• Na Vincent Mpepo

    Waumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Mtaa wa Kwembe, wameungana na watu wengine duniani kuadhimisha Siku ya Wapendanao kwa namna ya kipekee, ambapo wanandoa walipatiwa mafunzo na uzoefu mbalimbali kama njia ya kukumbushana wajibu na haki zao katika ndoa taasisi inayotajwa kuwa msingi wa familia, jamii na taifa kwa ujumla.

    Hafla hiyo iliyofanyika jana katika ukumbi wa kanisa hilo, iliongozwa na viongozi wa mtaa wa kanisa pamoja na wawezeshaji kutoka ndani na nje ya kanisa.

    Katika mafundisho yaliyotolewa, ilibainika kuwa ukosefu wa elimu ya ndoa katika jamii ni moja ya vikwazo vikubwa vinavyosababisha ndoa kushindwa kukua, kutoeleweka na kuyumba.

    Akitoa mada katika maadhimisho hayo, Mwalimu na Mwanasaikolojia, Bupe Mwabenga, alisema jamii imekuwa haijali uwekezaji wa kutosha katika elimu ya ndoa, hali inayosababisha baadhi ya wanandoa kutoitambua ndoa kwa uzito unaostahili na kuichukulia kama jambo la kawaida.

    “Kumekuwa na mtazamo kuwa elimu ya ndoa ni jambo la kawaida na hivyo kutopewa kipaumbele, jambo ambalo si sahihi,” alisema Mwanasaikolojia Bupe.

    Alisema athari za ukosefu wa elimu ya ndoa ni pamoja na migogoro ya kifamilia, kuvunjika kwa ndoa na kuathirika kwa afya ya akili miongoni mwa wanandoa, hali inayowaacha watoto wakikua katika mazingira yasiyo salama kihisia na kimaadili.

    “Ifike wakati kila mwanandoa aache kumchukulia poa mwenza wake,” alisisitiza.

    Aidha, alitaja sababu nyingine zinazosababisha changamoto katika ndoa kuwa ni pamoja na athari za utandawazi, baadhi ya wanandoa kutojua kusudi la kuingia katika ndoa, pamoja na kutoelewa haki na wajibu wao ndani ya ndoa.

    Akizungumzia tabia ya wanandoa kujikita zaidi katika udhaifu wa wenza wao, Bupe alisema hali hiyo huchangia migogoro isiyo ya lazima, huku akisisitiza kuwa hakuna mwanadamu mkamilifu.

    “Mbinu mojawapo ya kuishi vyema katika ndoa ni kuyatambua madhaifu na mazuri ya mwenza wako, na zaidi kujikita katika kuyakuza mazuri yake badala ya kuganda na madhaifu,” alisema.

    Kuhusu changamoto za utandawazi, Bupe alisema jamii imejikita mno katika utafutaji wa mali na vyeo kana kwamba pesa ndiyo suluhisho la kila changamoto, hali inayochochea kiburi na kuathiri mahusiano ya ndoa.

    “Baadhi ya athari za pesa au cheo, hususan kwa wanawake, zimesababisha wanaume kujenga ukuta wa kujihami, jambo linalodhoofisha ustawi wa ndoa,” alifafanua.

    Kwa upande wake, mwezeshaji mwingine wa mada, James Betram, alisisitiza umuhimu wa kila mwanandoa kujijengea sababu ya kupendwa na mwenza wake, licha ya mafundisho ya kibiblia yanayoeleza kuwa upendo haujivuni wala haufanyi ubaguzi.

    Aliongeza kuwa baadhi ya mabadiliko ya kisasa yamesababisha wanandoa kutochukulia ndoa kwa uzito unaostahili, hali inayofanya ndoa kuonekana kama jambo la mazoea.

    “Ni muhimu kwa wanandoa kudumisha mawasiliano, kujali hisia za wenza wao na kuwa na moyo wa kusameheana ili kujenga mahusiano yenye afya na ustawi wa familia,” alisema Betram.

    Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Malezi na Uinjilisti ya kanisa hilo, Mratibu wa shughuli hiyo, Michael Mwambage, alisema ni wajibu wa kanisa kuendelea kuimarisha taasisi ya ndoa kwa kutoa elimu na jukwaa la kubadilishana uzoefu.

    “Ni vyema wanandoa kukutana kanisani, kujifunza na kubadilishana uzoefu badala ya kusherehekea Siku ya Wapendanao kwa namna nyingine zisizo na tija ya kudumu,” alisema Mwambage.

  • Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

    Katika mwendelezo wa utoaji wa elimu kwa umma, Jeshi la polisi limeendelea na kazi hiyo ambapo jana, Mratibu wa Program ya Usalama Wetu Kwanza Wilaya ya Kati na Kariakoo Mkaguzi Msaidizi wa Polisi (Insp) Martin Shila alifika katika Shule ya Msingi Olympio Iliyopo Upanga Dar es salaam na kuzungumza na wanafunzi wa Shule hiyo.

    Katika tukio hilo Insp Shilla aliwaeleza watoto hao kuwa kila mtu ana mchango katika kuzuia ukatili hivyo kuwataka kuwajibika katika kupambana na changamoto hiyo katika katika jamii.

    Aidha katika hatua nyingine Insp Shilla alibainisha mazingira hatarishi yanayoweza kusababisha ukatili kutokea na kuwaasa kutoa taarifa katika vituo vya polisi, ofisi za serikali za mitaa na mamlaka nyingine za kisheria.

  • Na Mwandishi Wetu, Dar es salaam

    Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Kariakoo Mrakibu wa Polisi (SP) Rosemary Kitwara amewataka wananchi kujiepusha na taarifa za upotoshaji zinazotolewa na watu mbalimbali wasio na mamlaka ya kutoa taarifa kwa jamii.

    SP Kitwara aliyasema hayo jana wakati wakati akizungumza na wafanyabiashara wa Kariakoo Dar es salaam ambapo amewaasa kupuuza taarifa za uongo zinazosambazwa katika mitandao ya kijamii ambazo vyanzo vyake si sahahi na hivyo kusababisha taharuki katika jamii.

    Pia amewaasa wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla kutojihusisha na  uhalifu na kuwaomba kutoa taarifa za wahalifu uharifu ili kuzuia vitendo hivyo katika eneo hilo la biashara na sehemu zingine.

  • Na Issa Mwadangala

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe limetoa taarifa ya matukio mawili ambapo katika tukio moja limeripoti kifo cha Feriki Kareai (54) Mkulima, Mkazi wa Kijiji cha Lukululu Wilaya ya Mbozi Mkoani Songwe, amabaye alikutwa amefariki dunia huku mwili wake ukiwa umefukiwa na kifusi pembeni mwa Mto Itemba.

    Kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la Polisi Mkoni humo, kifo hicho kilichotokea tarehe 01 Februari, 2026 saa 07:00 mchana katika maeneo ya Mto Itemba, Kijiji cha Lukululu, Kata ya Mlangali, Tarafa ya Iyula, Wilaya ya Mbozi, Mkoa wa Songwe.


    Uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa chanzo cha kifo ni marehemu kufukiwa na kifusi alipokuwa  anachimba madini aina ya dhahabu, hali iliyopelekea kifusi hicho kuporomoka na kumfukia  Hivyo kusababisha kifo chake.

    Na katika hatua nyingine, jeshi  hilo limetoa taarifa ya tukio la uhalifu lililotokea tarehe 04 Februari, 2026 saa 04:00 asubuhi, katika eneo la Kisimani, Mtaa wa Unyamwanga, Kata ya Tunduma, Wilaya ya Momba, Mkoa wa Songwe.

    Katika tukio hilo, Yengo Mwapina Mkazi wa Sogea Wilaya ya Momba Mkoani Songwe, alishambuliwa na watu watatu wasiojulikana akiwa njiani akitoka Benki ya NBC Tunduma.

    Kwa mujibu wa taarifa hiyo, washambuliaji hao walimfyatulia risasi na kumsababishia jeraha kiunoni upande wa kushoto na kumnyang’anya fedha taslimu kiasi cha Shilingi Milioni Hamsini na Nne (54,000,000) za kitanzania.

    Muhanga alikimbizwa katika Kituo cha Afya Tunduma ambapo alipatiwa matibabu ya awali na baadaye alihamishiwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Songwe kwa ajili ya matibabu zaidi.

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe linaendelea na uchunguzi wa kina sambamba na msako mkali ili kuwabaini na kuwakamata watuhumiwa wa tukio hilo na kuwafikisha Mahakamani kwa hatua zaidi.

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe linatoa wito kwa wananchi kutojihusisha na shughuli za uchimbaji wa madini kiholela na bila kufuata taratibu za usalama na linawaomba wananchi kutoa taarifa zitakazosaidia kufanikisha kuwakamata watuhumiwa waliohusika katika tukio la unyang’anyi kwa kutumia silaha.

  • By Alvar Mwakyusa

    Tanzania is expected to experience varied rainfall during the Masika season from March to May 2026, with wetter conditions in some regions and drier weather in others, the Tanzania Meteorological Authority (TMA) has said.

    TMA Director General and Vice Chair of the Intergovernmental Panel on Climate Change, Dr Ladislaus Chang’a, said enhanced rainfall activity is likely in April, raising concerns over flooding, crop damage and outbreaks of water- and vector-borne diseases in vulnerable areas.

    He urged communities, authorities and sectors to take timely action and follow daily and ten-day forecasts for localized guidance.

    The Masika rains mainly affect the country’s bimodal rainfall zones, including the Lake Victoria Basin, Northern Coast, Northeastern Highlands and northern Kigoma. Normal to above-normal rainfall is expected over most parts of the Northern Coast, western Lake Victoria Basin—including Kagera and Geita—and northern Kigoma.

    These areas could experience periods of excessive soil moisture and localized flooding, which may disrupt farming, damage infrastructure and contaminate water sources.

    Normal to below-normal rainfall is forecast for the Northeastern Highlands, covering Arusha, Manyara and Kilimanjaro, and parts of the Lake Victoria Basin such as Mwanza, Shinyanga, Mara and Simiyu.

    Reduced river flows and declining reservoir levels may lead to water shortages for domestic use, livestock and irrigation.

    The rains are expected to start in late February to early March over the Lake Victoria Basin, early to mid-March along the Northern Coast, and mid-March in the Northeastern Highlands, before ending between late May and early June, depending on location.

    Health officials warn that heavy rains could increase malaria, cholera and other water-related diseases, particularly where flooding contaminates water sources and drier areas may also face health challenges linked to unsafe water.

    The outlook also highlights possible impacts on agriculture, livestock, transport, energy and water sectors whereas farmers in wetter areas may face waterlogging and crop losses, while drier zones risk reduced yields.

    Flooding could disrupt roads, railways and marine transport, and fluctuating water levels may affect hydropower generation and increase water treatment costs.

    TMA attributes the seasonal pattern to largely neutral sea surface temperatures in the Indian and Pacific Oceans, with weak westerly winds from the Congo Basin expected to enhance moisture inflow into parts of the western Lake Victoria Basin later in the season.

    Authorities, communities and the private sector are urged to use forecast in planning and preparedness measures, and to rely on official updates issued by TMA.

  • Na Alvar Mwakyusa

    Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetangaza mwelekeo wa mvua za msimu wa Masika kwa mwaka 2026, ikieleza kuwa baadhi ya maeneo yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka yanatarajiwa kupata mvua za wastani hadi juu ya wastani, huku maeneo mengine yakitarajiwa kupata mvua za wastani hadi chini ya wastani.

    Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Februari 5, 2026, mvua za Masika zinazotarajiwa kuanza mwezi Machi hadi Mei zitahusisha zaidi ukanda wa Ziwa Victoria, Nyanda za juu Kaskazini Mashariki, Pwani ya Kaskazini pamoja na Kaskazini mwa mkoa wa Kigoma.

    TMA imeeleza kuwa ongezeko la mvua linatarajiwa zaidi mwezi Aprili, hali inayoweza kuambatana na athari mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

    Akizungumza wakati wa kutangaza mwelekeo huo, Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Ladislaus Chang’a, ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), alisema ni muhimu kwa jamii kutumia taarifa za utabiri wa hali ya hewa katika kupanga na kutekeleza shughuli zao za kila siku.

    Alisema mvua hizo, pamoja na faida zake katika sekta mbalimbali, zinaweza pia kusababisha changamoto ikiwemo mafuriko, uharibifu wa miundombinu na uchafuzi wa vyanzo vya maji endapo tahadhari hazitazingatiwa kwa wakati.

    Alisisitiza umuhimu wa wananchi na wadau wa sekta mbalimbali kuendelea kufuatilia utabiri wa kila siku na tahadhari rasmi zinazotolewa na TMA.

    Katika ukanda wa Ziwa Victoria, mvua za wastani hadi juu ya wastani zinatarajiwa katika mikoa ya Kagera na Geita pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma, huku mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Mara na Simiyu ikitarajiwa kupata mvua za wastani hadi chini ya wastani.

    Kwa upande wa pwani ya kaskazini ikiwemo Dar es Salaam, Tanga, Pwani na visiwa vya Unguja na Pemba, mvua za wastani hadi juu ya wastani zinatarajiwa kuanza mapema mwezi Machi na kuisha mwishoni mwa Mei au mwanzoni mwa Juni.

    Nyanda za juu Kaskazini Mashariki zinazojumuisha mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro zinatarajiwa kupata mvua za wastani hadi chini ya wastani, huku mvua hizo zikitarajiwa kuanza katikati ya mwezi Machi na kuisha mwishoni mwa Mei.

    TMA imeonya kuwa, licha ya mwelekeo wa jumla wa mvua, matukio ya vipindi vya mvua kubwa yanaweza kujitokeza hata katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua chache, hali inayoweza kuongeza hatari ya mafuriko, uharibifu wa mali na kuibuka kwa magonjwa yanayotokana na uchafuzi wa maji.

    Wadau wa sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, mifugo, afya, usafiri, ujenzi na menejimenti za maafa wametakiwa kuzingatia taarifa hizi katika kupanga na kutekeleza shughuli zao, huku wananchi wakihimizwa kuendelea kufuatilia taarifa rasmi za hali ya hewa zinazotolewa na TMA.

  • Na Vincent Mpepo, Dodoma

    Watumishi wa Idara ya Masomo ya Habari na Ukutubi chini ya Kitivo cha Sanaa na Sayansi za Jamii, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, wametakiwa kufanyia kazi changamoto mbalimbali za wanafunzi na masuala mengine kwa wakati.

    Hayo yalisemwa na Mkuu wa Idara, Dkt. Henry Mambo, wakati akifunga kikao kazi cha idara hiyo cha siku nne kilichofanyika katika kituo cha Mkoa cha chuo hicho cha Dodoma.

    Dkt. Mambo alisisitiza kuwa watumishi wa idara hiyo wanatakiwa kushughulikia majukumu yao ya msingi, ikiwemo kufundisha, kufanya tafiti na kazi nyingine zitazosaidia maendeleo ya idara, kitivo na chuo kwa ujumla.

    Mhadhiri Mwandamizi Athumani Samzugi aliwataka watumishi wa Idara hiyo kushikamana na kusaidiana kitaaluma, akisisitiza umuhimu wa kufanya tafiti za pamoja kutokana na masomo yanayofanana katika idara.

    Mratibu wa masomo ya Ukutubi katika Idara hiyo, Ntimi Kasumo, aliwakumbusha watumishi hao kuendana na mabadiliko ya kiutendaji, ikiwemo katika usahihishaji, uwekaji wa kumbukumbu za matokeo na uwasilishaji kwa wakati.

    Aidha, aliwashauri wahadhiri wanaofundisha programu za uzamili kutoa alama kwa wakati ili kuendana na utendajikazi wa menejimenti ya chuo hicho.

  • Na Farida Mkumba

    Wanafunzi wa Chuo cha Serikali za Mitaa Kampasi ya Shinyanga wametembelea Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Shinyanga kuwaona wagonjwa, kufanya usafi eneo lote linalozunguka Hospitali hiyo, kujitolea damu na kutoa misaada mbalimbali za Kijamii.

    Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi wangonjwa na wananchi mbalimbali wameeleza namna wanavyoridhishwa na uwepo wa Chuo cha Serikali za Mitaa Mkoani Shinyanga kwa kuwa uwepo wake unadhihirika katika mambo mbalimbali yanayohusu jamii.

    Pamoja na mambo mengine, wanafunzi hao wamechanga pesa na kwenda kuziona jamii zenye uhitaji na hii ni katika kuonesha kuwa pamoja na kujipatia elimu kama sehemu ya jamii wanashiriki shughuli mbalimbali za kijamii.

    Kwa upande wa Maneja Kampasi wa Chuo hicho Mkoani Shinyanga Dkt.John Kasubi amesema kuwa Chuo kitaendelea kujitolea kwa Jamii ya Shinyanga kila kinapopata fursa katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huo na kuwataka wananchi wakipe ushirikiano ili kuionesha Jamii kuwa mbali na utoaji wa elimu pia Chuo kinajitolea kuisaidia jamii inayokizunguka chuo hicho.

  • Na Mwandishi Wetu

    Naibu Waziri wa Maji, Mhandisi Kundo Mathew, amemuagiza Mkandarasi Kampuni ya Afcons ya India kuzingatia maelekezo ya serikali kuhusu viwango vipya vya mishahara kwa wafanyakazi wa ngazi za chini, vinavyotaka kulipwa shilingi 16,500 kwa siku sawa na shilingi 515,000 kwa mwezi.

    Agizo hilo amelitoa leo wakati wa ukaguzi wa Mradi wa Maji wa Miji 28 katika mji wa Kayanga, wilayani Karagwe, baada ya kubaini kuwa mkandarasi huyo anawalipa vibarua shilingi 12,500 kwa siku, kinyume na maelekezo ya serikali.

    Alisema serikali ilielekeza viwango hivyo vipya vya mishahara kuanza kutumika Januari Mosi mwaka huu, na kusisitiza kuwa malipo hayo yaanze mara moja pamoja na kusainiwa kwa mikataba mipya inayoendana na mabadiliko hayo.

    “Nakuelekeza kuwasilisha nakala za mikataba hiyo mipya katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na kwa viongozi wa sekta ya maji katika mkoa husika”, alisema Kundo.

    Sanjali na hilo, alionesha kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi huo, ambao awali ulipangwa kukamilika Desemba 2025 kabla ya kuongezewa muda hadi Septemba mwaka huu.

    Kutokana na hali hiyo, amemuagiza Mkuu wa Wilaya kwa kushirikiana na viongozi wa sekta ya maji mkoani kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini iwapo vifaa vya utekelezaji wa mradi vimeagizwa na kama mpango kazi uliopo unatekelezeka kwa muda uliopangwa.

    Alisema Wizara ya Maji haitavumilia uzembe wa mkandarasi wakati wananchi wakiendelea kupata changamoto ya huduma ya maji safi na salama.

    Mradi huo wa Maji wa Miji 28 wa Kayanga, unagharimu kiasi cha shilingi bilioni 64.32 na unatarajiwa kuwanufaisha wakazi 352,790, na mpaka sasa umefikia asilimia 70 ya utekelezaji.

  • Na Mwandishi Wetu

    Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) imekutana na kuzungumza na wananchi wa Mtaa wa Golani, Kata ya Kimara, Wilaya ya Ubungo kwa lengo la kutatua changamoto ya upatikanaji huduma ya maji katika mtaa huo.

    Akizungumza kwa niaba ya Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano, Bi. Everlasting Lyaro amewatoa hofu wananchi wa Golani kwamba Mamlaka inatambua changamoto ya maji katika mtaa huo na zipo hatua za muda mfupi na mrefu ambazo zinachukuliwa ili kuhakikisha huduma hiyo inapatikana.

    “Kwanza tuwaombe radhi wananchi wa hapa Golani kwa changamoto ya maji mnayoipitia, tunatambua maji ni haki ya kila mmoja wetu”, alisema Bi. Everlasting.

    Alisema kwa kuanza Mamlaka italeta matenki Matano (05) yenye ujazo wa Lita 10,000 kila moja na kuyajaza maji yatakayouzwa kwa bei elekezi zoezi na zoezi hilo litafanyika kuanzia 15.01.2025 ili kukabiliana na changamoto hiyo kama hatua za awali ambazo ni za muda mfupi.

    “Tutaratibu mgao wa maji katika eneo hili ambapo mtapata maji mara tatu kwa wiki, Alhamisi, Jumapili na Jumatatu”, alisema Bi. Evarlasting.

    Akizungumzia utatuzi wa changamoto hiyo kwa mpango wa muda mrefu alisema DAWASA itajenga kituo cha kusukuma maji eneo la kwa Mama Stela kitakachosaidia maji kufika sehemu mbalimbali zilizookua hazipati huduma hiyo hapo awali.

    Kwa upande wake, Meneja wa Mkoa wa kihuduma DAWASA Kinyerezi, Mhandisi Antony Budaga alisema watumishi hawatakaa ofisi badala yake watatoka kuwafikia wananchi na kuhakikisha yaliyopangwa katika kikao hicho yanatekelezwa.

    Mkazi wa Golani, Rajabu Said ameshukuru jitihada zinazofanyika kuhakikisha changamoto ya maji mtaani hapo inakwisha kwamba wananchi wanapata matumaini ya upatikanaji wa huduma ya maji amabayo itawaondolea kero ya ununuzi wa maji kwa watoa huduma binafsi inayowagharimu fedha nyingi.