• Na Pilastus Nyaulingo

    Katika jamii nyingi, mwanaume hukua akifundishwa kuwa imara, kuvumilia changamoto na kutokuonyesha udhaifu mbele ya wengine. Kauli kama “Wewe ni mwanaume,” “Usilie,” au “Vumilia tu” zimekuwa sehemu ya malezi ya wavulana na wanaume.

    Lakini nyuma ya maneno hayo kuna swali ambalo mara nyingi halizungumzwi: Mwanaume anapokuwa na maumivu, msongo au matatizo, anamweleza nani?

    Matarajio hayo yanaweza kumfanya mwanaume aamini kuwa kuomba msaada ni ishara ya udhaifu, hivyo kuchagua kubeba matatizo yake kimyakimya.

    Hali hiyo imeendelea kuibua mjadala kuhusu namna jamii inavyomfundisha mwanaume maana ya kuwa “mwanaume halisi” na madhara yanayoweza kujitokeza pale hisia zinapofichwa kwa muda mrefu.

    Utafiti uliofanyika Tanzania kuhusu afya ya akili ya akina baba mjini Mwanza umebaini kuwa takribani akina baba wote waliohusishwa katika utafiti huo walieleza kuwa jukumu lao kuu ni kuwa watoa mahitaji ya familia. Hata hivyo, ukosefu wa ajira na kipato kidogo ulihusishwa na msongo wa kiuchumi, huku baadhi ya wanaume wakihusisha uwezo wa kuitunza familia na uthibitisho wa uanaume wao.

    MWANAUME ANAPOFUNDISHWA KUTOKUONESHA HISIA

    Michael Baruti, mwandishi wa habari wa Tanzania ambaye ameendesha mazungumzo kuhusu afya ya akili ya wanaume kupitia vipindi vyake mtandaoni, amesema jamii imekuwa ikiwafundisha wanaume kwamba hawapaswi kulia wala kuonyesha hisia.

    “Jamii yetu inatuambia kwamba wanaume hawapaswi kulia. Hawapaswi kufunguka na kuwa na hisia,” alisema Baruti.

    Baruti alisema changamoto hiyo ilimfanya aanzishe mazungumzo kuhusu afya ya akili ya wanaume baada ya kupitia mwenyewe kipindi kigumu kilichoathiri kazi, familia na mahusiano yake.

    Baada ya kupata msaada wa kitaalamu, anasema alianza kuwaeleza marafiki zake kuhusu kile alichokuwa akipitia na kugundua kuwa wanaume wengi walikuwa wakikabili changamoto kama hizo, lakini walikuwa wamezoea kuzichukulia kama sehemu ya maisha kwa sababu tu ni wanaume.

    Anasema baadhi ya wanaume wamefundishwa tangu utotoni kwamba wanapaswa kukabiliana na matatizo yao wenyewe na kwamba kushindwa ni jambo lisilokubalika kwa mwanaume. Hata hivyo, anasema mtazamo huo unaweza kuwa sahihi au usiwe sahihi, kutegemea aina na muktadha wa changamoto anayokabiliana nayo mtu.

    MTAALAMU: HISIA SI ZA WANAWAKE PEKEE

    Nadia Ahmed, mshauri na mwanasaikolojia anayeshiriki katika mijadala kuhusu afya ya akili ya wanaume, amesema hakuna sababu ya kuwazuia wanaume kuonyesha hisia zao kwa sababu hisia ni sehemu ya asili ya binadamu.

    “Kibaiolojia, wanaume na wanawake wana mabadiliko ya kikemikali yanayofanana. Wanaume wanaweza kuhisi hisia zote sawa na wanawake, na hilo linadhihirisha kuwa si suala la jinsia, bali ni hisia za kawaida ambazo zinapaswa kushughulikiwa kwa njia yenye afya,” anasema Ahmed.

    Ahmed anashauri watu kukubali hisia za huzuni badala ya kuzikataa, akieleza kuwa kufanya hivyo kunaweza kumsaidia mtu kujenga njia bora za kukabiliana na changamoto.

    Mtazamo huo unatoa picha tofauti na dhana kwamba mwanaume anapaswa kuwa mtu asiyeathirika na matatizo. Mwanaume anaweza kuwa mwenye nguvu, mwenye wajibu wa familia na bado akawa na huzuni, hofu au msongo unaohitaji kuzungumziwa.

    MAJUKUMU YA KUWA MTOAJI WA FAMILIA

    Kwa wanaume wengi, jukumu la kuwa mtoaji wa mahitaji ya familia limekuwa sehemu kubwa ya utambulisho wao. Chakula, kodi, ada za watoto, matibabu na mahitaji mengine yanaweza kuonekana kuwa wajibu ambao mwanaume anapaswa kuhakikisha unapatikana bila kujali hali yake.

    Utafiti wa akina baba mjini Mwanza umeonesha kuwa matarajio hayo yanaweza kuhusishwa na msongo wa kiuchumi, hasa pale ambapo mwanaume hana ajira au kipato cha kutosha.

    Watafiti walibaini pia kuwa baadhi ya akina baba walihusisha uwezo wa kuwa mtoaji wa familia na maana ya kuwa mwanaume.

    Hii ina maana kwamba mwanaume anayeshindwa kutimiza mahitaji yote ya familia anaweza asiwe anakabiliana na tatizo la fedha pekee, bali pia hisia za kushindwa kutimiza kile ambacho jamii imemfundisha kuwa ni wajibu wake.

    Changamoto hiyo inaweza kuwa kubwa zaidi wakati mwanaume hana mtu wa kuzungumza naye kwa sababu anaogopa kuonekana dhaifu au kushindwa.

    UKIMYA UNAPOBADILIKA KUWA NJIA YA KUKABILIANA NA MATATIZO

    Baruti anasema baadhi ya wanaume wanapokabiliwa na matatizo huamua kuyaficha badala ya kuzungumza, hali ambayo wakati mwingine inaweza kuwafanya kujiingiza katika matumizi ya pombe au dawa za kulevya na tabia nyingine hatarishi zisizosaidia kutatua tatizo lililopo.

    Utafiti wa mwaka 2026 uliofanywa na watafiti wanaohusishwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi cha Muhimbili (MUHAS), Chuo Kikuu cha Oslo, pamoja na taasisi nyingine, uliangalia msongo wa akili miongoni mwa wanaume nchini Tanzania.

    Utafiti huo ulibaini uhusiano kati ya changamoto za kijamii, unyanyapaa, ukosefu wa msaada wa kijamii na afya ya akili.

    Tafiti kama hizi zinaonesha umuhimu wa kulitazama suala la afya ya akili kwa wanaume kwa upana zaidi, badala ya kusubiri tatizo liwe kubwa ndipo msaada utafutwe.

    UANAUME SI LAZIMA UJENGWE JUU YA UKIMYA

    Ongezeko la mijadala kuhusu afya ya akili ya wanaume linaonyesha kuwa kuna haja ya kuangalia upya baadhi ya mitazamo iliyorithishwa kutoka vizazi vilivyopita.

    Mwanaume anaweza kuwa jasiri bila kuficha hisia zake. Anaweza kuwa baba anayewajibika na bado akahitaji msaada. Anaweza kuwa mume anayelinda familia yake na bado akahitaji mtu wa kumsikiliza.

    Baruti anasema ni muhimu kuanza mabadiliko hayo tangu utotoni kwa kuacha kuwafundisha wavulana kwamba kulia ni ishara ya kutokuwa mwanaume.

    Amesema wazazi wanapaswa kuwauliza watoto wao wanavyojisikia na kuwapa nafasi ya kueleza hisia zao badala ya kuwafundisha kuzificha.

    Hili linaweka familia katika nafasi muhimu ya kusaidia kubadilisha mtazamo kuhusu uanaume. Mwanaume anayejua kuwa anaweza kuzungumza na mke wake, mzazi, rafiki au mtaalamu bila kuhukumiwa anaweza kuwa katika nafasi nzuri zaidi ya kukabiliana na changamoto.

    MSAADA HAUMFANYI MWANAUME KUWA DHAIFU

    Mjadala huu hauhusu kuondoa wajibu wa mwanaume katika familia wala kumfanya asiwe mwajibikaji. Badala yake, unahusu kutambua kwamba wajibu huo unaweza kuwa rahisi zaidi kutekelezwa pale anapokuwa na afya njema ya mwili na akili, akiwa pia na watu anaoweza kuwategemea.

    Mwanaume anayesema “Siko sawa” anapokuwa katika hali ngumu si lazima awe ameshindwa. Anaweza kuwa ametambua tatizo mapema na kuchukua hatua ya kutafuta suluhisho.

    Kwa mujibu wa Nadia Ahmed, hisia zinapaswa kushughulikiwa kwa njia yenye afya, jambo linalomaanisha kuwa kuzificha si lazima kuwe ishara ya nguvu.

    MWISHO WA UKIMYA

    Mwanaume si mashine inayotakiwa kufanya kazi bila kuchoka, kulipa gharama bila kulalamika na kukabiliana na kila tatizo bila kuhitaji msaada.

    Nyuma ya mwanaume anayeonekana imara kuna mtu mwenye hisia, hofu, matumaini, kushindwa na mafanikio. Kumruhusu mwanaume kuzungumza kuhusu anachopitia hakumvui uanaume; kunampa nafasi ya kuwa binadamu.

    Kwa hiyo, huenda wakati umefika wa kuacha kumuuliza mwanaume, “Kwa nini unalia?” na kuanza kumuuliza, “Nini kinakufanya uumie?”

    Kwa sababu wakati mwingine, kumsaidia mwanaume hakuanzi kwa kumpa suluhisho. Kunaweza kuanza kwa kumpa nafasi ya kusema ukweli kwamba hayuko sawa.

  • Na Mwandishi Wetu, Nachingwea – Lindi

    Wajasiriamali wa Wilaya ya Nachingwea, mkoani Lindi, wametakiwa kutumia kwa ufanisi mitaji wanayopewa na Halmashauri ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na kukuza shughuli zao za kiuchumi.

    Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Bi. Stella Kategile, wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wajasiriamali kutoka vikundi mbalimbali yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mondulane Messi.

    Kategile alisema matumizi sahihi ya mitaji yatawawezesha wajasiriamali kufikia malengo waliyojiwekea na kukuza biashara na shughuli zao za kiuchumi, badala ya kutumia fedha hizo kwa mambo tofauti na mpango waliouwasilisha na kuidhinishiwa.

    Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Jamii, James Mbakile, alisema wajasiriamali wanakabiliwa na changamoto mbalimbali katika uendeshaji wa shughuli zao, zikiwemo utoaji na usimamizi wa mitaji, usimamizi wa mapato na matumizi, ukosefu wa masoko, teknolojia pamoja na mabadiliko ya mazingira ya kibiashara.

    Naye Mkaguzi wa Ndani, Mesia Mlay, aliwataka wanachama wa vikundi kutunza kumbukumbu sahihi za fedha ili kuhakikisha uwazi na ufanisi katika uendeshaji wa shughuli zao.

    Alisema kutokuwepo kwa kumbukumbu sahihi kunasababisha changamoto mbalimbali, ikiwemo wanakikundi kushindwa kufahamu kiwango halisi cha fedha kinachoingia, kupotea kwa uaminifu miongoni mwa wanachama, pamoja na kushindwa kubaini kiasi cha fedha kinachodaiwa na kinachodaiwa na wengine.

    Aidha, Afisa Biashara wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Aurelia Haule, alieleza umuhimu wa vikundi vya wajasiriamali kujenga utamaduni wa kuweka akiba.

    Alisema akiba husaidia vikundi kukabiliana na dharura, kuwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuongeza uwekezaji, kujenga umoja na ushirika miongoni mwa wanachama, kutumia fursa za biashara kwa wakati na kuimarisha nidhamu ya matumizi ya fedha.

    Kwa upande wake, Afisa Sheria, Diana Mmary, alisema ukosefu wa mawasiliano thabiti miongoni mwa wanakikundi ni miongoni mwa vyanzo vikuu vya migogoro inayoweza kudhoofisha maendeleo ya vikundi.

    Alisema hali hiyo inaweza kusababisha baadhi ya wanachama kujiondoa katika vikundi na hivyo kuchelewesha utekelezaji wa malengo na mipango ya maendeleo.

    Mafunzo hayo yamehusisha zaidi ya vikundi 20 vya wajasiriamali pamoja na maafisa kutoka idara mbalimbali za Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, kwa lengo la kuwajengea uwezo katika usimamizi wa mitaji, fedha, kumbukumbu za kifedha, biashara na utatuzi wa changamoto zinazoweza kujitokeza katika uendeshaji wa vikundi.

  • Na Juma John Elisha

    Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Deogratius Ndejembi, ameapishwa rasmi kushika wadhifa huo katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino, Dodoma.

    Ndejembi ameapa mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, na hivyo kuanza rasmi majukumu yake mapya kama Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

    Uteuzi wa Ndejembi umefuatia kuondoka kwa aliyekuwa Makamu wa Rais, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ambaye alijiuzulu nafasi hiyo Agosti 25, 2026. Hatua hiyo ilisababisha kuwepo kwa nafasi wazi na kufungua mchakato wa kumpata Makamu wa Rais mpya.

    Hafla ya kuapishwa kwa Ndejembi imefanyika katika Ikulu ya Chamwino, Dodoma, ikiashiria mwanzo rasmi wa utekelezaji wa majukumu yake katika nafasi hiyo muhimu ya uongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

    Ndejembi anatarajiwa kushirikiana kwa karibu na Rais Samia Suluhu Hassan katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali, ikiwemo kusimamia maeneo atakayokabidhiwa kwa mujibu wa Katiba na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amezitaka taasisi za elimu kuhakikisha ubora wa elimu nchini unaendelea kuzingatiwa, akionya dhidi ya mfumo unaoweza kuwafanya wanafunzi kupata alama kubwa bila kuwa na uwezo na ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira.

    Dkt. Nchemba alitoa kauli hiyo leo wakati akifunga Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu mkoani Tanga, ambapo alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha wahitimu wanakuwa na uwezo halisi wa kutekeleza majukumu yao katika maeneo waliyosomea.

    Alisema taasisi zinazohusika na uhakiki wa ubora wa elimu zinapaswa kuhakikisha viwango vinaendelea kuzingatiwa ili elimu inayotolewa nchini iwe na tija kwa mwanafunzi na Taifa kwa ujumla.

    “Tusitengeneze mazingira ambayo kusoma kunakuwa rahisi na alama zinakuwa kubwa sana, halafu wahitimu wanapofika kazini wanapata sifuri kubwa. Hilo halikubaliki,” alisema Waziri Mkuu.

    Alisema ubora wa mafunzo ni muhimu zaidi katika sekta zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja, zikiwemo afya, uhandisi na elimu, kwa kuwa Taifa linahitaji wataalamu wenye uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa usahihi.

    “Hatuwezi kucheza kamari na afya za Watanzania kwa kuwafundisha wataalamu vibaya halafu tukatarajia matokeo mazuri. Tunahitaji walimu na wahandisi wenye uwezo; wanapojenga daraja au jengo, ni lazima liwe salama na lenye ubora,” alisema Dkt. Nchemba.

    Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, alisema Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu imekuwa sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Serikali katika kuimarisha elimu inayounganisha nadharia na ujuzi wa vitendo.

    Alisema hatua hiyo inalenga kuhakikisha wahitimu wanapata ujuzi na umahiri unaowawezesha kujiajiri na pia kukidhi mahitaji ya soko la ajira.

    Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameiagiza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na taasisi zake kuhakikisha ubunifu unaofanywa na Watanzania hauishii kwenye maonesho, bali unaendelezwa hadi kufikia uzalishaji na kuuzwa sokoni.

    Alisema Tanzania ina wabunifu wenye uwezo wa kutatua changamoto mbalimbali, lakini changamoto iliyopo ni kuhakikisha mawazo na bidhaa zao zinalindwa, zinaendelezwa na hatimaye kutumika katika maisha halisi.

    “Ni lazima tuondoke kwenye maonesho na kwenda kwenye maisha halisi, kuhakikisha kinachooneshwa kwenye matukio kama haya kinakuwa sehemu ya maisha ya kila siku na kinaingia sokoni,” alisema Waziri Mkuu.

    Alisema Serikali itaendelea kuwekeza katika sayansi, ujuzi na ubunifu kwa kuwa maeneo hayo ni muhimu katika kuibadilisha uchumi wa Taifa na kuongeza kasi ya maendeleo kupitia matumizi ya tafiti na teknolojia.

    “Hatutaweza kuendelea bila sayansi, teknolojia na utafiti na bila kutumia matokeo ya tafiti hizo. Hatuwezi kuongeza uzalishaji bila kutumia matokeo ya utafiti,” alisema.

    Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameitaka mipango ya maendeleo ya Uwanja wa Ndege wa Tanga kuzingatia mahitaji ya kiuchumi na kijamii ya mkoa huo kwa kipindi cha miaka 25 ijayo.

    Alisema miundombinu inayojengwa sasa inapaswa kuandaliwa kwa kuzingatia ongezeko la biashara, uwekezaji na usafiri wa anga katika siku zijazo, akieleza kuwa Tanga ina nafasi muhimu kama lango la kiuchumi kutokana na miradi mikubwa inayotekelezwa mkoani humo.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Abiria wanaotumia Kituo cha Mabasi cha Magufuli jijini Dar es Salaam wamelalamikia upungufu wa maeneo ya kukaa na msongamano katika vyoo, wakisema hali hiyo inawalazimu baadhi yao kusimama kwa muda mrefu au kukaa juu ya mizigo wakati wakisubiri mabasi yao.

    Malalamiko hayo yameibuka siku chache baada ya kituo hicho kuanza kupokea kwa wingi abiria wanaopanda na kushuka kituoni hapo, kufuatia maelekezo ya Serikali ya kusitisha shughuli hizo katikati ya jiji.

    Tangu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, kuagiza mabasi kurejea ndani ya kituo hicho, idadi ya abiria imeongezeka na kuongeza shinikizo katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya kusubiri.

    Richard Malima, abiria wa basi la kwenda Kyela mkoani Mbeya, alisema upungufu wa viti na maeneo ya kusubiri unapaswa kupewa kipaumbele kwa sababu baadhi ya abiria hutumia muda mrefu kituoni kabla ya safari zao.

    “Ingawa upungufu wa viti unaweza kuonekana kama changamoto ndogo, kituo kinachohudumia maelfu ya wasafiri kila siku kinapokosa maeneo ya kutosha ya kusubiri kinaweza kuathiri ubora wa huduma na ustawi wa abiria,” alisema Malima.

    Alishauri Serikali na uongozi wa kituo kuangalia uwezekano wa kuongeza maeneo maalumu ya kusubiri ili abiria waweze kukaa kwa usalama wakati wakisubiri safari zao.

    Linna Siya, abiria wa basi la kwenda Kanda ya Ziwa, amesema mazingira ya kusubiri yanahitaji kuboreshwa, hasa kwa abiria wanaotumia muda mrefu kituoni.

    Amesema baadhi ya abiria huambiwa kwenda ghorofani kusubiri, lakini wengine huamua kubaki chini karibu na mabasi kwa hofu ya kuyakosa yanapokuwa tayari kuondoka.

    “Unapofika hapa, mazingira yanachosha. Unaenda juu kununua tiketi, lakini hakuna sehemu ya kukaa katika ofisi hizo. Tunaambiwa tushuke chini na kusubiri hadi muda wa basi kuondoka,” alisema Siya.

    Alisema hali hiyo inaweza kuwa ngumu zaidi kwa wazee, wanawake wajawazito, watoto na watu wenye mahitaji maalumu ambao wanaweza kushindwa kusimama au kukaa juu ya mizigo kwa muda mrefu.

    Abiria mwingine, Omary Mohamed, alipendekeza kuwekwa kwa viti katika eneo la chini karibu na maegesho ya mabasi ili abiria waweze kusubiri bila kulazimika kwenda ghorofa ya juu.

    “Ushauri wangu ni kuweka viti huku chini. Kuna nafasi na watu wanaweza kusubiri badala ya kusimama kwa muda mrefu,” alisema Mohamed.

    Kituo hicho kina eneo maalumu la kusubiri abiria lililopo ghorofa ya kwanza. Hata hivyo, baadhi ya abiria wamesema hawapendi kutumia eneo hilo kwa sababu liko mbali na sehemu ambazo mabasi huegeshwa.

    Uchunguzi uliofanywa kituoni hapo, ulibaini kuwa eneo la kusubiri linatumika kwa shughuli mbalimbali za biashara, ikiwemo uuzaji wa nguo na vitabu, huduma za kuchaji simu na uuzaji wa chakula, hali inayopunguza nafasi inayopatikana kwa abiria wakati kituo kinapokuwa na msongamano.

    Abiria pia wamelalamikia malipo ya Sh300 wanapohitaji kutoka katika eneo la kusubiri, licha ya kuwa tayari wamelipa gharama nyingine wanapoingia kituoni.

    Kaimu Meneja wa Kituo cha Mabasi cha Magufuli, Naamini Nguve, alisema kituo kina eneo maalumu la kusubiri lililopo ghorofa ya kwanza na kwamba lina uwezo wa kuhudumia abiria.

    Alisema eneo hilo lina sehemu tatu na limewekewa televisheni, likiwawezesha abiria kupata sehemu ya kukaa na kujisitiri wakati wakisubiri mabasi yao.

    Kuhusu pendekezo la kuweka viti katika eneo la chini karibu na mabasi, Nguve alisema hatua hiyo inaweza kuleta changamoto kutokana na mpangilio wa kituo na maeneo yaliyotengwa kwa wafanyabiashara.

    Alisema kuweka viti katika eneo hilo kunaweza kusababisha mgongano wa matumizi ya nafasi kati ya abiria na wafanyabiashara waliokodi maeneo hayo.

    Kuhusu lifti isiyofanya kazi, Nguve alisema uongozi unaendelea na maboresho ili kuhakikisha huduma zinapatikana kwa ufanisi na kwa wakati kulingana na mahitaji ya kituo.

    Mbali na changamoto ya maeneo ya kusubiri, abiria na watu wanaofanya kazi kituoni hapo pia wamelalamikia msongamano katika vyoo.

    Juma Abdallah, mpagazi anayefanya kazi katika kituo hicho, amesema ongezeko la abiria limeongeza mahitaji ya huduma za vyoo.

    “Nimekuwa nikifanya kazi hapa nikibeba mizigo tangu jana. Kuna msongamano mkubwa kwenye vyoo na unalazimika kupanga foleni ili kupata huduma,” alisema Abdallah.

    Kwa upande wake, Johnson Peter amesema foleni wakati mwingine huongezwa na baadhi ya watu wanaotumia muda mrefu ndani ya vyoo licha ya kujua kuwa kuna watu wengine wanasubiri nje.

    “Unajua, baadhi ya watu huchukua muda mrefu ndani hata wanajua kuna watu wengi wanasubiri,” alisema Peter.

    Hata hivyo, Nguve alisema kituo kina vyoo vya kutosha na vya kisasa vinavyohudumia makundi mbalimbali, wakiwemo watu wenye mahitaji maalumu.

    Amesema kituo kina jumla ya vitalu 18 vya vyoo vyenye zaidi ya vyumba 140, lakini changamoto iliyopo ni baadhi ya abiria kutofahamu maeneo vilipo.

    Nguve alisema uongozi utaanza kutoa matangazo kwa abiria ili kuwaelekeza maeneo yenye vyoo na kuwasaidia kutumia huduma hizo kwa ufanisi.

    Ongezeko la abiria katika Kituo cha Mabasi cha Magufuli limekuja baada ya Serikali kuelekeza mabasi yanayofanya safari za mikoani kusitisha kupakia na kushusha abiria katikati ya jiji, hatua iliyofanya kituo hicho kuwa na shughuli nyingi zaidi.

    Hali hiyo imeongeza umuhimu wa kuhakikisha maeneo ya kusubiri, vyoo, lifti na huduma nyingine muhimu zinaendana na idadi ya abiria wanaotumia kituo hicho.

    Kwa abiria, changamoto kubwa ni kupata mazingira salama na yenye heshima wakati wakisubiri safari zao, huku uongozi wa kituo ukisisitiza kuwa baadhi ya huduma zipo lakini zinahitaji abiria kuelekezwa vizuri kuhusu maeneo zinakopatikana.

  • Na Jastini Bukebuke, Geita

    Mwanamke maarufu kwa jina la Mwinjilisti amewashangaza washiriki wa uzinduzi wa Geita Polisi Jamii Jogging Club uliofanyika jana katika Uwanja wa Kalangalala, Manispaa ya Geita, baada ya kushiriki kikamilifu katika mazoezi ya jogging licha ya umri wake mkubwa.

    Ushiriki wake ulimvutia Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela, ambaye alimpongeza na kumtia moyo kwa kumkabidhi vifaa vya michezo pamoja na fedha kama motisha, akimtambua kwa moyo wake wa dhati wa kuunga mkono michezo, afya na ustawi wa jamii.

    Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, SACP Safia Jongo, pia alimpongeza Mwinjilisti kwa kuwa mfano bora wa ushiriki wa jamii katika shughuli za michezo na afya.

    SACP Jongo alisisitiza umuhimu wa wananchi kutoka makundi na rika mbalimbali kushiriki katika shughuli za michezo, akieleza kuwa ushiriki wa jamii katika michezo husaidia kuimarisha afya, mshikamano na mahusiano mazuri kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.

    Uzinduzi wa Geita Polisi Jamii Jogging Club umeendelea kuonesha umuhimu wa ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na jamii katika kujenga jamii yenye afya, mshikamano na usalama.

    Ushiriki wa Mwinjilisti ulikuwa miongoni mwa vivutio vya uzinduzi huo, ukitoa somo kwamba umri si kikwazo katika kushiriki shughuli za kuimarisha afya na ustawi wa jamii.

    Mwinjilisti alionesha ustahimilivu wa hali ya juu wakati wa mazoezi hayo na kufanikiwa kuyamaliza bila kuonesha dalili za kuchoka, jambo lililowavutia na kuwapa hamasa washiriki wengine.

  • Na George Gabriel

    Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Edward Magala, ameyataka mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs) wilayani humo kubuni na kutekeleza miradi itakayowawezesha kujitegemea kifedha badala ya kutegemea fedha za wafadhili pekee.

    Magala alitoa wito huo hivi karibuni wakati akifungua Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu.

    Alisema ni muhimu kwa mashirika hayo kujenga uwezo wa kutekeleza miradi kwa ufanisi na weledi, huku yakizingatia maadili, misingi na vipaumbele vya jamii.

    Magala alionya kuwa utegemezi mkubwa wa fedha za wafadhili unaweza kuhatarisha mwendelezo wa miradi endapo ufadhili huo utakoma. Hivyo, alizitaka NGOs kubuni vyanzo mbadala vya mapato na kuimarisha ubunifu ili ziweze kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa uendelevu.

    Akizungumza baada ya mkutano huo, Anyesi John Mhalu alipongeza hatua ya Serikali ya kuwakutanisha wadau hao, akisema jukwaa hilo ni muhimu katika kujenga uwezo, kubadilishana uzoefu na kujadili namna bora ya kuboresha utendaji wa mashirika yasiyo ya kiserikali.

    Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Rudrick Charles, alisema Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali huratibiwa kwa kushirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum pamoja na Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NaCoNGO).

    Alisema kupitia jukwaa hilo, mashirika huwasilisha na kujadili taarifa za utekelezaji wa shughuli na miradi yao, pamoja na kubainisha changamoto na fursa zinazohusu utendaji wao.

    Jukwaa hilo lilishirikisha pia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na mashirika saba yasiyo ya kiserikali yanayotekeleza shughuli mbalimbali katika Wilaya ya Nanyumbu.

    Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa mwaka 2026 limebebwa na kaulimbiu: “Fikra Mpya Kuhusu Uendelevu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali: Ubunifu, Ubia na Upatikanaji wa Rasilimali Fedha Kupitia Vyanzo vya Ndani.”

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Kampuni ya Yas Tanzania imezindua huduma ya Yas Fiber jijini Dodoma, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa intaneti ya kasi kwa kaya, wafanyabiashara na taasisi katika mji unaoendelea kukua kwa kasi.

    Huduma hiyo ya nyuzi-optiki kwa sasa inapatikana katika maeneo ya Ilazo, Ipagala, Swaswa, Mjini Kati na Barabara za Namba, huku kampuni hiyo ikieleza kuwa itaendelea kupanua huduma katika maeneo mengine kulingana na mahitaji ya wananchi.

    Uzinduzi huo ulifanyika jijini Dodoma hivi karibuni na kuhudhuriwa na viongozi wa Serikali, wateja pamoja na wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya jiji, ukiwa sehemu ya juhudi za kuongeza miundombinu ya mawasiliano ya kisasa.

    Mkurugenzi Mtendaji wa Yas Fiber, Maxime Woimant, alisema kampuni hiyo inalenga kuchochea mabadiliko ya kidijitali Dodoma kwa kuhakikisha wakazi na wafanyabiashara wanapata muunganisho wa uhakika utakaowawezesha kufanya kazi, kujifunza na kupata huduma za kidijitali kwa ufanisi zaidi.

    “Tunajitolea kusaidia mabadiliko ya kidijitali ya Dodoma kwa kutoa muunganisho wa kuaminika ambao utawawezesha wakazi na wafanyabiashara kufanya kazi, kujifunza, kuendesha shughuli kwa ufanisi zaidi na kupata huduma za kidijitali,” alisema Woimant.

    Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, Jabir Shekimweri, aliyeshiriki katika uzinduzi huo, alisisitiza umuhimu wa kuwa na miundombinu ya kidijitali yenye uhakika wakati Dodoma ikiendelea kupanuka.

    Shekimweri alisema upanuzi wa huduma za mawasiliano unaweza kufungua fursa zaidi za kiuchumi na kijamii kupitia uchumi wa kidijitali.

    Katika uzinduzi mwingine wa huduma za Yas jijini Dodoma mwezi Machi 2026, Shekimweri alisema upanuzi wa huduma za mawasiliano unaweza kusaidia kuongeza shughuli za kiuchumi, kurahisisha upatikanaji wa huduma na kuimarisha muunganisho kwa wakazi.

    Kwa upande wake, Yas Tanzania imesema uzinduzi wa Yas Fiber unalenga pia kuongeza fursa za kujifunza mtandaoni, kuwasaidia wajasiriamali kufikia masoko mapya, kurahisisha uendeshaji wa biashara na kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali kwa kaya.

    Hatua hiyo inakuja wakati matumizi ya intaneti nchini yakiendelea kuongezeka. Kwa mujibu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), hadi Juni 2025 kulikuwa na watumiaji wa intaneti 54,078,530 nchini, huku teknolojia za 3G, 4G na 5G zikiendelea kuenea katika maeneo mbalimbali.

  • Na Juma John Elisha

    Dar es Salaam — Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, amesema atatumia haki yake ya kujitetea mwenyewe katika kesi ya uhaini inayomkabili, baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dar es Salaam, kuamua kuwa ana kesi ya kujibu.

    Uamuzi huo umetolewa leo, Agosti 21, 2026, na Jopo la Majaji watatu linaloongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru, akisaidiwa na Jaji James Karayemaha na Jaji Ferdinand Kiwonde.

    Uamuzi huo umefikiwa baada ya upande wa Jamhuri kuwasilisha ushahidi wake na Mahakama kusikiliza hoja za pande zote kuhusu iwapo ushahidi uliowasilishwa umeweka msingi wa kumtaka Lissu kuingia katika hatua ya kujitetea. Katika hatua hiyo, upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi 17.

    LISSU KUJITETEA MWENYEWE

    Baada ya Mahakama kutangaza kuwa ana kesi ya kujibu, Lissu amesema atatumia haki yake ya kisheria ya kujitetea na kutoa ushahidi wake mwenyewe kama shahidi wa upande wa utetezi.

    Hatua hiyo inaashiria kuanza kwa awamu mpya ya kesi, ambapo upande wa utetezi sasa utapata fursa ya kujibu ushahidi na hoja zilizowasilishwa na upande wa Jamhuri.

    Awali, Lissu alikuwa ameiomba Mahakama itamke kuwa hana kesi ya kujibu, akidai kuwa ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka haukufikia kiwango cha kumlazimisha kuingia katika hatua ya utetezi.

    KESI YA UHAINI INAYOMKABILI LISSU

    Lissu anakabiliwa na shtaka moja la uhaini chini ya kifungu cha 39(2)(d) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu. Shtaka hilo linahusishwa na kauli anazodaiwa kutoa kuhusu nia ya kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

    Upande wa mashtaka unadai kuwa kauli hizo zililenga kushinikiza uongozi wa Serikali na kuzuia mchakato wa uchaguzi, madai ambayo Lissu ameyapinga.

    Katika hoja zake za awali, Lissu alisisitiza kuwa ili kuthibitisha shtaka la uhaini, lazima kuwe na ushahidi unaoonyesha nia ya kutenda kitendo kinachodaiwa kuwa cha uhaini. Alidai pia kuwa ushahidi uliowasilishwa na Jamhuri haukuthibitisha msingi huo.

    HATUA INAYOFUATA

    Kwa uamuzi wa Mahakama kwamba Lissu ana kesi ya kujibu, shauri hilo sasa linaingia katika hatua ya utetezi. Lissu atapata nafasi ya kutoa ushahidi wake, huku upande wa mashtaka ukiwa na fursa ya kumuuliza maswali kwa mujibu wa taratibu za kawaida za kesi.

    Hatahivyo, uamuzi wa Mahakama kwamba Lissu ana kesi ya kujibu si hukumu ya kuwa ana hatia. Ni uamuzi kwamba ushahidi uliowasilishwa katika hatua ya mashtaka umeweka msingi wa kesi kuendelea katika hatua ya utetezi.

    Kesi hiyo imekuwa ikifuatiliwa kwa karibu kutokana na nafasi ya Lissu kama Mwenyekiti wa CHADEMA na uzito wa shtaka linalomkabili.