• Na George Gabriel

    Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Benjamin Masimbo, ameongoza Mkutano wa Baraza la Madiwani ambapo baraza lilipokea na kujadili taarifa za maendeleo ya kata pamoja na taarifa za Kamati za Kudumu za Halmashauri kwa robo ya nne ya mwaka wa fedha 2025/2026.

    Mkutano huo ulifanyika katika Ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, ambapo pamoja na ajenda nyingine, Mwenyekiti Masimbo alijibu maswali mbalimbali ya papo kwa papo yaliyoulizwa na wajumbe wa Baraza.

    Wajumbe walieleza kuridhishwa na ufafanuzi na majibu aliyoyatoa kuhusu masuala mbalimbali yaliyowasilishwa.

    Katika mkutano huo, Masimbo alieleza kutoridhishwa na mwenendo wa malipo ya zao la ufuta kwa wakulima katika msimu wa mwaka huu na kuagiza mamlaka husika kuhakikisha wakulima wote ambao bado hawajapokea malipo yao wanalipwa kwa wakati.

    Pia alizitaka mamlaka zinazohusika kushughulikia changamoto zilizojitokeza katika ununuzi wa zao hilo na kusisitiza kuwa kasoro hizo zisijirudie katika msimu ujao wa ununuzi wa korosho.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Nanyumbu, Rashid Mrope, alisisitiza umuhimu wa kuboresha huduma za bima ya afya ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma hizo kwa wananchi.

    Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Katibu Tawala wa Wilaya, Juma Kanyinda, aliwataka viongozi na watendaji kusimamia kikamilifu utekelezaji wa majukumu yao. Aliwataka kuongeza juhudi katika kudhibiti utoro shuleni, kuimarisha usafi wa mazingira na kuhakikisha ujenzi wa vyoo unaendelea kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.

    Mkutano huo ulihitimishwa kwa wito kwa viongozi na watendaji kuendelea kushirikiana katika kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo na kuboresha huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Nanyumbu.

  • Na George Gabriel

    Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Donald Msengi, ameridhishwa na maandalizi yanayofanywa na Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu kuelekea Maonesho ya Nanenane 2026, huku akisisitiza kuwa kazi zilizobaki zikamilishwe kwa wakati na kwa ubora unaostahili.

    Kanali Msengi alitoa kauli hiyo jana baada ya kukagua banda la Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, ambapo alipongeza hatua zilizofikiwa katika maandalizi ya maonesho hayo.

    Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Ibrahim Mwanauta, alisema halmashauri imejipanga kikamilifu kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na Mkuu wa Mkoa ili kuhakikisha banda la Nanyumbu linakuwa miongoni mwa mabanda bora katika Maonesho ya Nanenane 2026.

    Mwanauta aliwataka wakuu wote wa idara na vitengo kushiriki kikamilifu katika maandalizi hayo, hususan maafisa wa kilimo, mifugo na biashara, kwa kuandaa maonesho yatakayoonesha ubunifu, matumizi ya teknolojia na mafanikio yaliyopatikana kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

    Alisema maonesho hayo ni fursa muhimu ya kuitangaza Wilaya ya Nanyumbu, kuvutia wawekezaji, kutoa elimu kwa wananchi na kuonesha huduma mbalimbali zinazotolewa na halmashauri.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Magala, amewasihi wananchi wa wilaya hiyo na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi kutembelea Maonesho ya Nanenane 2026 yatakayofanyika katika Viwanja vya Ngongo, mkoani Lindi.

    Alisema maonesho hayo ni jukwaa muhimu la kujifunza teknolojia za kisasa katika sekta za kilimo, mifugo, uvuvi na biashara, pamoja na kupata fursa za masoko na uwekezaji zitakazochangia kukuza uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla.

    Maonesho ya Nanenane 2026 Kanda ya Kusini yanatarajiwa kufanyika kuanzia Agosti 1 hadi 8, 2026, katika Viwanja vya Ngongo mkoani Lindi, yakiwa na kaulimbiu isemayo: “Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.”

    Serikali imeendelea kuwahimiza wananchi kutumia maonesho hayo kama fursa ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuhamasisha matumizi ya teknolojia mpya ili kuongeza tija katika uzalishaji na kuchochea maendeleo ya uchumi.

  • Na Andrea Mbona, Mbulu

    Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Manyara, Mrakibu wa Polisi Mikael Mwakasungura, ametembelea Wilaya ya Mbulu na kufanya kikao cha kazi na askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani wa wilaya hiyo, akiwakumbusha wajibu wao wa kusimamia sheria za usalama barabarani kwa weledi na uadilifu.

    Akizungumza katika kikao hicho, Mrakibu Mwakasungura alisema askari wanapaswa kutambua dhamana waliyonayo katika kusimamia sheria za usalama barabarani ili kusaidia kupunguza ajali ambazo zimekuwa zikisababisha vifo na majeruhi nchini.

    Alisisitiza kuwa utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia sheria, weledi na uadilifu ni msingi wa kuendelea kujenga imani na ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.

    “Fanyeni kazi kwa kuzingatia misingi ya sheria, weledi na uadilifu ili muendelee kuaminiwa na jamii,” alisema Mrakibu Mwakasungura.

    Katika ziara hiyo, Mrakibu Mwakasungura aliambatana na Mkuu wa Kitengo cha Usalama Barabarani Mkoa wa Manyara, Mrakibu Msaidizi wa Polisi ASP Mohamed Mlulu, ambaye aliwataka askari hao kufahamu na kutumia ipasavyo mifumo ya kielektroniki inayorahisisha utendaji kazi.

    Alisema mifumo hiyo ni muhimu katika usajili, uhifadhi na usimamizi wa taarifa mbalimbali zinazohusu usalama barabarani, hivyo ni lazima askari waendelee kuijua na kuitumia kwa ufanisi.

    Akizungumza kwa niaba ya askari wa Usalama Barabarani Wilaya ya Mbulu, Sajenti Brayan Mlawa alimshukuru Mkuu wa Kikosi kwa mafunzo na maelekezo aliyoyatoa, akiahidi kuwa askari hao wataendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kwa kuzingatia sheria.

    Akihitimisha ziara hiyo, Mrakibu Mwakasungura aliwataka askari kuendelea kutoa elimu kwa wamiliki wa vyombo vya moto na madereva kuhusu ukaguzi wa magari kwa njia ya kidijitali, hususan wakati huu ambapo ‘Wiki ya Nenda kwa Usalama’ inaelekea kuhitimishwa.

  • Na Damasi Kalembwe

    Jeshi la Polisi, kupitia Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Kinondoni, SP Edna Maro, limetoa elimu ya usalama kwa wafanyakazi wa Hoteli ya Golden Tulip iliyopo Masaki, Dar es Salaam, likiwataka kutambua kuwa kila mmoja ana wajibu wa kulinda mali za hoteli na kutekeleza majukumu yake kwa weledi huku akiepuka kujihusisha na vitendo vya uhalifu vinavyoweza kuharibu taswira ya hoteli na nchi kwa ujumla.

    Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, SP Maro alisema wizi ni kosa la jinai na kuwahimiza wafanyakazi kutoa taarifa kwa uongozi wa hoteli pamoja na Jeshi la Polisi wanapobaini viashiria vya uhalifu.

    Aidha, aliwataka kuwa walinzi wa wenzao, kuwapokea wageni na viongozi kwa heshima, kudumisha umoja mahali pa kazi na kufahamu adhabu zinazotokana na makosa ya wizi kwa mujibu wa sheria.

    Kwa upande wake, Mkaguzi wa Polisi wa Kata ya Msasani, Mkaguzi Joel Kaaya, aliwakumbusha umuhimu wa huduma bora kwa wateja wanaoingia na kutoka hotelini kwa kuwa huchangia kuimarisha usalama, kuongeza imani ya wageni na kukuza sekta ya utalii nchini.

    Akizungumza kwa niaba ya uongozi wa hoteli, Bi. Grace Karsan alilishukuru Jeshi la Polisi kwa kutoa mafunzo hayo, akisema yameongeza uelewa wa wafanyakazi kuhusu masuala ya usalama.

    Naye Miraji Juma, akizungumza kwa niaba ya wafanyakazi, aliomba mafunzo kama hayo yaendelee kutolewa mara kwa mara katika hoteli mbalimbali ili kuongeza uelewa wa masuala ya usalama na kuwajengea wafanyakazi uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

  • Na Damasi Kalembwe

    Mashindano ya michezo ya Polisi Jamii Cup katika Mkoa wa Kinondoni yamezinduliwa rasmi Julai 27, 2026, katika viwanja vya michezo vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

    Uzinduzi huo ulihudhuriwa na Mgeni Rasmi, Mkuu wa Ushirikishwaji wa Jamii Mkoa wa Kinondoni, ACP Ally Wendo, aliyeambatana na Wakuu wa Himaya za Kinondoni na Kawe pamoja na Maafisa Watendaji wa Wilaya (DCEO) wa maeneo hayo.

    Akizungumza kwa niaba ya askari na washiriki wote, Koplo Itumbi Wambura alisema mashindano hayo ni fursa muhimu ya kuwakutanisha askari polisi na wananchi wanaowahudumia, hivyo kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya pande hizo mbili.

    Alisema lengo kuu la mashindano hayo ni kupata wachezaji mahiri watakaounda timu imara ya mkoa, sambamba na kuhamasisha afya bora kupitia mazoezi na michezo.

    Aidha, mashindano hayo yanalenga kuongeza mshikamano, kufahamiana na kujenga ushirikiano wa dhati kati ya Jeshi la Polisi, jamii na wajumbe kutoka wilaya zote tano zinazoshiriki.

    Katika siku ya ufunguzi, timu mbalimbali zilishiriki katika michezo ya riadha, kuvuta kamba, mpira wa miguu na mpira wa pete. Washiriki walionyesha ushindani mkubwa katika kila mchezo wakilenga kuzipatia ushindi himaya zao.

    Matokeo ya michezo ya ufunguzi yalionesha Mkoa wa Kinondoni ukiibuka bingwa katika riadha na mpira wa pete. Kwa upande wa mchezo wa kuvuta kamba, Himaya ya Kawe iliibuka mshindi, huku mchezo wa mpira wa miguu kati ya Kinondoni na Kawe ukimalizika kwa sare ya mabao 2-2.

  • Na Jastini Bukebuke

    Walimu wa Shule ya Msingi Simbaguji, iliyopo Kata ya Kanyala, Wilaya ya Geita, wametakiwa kuimarisha usimamizi wa vilabu vya kupinga ukatili wa kijinsia shuleni ili viendelee kuwajengea wanafunzi uelewa wa haki zao, ujasiri wa kutoa taarifa, maadili mema na uwezo wa kujilinda dhidi ya ukatili pamoja na vitendo vingine vinavyohatarisha usalama wao.

    Wito huo ulitolewa jana na Polisi Kata wa Kanyala, Inspekta Said Juma, alipokuwa akitoa elimu ya kinga kwa walimu na wanafunzi wa shule hiyo.

    Akizungumza katika elimu hiyo, Inspekta Juma alisema vilabu vya kupinga ukatili wa kijinsia ni nyenzo muhimu katika kuwafundisha wanafunzi kutambua haki zao, kutoa taarifa kwa wakati wanapobaini viashiria vya ukatili na kujiepusha na mazingira yanayoweza kuhatarisha usalama wao.

    Aidha, aliwataka walimu kuhakikisha vilabu hivyo vinaendelea kufanya kazi kwa ufanisi kupitia mikutano ya mara kwa mara, utoaji wa elimu endelevu na ushirikiano wa karibu kati ya shule, wazazi na jamii ili kuimarisha ulinzi wa watoto.

    Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Simbaguji, Renatus Misago Chigunga, alilipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kutoa elimu ya kinga shuleni.

    Alisema ushirikiano huo unachangia kuongeza uelewa wa wanafunzi kuhusu masuala ya usalama, kuimarisha maadili mema na kujenga mazingira salama na rafiki ya kujifunzia.

  • Na George Gabriel

    Wananchi wa Kijiji cha Masugulu, Wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara, wameiomba Serikali kuhakikisha Mradi wa Maji wa Mto Ruvuma–Mangaka unakamilika kwa wakati ili waanze kunufaika na huduma ya maji safi na salama.

    Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Mwanahawa Juma alisema licha ya mradi huo kuanza kutekelezwa, bado wanaiomba Serikali kuongeza kasi ya utekelezaji ili kutimiza ahadi ya kuwapatia maji ya uhakika na kuondoa kero ya muda mrefu.

    “Tunaishukuru Serikali kwa kuleta mradi huu mkubwa, lakini tunaomba ukamilike haraka kwa sababu tumekuwa tukiusubiri kwa muda mrefu tangu Rais alipotuahidi,” alisema Mwanahawa.

    Naye Mzee Shaibu Lipindi alisema upatikanaji wa maji ya uhakika utapunguza adha ambayo wananchi wamekuwa wakikabiliana nayo kwa miaka mingi. Aliipongeza Serikali kwa kuendelea kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo yenye manufaa kwa wananchi.

    Kwa upande wake, mwakilishi wa mkandarasi, AFCONS Infrastructure Ltd, alisema kampuni hiyo imepokea maelekezo ya Mkuu wa Mkoa ya kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo. Aliahidi kuwa watafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha mradi unakamilika ndani ya muda uliopangwa.

    Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Donald Msengi, alimtaka mkandarasi kuongeza nguvu kazi, vifaa na rasilimali nyingine muhimu ili kuhakikisha mradi huo wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 38.1 unakamilika kwa wakati na kuanza kutoa huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Nanyumbu na maeneo ya jirani.

    Serikali imeendelea kusisitiza kuwa upatikanaji wa maji safi na salama ni miongoni mwa vipaumbele vyake katika kuboresha maisha na kuchochea maendeleo ya wananchi.

    Maoni ya wananchi pamoja na agizo la Mkuu wa Mkoa kwa mkandarasi yalitolewa wakati wa ziara ya Kanali Donald Msengi ya kukagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo.

  • Na Cosmas Msuha

    Zaidi ya shilingi bilioni 38 zimetumika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika Wilaya ya Kongwa, mkoani Dodoma, katika mwaka wa fedha 2025/2026, huku Serikali ikiahidi kuendelea kuboresha huduma za elimu, afya, maji, mawasiliano na miundombinu.

    Hayo yameelezwa hivi karibuni na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Laikala baada ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani humo, ikiwemo ujenzi wa jengo jipya la Ofisi ya Mkuu wa Wilaya pamoja na Vituo vya Afya vya Laikala na Sagara.

    Akizungumza na wananchi wa kata za Laikala na Sagara, Waziri Kairuki alisema fedha hizo zimewezesha utekelezaji wa miradi katika sekta za afya, elimu, maji, kilimo, umwagiliaji na miundombinu.

    “Hadi Juni 2026, Serikali imeelekeza shilingi bilioni 38.6 kutekeleza miradi ya afya, elimu, kilimo, umwagiliaji na miundombinu mingine ya maendeleo katika Wilaya ya Kongwa,” alisema Kairuki.

    Aliongeza kuwa Serikali imejenga zaidi ya madarasa 640, maabara za sayansi karibu 50 na kuajiri walimu wa kutosha ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.

    Aidha, aliahidi kupeleka kompyuta 44 katika shule mbili za wilaya hiyo pamoja na kuendelea kujenga madarasa ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF), kwa lengo la kuwawezesha wanafunzi kupata ujuzi wa teknolojia.

    Katika sekta ya maji, alisema upatikanaji wa huduma hiyo wilayani Kongwa umefikia asilimia 76.8, huku Serikali ikijiandaa kuchimba visima 19 katika vijiji ambavyo bado havijafikiwa na huduma ya maji safi na salama.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Saimon Mayeka, alisema wilaya hiyo imepata mafanikio makubwa katika utoaji wa huduma za jamii. Alieleza kuwa idadi ya shule za sekondari imeongezeka kutoka 26 hadi 41 baada ya kujengwa shule mpya 15, huku ongezeko la vituo vya afya likichangia kuboresha huduma za afya na kupunguza vifo vya mama na watoto.

    Kwa mujibu wa Mayeka Wilaya ya Kongwa ina jumla ya shule za sekondari 45, zikiwemo 39 za Serikali na sita za binafsi.

  • Na Jastini Bukebuke

    Mkuu wa Kituo cha Polisi Kasamwa, Inspekta Said Juma, akishirikiana na askari wa kituo hicho, wamewafariji wagonjwa wanaopatiwa matibabu katika Kituo cha Afya Kasamwa kwa kuwapa pole na kuwakabidhi mahitaji muhimu.

    Tukio hilo lilifanyika Julai 25, 2026, katika Kituo cha Afya Kasamwa, Wilaya ya Geita, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Jeshi la Polisi kuendelea kuwa karibu na wananchi na kuimarisha mahusiano mema kupitia falsafa ya Polisi Jamii.

    Akipokea msaada huo, Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Kasamwa, Dkt. Emmanuel Ziragira, alilishukuru Jeshi la Polisi kwa kuonesha moyo wa kujali na kuwafariji wagonjwa. Alisema matendo hayo yanawapa faraja na kuongeza matumaini kwa wananchi wanaopitia changamoto za kiafya.

    Kupitia tukio hilo, Jeshi la Polisi limeendelea kudhihirisha kuwa jukumu lake halijikiti katika kulinda amani na usalama pekee, bali pia kujenga mahusiano ya karibu na jamii kupitia matendo ya huruma na huduma kwa wananchi.

    Aidha, wananchi wamehimizwa kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu kwa wakati, ili kuimarisha amani, usalama na utulivu katika jamii.

  • Na Damasi Kalembwe

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni limewataka wamiliki wote wa vyombo vya moto kujitokeza kuhakiki magari yao na kuzingatia taratibu za usalama barabarani, likisisitiza kuwa kampeni ya “Nenda kwa Usalama” inalenga kupunguza ajali na kulinda maisha ya watumiaji wote wa barabara.

    Zoezi hilo linafanyika katika Kituo cha Polisi Oysterbay cha Zamani kuanzia Julai 23, 2026, chini ya usimamizi wa Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, SSP Adamson Mwangamilo.

    Sambamba na zoezi hilo, wananchi wanaendelea kupatiwa elimu kuhusu matumizi salama ya vyombo vya usafiri, ikiwemo magari na pikipiki, pamoja na namna ya kujaza taarifa katika mfumo wa ukaguzi wa magari ili kupata stika za MIMIS.

    Hatua hiyo inalenga kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma na kuimarisha usalama barabarani.

    Miongoni mwa wananchi walioshiriki katika zoezi hilo ni Shabani Omary, ambaye amelipongeza Jeshi la Polisi pamoja na Serikali kwa kuanzisha mfumo wa kisasa wa ukaguzi wa magari.

    Amesema mfumo huo umeongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa kupunguza muda wa kusubiri na kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

    Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Kipolisi Kinondoni kinaendelea na zoezi la uhakiki wa magari na utoaji wa stika za “Nenda kwa Usalama” ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kuimarisha usalama barabarani na kuhamasisha uzingatiaji wa sheria za usalama wa barabarani.