
Na George Gabriel
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Benjamin Masimbo, ameongoza Mkutano wa Baraza la Madiwani ambapo baraza lilipokea na kujadili taarifa za maendeleo ya kata pamoja na taarifa za Kamati za Kudumu za Halmashauri kwa robo ya nne ya mwaka wa fedha 2025/2026.
Mkutano huo ulifanyika katika Ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, ambapo pamoja na ajenda nyingine, Mwenyekiti Masimbo alijibu maswali mbalimbali ya papo kwa papo yaliyoulizwa na wajumbe wa Baraza.
Wajumbe walieleza kuridhishwa na ufafanuzi na majibu aliyoyatoa kuhusu masuala mbalimbali yaliyowasilishwa.

Katika mkutano huo, Masimbo alieleza kutoridhishwa na mwenendo wa malipo ya zao la ufuta kwa wakulima katika msimu wa mwaka huu na kuagiza mamlaka husika kuhakikisha wakulima wote ambao bado hawajapokea malipo yao wanalipwa kwa wakati.
Pia alizitaka mamlaka zinazohusika kushughulikia changamoto zilizojitokeza katika ununuzi wa zao hilo na kusisitiza kuwa kasoro hizo zisijirudie katika msimu ujao wa ununuzi wa korosho.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Nanyumbu, Rashid Mrope, alisisitiza umuhimu wa kuboresha huduma za bima ya afya ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma hizo kwa wananchi.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Katibu Tawala wa Wilaya, Juma Kanyinda, aliwataka viongozi na watendaji kusimamia kikamilifu utekelezaji wa majukumu yao. Aliwataka kuongeza juhudi katika kudhibiti utoro shuleni, kuimarisha usafi wa mazingira na kuhakikisha ujenzi wa vyoo unaendelea kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.
Mkutano huo ulihitimishwa kwa wito kwa viongozi na watendaji kuendelea kushirikiana katika kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo na kuboresha huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Nanyumbu.





















