• Na Pilastus Nyaulingo

    Kwa mwanafunzi anayekaa darasani siku nzima, kengele ya mwisho inapolia inaweza kumaanisha mwisho wa masomo. Lakini kwa baadhi ya watoto wanaoishi katika maeneo ambayo upatikanaji wa umeme bado ni changamoto, mwisho wa vipindi vya darasani unaweza pia kumaanisha mwisho wa nafasi ya kujisomea kwa siku hiyo.

    Hii ni kwa sababu elimu haishii ndani ya darasa. Kuna vitabu vya kusoma baada ya masomo, kazi za kufanya nyumbani, maandalizi ya mitihani na maarifa ya kutafuta nje ya muda rasmi wa vipindi. Bila mwanga wa kutosha, muda huo unaweza kupotea.

    Katika Tanzania, mjadala kuhusu upatikanaji wa nishati umeendelea kuhusishwa na upatikanaji wa huduma muhimu, ikiwemo elimu.

    Kwa mujibu wa Ripoti ya Benki ya Dunia imeonesha namna upatikanaji wa umeme unavyoweza kuboresha mazingira ya kujifunza, matumizi ya teknolojia na huduma nyingine shuleni.

    Muda wa Kusoma Haupaswi Kuishia Jua Linapozama

    Kwa mwanafunzi wa shule ya sekondari, muda wa kujisomea baada ya vipindi unaweza kuwa muhimu katika kuelewa masomo, kufanya kazi za shule au kujiandaa kwa mitihani.

    Lakini pale ambapo shule au mazingira ya nyumbani hayana umeme wa uhakika, mwanafunzi anaweza kulazimika kusoma kwa mwanga hafifu au kuacha kabisa kusoma wakati wa usiku.

    Uzoefu wa Shule ya Sekondari Lukaranga unaonyesha tofauti ambayo umeme unaweza kuleta katika mazingira ya elimu.

    Baada ya shule hiyo kupata umeme, wanafunzi waliweza kutumia muda wa jioni kujisomea katika mazingira yenye mwanga na usalama zaidi.

    Japhet Tobeka, aliyekuwa mwanafunzi wa Kidato cha Nne wakati huo, anaeleza namna upatikanaji wa umeme ulivyowapa wanafunzi nafasi ya kurudi shuleni jioni na kuendelea na masomo katika mazingira bora zaidi.

    Kauli hiyo inaonyesha kuwa umeme si suala la kuwasha taa pekee. Ni miundombinu inayoweza kuongeza muda ambao mwanafunzi anaweza kutumia kujifunza.

    Kwa mtoto wa kike, muda huo unaweza kuwa na umuhimu zaidi, hasa katika mazingira ambayo majukumu ya nyumbani au changamoto nyingine zinaweza kupunguza muda wake wa kusoma.

    Kwa Nini Suala Hili Ni Muhimu Zaidi kwa Wasichana?

    Wasichana wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazoweza kuathiri mwendelezo wa elimu, hasa wanapofikia umri wa balehe.

    Kwa mujibu wa ripoti za Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto ( UNICEF Tanzania) zinaeleza kuwa mamilioni ya watoto wenye umri wa kwenda shule hawapo shuleni, huku wasichana kutoka maeneo ya vijijini na kaya maskini wakiwa miongoni mwa wanaoweza kukabiliwa zaidi na vikwazo vya kuendelea na elimu.

    Changamoto hizo zinaweza kuhusisha umaskini, huduma duni za maji na usafi, changamoto wakati wa hedhi pamoja na ndoa za utotoni.

    Hivyo, tunapozungumzia umeme shuleni, hatupaswi kuutazama kama suala linalojitegemea. Ni sehemu ya mazingira mapana yanayoweza kumsaidia mtoto wa kike kubaki shuleni, kujifunza kwa ufanisi na kutumia muda wake vizuri.

    Shule yenye mwanga wa kutosha inaweza pia kuwa mazingira salama zaidi kwa wanafunzi wanaohitaji kubaki shuleni baada ya muda wa kawaida wa masomo.

    Umeme Unabadilisha Zaidi ya Taa

    Faida ya umeme shuleni haiishii kwenye kusoma vitabu usiku.

    Umeme unaweza kuwezesha matumizi ya kompyuta, vifaa vya kidijitali, uchapishaji wa vifaa vya kujifunzia na matumizi ya teknolojia nyingine zinazohitaji nishati.

    Hili linaonekana pia katika uzoefu wa Shule ya Sekondari Lukaranga.

    Kabla ya shule hiyo kupata umeme, walimu walikabiliwa na changamoto katika kupata na kuandaa baadhi ya vifaa vya kufundishia. Baada ya umeme kupatikana, mazingira ya kazi yalibadilika na matumizi ya vifaa vya kielektroniki yakawa rahisi zaidi.

    Mwalimu Flora Chacha anaeleza kuwa kabla ya shule kupata umeme, changamoto ya upatikanaji wa vifaa vya kuchapisha iliwalazimu wakati mwingine kwenda maeneo mengine kupata huduma hiyo. Baada ya shule kuunganishwa na umeme, walimu waliweza kuchapisha nakala za vitabu na kutumia vifaa vya sauti katika ufundishaji.

    Mabadiliko hayo yanaonyesha uhusiano uliopo kati ya nishati na ubora wa elimu. Kadiri shule inavyokuwa na uwezo wa kutumia teknolojia, ndivyo inavyoweza kupanua njia ambazo mwanafunzi anajifunza.

    Kwa mtoto wa kike, ambaye tayari anaweza kukutana na vikwazo vingine vya kijamii na kiuchumi, mazingira bora ya kujifunza yanaweza kuwa na umuhimu mkubwa katika kuendelea na masomo.

    Umeme Unamsaidia Pia Mwalimu

    Mjadala wa umeme na elimu wakati mwingine huangalia zaidi upande wa mwanafunzi, lakini mwalimu naye anahitaji mazingira yanayomwezesha kufanya kazi yake vizuri.

    Mkuu wa Shule ya Sekondari Lukaranga, Joseph Tongora, anasema kabla ya shule kupata umeme walikabiliwa na changamoto katika kufanya tathmini za mara kwa mara, jambo lililoathiri namna walivyoweza kufuatilia maendeleo ya wanafunzi.

    Baada ya shule kupata umeme, walimu waliweza kufanya tathmini za kila wiki kwa urahisi zaidi.

    Hili ni muhimu kwa sababu ubora wa elimu hauamuliwi na mwanafunzi pekee. Mwalimu anahitaji vifaa, muda na mazingira yanayomwezesha kutambua changamoto za mwanafunzi na kumsaidia kwa wakati.

    Kwa hiyo, umeme unapowezesha mwalimu kuandaa vifaa, kufanya tathmini na kutumia teknolojia, athari yake inaweza kufika hadi kwa mwanafunzi.

    Kutoka Mwanga Hadi Fursa

    Tanzania imepiga hatua katika kuongeza upatikanaji wa umeme. Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, upatikanaji wa umeme nchini uliongezeka kutoka asilimia 14 mwaka 2011 hadi asilimia 46 mwaka 2022.

    Hata hivyo, tofauti kati ya maeneo ya mijini na vijijini bado ilikuwa kubwa, huku upatikanaji ukiwa asilimia 73.2 mijini ikilinganishwa na asilimia 24.5 vijijini.

    Takwimu hizi zinaonyesha kwa nini mjadala wa umeme na elimu hauwezi kutenganishwa na mjadala wa maendeleo ya vijijini.

    Iwapo shule ya kijijini haina umeme, wanafunzi wake wanaweza kukosa baadhi ya fursa ambazo wanafunzi wa shule zilizounganishwa kwenye umeme wanazipata na hiyo ikwa ni sababu mojawapo kuwatofatisha na wengine wenye huduma ya umeme.

    Tofauti hiyo inaweza kuonekana katika matumizi ya teknolojia, muda wa kujisomea na uwezo wa walimu kutumia vifaa mbalimbali vya kufundishia.

    Ndiyo maana uwekezaji katika nishati unaweza pia kuonekana kama uwekezaji katika usawa wa elimu.

    Changamoto Bado Haijaisha

    Pamoja na maendeleo yaliyopatikana, upatikanaji wa umeme pekee hauwezi kutatua changamoto zote za elimu.

    Shule inahitaji walimu wenye ujuzi, vifaa vya kujifunzia, madarasa salama, maji, vyoo vinavyofaa, vitabu na mazingira yanayomruhusu mwanafunzi kujifunza kwa utulivu.

    Lakini pia ni muhimu kutambua kwamba miundombinu moja inaweza kuwezesha nyingine kufanya kazi vizuri zaidi.

    Kompyuta haiwezi kutumika bila umeme. Vifaa vya kuchapisha haviwezi kufanya kazi bila nishati. Mwanafunzi hawezi kutumia baadhi ya teknolojia za kujifunzia bila chanzo cha umeme.

    Kwa hiyo, nishati ni sehemu ya msingi ya mazingira ya kisasa ya elimu.

    Swali si Kama Tunaweka Umeme Pekee

    Tunapofikiria kuhusu elimu ya mtoto wa kike, mara nyingi tunazungumzia ada, sare, vitabu na walimu. Hayo yote ni muhimu.

    Lakini mazingira yanayomzunguka mtoto pia yanaamua kwa kiwango fulani kama ataweza kutumia fursa hiyo ya elimu kikamilifu.

    Umeme unaweza kuonekana kama kitu kidogo unapoutazama kama taa inayowaka ukutani. Lakini kwa mwanafunzi anayehitaji saa moja zaidi ya kujisomea, kwa mwalimu anayehitaji kuandaa vifaa vya somo au kwa shule inayotaka kutumia teknolojia, mwanga huo unaweza kumaanisha mengi zaidi.

    Uzoefu wa Shule ya Sekondari Lukaranga unaonyesha kuwa mabadiliko hayo yanaweza kuonekana katika maisha ya kila siku ya shule, kuanzia muda wa wanafunzi kujisomea hadi uwezo wa walimu kuandaa vifaa na kufanya tathmini.

    Hatimaye, kuhakikisha shule zina nishati ya uhakika si suala la kuongeza mwanga kwenye majengo pekee. Ni kuongeza muda wa kujifunza, uwezo wa kutumia teknolojia na mazingira yanayoweza kumsaidia mtoto kufikia ndoto zake.

    Kwa mtoto wa kike anayekua katika mazingira yenye changamoto, wakati mwingine tofauti kati ya kuendelea na safari ya elimu na kukata tamaa inaweza kuanza na jambo rahisi kama kupata mazingira salama na yenye mwanga wa kujifunzia.

  • Na Andrea Mbona, Mbulu

    Matumizi ya pombe miongoni mwa waendesha bodaboda yameelezwa kuwa miongoni mwa sababu zinazochangia ajali za barabarani, huku madereva wakitakiwa kuepuka ulevi hasa wanapokuwa kazini.

    Askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani wilayani Mbulu, Cpl Octavian, ametoa rai hiyo wakati akitoa elimu ya usalama barabarani kwa waendesha bodaboda katika eneo la stendi ya bodaboda Mbulu.

    Alisema pombe huwafanya baadhi ya madereva kujiamini kupita kiasi na kupunguza umakini wakati wa kuendesha, hali inayoweza kusababisha uzembe na ajali zinazosababisha vifo, majeraha na ulemavu.

    “Acheni kunywa pombe na kuendesha pikipiki. Ni hatari sana na ni sababu kubwa ya ajali nyingi,” alisema Cpl Octavian.

    Aidha, aliwataka waendesha bodaboda kuzingatia na kutii sheria za usalama barabarani wakati wote wanapokuwa kazini ili kujilinda wao, abiria na watumiaji wengine wa barabara.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa bodaboda wa kijiwe cha stendi, Amani Daniel, amemshukuru askari huyo kwa elimu hiyo, akisema ulevi umekuwa ukihusishwa na baadhi ya ajali zinazowahusisha waendesha pikipiki.

    “Ni kweli afande, kuhusu ulevi mara nyingi ajali zinapotokea tumekuwa tukiwakuta madereva wengi wakiwa katika hali ya ulevi, hivyo tunashukuru kwa kutukumbusha,” alisema Amani.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Tanzania inakabiliwa na changamoto katika kufikia malengo ya kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia, huku gharama za nishati, upatikanaji wa teknolojia na utekelezaji wa sera zikitajwa kuwa miongoni mwa mambo yanayohitaji kupewa kipaumbele.

    Wakizungumza kuhusu utekelezaji wa mpango wa Tanzania wa kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia, wadau wa nishati wamesema juhudi zaidi zinahitajika kuhakikisha wananchi wanapata nishati salama, nafuu na inayopatikana kwa urahisi.

    Nolasco Mlay kutoka Wizara ya Nishati alisema utekelezaji wa malengo ya nishati safi ya kupikia unahitaji ushirikiano wa Serikali, sekta binafsi, taasisi na wananchi ili kuhakikisha teknolojia hizo zinawafikia watumiaji kwa gharama nafuu.

    Alisema Serikali inaendelea kuweka mazingira wezeshi yatakayochochea ukuaji wa matumizi ya nishati safi, huku ikilenga kupunguza changamoto zinazowakabili wananchi katika upatikanaji wa uhakika wa nishati hiyo.

    Kwa upande wake, Dkt. Prosper Magali wa Tanzania Renewable Energy Association (TAREA) alisema upanuzi wa matumizi ya nishati safi ya kupikia unahitaji kuangalia uwezo wa wananchi kumudu gharama za teknolojia na nishati hizo.

    Alisema pamoja na kuwepo kwa teknolojia mbalimbali za nishati safi, wananchi wanahitaji elimu kuhusu faida zake pamoja na mifumo inayowezesha upatikanaji wake kwa gharama nafuu.

    Alisema ongezeko la matumizi ya nishati safi ya kupikia linaweza kuwa na manufaa katika maeneo mbalimbali, ikiwemo kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, kulinda mazingira na kupunguza madhara yanayohusishwa na matumizi ya nishati zinazozalisha moshi mwingi.

    Hatua hizo zinaweza kuboresha afya za wananchi, hasa wanawake na watoto wanaokaa muda mwingi karibu na maeneo ya kupikia, huku zikisaidia kaya kupunguza muda na gharama za kutafuta kuni au kununua nishati za kupikia.

    Kwa Tanzania, matumizi makubwa ya nishati safi yatasaidia kupunguza ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na uzalishaji wa mkaa, hivyo kuchangia uhifadhi wa mazingira.

    Hata hivyo, wataalamu wanaeleza kuwa kufikia malengo ya taifa kutahitaji uwekezaji zaidi, ushirikiano wa wadau na kuongeza uelewa wa wananchi ili kuongeza idadi ya kaya zinazotumia nishati salama na nafuu.

  • Na George Gabriel

    Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, amekipongeza Kikundi cha Vijana Kazi Imara cha Kata ya Nanyumbu, Wilaya ya Nanyumbu, kwa uaminifu katika marejesho ya mikopo, ubunifu na ubora wa bidhaa wanazozalisha.

    Kapinga alitoa pongezi hizo jana wakati wa ziara yake wilayani Nanyumbu, ambapo alikagua shughuli mbalimbali zinazofanywa na vijana hao, ikiwemo useremala, ushonaji wa nguo kwa kutumia cherehani pamoja na biashara ya mama ntilie.

    Katika ukaguzi huo, Kapinga alivutiwa na ubunifu wa kikundi hicho katika utengenezaji wa vitanda, akieleza kuwa hatua hiyo ni mfano mzuri wa namna vijana wanavyoweza kutumia fursa zinazotolewa na Serikali kuongeza kipato na kujiajiri.

    Aidha, alipongeza uaminifu wa kikundi hicho katika kurejesha mkopo wa Shilingi milioni 14.5, ambapo hadi sasa kimefanikiwa kurejesha Shilingi milioni 2.112, hatua aliyosema inaonesha uwajibikaji wa wanakikundi.

    Katika kuwatia moyo vijana hao, Kapinga alikabidhi Shilingi milioni moja (TSh 1,000,000), huku akiwataka kuendelea kudumisha uaminifu, kuimarisha ubunifu na kuongeza ubora wa bidhaa zao ili ziweze kushindana katika soko.

    Aidha, katika ziara hiyo, Kapinga alitoa mitungi ya gesi kwa wajasiriamali, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuhamasisha matumizi ya nishati safi na salama katika shughuli za uzalishaji na matumizi ya kila siku.

    Akizungumza na mwandishi baada ya kupokea mtungi wa gesi, Mwajuma Mchakama aliipongeza Serikali kwa kuwajali wananchi na kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi, akisema hatua hiyo itasaidia kupunguza matumizi ya kuni na mkaa, pamoja na kuboresha mazingira ya kufanyia shughuli zao.

    Naye Zamda Ally, mmoja wa wanufaika wa mitungi hiyo ya gesi, aliishukuru Serikali kwa msaada huo, akieleza kuwa ni hatua muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata fursa ya kutumia nishati safi, salama na rafiki kwa mazingira.

    Wananchi hao kwa pamoja waliipongeza Serikali kwa kuendelea kusogeza huduma na fursa mbalimbali kwa wananchi, wakisema matumizi ya nishati safi yatasaidia kupunguza athari za matumizi ya nishati zinazoharibu mazingira, pamoja na kuboresha afya na maisha ya familia.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Wataalamu wa teknolojia ya habari na mawasiliano wameitaka Tanzania kuimarisha imani ya wananchi katika huduma za kidijitali, ikiwemo usalama wa mtandao, ulinzi wa taarifa binafsi na ujuzi wa kidijitali, ili nchi iweze kunufaika zaidi na teknolojia ya akili bandia (AI) na uchumi wa kidijitali.

    Wito huo umetolewa katika Jukwaa la Tanzania Digital Trust Initiative, lililowakutanisha maofisa wa serikali, wadhibiti, wataalamu wa teknolojia, viongozi wa sekta na wadau wengine kujadili namna ya kujenga mazingira salama na ya kuaminika katika matumizi ya teknolojia nchini.

    Akizungumza katika jukwaa hilo, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya TEHAMA, Dkt. Nkundwe Mwasaga, alisema Tanzania imepiga hatua kubwa tangu kupitishwa kwa Sera ya Taifa ya TEHAMA ya mwaka 2003, na kwamba miundombinu iliyojengwa inapaswa kutafsiriwa kuwa manufaa ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi.

    Alisema Sera ya Taifa ya TEHAMA ya mwaka 2003 iliweka mkazo katika uanzishaji wa taasisi, miundombinu ya taifa ya TEHAMA na ujuzi wa TEHAMA, huku sera ya mwaka 2016 ikiongeza msisitizo katika mifumo na majukwaa ya kidijitali.

    “Tanzania imeingia katika uchumi wa kidijitali na hatua inayofuata ni kujenga miundombinu ya uaminifu itakayowawezesha wananchi kutumia huduma za kidijitali kwa usalama na uhakika,” alisema Dkt. Mwasaga.

    Alisema suala la uaminifu ni muhimu zaidi katika biashara za mtandaoni na huduma za kifedha za kidijitali, ambako wananchi wanahitaji kuwa na uhakika kwamba malipo wanayofanya ni salama, taarifa zao binafsi zinalindwa na bidhaa wanazonunua mtandaoni zitawafikia.

    “Biashara za mtandaoni zinategemea uaminifu. Bila uaminifu, uchumi wa kidijitali hauwezi kustawi,” alisema Dkt. Mwasaga.

    Akizungumzia matumizi ya akili bandia, Dkt. Mwasaga alisema Tanzania haipaswi kutumia teknolojia hiyo kwa kufuata mwenendo wa dunia pekee, bali inapaswa kuangalia namna inavyoweza kutumika kutatua changamoto na kuendana na vipaumbele vya maendeleo ya nchi.

    Alitaja sekta za viwanda, kilimo na maendeleo ya uchumi kuwa miongoni mwa maeneo ambayo matumizi sahihi ya AI yanaweza kutoa mchango mkubwa.

    Kwa mujibu wa Dkt. Mwasaga, manufaa ya AI yatategemea uwekezaji katika elimu na ujuzi, akitanabaisha kuwa maandalizi duni yanaweza kusababisha teknolojia hiyo kuongeza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana kutokana na baadhi ya kazi kuchukuliwa na mifumo inayotumia akili bandia.

    Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Privacy Professionals Association (TPPA), Tumwesigye Evans, alisema taasisi hiyo ina jukumu la kulinda taarifa binafsi za watumiaji kadri matumizi ya AI na uchumi wa kidijitali yanavyopanuka.

    Alisema TPPA imesaini Mkataba wa Makubaliano (MoU) na Sandbox Security ya India, pamoja na TAFINA, kwa lengo la kuimarisha uaminifu katika huduma za kidijitali nchini.

    “Kadri mabadiliko haya yanavyoendelea, ni muhimu kuimarisha imani ya wananchi katika huduma na teknolojia za kidijitali,” alisema Evans.

    Alisema ushirikiano huo unalenga kuunganisha ulinzi wa kisheria na hatua za kiufundi na kiusalama ili kulinda watumiaji wa huduma za kidijitali.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Kanda wa Mauzo na Masoko wa Sandbox, Amrita Choudhury, alisema ujenzi wa uaminifu katika matumizi ya teknolojia hauwezi kufanywa na taasisi au sekta moja pekee, bali unahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali.

    Wadau hao walisema kuimarisha uaminifu wa wananchi katika mazingira ya kidijitali ni muhimu wakati Tanzania ikiendelea kupanua matumizi ya huduma za mtandaoni, biashara za kidijitali na teknolojia mpya kama akili bandia.

    Kwa Tanzania, wataalamu wanaamini kuwa kujenga mazingira ya kidijitali yanayoaminika kutasaidia kuongeza matumizi ya huduma za mtandaoni, kulinda watumiaji dhidi ya hatari za kidijitali na kuwezesha teknolojia kuchangia zaidi katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

  • Na Yusra Temba

    Mlimbwende Jihan Dimack ameibuka mshindi wa taji la Miss Grand Tanzania 2026, baada ya kuwashinda washiriki wengine kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania katika shindano lililojumuisha vipengele vya mahojiano, mawasilisho, matembezi ya jukwaani na uwezo wa kujieleza mbele ya majaji na hadhira.

    Ushindi huo ulishuhudiwa na wadau mbalimbali wa tasnia ya burudani, urembo na ulimwengu wa mitindo katika fainali zilizofanyika usiku wa Jumamosi katika Ukumbi wa The Super Dome, Masaki, Dar es Salaam.

    Ushindi wa Jihan Dimack unaendelea kuimarisha safari ya Tanzania katika mashindano ya Miss Grand International, baada ya mwakilishi wa mwaka 2025, Beatrice Alex, kuweka rekodi ya kuwa Mtanzania aliyefika mbali zaidi katika historia ya mashindano hayo.

    Matokeo hayo yameongeza matarajio makubwa kwa mwakilishi wa mwaka 2026, ambaye anatarajiwa kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania katika jukwaa la kimataifa.

    Jihan Dimack sasa ataiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Miss Grand International 2026, yanayotarajiwa kufanyika nchini India.

    Kwa mwaka huu, mashindano hayo yametoa jumla ya warembo tisa watakaoiwakilisha Tanzania katika majukwaa mbalimbali ya kimataifa ya urembo. Warembo hao ni Jihan Dimack – Miss Grand International, Sharon Julius – Miss Elite, Celine Edson – Miss Earth, Rose Uisso – Miss Global, Eve Godwin – Miss Africa International, Namala Patrick – Miss Tourism Africa, Prisca Lyimo – Miss Cosmo, Zulfa Yazid – Miss Africa Golden, na Janeth Anselme – Miss Intercontinental.

    Kwa upande wake, Janeth Anselme, mshindi wa taji la Miss Intercontinental Tanzania 2026, alisema anamshukuru Mungu kwa hatua aliyofikia na kwamba ushindi huo ni mwanzo wa safari mpya ya kutimiza ndoto zake.

    Janeth alisema anafurahia ushindi huo na anatamani kutumia taji hilo kuleta mchango chanya katika jamii.

    Miongoni mwa wadau waliohudhuria fainali hizo alikuwa muigizaji Angel Mazanda, maarufu kwa jina la Chioma, ambaye alisema amefurahishwa na ushindi wa Prisca Lyimo, aliyetwaa taji la Miss Cosmo Tanzania 2026.

    Angel alisema anaamini Prisca ana uwezo mkubwa wa kufanya vizuri katika majukwaa ya kimataifa.

    Kwa upande wake, mama wa mrembo aliyeshinda taji la Miss Africa International Tanzania 2026, Rose Shayo, alitoa shukrani kwa uongozi wa Miss Grand Tanzania kwa kuandaa mashindano hayo na kutoa fursa kwa mabinti wa Kitanzania kuonesha vipaji na uwezo wao.

    Pia aliwashauri wazazi, hususan akina mama, kuwapa ushirikiano mabinti zao wanaotamani kuingia katika tasnia ya urembo ili waweze kutimiza ndoto zao.

    Mashindano ya Miss Grand Tanzania ni jukwaa la kitaifa linalolenga kumpata mrembo atakayeiwakilisha Tanzania katika mashindano ya kimataifa ya Miss Grand International.

    Mbali na kuangazia uzuri wa washiriki, mashindano hayo yanasisitiza pia uongozi, mawasiliano, kujiamini na ushiriki wa wanawake vijana katika masuala ya kijamii.

  • Na Juma John Elisha

    Usajili wa mshambuliaji wa Kitanzania, Selemani Mwalimu “Gomez”, kwenda Yanga SC umegeuka kuwa moja ya habari kubwa katika dirisha la usajili kuelekea msimu wa 2026/27, hasa kutokana na namna ulivyokuja baada ya Simba SC kuwahakikishia mashabiki wake kuwa mchezaji huyo angeendelea kuitumikia klabu hiyo.

    Yanga imemtambulisha rasmi Mwalimu kuwa mchezaji wake mpya, hatua inayofungua ukurasa mpya katika safari ya mshambuliaji huyo na kuongeza ushindani wa moja kwa moja kati ya vigogo hao wawili wa soka la Tanzania.

    Mwalimu alianza wapi?

    Mwalimu, ambaye ni mshambuliaji wa Tanzania, alijiunga na Simba msimu wa 2025/26 akitokea Wydad AC ya Morocco kwa mkopo wa msimu mmoja.

    Kabla ya safari yake kwenda Morocco, tayari alikuwa amejijengea jina katika soka la Tanzania, ikiwemo kipindi chake akiwa Fountain Gate, ambako alionyesha uwezo wa kufunga na kuleta tofauti katika eneo la ushambuliaji.

    Akiwa Simba, Mwalimu aliendelea kuonyesha uwezo wa kuamua michezo yenye presha. Miongoni mwa matukio yaliyomuweka zaidi kwenye ramani ni bao alilofunga katika fainali ya Kombe la Muungano dhidi ya Yanga, ambapo Simba ilishinda 1-0 baada ya muda wa nyongeza.

    Simba iliamini Mwalimu angebaki Msimbazi

    Baada ya msimu wa 2025/26 kumalizika, hatma ya Mwalimu ilibaki kuwa kitendawili.

    Simba ilitangaza kuwa imefikia makubaliano ya kuendelea na mshambuliaji huyo kwa msimu wa 2026/27. Hata hivyo, suala hilo liliendelea kuwa na sintofahamu kutokana na msimamo wa Wydad, huku Mwalimu akirejea Morocco.

    Hali hiyo iliibua maswali kuhusu iwapo angeendelea na Simba au angehamia klabu nyingine.

    Kilele cha sakata hilo kilifika Agosti 8, 2026, wakati Mwalimu alipoonekana kupitia ujumbe uliowasilishwa katika hafla ya Simba Day, akithibitisha kuwa angeendelea kuwa sehemu ya Simba.

    Ofisa Habari wa Simba, Ahmed Ally, pia alisema klabu hiyo ilikuwa imefikia makubaliano na Wydad kwa ajili ya kumrudisha mchezaji huyo Msimbazi.

    Taarifa zilizotangulia zilieleza pia kuwa Simba ilikuwa imeongeza muda wa mkopo wa Mwalimu kutoka Wydad kwa msimu wa 2026/27.

    Yanga yaingia dakika za mwisho

    Hata hivyo, katika mgeuko ambao huenda ukawa miongoni mwa matukio yaliyoshangaza zaidi kwenye dirisha hili la usajili, Yanga imeibuka na kumtambulisha Mwalimu leo, Agosti 11, 2026.

    Hatua hiyo imekuja siku chache tu baada ya Simba kuwahakikishia mashabiki wake kuwa mshambuliaji huyo angeendelea kuichezea klabu hiyo.

    Taarifa mbalimbali za leo zinaeleza kuwa Yanga imefikia makubaliano ya kumleta Mwalimu kutoka Wydad, huku baadhi ya taarifa zikieleza kuwa usajili huo umefanyika kwa mfumo wa mkopo.

    Hata hivyo, masharti yote ya makubaliano hayo bado hayajawekwa wazi, hivyo maelezo ya mwisho kuhusu muda na aina ya mkataba yanasubiri uthibitisho rasmi wa klabu.

    Kwa nini usajili huu ni pigo kwa Simba?

    Uzito wa usajili huu haupo tu katika Yanga kumpata Mwalimu, bali zaidi katika namna alivyotoka kwenye mipango ya Simba na kuhamia kwa watani wao wakubwa.

    Simba tayari ilikuwa imemjumuisha mshambuliaji huyo katika mipango yake ya msimu mpya. Zaidi ya hapo, Mwalimu alikuwa sehemu ya kikosi kilichoshinda Kombe la Muungano na alishawahi kuonyesha uwezo wa kufanya vizuri katika michezo yenye presha kubwa.

    Kwa Yanga, usajili huu unaongeza chaguo katika safu ya ushambuliaji kwa kumpata mchezaji ambaye tayari anaifahamu ligi ya Tanzania na amepata pia uzoefu wa kucheza nje ya nchi akiwa na Wydad.

    Kwa mtazamo mpana, usajili huu hauwezi kutazamwa kama uhamisho wa kawaida wa mchezaji pekee. Ni hatua inayoongeza joto katika ushindani wa usajili kati ya Simba na Yanga, hasa baada ya timu hizo mbili kuendelea kupambana kwa nguvu katika kuvutia wachezaji bora.

    Kutoka Msimbazi hadi Jangwani

    Safari ya Mwalimu katika miezi ya hivi karibuni imekuwa na misukosuko.

    Wydad → Simba kwa mkopo → sintofahamu kuhusu hatma yake → kurejea Morocco → kuhusishwa tena na Simba → hatimaye Yanga.

    Mlolongo huo umeifanya kadhia ya Mwalimu kuwa moja ya simulizi zinazovuta zaidi kwenye dirisha la usajili la msimu wa 2026/27.

    Sasa mshambuliaji huyo anaingia katika changamoto mpya akiwa upande wa pili wa vita ya jadi ya Simba na Yanga.

    Na swali linalosubiriwa kwa hamu ni moja:

    Atakutana vipi na Simba siku Yanga itakapokutana na Wekundu wa Msimbazi?

    Jibu la swali hilo linaweza kuifanya mechi ya Simba na Yanga msimu wa 2026/27 kuwa na mvuto wa ziada, hasa iwapo Mwalimu atakuwa sehemu ya kikosi cha Yanga kitakachokabiliana na klabu yake ya zamani.

  • Na Pilastus Nyaulingo, Tanga

    Wito umetolewa kwa madereva wa bodaboda nchini kuongeza tahadhari wanapopokea abiria, hasa wanaowaomba safari za umbali mrefu, kufuatia kifo cha dereva mwenye umri wa miaka 18, Rajab Arufan, aliyefariki baada ya kwenda katika safari ya Lukozi, Wilaya ya Lushoto.

    Rajab, aliyekuwa akifanya kazi katika kituo cha bodaboda Mabanda ya Papa jijini Tanga, aliondoka kwa safari hiyo akiamini ni ya kawaida, lakini baadaye mwili wake uligundulika katika eneo la Magamba, Lushoto.

    Kwa mujibu wa watu waliokuwa karibu naye, Rajab alikuwa amemfahamu abiria aliyempa safari hiyo kwa takribani wiki mbili na awali alikuwa amewahi kumsafirisha katika maeneo ya Pangani na Horohoro.

    Rafiki yake, Hemed Said, alisema Rajab alikuwa kijana mwenye bidii aliyejiajiri kupitia kazi ya bodaboda na siku ya safari alimweleza kuwa alikuwa amepata safari ya kwenda Lushoto.

    Said alisema baada ya Rajab kutorejea na simu yake kutopatikana, walitoa taarifa kwa familia yake na baadaye walipata taarifa za kifo chake baada ya mwili kugundulika Magamba.

    Dereva mwenzake, Karim Abdallah, alisema abiria huyo hakufahamika katika kituo cha Mabanda ya Papa, huku Rajab akiwa amewaeleza wenzake kuwa alikuwa akimpa safari ndefu na malipo mazuri.

    Naye Salum Bakari, aliyewahi kufanya biashara pamoja na Rajab, alisema alimshauri kutosafiri peke yake baada ya kumweleza kuhusu safari hiyo, akisisitiza kuwa si rahisi kumwamini kila mteja.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Madereva Bodaboda Mkoa wa Tanga, Mohamed Chande, alisema madereva wanapaswa kuwa makini zaidi wanapochukua abiria wasiowafahamu, hasa wanaowaomba safari ndefu.

    Chande alisema ingawa matukio ya mauaji ya madereva yamepungua ikilinganishwa na kipindi kilichopita, bado kuna haja ya madereva kutoa taarifa mapema wanapokuwa na mashaka kuhusu abiria au safari wanazopewa.

    Alisema chama hicho kinaendelea kuhimiza ushirikiano kati ya madereva na vyombo vya usalama ili kuzuia matukio kama hayo.

    Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Almachius Mchunguzi, alisema Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi kuhusu tukio hilo na kuwataka wananchi kushirikiana na vyombo vya usalama kuwabaini wahusika wa vitendo vya uhalifu.

    Kifo cha Rajab kimeongeza wito wa kuimarishwa kwa usalama wa madereva wa bodaboda, huku wadau wakisisitiza umuhimu wa madereva kuchukua tahadhari kabla ya kukubali safari za umbali mrefu au kwenda maeneo wasiyoyafahamu.

  • Na Pilastus Nyaulingo, Dodoma

    Wadau wa sekta ya kilimo na mazingira wameeleza kuwa kilimo mseto cha miti na mazao kinaweza kuwa fursa muhimu kwa vijana kujiajiri, kuongeza kipato na kuchangia kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.

    Kauli hiyo imetolewa katika mkutano wa wadau uliofanyika Dodoma, pembezoni mwa maonesho ya Nane Nane, ambapo washiriki walijadili namna ya kuendeleza kilimo mseto kama njia ya kuboresha maisha ya jamii na kuongeza fursa za kiuchumi kwa vijana.

    Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi wa Nchi wa Vi Agroforestry Tanzania, Martha Olotu, alisema kilimo mseto kina fursa mbalimbali za kiuchumi kwa vijana, huku kikiendelea kuwa sehemu ya suluhisho la changamoto zinazoikabili sekta ya kilimo na mazingira.

    Alisema vijana wanapaswa kupewa nafasi kubwa zaidi katika sekta hiyo kwa kuwa wanaweza kutumia maarifa, teknolojia na ubunifu kuanzisha shughuli zinazohusiana na kilimo mseto na kujenga vyanzo vya kipato.

    “Uwekezaji katika kilimo mseto utasaidia vijana kujenga ajira na biashara zinazohusiana na uzalishaji wa mazao, miti na shughuli nyingine za kilimo zinazolenga kuhifadhi mazingira,” alisema Olotu.

    Kwa upande wake, mmoja wa maafisa walioshiriki katika mjadala huo, Edna Paul, alisema kilimo mseto kina nafasi muhimu katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuboresha uzalishaji wa chakula.

    Alisema mfumo huo huwezesha kuboresha rutuba ya udongo, kuongeza uzalishaji wa chakula na kuchangia kupunguza changamoto za utapiamlo katika jamii.

    Alisema kuunganisha miti na mazao katika mifumo ya kilimo kutasaidia wakulima kutumia ardhi kwa ufanisi zaidi huku wakilinda mazingira na kujenga uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa.

    Mkurugenzi wa Civil Social Protective Foundation na mshirika wa Vi Agroforestry, Nemesi Kiliya, alisema kuna umuhimu wa ushirikiano wa wadau mbalimbali katika kukuza kilimo mseto nchini.

    Alisema mpango wa kuanzisha jukwaa la kitaifa la wadau wa kilimo mseto utasaidia kuimarisha ushirikiano, kubadilishana uzoefu na kuongeza uwekezaji katika sekta hiyo kwa njia endelevu.

    Alisema jukwaa hilo pia litasaidia kuwaunganisha vijana, wakulima, mashirika na taasisi zinazohusika na sekta za kilimo na mazingira.

    Mkazi wa Nzuguni, Dodoma, Aidani Naftari, alisema kilimo mseto ni fursa inayoweza kuwasaidia vijana kujipatia kipato huku wakishiriki katika uhifadhi wa mazingira.

    “Kwa mtazamo wangu, vijana wengi tunatafuta ajira, lakini si lazima kila mtu aajiriwe kwenye ofisi. Tukipata elimu, mtaji na teknolojia sahihi, tunaweza kutumia kilimo na upandaji miti kujiajiri na kujenga maisha yetu,” alisema Naftari.

    Alisema serikali na wadau wanapaswa kuendelea kuwawezesha vijana ili fursa hiyo isiishie kwenye mijadala pekee, bali iwe chanzo cha ajira na maendeleo kwa jamii.

  • Na Pilastus Nyaulingo, Ushetu, Shinyanga

    Halmashauri ya Ushetu kupitia Idara ya Elimu imemkabidhi Tuzo ya Heshima Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel Cherehani, kwa kutambua mchango wake katika kuimarisha sekta ya elimu na kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za elimu katika halmashauri hiyo.

    Tuzo hiyo ilikabidhiwa jana katika hafla iliyosisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya viongozi, watumishi wa umma na wadau wa elimu katika kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia, kwa lengo la kuinua kiwango cha elimu kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.

    Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Ushetu, Hadija Kabojela, alisema tangu Cherehani aingie madarakani amekuwa akitoa ushirikiano mkubwa katika kuendeleza sekta ya elimu, ikiwemo kuisemea katika ngazi mbalimbali na kutoa motisha kwa walimu na wanafunzi.

    Kabojela alisema ushirikiano huo umechangia kuimarisha juhudi za maendeleo ya elimu katika halmashauri hiyo na kuongeza hamasa kwa walimu na wanafunzi kuendelea kufanya vizuri kitaaluma.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Ushetu, Gagi Lala Gagi, alisema halmashauri hiyo inajivunia ushirikiano uliopo na mbunge huyo, akieleza kuwa amekuwa mstari wa mbele kutetea maslahi ya wananchi na kuchangia upatikanaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo miradi ya sekta ya elimu.

    Alisema uwekezaji katika elimu ni msingi wa maendeleo ya jamii, huku ushirikiano kati ya viongozi na wadau ukiendelea kuwa muhimu katika kuboresha huduma zinazowagusa moja kwa moja wanafunzi na walimu.

    Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel Cherehani, aliishukuru Idara ya Elimu pamoja na watumishi wa Halmashauri ya Ushetu kwa kutambua mchango wake katika sekta hiyo.

    Alisema tuzo hiyo imempa nguvu na motisha ya kuendelea kushirikiana na halmashauri katika kuendeleza sekta ya elimu pamoja na huduma nyingine za kijamii kwa manufaa ya wananchi wa Ushetu.

    Aidha, aliahidi kuendelea kuunga mkono juhudi za kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia, pamoja na kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha sekta ya elimu inaendelea kupata mafanikio.

    Kutolewa kwa tuzo hiyo kumeelezwa kuwa ni sehemu ya kuhamasisha ushirikiano kati ya viongozi na wadau wa maendeleo katika kuimarisha sekta ya elimu, ambayo ni msingi wa maendeleo endelevu ya jamii.