekta ya dhahabu, lakini UNDP imeonyesha njia kwa kusaidia kundi hili”, alisema Bi. Mkuli.

    Kwa upande wake, mkufunzi kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkoa wa Morogoro, Mjiolojia Asifiwe Ngala, alielezea umuhimu wa wachimbaji kujifunza uchoraji wa ramani za kijiolojia na  kuelewa aina mbalimbali za miamba na madini yaliyomo ndani yake ili kuboresha shughuli zao.

    “Ujuzi huu utasaidia kuongeza ufanisi katika utambuzi wa rasilimali asilia, kupunguza uchimbaji wa kubahatisha ili kuongeza tija katika uzalishaji,” alisema Ngala.

    Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, Vincent Mosha kutoka Kijiji cha Kinyenze, Manispaa ya Morogoro, alisema programu hiyo ni muhimu kwa maendeleo ya wachimbaji wadogo.

    Alieleza kuwa mafunzo hayo yatawasaidia wachimbaji kuepuka uharibifu wa mazingira, kufanya kazi kwa ushirikiano, kuweka akiba, na kusimamia vizuri mapato yao.

    “Mafunzo haya yana mchango mkubwa katika kuboresha maisha ya wachimbaji na familia zao pamoja na kukuza sekta ya madini kwa ujumla,” alisema Mosha.

    Mafunzo hayo yanatarajiwa kufanyika katika mikoa minne kati ya minane iliyofanyiwa utafiti wa maendeleo ya madini, ambayo ni Singida, Dodoma, Morogoro na Tanga.