• Na Mwandishi Wetu, Nachingwea – Lindi

    Wajasiriamali wa Wilaya ya Nachingwea, mkoani Lindi, wametakiwa kutumia kwa ufanisi mitaji wanayopewa na Halmashauri ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na kukuza shughuli zao za kiuchumi.

    Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Bi. Stella Kategile, wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wajasiriamali kutoka vikundi mbalimbali yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mondulane Messi.

    Kategile alisema matumizi sahihi ya mitaji yatawawezesha wajasiriamali kufikia malengo waliyojiwekea na kukuza biashara na shughuli zao za kiuchumi, badala ya kutumia fedha hizo kwa mambo tofauti na mpango waliouwasilisha na kuidhinishiwa.

    Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Jamii, James Mbakile, alisema wajasiriamali wanakabiliwa na changamoto mbalimbali katika uendeshaji wa shughuli zao, zikiwemo utoaji na usimamizi wa mitaji, usimamizi wa mapato na matumizi, ukosefu wa masoko, teknolojia pamoja na mabadiliko ya mazingira ya kibiashara.

    Naye Mkaguzi wa Ndani, Mesia Mlay, aliwataka wanachama wa vikundi kutunza kumbukumbu sahihi za fedha ili kuhakikisha uwazi na ufanisi katika uendeshaji wa shughuli zao.

    Alisema kutokuwepo kwa kumbukumbu sahihi kunasababisha changamoto mbalimbali, ikiwemo wanakikundi kushindwa kufahamu kiwango halisi cha fedha kinachoingia, kupotea kwa uaminifu miongoni mwa wanachama, pamoja na kushindwa kubaini kiasi cha fedha kinachodaiwa na kinachodaiwa na wengine.

    Aidha, Afisa Biashara wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Aurelia Haule, alieleza umuhimu wa vikundi vya wajasiriamali kujenga utamaduni wa kuweka akiba.

    Alisema akiba husaidia vikundi kukabiliana na dharura, kuwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuongeza uwekezaji, kujenga umoja na ushirika miongoni mwa wanachama, kutumia fursa za biashara kwa wakati na kuimarisha nidhamu ya matumizi ya fedha.

    Kwa upande wake, Afisa Sheria, Diana Mmary, alisema ukosefu wa mawasiliano thabiti miongoni mwa wanakikundi ni miongoni mwa vyanzo vikuu vya migogoro inayoweza kudhoofisha maendeleo ya vikundi.

    Alisema hali hiyo inaweza kusababisha baadhi ya wanachama kujiondoa katika vikundi na hivyo kuchelewesha utekelezaji wa malengo na mipango ya maendeleo.

    Mafunzo hayo yamehusisha zaidi ya vikundi 20 vya wajasiriamali pamoja na maafisa kutoka idara mbalimbali za Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, kwa lengo la kuwajengea uwezo katika usimamizi wa mitaji, fedha, kumbukumbu za kifedha, biashara na utatuzi wa changamoto zinazoweza kujitokeza katika uendeshaji wa vikundi.

  • Na Juma John Elisha

    Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Deogratius Ndejembi, ameapishwa rasmi kushika wadhifa huo katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino, Dodoma.

    Ndejembi ameapa mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, na hivyo kuanza rasmi majukumu yake mapya kama Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

    Uteuzi wa Ndejembi umefuatia kuondoka kwa aliyekuwa Makamu wa Rais, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ambaye alijiuzulu nafasi hiyo Agosti 25, 2026. Hatua hiyo ilisababisha kuwepo kwa nafasi wazi na kufungua mchakato wa kumpata Makamu wa Rais mpya.

    Hafla ya kuapishwa kwa Ndejembi imefanyika katika Ikulu ya Chamwino, Dodoma, ikiashiria mwanzo rasmi wa utekelezaji wa majukumu yake katika nafasi hiyo muhimu ya uongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

    Ndejembi anatarajiwa kushirikiana kwa karibu na Rais Samia Suluhu Hassan katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali, ikiwemo kusimamia maeneo atakayokabidhiwa kwa mujibu wa Katiba na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amezitaka taasisi za elimu kuhakikisha ubora wa elimu nchini unaendelea kuzingatiwa, akionya dhidi ya mfumo unaoweza kuwafanya wanafunzi kupata alama kubwa bila kuwa na uwezo na ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira.

    Dkt. Nchemba alitoa kauli hiyo leo wakati akifunga Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu mkoani Tanga, ambapo alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha wahitimu wanakuwa na uwezo halisi wa kutekeleza majukumu yao katika maeneo waliyosomea.

    Alisema taasisi zinazohusika na uhakiki wa ubora wa elimu zinapaswa kuhakikisha viwango vinaendelea kuzingatiwa ili elimu inayotolewa nchini iwe na tija kwa mwanafunzi na Taifa kwa ujumla.

    “Tusitengeneze mazingira ambayo kusoma kunakuwa rahisi na alama zinakuwa kubwa sana, halafu wahitimu wanapofika kazini wanapata sifuri kubwa. Hilo halikubaliki,” alisema Waziri Mkuu.

    Alisema ubora wa mafunzo ni muhimu zaidi katika sekta zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja, zikiwemo afya, uhandisi na elimu, kwa kuwa Taifa linahitaji wataalamu wenye uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa usahihi.

    “Hatuwezi kucheza kamari na afya za Watanzania kwa kuwafundisha wataalamu vibaya halafu tukatarajia matokeo mazuri. Tunahitaji walimu na wahandisi wenye uwezo; wanapojenga daraja au jengo, ni lazima liwe salama na lenye ubora,” alisema Dkt. Nchemba.

    Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, alisema Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu imekuwa sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Serikali katika kuimarisha elimu inayounganisha nadharia na ujuzi wa vitendo.

    Alisema hatua hiyo inalenga kuhakikisha wahitimu wanapata ujuzi na umahiri unaowawezesha kujiajiri na pia kukidhi mahitaji ya soko la ajira.

    Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameiagiza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na taasisi zake kuhakikisha ubunifu unaofanywa na Watanzania hauishii kwenye maonesho, bali unaendelezwa hadi kufikia uzalishaji na kuuzwa sokoni.

    Alisema Tanzania ina wabunifu wenye uwezo wa kutatua changamoto mbalimbali, lakini changamoto iliyopo ni kuhakikisha mawazo na bidhaa zao zinalindwa, zinaendelezwa na hatimaye kutumika katika maisha halisi.

    “Ni lazima tuondoke kwenye maonesho na kwenda kwenye maisha halisi, kuhakikisha kinachooneshwa kwenye matukio kama haya kinakuwa sehemu ya maisha ya kila siku na kinaingia sokoni,” alisema Waziri Mkuu.

    Alisema Serikali itaendelea kuwekeza katika sayansi, ujuzi na ubunifu kwa kuwa maeneo hayo ni muhimu katika kuibadilisha uchumi wa Taifa na kuongeza kasi ya maendeleo kupitia matumizi ya tafiti na teknolojia.

    “Hatutaweza kuendelea bila sayansi, teknolojia na utafiti na bila kutumia matokeo ya tafiti hizo. Hatuwezi kuongeza uzalishaji bila kutumia matokeo ya utafiti,” alisema.

    Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameitaka mipango ya maendeleo ya Uwanja wa Ndege wa Tanga kuzingatia mahitaji ya kiuchumi na kijamii ya mkoa huo kwa kipindi cha miaka 25 ijayo.

    Alisema miundombinu inayojengwa sasa inapaswa kuandaliwa kwa kuzingatia ongezeko la biashara, uwekezaji na usafiri wa anga katika siku zijazo, akieleza kuwa Tanga ina nafasi muhimu kama lango la kiuchumi kutokana na miradi mikubwa inayotekelezwa mkoani humo.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Abiria wanaotumia Kituo cha Mabasi cha Magufuli jijini Dar es Salaam wamelalamikia upungufu wa maeneo ya kukaa na msongamano katika vyoo, wakisema hali hiyo inawalazimu baadhi yao kusimama kwa muda mrefu au kukaa juu ya mizigo wakati wakisubiri mabasi yao.

    Malalamiko hayo yameibuka siku chache baada ya kituo hicho kuanza kupokea kwa wingi abiria wanaopanda na kushuka kituoni hapo, kufuatia maelekezo ya Serikali ya kusitisha shughuli hizo katikati ya jiji.

    Tangu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, kuagiza mabasi kurejea ndani ya kituo hicho, idadi ya abiria imeongezeka na kuongeza shinikizo katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya kusubiri.

    Richard Malima, abiria wa basi la kwenda Kyela mkoani Mbeya, alisema upungufu wa viti na maeneo ya kusubiri unapaswa kupewa kipaumbele kwa sababu baadhi ya abiria hutumia muda mrefu kituoni kabla ya safari zao.

    “Ingawa upungufu wa viti unaweza kuonekana kama changamoto ndogo, kituo kinachohudumia maelfu ya wasafiri kila siku kinapokosa maeneo ya kutosha ya kusubiri kinaweza kuathiri ubora wa huduma na ustawi wa abiria,” alisema Malima.

    Alishauri Serikali na uongozi wa kituo kuangalia uwezekano wa kuongeza maeneo maalumu ya kusubiri ili abiria waweze kukaa kwa usalama wakati wakisubiri safari zao.

    Linna Siya, abiria wa basi la kwenda Kanda ya Ziwa, amesema mazingira ya kusubiri yanahitaji kuboreshwa, hasa kwa abiria wanaotumia muda mrefu kituoni.

    Amesema baadhi ya abiria huambiwa kwenda ghorofani kusubiri, lakini wengine huamua kubaki chini karibu na mabasi kwa hofu ya kuyakosa yanapokuwa tayari kuondoka.

    “Unapofika hapa, mazingira yanachosha. Unaenda juu kununua tiketi, lakini hakuna sehemu ya kukaa katika ofisi hizo. Tunaambiwa tushuke chini na kusubiri hadi muda wa basi kuondoka,” alisema Siya.

    Alisema hali hiyo inaweza kuwa ngumu zaidi kwa wazee, wanawake wajawazito, watoto na watu wenye mahitaji maalumu ambao wanaweza kushindwa kusimama au kukaa juu ya mizigo kwa muda mrefu.

    Abiria mwingine, Omary Mohamed, alipendekeza kuwekwa kwa viti katika eneo la chini karibu na maegesho ya mabasi ili abiria waweze kusubiri bila kulazimika kwenda ghorofa ya juu.

    “Ushauri wangu ni kuweka viti huku chini. Kuna nafasi na watu wanaweza kusubiri badala ya kusimama kwa muda mrefu,” alisema Mohamed.

    Kituo hicho kina eneo maalumu la kusubiri abiria lililopo ghorofa ya kwanza. Hata hivyo, baadhi ya abiria wamesema hawapendi kutumia eneo hilo kwa sababu liko mbali na sehemu ambazo mabasi huegeshwa.

    Uchunguzi uliofanywa kituoni hapo, ulibaini kuwa eneo la kusubiri linatumika kwa shughuli mbalimbali za biashara, ikiwemo uuzaji wa nguo na vitabu, huduma za kuchaji simu na uuzaji wa chakula, hali inayopunguza nafasi inayopatikana kwa abiria wakati kituo kinapokuwa na msongamano.

    Abiria pia wamelalamikia malipo ya Sh300 wanapohitaji kutoka katika eneo la kusubiri, licha ya kuwa tayari wamelipa gharama nyingine wanapoingia kituoni.

    Kaimu Meneja wa Kituo cha Mabasi cha Magufuli, Naamini Nguve, alisema kituo kina eneo maalumu la kusubiri lililopo ghorofa ya kwanza na kwamba lina uwezo wa kuhudumia abiria.

    Alisema eneo hilo lina sehemu tatu na limewekewa televisheni, likiwawezesha abiria kupata sehemu ya kukaa na kujisitiri wakati wakisubiri mabasi yao.

    Kuhusu pendekezo la kuweka viti katika eneo la chini karibu na mabasi, Nguve alisema hatua hiyo inaweza kuleta changamoto kutokana na mpangilio wa kituo na maeneo yaliyotengwa kwa wafanyabiashara.

    Alisema kuweka viti katika eneo hilo kunaweza kusababisha mgongano wa matumizi ya nafasi kati ya abiria na wafanyabiashara waliokodi maeneo hayo.

    Kuhusu lifti isiyofanya kazi, Nguve alisema uongozi unaendelea na maboresho ili kuhakikisha huduma zinapatikana kwa ufanisi na kwa wakati kulingana na mahitaji ya kituo.

    Mbali na changamoto ya maeneo ya kusubiri, abiria na watu wanaofanya kazi kituoni hapo pia wamelalamikia msongamano katika vyoo.

    Juma Abdallah, mpagazi anayefanya kazi katika kituo hicho, amesema ongezeko la abiria limeongeza mahitaji ya huduma za vyoo.

    “Nimekuwa nikifanya kazi hapa nikibeba mizigo tangu jana. Kuna msongamano mkubwa kwenye vyoo na unalazimika kupanga foleni ili kupata huduma,” alisema Abdallah.

    Kwa upande wake, Johnson Peter amesema foleni wakati mwingine huongezwa na baadhi ya watu wanaotumia muda mrefu ndani ya vyoo licha ya kujua kuwa kuna watu wengine wanasubiri nje.

    “Unajua, baadhi ya watu huchukua muda mrefu ndani hata wanajua kuna watu wengi wanasubiri,” alisema Peter.

    Hata hivyo, Nguve alisema kituo kina vyoo vya kutosha na vya kisasa vinavyohudumia makundi mbalimbali, wakiwemo watu wenye mahitaji maalumu.

    Amesema kituo kina jumla ya vitalu 18 vya vyoo vyenye zaidi ya vyumba 140, lakini changamoto iliyopo ni baadhi ya abiria kutofahamu maeneo vilipo.

    Nguve alisema uongozi utaanza kutoa matangazo kwa abiria ili kuwaelekeza maeneo yenye vyoo na kuwasaidia kutumia huduma hizo kwa ufanisi.

    Ongezeko la abiria katika Kituo cha Mabasi cha Magufuli limekuja baada ya Serikali kuelekeza mabasi yanayofanya safari za mikoani kusitisha kupakia na kushusha abiria katikati ya jiji, hatua iliyofanya kituo hicho kuwa na shughuli nyingi zaidi.

    Hali hiyo imeongeza umuhimu wa kuhakikisha maeneo ya kusubiri, vyoo, lifti na huduma nyingine muhimu zinaendana na idadi ya abiria wanaotumia kituo hicho.

    Kwa abiria, changamoto kubwa ni kupata mazingira salama na yenye heshima wakati wakisubiri safari zao, huku uongozi wa kituo ukisisitiza kuwa baadhi ya huduma zipo lakini zinahitaji abiria kuelekezwa vizuri kuhusu maeneo zinakopatikana.

  • Na Jastini Bukebuke, Geita

    Mwanamke maarufu kwa jina la Mwinjilisti amewashangaza washiriki wa uzinduzi wa Geita Polisi Jamii Jogging Club uliofanyika jana katika Uwanja wa Kalangalala, Manispaa ya Geita, baada ya kushiriki kikamilifu katika mazoezi ya jogging licha ya umri wake mkubwa.

    Ushiriki wake ulimvutia Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela, ambaye alimpongeza na kumtia moyo kwa kumkabidhi vifaa vya michezo pamoja na fedha kama motisha, akimtambua kwa moyo wake wa dhati wa kuunga mkono michezo, afya na ustawi wa jamii.

    Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, SACP Safia Jongo, pia alimpongeza Mwinjilisti kwa kuwa mfano bora wa ushiriki wa jamii katika shughuli za michezo na afya.

    SACP Jongo alisisitiza umuhimu wa wananchi kutoka makundi na rika mbalimbali kushiriki katika shughuli za michezo, akieleza kuwa ushiriki wa jamii katika michezo husaidia kuimarisha afya, mshikamano na mahusiano mazuri kati ya Jeshi la Polisi na wananchi.

    Uzinduzi wa Geita Polisi Jamii Jogging Club umeendelea kuonesha umuhimu wa ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na jamii katika kujenga jamii yenye afya, mshikamano na usalama.

    Ushiriki wa Mwinjilisti ulikuwa miongoni mwa vivutio vya uzinduzi huo, ukitoa somo kwamba umri si kikwazo katika kushiriki shughuli za kuimarisha afya na ustawi wa jamii.

    Mwinjilisti alionesha ustahimilivu wa hali ya juu wakati wa mazoezi hayo na kufanikiwa kuyamaliza bila kuonesha dalili za kuchoka, jambo lililowavutia na kuwapa hamasa washiriki wengine.

  • Na George Gabriel

    Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Edward Magala, ameyataka mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs) wilayani humo kubuni na kutekeleza miradi itakayowawezesha kujitegemea kifedha badala ya kutegemea fedha za wafadhili pekee.

    Magala alitoa wito huo hivi karibuni wakati akifungua Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu.

    Alisema ni muhimu kwa mashirika hayo kujenga uwezo wa kutekeleza miradi kwa ufanisi na weledi, huku yakizingatia maadili, misingi na vipaumbele vya jamii.

    Magala alionya kuwa utegemezi mkubwa wa fedha za wafadhili unaweza kuhatarisha mwendelezo wa miradi endapo ufadhili huo utakoma. Hivyo, alizitaka NGOs kubuni vyanzo mbadala vya mapato na kuimarisha ubunifu ili ziweze kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa uendelevu.

    Akizungumza baada ya mkutano huo, Anyesi John Mhalu alipongeza hatua ya Serikali ya kuwakutanisha wadau hao, akisema jukwaa hilo ni muhimu katika kujenga uwezo, kubadilishana uzoefu na kujadili namna bora ya kuboresha utendaji wa mashirika yasiyo ya kiserikali.

    Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Rudrick Charles, alisema Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali huratibiwa kwa kushirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum pamoja na Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NaCoNGO).

    Alisema kupitia jukwaa hilo, mashirika huwasilisha na kujadili taarifa za utekelezaji wa shughuli na miradi yao, pamoja na kubainisha changamoto na fursa zinazohusu utendaji wao.

    Jukwaa hilo lilishirikisha pia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na mashirika saba yasiyo ya kiserikali yanayotekeleza shughuli mbalimbali katika Wilaya ya Nanyumbu.

    Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa mwaka 2026 limebebwa na kaulimbiu: “Fikra Mpya Kuhusu Uendelevu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali: Ubunifu, Ubia na Upatikanaji wa Rasilimali Fedha Kupitia Vyanzo vya Ndani.”

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Kampuni ya Yas Tanzania imezindua huduma ya Yas Fiber jijini Dodoma, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa intaneti ya kasi kwa kaya, wafanyabiashara na taasisi katika mji unaoendelea kukua kwa kasi.

    Huduma hiyo ya nyuzi-optiki kwa sasa inapatikana katika maeneo ya Ilazo, Ipagala, Swaswa, Mjini Kati na Barabara za Namba, huku kampuni hiyo ikieleza kuwa itaendelea kupanua huduma katika maeneo mengine kulingana na mahitaji ya wananchi.

    Uzinduzi huo ulifanyika jijini Dodoma hivi karibuni na kuhudhuriwa na viongozi wa Serikali, wateja pamoja na wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya jiji, ukiwa sehemu ya juhudi za kuongeza miundombinu ya mawasiliano ya kisasa.

    Mkurugenzi Mtendaji wa Yas Fiber, Maxime Woimant, alisema kampuni hiyo inalenga kuchochea mabadiliko ya kidijitali Dodoma kwa kuhakikisha wakazi na wafanyabiashara wanapata muunganisho wa uhakika utakaowawezesha kufanya kazi, kujifunza na kupata huduma za kidijitali kwa ufanisi zaidi.

    “Tunajitolea kusaidia mabadiliko ya kidijitali ya Dodoma kwa kutoa muunganisho wa kuaminika ambao utawawezesha wakazi na wafanyabiashara kufanya kazi, kujifunza, kuendesha shughuli kwa ufanisi zaidi na kupata huduma za kidijitali,” alisema Woimant.

    Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, Jabir Shekimweri, aliyeshiriki katika uzinduzi huo, alisisitiza umuhimu wa kuwa na miundombinu ya kidijitali yenye uhakika wakati Dodoma ikiendelea kupanuka.

    Shekimweri alisema upanuzi wa huduma za mawasiliano unaweza kufungua fursa zaidi za kiuchumi na kijamii kupitia uchumi wa kidijitali.

    Katika uzinduzi mwingine wa huduma za Yas jijini Dodoma mwezi Machi 2026, Shekimweri alisema upanuzi wa huduma za mawasiliano unaweza kusaidia kuongeza shughuli za kiuchumi, kurahisisha upatikanaji wa huduma na kuimarisha muunganisho kwa wakazi.

    Kwa upande wake, Yas Tanzania imesema uzinduzi wa Yas Fiber unalenga pia kuongeza fursa za kujifunza mtandaoni, kuwasaidia wajasiriamali kufikia masoko mapya, kurahisisha uendeshaji wa biashara na kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali kwa kaya.

    Hatua hiyo inakuja wakati matumizi ya intaneti nchini yakiendelea kuongezeka. Kwa mujibu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), hadi Juni 2025 kulikuwa na watumiaji wa intaneti 54,078,530 nchini, huku teknolojia za 3G, 4G na 5G zikiendelea kuenea katika maeneo mbalimbali.

  • Na Juma John Elisha

    Dar es Salaam — Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, amesema atatumia haki yake ya kujitetea mwenyewe katika kesi ya uhaini inayomkabili, baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dar es Salaam, kuamua kuwa ana kesi ya kujibu.

    Uamuzi huo umetolewa leo, Agosti 21, 2026, na Jopo la Majaji watatu linaloongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru, akisaidiwa na Jaji James Karayemaha na Jaji Ferdinand Kiwonde.

    Uamuzi huo umefikiwa baada ya upande wa Jamhuri kuwasilisha ushahidi wake na Mahakama kusikiliza hoja za pande zote kuhusu iwapo ushahidi uliowasilishwa umeweka msingi wa kumtaka Lissu kuingia katika hatua ya kujitetea. Katika hatua hiyo, upande wa mashtaka uliwasilisha mashahidi 17.

    LISSU KUJITETEA MWENYEWE

    Baada ya Mahakama kutangaza kuwa ana kesi ya kujibu, Lissu amesema atatumia haki yake ya kisheria ya kujitetea na kutoa ushahidi wake mwenyewe kama shahidi wa upande wa utetezi.

    Hatua hiyo inaashiria kuanza kwa awamu mpya ya kesi, ambapo upande wa utetezi sasa utapata fursa ya kujibu ushahidi na hoja zilizowasilishwa na upande wa Jamhuri.

    Awali, Lissu alikuwa ameiomba Mahakama itamke kuwa hana kesi ya kujibu, akidai kuwa ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka haukufikia kiwango cha kumlazimisha kuingia katika hatua ya utetezi.

    KESI YA UHAINI INAYOMKABILI LISSU

    Lissu anakabiliwa na shtaka moja la uhaini chini ya kifungu cha 39(2)(d) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu. Shtaka hilo linahusishwa na kauli anazodaiwa kutoa kuhusu nia ya kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

    Upande wa mashtaka unadai kuwa kauli hizo zililenga kushinikiza uongozi wa Serikali na kuzuia mchakato wa uchaguzi, madai ambayo Lissu ameyapinga.

    Katika hoja zake za awali, Lissu alisisitiza kuwa ili kuthibitisha shtaka la uhaini, lazima kuwe na ushahidi unaoonyesha nia ya kutenda kitendo kinachodaiwa kuwa cha uhaini. Alidai pia kuwa ushahidi uliowasilishwa na Jamhuri haukuthibitisha msingi huo.

    HATUA INAYOFUATA

    Kwa uamuzi wa Mahakama kwamba Lissu ana kesi ya kujibu, shauri hilo sasa linaingia katika hatua ya utetezi. Lissu atapata nafasi ya kutoa ushahidi wake, huku upande wa mashtaka ukiwa na fursa ya kumuuliza maswali kwa mujibu wa taratibu za kawaida za kesi.

    Hatahivyo, uamuzi wa Mahakama kwamba Lissu ana kesi ya kujibu si hukumu ya kuwa ana hatia. Ni uamuzi kwamba ushahidi uliowasilishwa katika hatua ya mashtaka umeweka msingi wa kesi kuendelea katika hatua ya utetezi.

    Kesi hiyo imekuwa ikifuatiliwa kwa karibu kutokana na nafasi ya Lissu kama Mwenyekiti wa CHADEMA na uzito wa shtaka linalomkabili.

  • Na Pilastus Nyaulingo

    Wanaishi nyumba moja. Wanalala kitanda kimoja. Wanaweza hata kula chakula mezani pamoja. Lakini wakati mwingine au wakati wote, kila mmoja anaishi katika dunia yake.

    Mmoja anashika simu kuangalia WhatsApp. Mwingine anaingia Instagram, TikTok au Facebook. Dakika zinapita, saa zinapita, siku zinapita mazungumzo yanapungua na ukimya unatawala.

    Kwa nje, ndoa inaonekana na kila kitu kinachohitajika. Lakini ndani yake, mmoja au wote wawili wanaweza kuwa wanapitia hisia za upweke.

    Hapo ndipo simu inapoanza kupata nafasi nyingine katika maisha ya wanandoa. Badala ya kuwa chombo cha kuwasiliana tu, simu inaweza kuwa sehemu ya kukimbilia wakati mtu anahisi hana mtu wa kuzungumza naye. Inaweza kumpa burudani, mazungumzo na watu wengine au hisia ya kwamba kuna mtu anayemsikiliza.

    Lakini swali linabaki: Je, simu inawasaidia wanandoa kukabiliana na upweke, au wakati mwingine inazidi kuwapeleka mbali zaidi?

    UPWEKE UPO HATA KATIKA NDOA

    Tunaposema mtu yuko peke yake, mara nyingi tunafikiria mtu asiye na mwenza, familia au marafiki. Lakini upweke unaweza kuwa tofauti. Mtu anaweza kuwa na mwenza lakini akahisi hana mtu anayemsikiliza, anayemwelewa au anayeshirikiana naye kihisia.

    Katika ndoa, hususani za miongo hii, hali hii hujitokeza mawasiliano yanapopungua, wanandoa wanapokuwa na ratiba zinazowatenganisha, migogoro inapokaa muda mrefu bila kutatuliwa au kila mmoja anapojenga maisha yake bila kumshirikisha mwenzake.

    Utafiti wa Mhadhiri Msaidizi katika Idara ya Uandishi wa Habari na Masomo ya Mawasiliano, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Vincent Mpepo wa mwaka 2017, uliohusu athari za mitandao ya kijamii katika mawasiliano ya wanandoa katika Mkoa wa Dar es Salaam, ulihusisha washiriki 117 kutoka Ilala, Kinondoni na Temeke.

    Utafiti huo ulionyesha kuwa mitandao ya kijamii inaweza kuwa na mchango chanya katika mawasiliano ya wanandoa. Asilimia 80 ya washiriki walisema mawasiliano kupitia mitandao ya kijamii yalisaidia kuimarisha uhusiano wao, huku asilimia 12 wakiwa hawana uhakika na asilimia nane wakisema hayakusaidia kuimarisha uhusiano.

    Mpepo alipendekeza wanandoa kupata elimu kuhusu matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii na kuwa makini na masuala ya faragha na usiri katika matumizi ya teknolojia hiyo.

    Hapa ndipo tunapoona kwamba tatizo si simu yenyewe. Tatizo linaweza kuwa namna simu na mitandao ya kijamii vinavyotumiwa ndani ya mahusiano.

    SIMU INAPOKUWA MAHALI PA KUKIMBILIA

    Kwa mwanandoa anayehisi kupuuzwa au kutosikilizwa, simu inaweza kuwa na mvuto mkubwa.

    Anaweza kuingia kwenye mitandao ya kijamii na kuanza kuzungumza na watu wengine. Anaweza kutazama video kwa muda mrefu, kusoma maoni, kushiriki kwenye vikundi au kuwasiliana na rafiki ambaye anahisi anamwelewa zaidi.

    Hapo simu inaweza kuanza kufanya kazi kama aina ya rafiki wa kidijitali.

    Tatizo linatokea ambapo muda unaotumika kutafuta faraja kwenye simu unaanza kuchukua nafasi ya muda ambao ungeweza kutumika kujenga, kuboresha uhusiano wa wanandoa.

    Katika utafiti huo wa mwaka 2017 unaonyesha upande mmoja muhimu wa jambo hili: mitandao ya kijamii inaweza kusaidia wanandoa kuwasiliana na kuimarisha uhusiano wao, lakini matumizi yake yanahitaji mipaka na uelewa wa namna yanavyoweza kuathiri faragha na mawasiliano ya wanandoa.

    Kwa hiyo, simu inaweza kuwa daraja la mawasiliano au ikawa njia ya kukwepa mazungumzo ya ana kwa ana, kutegemea namna inavyotumiwa.

    WANANDOA WANAWEZA KUWA KARIBU KIDIJITALI LAKINI MBALI KIHISIA

    Mwanandoa anaweza kutuma ujumbe kwa mwenza wake akiwa kazini. Anaweza kumpigia simu, kumtumia picha au hata kumjibu ndani ya sekunde chache au pia asijibu huku pia mwenza anaweza kuona aina fulani ya kupuuzwa.

    Lakini mawasiliano yote hayo yanaweza kuwepo huku mazungumzo muhimu ya ndani ya ndoa yakikosekana.

    “Unaendeleaje?” inaweza kuulizwa, lakini hakuna anayefika kwenye swali la “Umeshindaje?”

    Hapo ndipo tofauti kati ya mawasiliano na ukaribu wa kihisia vinapoonekana.

    Utafiti wa Estella Alfred Mwambene wa mwaka 2019 kuhusu matumizi ya simu katika ndoa huko Iringa uliangalia namna matumizi ya teknolojia yanavyoathiri maisha ya familia na mawasiliano ya wanandoa.

    Utafiti huo ulihusisha wanandoa pamoja na viongozi wa jamii na watoto, na uliangazia namna simu zinavyoweza kusaidia mawasiliano lakini pia kuleta changamoto pale matumizi yanapokuwa ya kupita kiasi.

    Matokeo hayo yanaonyesha kuwa uwezo wa kuwasiliana kwa simu siyo lazima kubebe maana halisi ya ukaribu wa kihisia kwa wanandoa hao.

    Mwanandoa anaweza kuwa anawasiliana kila siku na mwenza wake kupitia simu, lakini bado akahisi hasikilizwi, haeleweki au anapuuzwa.

    SIMU INAPOCHUKUA NAFASI YA MWENZA….

    Kuna wakati mtu haishiki simu kwa sababu ana jambo maalumu la kufanya. Anaishika kwa sababu amezoea.

    Anaangalia ujumbe. Anafungua TikTok. Anarudi WhatsApp. Anaangalia Instagram na katika mitandao mingine au programu tumizi.

    Kwa mwanandoa anayehisi upweke, mzunguko huu unaweza kumpa hisia ya kuwa ana watu karibu naye.

    Lakini ukaribu wa kidijitali si lazima uwe sawa na ukaribu wa kihisia.

    Mtu anaweza kupata jumbe nyingi mtandaoni lakini bado akahisi hana mtu wa kumweleza kinachomsibu moyoni.

    Hili linafanya swali la matumizi ya simu ndani ya ndoa kuwa kubwa kuliko suala la muda wa kutumia skrini. Linakuwa suala la mahusiano.

    SIMU NA MIGOGORO YA NDOA…

    Mwaka 2026, Haji Ally Mkande kutoka Chuo cha Maendeleo ya Jamii ya Jamii Tengeru alichapisha utafiti uliochunguza matumizi na athari za simu katika migogoro ya ndoa mkoani Dar es Salaam.

    Utafiti huo ulihusisha washiriki 30, wakiwemo wanaume 10 waliooa, wanawake 10 walioolewa, wakwe wanne, watoto wanne na maafisa wawili wa ustawi wa jamii.

    Utafiti huo ulionyesha kuwa simu zinaweza kuwa chombo muhimu cha mawasiliano kati ya wanandoa, lakini matumizi yasiyofaa yanaweza pia kuongeza migogoro, hasa pale yanapohusisha usiri, mawasiliano ya nje ya ndoa na tuhuma za kutokuwa waaminifu.

    Hii inaonyesha kuwa simu si lazima iwe chanzo pekee cha migogoro ya ndoa. Wakati mwingine inaweza kuwa chombo kinachorahisisha au kuonyesha matatizo ambayo tayari yapo ndani ya uhusiano.

    USIRI WA SIMU UNAPOJENGA UKUTA…

    Kuna tofauti kati ya kuwa na faragha na kuwa na usiri.

    Kila mwanandoa ana haki ya kuwa na nafasi yake binafsi. Lakini pale simu inapokuwa eneo ambalo mwenza haruhusiwi kabisa kulikaribia, kila ujumbe unafichwa, kufutwa na matumizi yake yanaambatana na hofu ya kugundulika, mashaka yanaweza kuanza.

    Mwanandoa anaweza kujiuliza: “Kwa nini simu yake siku zote iko kimya?” “Kwa nini akipokea simu anatoka nje?” “Kwa nini ujumbe fulani unafutwa?” “Kwa nini muda mwingi anaonekana kuwa karibu na watu wa mtandaoni kuliko mimi?”

    Maswali haya yanaweza kuzaa mashaka hata kabla ya mtu kuwa na ushahidi wa jambo lolote.

    Utafiti wa Mkande unaonyesha umuhimu wa kuangalia namna matumizi ya simu yanavyohusiana na migogoro ya ndoa, mawasiliano na masuala ya uaminifu.

    Kwa hiyo, tatizo linaweza lisianze na usaliti wenyewe, bali linaweza kuanza na kuvunjika kwa uaminifu na mawasiliano.

    SIMU INAWEZA PIA KUWA SEHEMU YA SULUHISHO

    Pamoja na changamoto hizo, si sahihi kuifanya simu ionekane kama adui wa ndoa.

    Kwa wanandoa wanaoishi mbali kutokana na kazi, biashara au majukumu mengine, simu inaweza kuwa muhimu sana.

    Mwanandoa anaweza kumpigia mwenza wake wakati wa mapumziko kazini, kumjulisha anachofanya, kumjulia hali au kumtumia ujumbe wa kumtia moyo.

    Mitandao ya kijamii pia inaweza kuwa sehemu ya kushirikishana mambo yanayowafurahisha.

    Utafiti wa Mpepo wa mwaka 2017 unaunga mkono upande huu chanya. Asilimia 80 ya washiriki wake walisema mawasiliano kupitia mitandao ya kijamii yalisaidia kuimarisha uhusiano wao.

    Kwa hiyo, suala si kuondoa simu kwenye ndoa. Ni kuhakikisha simu haiondoi ndoa kwenye maisha ya wanandoa.

    WAKATI SIMU INAPOCHUKUA NAFASI YA MAZUNGUMZO

    Fikiria wanandoa wawili wamekaa sebuleni.

    Mume anaangalia simu. Mke anaangalia simu.

    Wote wako pamoja, lakini hakuna anayezungumza na mwenzake.

    Hii inaweza kuonekana kama jambo dogo, lakini ikiwa ni tabia ya kila siku na endelevu, inapunguza muda wa mawasiliano ya ana kwa ana.

    Utafiti wa mwaka 2019 kuhusu matumizi ya simu mahiri katika ndoa huko Iringa ulionyesha changamoto zinazoweza kujitokeza pale simu zinapotumika kupita kiasi, ikiwemo kuvurugika kwa mawasiliano ya ana kwa ana na muda wa familia.

    Hapo ndipo matumizi ya simu yanapohitaji mipaka.

    Siyo kila dakika ya mapumziko lazima ijazwe na matumizi ya simu au skrini.

    Wakati mwingine ndoa inahitaji dakika chache ambazo hakuna anayeshika simu.

    UPWEKE HAUJIBIWI KWA DATA,BANDO PEKEE

    Kuna jambo moja muhimu ambalo wanandoa wanapaswa kulifikiria.

    Kama mtu anatumia simu kila usiku kwa sababu hataki kukaa kimya na mwenza wake, huenda tatizo si simu.

    Huenda kuna mazungumzo ambayo hayajafanyika.

    Huenda kuna maumivu ambayo hayajasikilizwa.

    Huenda kuna migogoro ambayo imeachwa kwa muda mrefu.

    Huenda mmoja anahisi hapendwi, au anapuuzwa.

    Au huenda wote wawili wamekuwa wakiishi ndani ya ratiba yenye majukumu mengi kiasi kwamba wamesahau kujenga urafiki wao wenyewe.

    Katika hali kama hiyo, simu inaweza kutoa usumbufu wa muda lakini isitatue chanzo cha upweke.

    Ni dhahiri mazungumzo yanahitajika kati ya wanandoa ili kubaini chanzo cha upweke huo na kupatikana kwa suluhu isiyohusisha matumizi ya simu kama kimbilio au kichaka cha upweke.

    WANANDOA WANAHITAJI KUJENGA MUDA WAO

    Kuna umuhimu wa wanandoa kuwa na muda ambao ni wao.

    Muda wa kuzungumza, muda wa kula pamoja, muda wa kutembea. Muda wa kucheka, muda wa kuzungumzia fedha, watoto, kazi, mahusiano yao na mambo yanayowasumbua.

    Na wakati mwingine, muda wa kukaa bila simu.

    Hili si suala la teknolojia pekee. Ni suala la kuweka uhusiano mbele wakati ambapo kila mmoja anaweza kuwa na ulimwengu wake wa kidijitali.

    Utafiti wa mwaka 2024 kuhusu mahusiano ya wanandoa na mitandao ya kijamii ulionyesha kuwa matumizi ya mitandao yanaweza kuathiri namna wanandoa wanavyowasiliana na kuhusiana, jambo linaloonyesha umuhimu wa kuweka mipaka na kuwa na mawasiliano ya wazi kuhusu matumizi ya teknolojia ndani ya ndoa.

    SIMU ISIWE SEHEMU YA KUFICHA UPWEKE

    Mwanandoa anayejihisi mpweke si lazima aihitaji simu zaidi ya mwenza wake.

    Anaweza kuwa anahitaji mwenza wake zaidi.

    Anahitaji kuzungumza.

    Anahitaji kusikilizwa.

    Anahitaji kuulizwa anaendeleaje bila mazungumzo kuishia kwenye bili, watoto, chakula, kazi au majukumu ya nyumbani.

    Kwa sababu ndoa inaweza kuwa na kila kitu kinachoonekana nje lakini ikawa na upweke mkubwa ndani.

    Na wakati huo, simu inaweza kuwa rahisi zaidi kuishika kuliko kumtazama mwenza machoni na kusema:

    “Nahisi niko peke yangu.”

    Hilo ndilo jambo ambalo wanandoa wanahitaji kulifikiria.

    TEKNOLOJIA ISIJENGE UKUTA KATI YA WENZA

    Simu imebadilisha namna tunavyowasiliana. Imefanya iwe rahisi kumpata mwenza aliye mbali, kutuma ujumbe, kupiga video na kushirikishana maisha ya kila siku.

    Lakini teknolojia hiyo hiyo inaweza kuwa chanzo cha umbali ikiwa itaanza kuchukua nafasi ya mawasiliano ya kweli.

    Tafiti za Tanzania za mwaka 2017, 2019 na 2026 zinaonyesha namna tofauti kwamba simu na mitandao ya kijamii zinaweza kuwa na faida katika mahusiano, lakini matumizi yasiyo na mipaka yanaweza pia kuvuruga mawasiliano, kuongeza usiri, kuathiri uaminifu na kuleta migogoro.

    Kwa hiyo, suluhisho si kuwaambia wanandoa waache kutumia simu.

    Suluhisho ni kujenga utamaduni ambao simu inakuwa chombo cha kuimarisha ndoa, si mahali pa kukimbilia kila mmoja anapohisi mpweke.

    Kwa sababu mwisho wa siku, mtu anaweza kuwa na maelfu ya watu kwenye simu yake lakini bado akahitaji mtu mmoja tu aliyeko pembeni yake, na si mwingine ni mwenza wake.

    Na kama mtu huyo ni mwenza wake, basi labda kabla hajafungua simu kutafuta mtu wa kuzungumza naye, anapaswa kwanza kuuliza:

    “Tumepata lini muda wa kuzungumza?”

    Huenda jibu la upweke ndani ya ndoa lisianzie kwenye simu. Huenda linaanzia kwenye mazungumzo yaliyokosekana kati ya watu wawili wanaoishi chini ya paa moja.