• Na Greyson Makabe

    Marekebisho ya Sheria ya Mwenendo wa Madai (Civil Procedure Code), yaliyofanyika mwaka 2023, yameendelea kuzua mjadala mpana miongoni mwa mawakili, wasomi wa sheria na wadau wa mfumo wa haki nchini.

    Miongoni mwa marekebisho yanayobishaniwa zaidi ni kifungu cha 13, kinachowataka wahusika wa mgogoro wa madai kutafuta suluhu kupitia upatanisho kabla ya kufungua shauri mahakamani.

    Lengo la kifungu hiki ni kuhamasisha utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala (Alternative Dispute Resolution – ADR), ili kupunguza mzigo wa mashauri mahakamani na kuwapa wahusika nafasi ya kumaliza migogoro yao kwa maelewano. Hata hivyo, utekelezaji wake umeibua changamoto mbalimbali zinazohusiana na upatikanaji wa haki kwa wakati.

    Katika mahojiano na mawakili na wataalamu mbalimbali wa sheria, wengi wameeleza kuwa, ingawa dhamira ya kifungu hicho ni njema, hakikuandaliwa sambamba na utaratibu rasmi wa utekelezaji wake. Kwa sasa hakuna mfumo maalumu unaowaongoza wahusika namna ya kufanya upatanisho, nani atasimamia mchakato huo, wala namna ya kuthibitisha kuwa juhudi za usuluhishi zilifanyika na zikashindikana.

    Kwa mtazamo wao, hali hiyo imeifanya sheria hiyo kuwa ngumu kutekelezeka, hasa kwa watu ambao tayari wamefikia hatua ya kushindikana kabisa kuelewana.

    Wanasema ni vigumu kuwatarajia mahasimu ambao hata kuzungumza au kusalimiana ni changamoto, wakae tena mezani kutafuta suluhu bila uwepo wa chombo rasmi cha kuwaongoza.

    Athari za kifungu hicho tayari zimeanza kuonekana mahakamani ambapo baadhi ya mashauri yamekuwa yakitupiliwa mbali kwa sababu wahusika hawakufuata masharti ya kifungu cha 13 kabla ya kufungua kesi.

    Miongoni mwa maamuzi yanayonukuliwa mara kwa mara ni ya Jaji Beda katika shauri la A. Z. Bade Kilamala Alipinde na Mwenzake dhidi ya Saed Yeslam Saed, Kesi Na. 000032909 ya mwaka 2024.

    Katika uamuzi huo, mahakama ilisisitiza kuwa shauri lolote ambalo halijafuata utaratibu uliowekwa na kifungu cha 13 haliwezi kusikilizwa na linapaswa kutupiliwa mbali kwa kuvunja matakwa ya sheria.

    Kwa mujibu wa wadau wa sheria, maamuzi ya aina hiyo yamewaongezea wananchi gharama zisizo za lazima.

    Mbali na ada ya kufungua kesi katika Mahakama Kuu, ambayo inaweza kufikia au kuzidi shilingi 150,000 kutegemeana na aina ya shauri, mlalamikaji hulazimika pia kugharamia wakili, maandalizi ya nyaraka na gharama nyingine za uendeshaji wa shauri. Kesi inapofutwa kwa sababu ya kutokufuata utaratibu huo, gharama hizo hupotea bila shauri kusikilizwa.

    Hata hivyo, si majaji wote wamekuwa na mtazamo unaofanana kuhusu tafsiri ya kifungu hicho.

    Katika shauri la Imalaseko Investment v Amer Mohamed Mbarak Company Limited & Another (Land Case No. 29281 of 2024), Jaji wa Mahakama Kuu, Mheshimiwa Hemed, alitoa mtazamo tofauti. Katika uamuzi wake alieleza kuwa kifungu cha 13 hakijaweka utaratibu mahsusi wa namna wadaawa wanavyopaswa kukutana kwa ajili ya usuluhishi kabla ya kufika mahakamani.

    Alisisitiza kuwa sheria haijaeleza ni taasisi gani itasimamia mchakato huo wala mahali ambapo wahusika wanapaswa kwenda ikiwa upatanisho unahitajika.

    Kwa msingi huo, aliona kuwa mahakama ina wajibu wa kuhakikisha haki inapatikana na si kuzuia wananchi kuifikia kutokana na mapungufu yaliyopo katika utekelezaji wa sheria. Alisisitiza pia kuwa moja ya majukumu ya msingi ya mahakama ni kutatua migogoro katika jamii, hivyo tafsiri ya sheria inapaswa kuzingatia haki badala ya kuangalia taratibu pekee.

    Wananchi mbalimbali niliowahoji, ambao hawakutaka majina yao yachapishwe, nao wameeleza wasiwasi wao kuhusu kifungu hicho. Wamesema kingekuwa na manufaa zaidi kama Serikali ingeweka mfumo rasmi wa usuluhishi unaofanana na mifumo iliyopo katika maeneo mengine ya sheria.

    Kwa mfano, katika migogoro inayosikilizwa na mabaraza ya kata, mlalamikaji hulazimika kwanza kupitia hatua ya upatanisho na hupewa cheti cha usuluhishi kabla ya kuendelea na hatua zinazofuata.

    Vivyo hivyo, katika mashauri ya ndoa, wahusika hulazimika kupitia mabaraza ya usuluhishi wa ndoa kabla ya kufungua shauri la talaka mahakamani.

    Kwa maoni ya wananchi hao, mfumo kama huo ungewekwa pia katika mashauri ya madai ili kila mlalamikaji apate cheti kinachoonyesha kuwa juhudi za usuluhishi zilifanyika na hazikufanikiwa. Hatua hiyo ingeondoa sintofahamu iliyopo sasa na kupunguza uwezekano wa mashauri kutupiliwa mbali kwa sababu za kiutaratibu.

    Kwa ujumla, mjadala kuhusu kifungu cha 13 unaonyesha mvutano kati ya dhamira ya kuhimiza utatuzi wa migogoro nje ya mahakama na haki ya kila mwananchi kupata fursa ya kusikilizwa mahakamani bila vikwazo visivyo na utaratibu wa wazi.

    Wadau wengi wanaamini kuwa ili kifungu hicho kifikie malengo yaliyokusudiwa, ni muhimu Serikali iweke mfumo wa kitaasisi wa usuluhishi wenye taratibu, mamlaka na uthibitisho rasmi. Bila kufanya hivyo, kuna hatari ya kifungu hicho kuendelea kutafsiriwa kwa namna tofauti na mahakama mbalimbali, jambo linaloweza kuathiri usawa wa haki na kuongeza gharama kwa wananchi.

  • Na George Gabriel

    Serikali imewataka wataalamu wa tiba asili na tiba mbadala nchini kuendelea kutoa huduma kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo iliyowekwa ili kuhakikisha usalama wa wananchi na kuongeza uaminifu wa huduma hizo katika jamii.

    Wito huo umetolewa hivi karibuni na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Ibrahim Mwanauta, wakati akifungua Mkutano wa Mwaka wa Wataalamu wa Tiba Asili na Tiba Mbadala uliofanyika katika Ukumbi wa Halmashauri hiyo.

    Mwanauta alisema Serikali inatambua mchango mkubwa wa wataalamu wa tiba asili katika kuboresha huduma za afya, lakini akasisitiza kuwa huduma hizo zinapaswa kutolewa kwa kuzingatia sheria, maadili na weledi wa taaluma hiyo.

    “Tiba asili ni sehemu muhimu ya huduma za afya, lakini ni lazima itolewe kwa kuzingatia sheria, maadili na weledi ili kulinda afya za wananchi,” alisema Mwanauta.

    Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Dkt. Marco Mazanzagar, aliwataka wataalamu wote kuhakikisha wanajisajili na kupata leseni kutoka Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala kabla ya kuanza kutoa huduma.

    Alionya kuwa utoaji wa huduma bila leseni ni kinyume cha sheria na unaweza kuhatarisha afya za wananchi.

    Naye Mratibu wa Tiba Asili na Tiba Mbadala Mkoa wa Mtwara, Deogratius Kikota, aliwahamasisha wataalamu kushiriki maadhimisho ya kilele cha Tiba Asili na Tiba Mbadala ngazi ya Mkoa wa Mtwara yatakayofanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba mwezi Agosti 2026.

    Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Wataalamu wa Tiba Asili Tanzania (BAWATA), Halidi Mohamed Mdoe, aliipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu kwa ushirikiano wake na wataalamu wa tiba asili, akiahidi kuwa chama hicho kitaendelea kuwapatia wanachama wake ushauri, mafunzo na msaada wa kitaalamu ili kuboresha utoaji wa huduma.

    Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mkutano huo, mtaalamu wa tiba asili Juma Hamisi alisema mafunzo na maelekezo yaliyotolewa yamewaongezea uelewa kuhusu wajibu wa kuzingatia sheria na taratibu za utoaji wa huduma.

    “Mkutano huu umetukumbusha wajibu wetu wa kufanya kazi kwa weledi na kufuata sheria. Tutayafanyia kazi maelekezo yote tuliyopewa kwa manufaa ya wananchi,” alisema Hamisi.

    Mkutano huo uliwakutanisha wataalamu wa tiba asili na tiba mbadala kutoka maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Nanyumbu kwa lengo la kujadili maendeleo ya sekta hiyo, kuimarisha ushirikiano na Serikali pamoja na kuboresha huduma zinazotolewa kwa jamii.

  • Na Jastini Bukebuke, Geita

    Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Ludete wamepatiwa elimu kuhusu majukumu ya Dawati la Jinsia na Watoto jana walipotembelea Kituo cha Polisi Katoro kilichopo Mji Mdogo wa Katoro, Wilaya ya Geita kwa lengo la kujifunza shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Jeshi la Polisi.

    Akizungumza na wanafunzi hao, Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Geita, SP Severia Nauyo, alisema ziara hiyo imelenga kuwajengea wanafunzi uelewa kuhusu namna Polisi Jamii inavyotekeleza majukumu yake ya kutoa elimu kwa wananchi, kuimarisha ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na jamii, pamoja na kushirikisha makundi mbalimbali katika kuzuia uhalifu na kuimarisha usalama.

    SP Nauyo aliwapongeza wanafunzi hao wa Kidato cha Nne kwa kuonyesha uthubutu na utayari wa kujifunza kuhusu majukumu ya Jeshi la Polisi, hususan namna Dawati la Jinsia na Watoto linavyopokea na kushughulikia malalamiko na migogoro ya kijamii kwa kuzingatia sheria, taratibu na haki za wahusika.

    Aidha, aliwahimiza wanafunzi hao kuwa mabalozi wa amani kwa kutoa taarifa kwa walimu, wazazi, walezi na Jeshi la Polisi pindi wanapoona viashiria vya uhalifu, ukatili wa kijinsia, unyanyasaji wa watoto au vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama na amani katika jamii.

    Kwa upande wao, wanafunzi wa Shule ya Sekondari Ludete walilishukuru Jeshi la Polisi kwa kuwapatia elimu hiyo muhimu, wakieleza kuwa imewaongezea uelewa kuhusu majukumu ya Dawati la Jinsia na Watoto pamoja na umuhimu wa kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kudumisha amani, usalama na utulivu.

    Pia walilipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kutoa huduma kwa wananchi kwa weledi, haki na bila ubaguzi, jambo ambalo limeendelea kuimarisha imani ya jamii kwa Jeshi hilo.

  • Na Jastini Bukebuke, Geita

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limeendelea kuimarisha usalama barabarani kwa kutoa elimu kwa madereva wa magari madogo na makubwa wanaofanya kazi katika kampuni za GGML na Capital Drilling.

    Elimu hiyo ilitolewa katika eneo la Shift Change Site, Kata ya Nyalwanzaja, Tarafa ya Busanda, Wilaya ya Geita, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kupunguza ajali na kuongeza uelewa wa madereva kuhusu umuhimu wa kuzingatia sheria za usalama barabarani.

    Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mkaguzi wa Polisi, INSP Gabriel Rwehimbiza, aliwataka madereva kuhakikisha wanamiliki leseni halali za udereva na kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za uendeshaji wa magari ndani ya mgodi ili kuzuia ajali na kulinda maisha yao pamoja na ya watumiaji wengine wa barabara.

    Alisema madereva wanapaswa kuwa mabalozi wa usalama kwa kuwaelimisha wenzao kuhusu umuhimu wa kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani.

    Aidha, alionya kuwa hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya madereva watakaobainika kukiuka sheria, ikiwemo kufungiwa leseni za udereva kwa mujibu wa vifungu vya 33 na 34 vya Sheria ya Usalama Barabarani, Sura ya 168, Marejeo ya mwaka 2023.

    Kwa upande wake, Mkufunzi wa IHET, Steven Reuben, amelipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kutoa elimu inayochangia kuongeza uelewa wa madereva kuhusu usalama na nidhamu ya uendeshaji wa magari ndani ya mgodi.

    Reuben aliwataka madereva kuhakikisha abiria wote wanaotumia magari wanafunga mikanda ya usalama, kuzingatia viwango vya mwendo vilivyowekwa na kudumisha umbali salama wanapokuwa karibu na magari makubwa ya mgodini ili kupunguza hatari ya ajali.

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limeendelea kutoa wito kwa madereva wote kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani wakati wote, likisisitiza kuwa kufuata sheria ni msingi wa kulinda maisha, mali na kuhakikisha mazingira salama ya kazi na usafiri.

  • Na Damasi Kalembwe

    Kikosi cha Usalama Barabarani kwa kushirikiana na uongozi wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (UDART) kilifanya kikao kazi na madereva wa mabasi ya mwendokasi katika ukumbi wa Chuo cha Teknolojia cha Dar es salaam (DIT) ili ,  kujadili na kuweka mikakati ya kupunguza ajali zinazotokea katika mfumo wa usafiri wa mabasi yaendayo haraka.

    Katika kikao hicho, ilielezwa kuwa kati ya asilimia 65 na 70 ya ajali zinazohusisha mabasi ya mwendokasi husababishwa na makosa ya kibinadamu, ikiwemo ulevi, uzembe na mwendo kasi usiozingatia sheria huku asilimia zilizobaki ni ajali kutokana na changamoto za miundombinu pamoja na hitilafu za kiufundi katika baadhi ya magari.

    Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Kinondoni, SSP Adamson Mwangamilo, alisisema ni muhimu kufunga viashiria vya mwanga kwenye vizuizi barabarani ili kuongeza usalama, huku akiwahimiza wananchi kutumia daraja la juu la waenda kwa miguu eneo la Kimara Mwisho badala ya kuvuka barabara kiholela, hatua itakayosaidia kupunguza ajali na msongamano wa magari.

    Kwa upande wake, Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Ilala (RTO), SSP Salum M. Morimori, alionya kuwa vitendo vya uzembe, ulevi wakati wa kuendesha, pamoja na kukaidi taa na alama za usalama barabarani havitavumiliwa.

    Aliwataka madereva kuzingatia kanuni za udereva wa kujihami ili kupunguza ajali, hususan katika maeneo yenye msongamano mkubwa kama Kivukoni na Msimbazi.

    Naye Mkurugenzi wa UDART, Pius Ng’ingo, aliahidi kushughulikia changamoto za kiufundi zinazohusu mabasi ya mwendokasi na kuimarisha usimamizi wa nidhamu kwa madereva na watumishi wote ili kuongeza usalama wa huduma zinazotolewa.

    Akizungumza kwa niaba ya madereva, Nassoro Hoza aliahidi ushirikiano wa karibu na Jeshi la Polisi pamoja na uongozi wa UDART katika kutekeleza kaulimbiu ya “Utii wa Sheria Bila Shuruti”, akisema madereva watazingatia udereva wa kujihami ili kulinda maisha ya abiria, watumiaji wengine wa barabara na vyombo vya usafiri wanavyoviendesha.

    Kikao hicho ni sehemu ya juhudi zinazoendelea za Jeshi la Polisi na UDART za kuimarisha usalama barabarani, kupunguza ajali na kuhakikisha huduma za usafiri wa mabasi ya mwendokasi zinaendelea kutolewa kwa usalama na ufanisi.

  • Na Damasi Kalembwe

    Jeshi la Polisi Mkoa wa Kinondoni, kupitia Kitengo cha Ushirikishwaji wa Jamii, limetoa msaada wa mahitaji mbalimbali kwa vituo vya kulelea watoto wenye mahitaji maalumu vya New Life na Huruma Children Home, vilivyopo Wilaya ya Kinondoni, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ustawi wa watoto hao na kudumisha mahusiano mema kati ya Jeshi la Polisi na jamii.

    Mkuu wa Kitengo cha Ushirikishwaji wa Jamii Mkoa wa Kinondoni, ACP Ally Shughuli Wendo, aliyemwakilisha Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, SACP Mtatiro Kitinkwi, aliongoza ziara hiyo akiwa ameambatana na maafisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali.

    Katika ziara hiyo, Jeshi la Polisi lilikabidhi msaada uliojumuisha unga, mchele, sukari, mafuta ya kula, taulo za kike, pampasi na mahitaji mengine muhimu kwa ajili ya kusaidia malezi na ustawi wa watoto wanaolelewa katika vituo hivyo.

    Akizungumza kwa niaba ya watoto wanaolelewa katika vituo hivyo, Abdul Issa alilishukuru Jeshi la Polisi kwa msaada huo, akieleza kuwa umewaletea faraja na matumaini, huku ukidhihirisha moyo wa kujitolea na kuwajali watoto wenye mahitaji maalumu.

    Alisema mchango huo una umuhimu mkubwa katika kuboresha mazingira ya malezi na kukidhi baadhi ya mahitaji muhimu ya kila siku ya watoto hao.

    Ziara hiyo ni sehemu ya shughuli za ushirikishwaji wa jamii zinazotekelezwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Kinondoni, zenye lengo la kuimarisha uhusiano kati ya Polisi na wananchi, pamoja na kuhamasisha jamii kushiriki katika kuwasaidia watoto na makundi mengine yenye mahitaji maalumu.

  • Na Mwandishi Wetu, Haydom, Manyara

    Madereva wa magari na pikipiki katika Mji Mdogo wa Haydom, Wilaya ya Mbulu mkoani Manyara, wamekumbushwa kuendelea kuzingatia sheria za usalama barabarani ili kupunguza ajali na kulinda maisha ya watumiaji wa barabara.

    Wito huo umetolewa na Koplo (CPL) Andrea Mbona wa Kikosi cha Usalama Barabarani Haydom, ambaye aliwataka madereva kuzingatia taratibu zote za usalama, ikiwemo kufunga mikanda wanapoendesha magari na kuzingatia alama mbalimbali za barabarani.

    Alisisitiza umuhimu wa kuwa makini wanapofika kwenye vivuko vya watembea kwa miguu na maeneo yanayovukwa na wanyama, akieleza kuwa kufuata sheria na tahadhari hizo kutasaidia kupunguza ajali za barabarani.

    Mmoja wa madereva, Emanuel Evarist, alisema anashukuru kwa elimu hiyo ya usalama barabarani, akieleza kuwa wakati mwingine madereva huendesha kwa mazoea na kusahau kuzingatia sheria.

    Alisema elimu hiyo ni muhimu kwa kuwa inawakumbusha madereva wajibu wao wa kuendesha kwa kuzingatia sheria na kuongeza kuwa inapaswa kutolewa mara kwa mara ili kuendelea kujenga uelewa na nidhamu barabarani.

    Naye dereva, Israel Mohe, amelipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kutoa elimu kwa madereva na watumiaji wengine wa barabara.

    “Kwa kweli, mimi kama dereva ninalipongeza Jeshi la Polisi kwa namna linavyoendelea kutoa elimu ya usalama barabarani. Kwa kipindi hiki, jeshi limejikita zaidi katika utoaji wa elimu kuliko ilivyokuwa hapo awali,” alisema Mohe.

    Alisema utoaji wa elimu una mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa madereva na watumiaji wengine wa barabara, hatua inayosaidia kuimarisha usalama na kupunguza ajali.

  • Na George Gabriel

    Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Christopher Edward Magala, amefungua rasmi mafunzo ya awali ya Jeshi la Akiba kwa mwaka 2026 yanayofanyika katika Kata ya Likokona, yakilenga kuwajengea washiriki uzalendo, nidhamu na ujuzi wa msingi wa ulinzi na usalama wa Taifa.

    Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo uliofanyika Julai 13, 2026, katika viwanja vya Shule ya Msingi Likokona B, Magala alisema Jeshi la Akiba lina nafasi muhimu katika kuimarisha usalama wa nchi na kujenga uzalendo miongoni mwa wananchi. Aliwataka washiriki kuyatumia vyema mafunzo hayo na kuwa tayari kulitumikia Taifa watakapohitajika.

    Jumla ya washiriki 82 wamejiunga na mafunzo hayo, wakiwemo wanaume 73 na wanawake 9. Washiriki hao wanatarajiwa kupata mafunzo ya msingi ya kinadharia na vitendo yatakayowawezesha kutekeleza majukumu ya Jeshi la Akiba kwa ufanisi.

    Mmoja wa washiriki, Said Mtailika, alisema ameridhishwa na uamuzi wa Serikali kuendelea kutoa mafunzo ya Jeshi la Akiba kwa wananchi, akieleza kuwa yatamjengea uwezo wa kujitambua, kuimarisha nidhamu na kuongeza uzalendo.

    Aliwahimiza vijana wengine kutumia fursa hiyo badala ya kuipuuzia, akisema mafunzo hayo yana manufaa makubwa kwa maendeleo yao binafsi na kwa Taifa kwa ujumla.

    Naye mzazi Kalanje Abdarah aliwashukuru viongozi wa Serikali kwa kuanzisha mafunzo hayo wilayani Nanyumbu, akisema yatasaidia kuwajenga vijana katika maadili mema, nidhamu na kuwajibika kwa jamii.

    Aidha, aliwasihi washiriki wote kutokukata tamaa au kukimbia mafunzo kutokana na changamoto zinazoweza kujitokeza, bali wavumilie hadi watakapohitimu, kwani maarifa na stadi watakazopata yatakuwa msingi muhimu katika maisha yao ya baadaye.

    Mafunzo hayo yanatarajiwa kuendelea kwa kipindi kilichopangwa, huku washiriki wakipatiwa mafunzo mbalimbali ya kinadharia na vitendo yatakayowawezesha kutekeleza majukumu ya Jeshi la Akiba kwa weledi, nidhamu na uzalendo.

  • Na  Jastini Bukebuke

    Madereva wa bodaboda na bajaji za mizigo katika Mtaa wa Shinyanga A, Kata ya Nyakafulu, Wilaya ya Mbogwe mkoani Geita, wamepatiwa elimu kuhusu umuhimu wa ulinzi shirikishi na malezi bora ya watoto, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha usalama na ustawi wa jamii.

    Akitoa elimu hiyo juzi, Staff Sajenti (SSGT) wa Jeshi la Polisi, Mohamed Bujiku, aliwataka madereva hao kuacha tabia ya kufumbia macho vitendo vya uhalifu, akieleza kuwa baadhi ya wahalifu hutegemea ushirikiano wa madereva kusafirisha watuhumiwa, mali za wizi au mizigo inayohusishwa na vitendo vya kihalifu.

    Alisisitiza kuwa ushiriki wa madereva katika kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kuhusu watu au matukio yanayotiliwa shaka ni hatua muhimu ya kuzuia uhalifu na kulinda amani, usalama wa wananchi pamoja na mali zao.

    Aidha, aliwahimiza kushiriki kikamilifu katika shughuli za ulinzi shirikishi, akieleza kuwa mfumo huo ni nguzo muhimu ya kudumisha usalama, kuimarisha ushirikiano kati ya wananchi na Jeshi la Polisi, na kujenga jamii yenye amani, mshikamano na uwajibikaji.

    Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kijiwe hicho, Amon Kidenya, aliwataka madereva hao kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za usafirishaji barabarani ili kuepuka ajali.

    Pia alisisitiza kuwa malezi bora ya watoto ni jukumu la kila mwanajamii, akieleza kuwa ushirikiano wa wananchi katika kuhakikisha watoto wanalelewa katika maadili mema unachangia kwa kiasi kikubwa kupunguza vitendo vya uhalifu na kujenga kizazi chenye nidhamu, uzalendo na uwajibikaji.