
Na Cosmas Msuha
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi imesema katika mwaka wa fedha 2026/27 inatarajia kuajiri watumishi wapya 10,919 pamoja na kutekeleza vipaumbele vinane vinavyolenga kuimarisha usalama, huduma za uraia na matumizi ya teknolojia nchini.
Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo bungeni jijini Dodoma Mei 25, 2026, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi alisema ajira hizo ni sehemu ya mkakati wa kuongeza ufanisi katika vyombo vya usalama vilivyo chini ya wizara hiyo.
Aidha, Idara ya Uhamiaji Tanzania inatarajia kuajiri watumishi 1,000 huku Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) ikipanga kuajiri watumishi 84 ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Katika bajeti hiyo, Waziri Katambi alisema wizara itaendelea kuboresha miundombinu ya vyombo vya usalama ikiwemo makazi ya maofisa, wakaguzi, askari pamoja na watumishi wasio askari ili kuongeza mazingira bora ya kazi na ufanisi wa utendaji.
Pia wizara imepanga kuimarisha upatikanaji wa vitendea kazi, ikiwemo vyombo vya usafiri na usafirishaji kwa taasisi zote zilizo chini yake, hatua inayolenga kuongeza kasi ya utekelezaji wa majukumu ya kiusalama nchini.
Mheshimiwa Katambi alisema wizara itaendelea kufanya tafiti mbalimbali kubaini sababu za kuongezeka kwa makosa mapya pamoja na kuweka mikakati madhubuti ya kuyadhibiti. Aliongeza kuwa matumizi ya TEHAMA yataendelea kupewa kipaumbele katika utoaji wa huduma na usimamizi wa shughuli za wizara hiyo.
Katika miradi ya maendeleo, wizara itaanza ujenzi wa makao makuu ya NIDA jijini Dodoma, pamoja na ofisi 31 za usajili katika wilaya mbalimbali na kituo cha mafunzo na matengenezo ya vifaa vya TEHAMA mjini Kibaha.
Mbali na hilo, wizara imesema itaendelea kuimarisha shughuli za uzalishaji mali kupitia sekta za kilimo, mifugo, viwanda pamoja na utunzaji wa mazingira.


















