Polisi Kata wa Ihanamilo, INSP Yosepha Michael, Julai 20, 2026, alitoa elimu kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Nyakahengele, Wilaya ya Geita, Mkoa wa Geita, akiwahimiza kuwa wazalendo, wenye nidhamu na bidii katika masomo ili kujijengea msingi imara wa maisha yao ya baadaye.
Akizungumza wakati wa elimu hiyo, INSP Michael alisema elimu ni nguzo muhimu ya maendeleo ya mtu binafsi na taifa, hivyo aliwataka wanafunzi kuipenda shule, kuwaheshimu walimu na wazazi, pamoja na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuhatarisha masomo na mustakabali wao.
Aidha, aliwakumbusha kuzingatia tahadhari za kiusalama kwa kujilinda dhidi ya vitendo vya kihalifu. Aliwashauri kutembea kwa makundi wanapokwenda na wanaporudi kutoka shuleni, kuepuka kuzungumza na watu wasiowafahamu, pamoja na kutoa taarifa kwa walimu, wazazi au Jeshi la Polisi wanapobaini viashiria vya uhalifu au mazingira yasiyo salama.
Kwa upande wao, wanafunzi wa Shule ya Msingi Nyakahengele walilishukuru Jeshi la Polisi kwa elimu hiyo, wakisema imewaongezea uelewa kuhusu umuhimu wa elimu, uzalendo na mbinu za kujilinda dhidi ya vitendo vya kihalifu.
Pia waliahidi kuendelea kushirikiana, kuishi kwa upendo, kuzingatia maadili mema na kufuata ushauri walioupata ili kuendelea kuwa salama wawapo shuleni na wanaporejea nyumbani.
Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu imeendelea kuimarisha utendaji wa watumishi wa umma kwa kuendesha vikao kazi maalum vinavyolenga kuongeza uelewa kuhusu maadili ya utumishi, uwajibikaji na utoaji wa huduma bora kwa wananchi.
Vikao hivyo vilivyoratibiwa na Idara ya Utumishi na Utawala vilifanyika kuanzia Julai 14 hadi 17, 2026 katika Tarafa za Maratani, Nanyumbu, Nakopi na Mangaka.
Lengo la vikao hivyo lilikuwa kuwajengea watumishi uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo ya Serikali, sambamba na kutoa fursa ya kusikiliza changamoto, maoni na mapendekezo yao ili kuboresha mazingira ya kazi na utoaji wa huduma.
Akizungumza wakati wa vikao hivyo, Afisa Tawala wa Wilaya ya Nanyumbu, Mebu Kalembo, aliwataka watumishi kuwa waadilifu, wawajibikaji na wenye nidhamu katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Alisisitiza kuwa utendaji unaozingatia maadili ya utumishi wa umma ni msingi wa kuongeza ufanisi na kujenga imani ya wananchi kwa Serikali.
“Kila mtumishi anatakiwa kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora kwa wakati,” alisema Kalembo.
Katika mafunzo hayo, washiriki walipatiwa elimu kuhusu maadili ya utumishi wa umma, haki na wajibu wa mtumishi, mamlaka za kinidhamu, itifaki na ustaarabu mahali pa kazi, mawasiliano serikalini pamoja na matumizi ya Mfumo wa Kielektroni wa Kupokea Malalamiko, Ushauri na Pongezi (e-Mrejesho).
Kwa upande wake, Afisa Utumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Maulid Chidoli, aliwasilisha mada kuhusu Mfumo wa Kielektroni wa Tathmini ya Utendaji wa Watumishi wa Umma (PEPMIS), akieleza kuwa mfumo huo unasaidia kupima utendaji wa watumishi kwa uwazi, kuongeza uwajibikaji na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Aidha, aliwakumbusha watumishi kutumia mfumo huo ipasavyo kwa kuzingatia malengo ya kazi, huku akiwahimiza kutumia fursa mbalimbali zinazotolewa na Serikali, ikiwemo mikopo inayoratibiwa kupitia Hazina, kwa kufuata taratibu zilizowekwa.
Washiriki wa vikao hivyo walieleza kuwa mafunzo hayo yamewaongezea uelewa kuhusu wajibu wao, matumizi sahihi ya mifumo ya Serikali na mbinu za kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Hatua hiyo inaakisi dhamira ya Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu ya kuendelea kujenga utumishi wenye maadili, uwajibikaji na ufanisi, sambamba na kutekeleza azma ya Serikali ya kuboresha huduma za umma kwa manufaa ya wananchi wote.
Mkaguzi wa Polisi wa Kata ya Kijitonyama, INSP Kavula Mizeye, ametoa mafunzo kuhusu maadili, malezi bora na kupinga ukatili wa kijinsia kwa vijana na watoto 39 waliokusanyika katika Uwanja wa Mpira wa Vinyago, uliopo Mtaa wa Nzasa.
Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, INSP Mizeye alisema lengo ni kuwajenga vijana katika misingi bora ya maadili na malezi, huku akiwahimiza kujiepusha na matumizi ya dawa za kulevya, vitendo vya ukatili wa kijinsia, ikiwemo ubakaji, pamoja na kuachana na makundi ya kihalifu yanayoweza kuhatarisha usalama wao na wa jamii.
Aidha, aliwataka vijana hao kuwa mabalozi wa amani na usalama kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kupitia utoaji wa taarifa za siri na za kiintelijensia kuhusu viashiria au uwepo wa wahalifu katika maeneo yao, ili kusaidia kuzuia na kupambana na uhalifu.
Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo, Bw. Gervaz Nabyasinu alilishukuru Jeshi la Polisi kwa kuwapatia elimu hiyo, akisema imewajengea uelewa kuhusu wajibu wao katika kudumisha amani na usalama.
Alihaidi kuwa vijana hao watashirikiana kwa karibu na Jeshi la Polisi katika kufichua na kupambana na vitendo vya kihalifu vinavyoweza kujitokeza katika jamii.
Marekebisho ya Sheria ya Mwenendo wa Madai (Civil Procedure Code), yaliyofanyika mwaka 2023, yameendelea kuzua mjadala mpana miongoni mwa mawakili, wasomi wa sheria na wadau wa mfumo wa haki nchini.
Miongoni mwa marekebisho yanayobishaniwa zaidi ni kifungu cha 13, kinachowataka wahusika wa mgogoro wa madai kutafuta suluhu kupitia upatanisho kabla ya kufungua shauri mahakamani.
Lengo la kifungu hiki ni kuhamasisha utatuzi wa migogoro kwa njia mbadala (Alternative Dispute Resolution – ADR), ili kupunguza mzigo wa mashauri mahakamani na kuwapa wahusika nafasi ya kumaliza migogoro yao kwa maelewano. Hata hivyo, utekelezaji wake umeibua changamoto mbalimbali zinazohusiana na upatikanaji wa haki kwa wakati.
Katika mahojiano na mawakili na wataalamu mbalimbali wa sheria, wengi wameeleza kuwa, ingawa dhamira ya kifungu hicho ni njema, hakikuandaliwa sambamba na utaratibu rasmi wa utekelezaji wake. Kwa sasa hakuna mfumo maalumu unaowaongoza wahusika namna ya kufanya upatanisho, nani atasimamia mchakato huo, wala namna ya kuthibitisha kuwa juhudi za usuluhishi zilifanyika na zikashindikana.
Kwa mtazamo wao, hali hiyo imeifanya sheria hiyo kuwa ngumu kutekelezeka, hasa kwa watu ambao tayari wamefikia hatua ya kushindikana kabisa kuelewana.
Wanasema ni vigumu kuwatarajia mahasimu ambao hata kuzungumza au kusalimiana ni changamoto, wakae tena mezani kutafuta suluhu bila uwepo wa chombo rasmi cha kuwaongoza.
Athari za kifungu hicho tayari zimeanza kuonekana mahakamani ambapo baadhi ya mashauri yamekuwa yakitupiliwa mbali kwa sababu wahusika hawakufuata masharti ya kifungu cha 13 kabla ya kufungua kesi.
Miongoni mwa maamuzi yanayonukuliwa mara kwa mara ni ya Jaji Beda katika shauri la A. Z. Bade Kilamala Alipinde na Mwenzake dhidi ya Saed Yeslam Saed, Kesi Na. 000032909 ya mwaka 2024.
Katika uamuzi huo, mahakama ilisisitiza kuwa shauri lolote ambalo halijafuata utaratibu uliowekwa na kifungu cha 13 haliwezi kusikilizwa na linapaswa kutupiliwa mbali kwa kuvunja matakwa ya sheria.
Kwa mujibu wa wadau wa sheria, maamuzi ya aina hiyo yamewaongezea wananchi gharama zisizo za lazima.
Mbali na ada ya kufungua kesi katika Mahakama Kuu, ambayo inaweza kufikia au kuzidi shilingi 150,000 kutegemeana na aina ya shauri, mlalamikaji hulazimika pia kugharamia wakili, maandalizi ya nyaraka na gharama nyingine za uendeshaji wa shauri. Kesi inapofutwa kwa sababu ya kutokufuata utaratibu huo, gharama hizo hupotea bila shauri kusikilizwa.
Hata hivyo, si majaji wote wamekuwa na mtazamo unaofanana kuhusu tafsiri ya kifungu hicho.
Katika shauri la Imalaseko Investment v Amer Mohamed Mbarak Company Limited & Another (Land Case No. 29281 of 2024), Jaji wa Mahakama Kuu, Mheshimiwa Hemed, alitoa mtazamo tofauti. Katika uamuzi wake alieleza kuwa kifungu cha 13 hakijaweka utaratibu mahsusi wa namna wadaawa wanavyopaswa kukutana kwa ajili ya usuluhishi kabla ya kufika mahakamani.
Alisisitiza kuwa sheria haijaeleza ni taasisi gani itasimamia mchakato huo wala mahali ambapo wahusika wanapaswa kwenda ikiwa upatanisho unahitajika.
Kwa msingi huo, aliona kuwa mahakama ina wajibu wa kuhakikisha haki inapatikana na si kuzuia wananchi kuifikia kutokana na mapungufu yaliyopo katika utekelezaji wa sheria. Alisisitiza pia kuwa moja ya majukumu ya msingi ya mahakama ni kutatua migogoro katika jamii, hivyo tafsiri ya sheria inapaswa kuzingatia haki badala ya kuangalia taratibu pekee.
Wananchi mbalimbali niliowahoji, ambao hawakutaka majina yao yachapishwe, nao wameeleza wasiwasi wao kuhusu kifungu hicho. Wamesema kingekuwa na manufaa zaidi kama Serikali ingeweka mfumo rasmi wa usuluhishi unaofanana na mifumo iliyopo katika maeneo mengine ya sheria.
Kwa mfano, katika migogoro inayosikilizwa na mabaraza ya kata, mlalamikaji hulazimika kwanza kupitia hatua ya upatanisho na hupewa cheti cha usuluhishi kabla ya kuendelea na hatua zinazofuata.
Vivyo hivyo, katika mashauri ya ndoa, wahusika hulazimika kupitia mabaraza ya usuluhishi wa ndoa kabla ya kufungua shauri la talaka mahakamani.
Kwa maoni ya wananchi hao, mfumo kama huo ungewekwa pia katika mashauri ya madai ili kila mlalamikaji apate cheti kinachoonyesha kuwa juhudi za usuluhishi zilifanyika na hazikufanikiwa. Hatua hiyo ingeondoa sintofahamu iliyopo sasa na kupunguza uwezekano wa mashauri kutupiliwa mbali kwa sababu za kiutaratibu.
Kwa ujumla, mjadala kuhusu kifungu cha 13 unaonyesha mvutano kati ya dhamira ya kuhimiza utatuzi wa migogoro nje ya mahakama na haki ya kila mwananchi kupata fursa ya kusikilizwa mahakamani bila vikwazo visivyo na utaratibu wa wazi.
Wadau wengi wanaamini kuwa ili kifungu hicho kifikie malengo yaliyokusudiwa, ni muhimu Serikali iweke mfumo wa kitaasisi wa usuluhishi wenye taratibu, mamlaka na uthibitisho rasmi. Bila kufanya hivyo, kuna hatari ya kifungu hicho kuendelea kutafsiriwa kwa namna tofauti na mahakama mbalimbali, jambo linaloweza kuathiri usawa wa haki na kuongeza gharama kwa wananchi.
Serikali imewataka wataalamu wa tiba asili na tiba mbadala nchini kuendelea kutoa huduma kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo iliyowekwa ili kuhakikisha usalama wa wananchi na kuongeza uaminifu wa huduma hizo katika jamii.
Wito huo umetolewa hivi karibuni na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Ibrahim Mwanauta, wakati akifungua Mkutano wa Mwaka wa Wataalamu wa Tiba Asili na Tiba Mbadala uliofanyika katika Ukumbi wa Halmashauri hiyo.
Mwanauta alisema Serikali inatambua mchango mkubwa wa wataalamu wa tiba asili katika kuboresha huduma za afya, lakini akasisitiza kuwa huduma hizo zinapaswa kutolewa kwa kuzingatia sheria, maadili na weledi wa taaluma hiyo.
“Tiba asili ni sehemu muhimu ya huduma za afya, lakini ni lazima itolewe kwa kuzingatia sheria, maadili na weledi ili kulinda afya za wananchi,” alisema Mwanauta.
Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu, Dkt. Marco Mazanzagar, aliwataka wataalamu wote kuhakikisha wanajisajili na kupata leseni kutoka Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala kabla ya kuanza kutoa huduma.
Alionya kuwa utoaji wa huduma bila leseni ni kinyume cha sheria na unaweza kuhatarisha afya za wananchi.
Naye Mratibu wa Tiba Asili na Tiba Mbadala Mkoa wa Mtwara, Deogratius Kikota, aliwahamasisha wataalamu kushiriki maadhimisho ya kilele cha Tiba Asili na Tiba Mbadala ngazi ya Mkoa wa Mtwara yatakayofanyika katika Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba mwezi Agosti 2026.
Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Wataalamu wa Tiba Asili Tanzania (BAWATA), Halidi Mohamed Mdoe, aliipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu kwa ushirikiano wake na wataalamu wa tiba asili, akiahidi kuwa chama hicho kitaendelea kuwapatia wanachama wake ushauri, mafunzo na msaada wa kitaalamu ili kuboresha utoaji wa huduma.
Akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mkutano huo, mtaalamu wa tiba asili Juma Hamisi alisema mafunzo na maelekezo yaliyotolewa yamewaongezea uelewa kuhusu wajibu wa kuzingatia sheria na taratibu za utoaji wa huduma.
“Mkutano huu umetukumbusha wajibu wetu wa kufanya kazi kwa weledi na kufuata sheria. Tutayafanyia kazi maelekezo yote tuliyopewa kwa manufaa ya wananchi,” alisema Hamisi.
Mkutano huo uliwakutanisha wataalamu wa tiba asili na tiba mbadala kutoka maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Nanyumbu kwa lengo la kujadili maendeleo ya sekta hiyo, kuimarisha ushirikiano na Serikali pamoja na kuboresha huduma zinazotolewa kwa jamii.
Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Ludete wamepatiwa elimu kuhusu majukumu ya Dawati la Jinsia na Watoto jana walipotembelea Kituo cha Polisi Katoro kilichopo Mji Mdogo wa Katoro, Wilaya ya Geita kwa lengo la kujifunza shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Jeshi la Polisi.
Akizungumza na wanafunzi hao, Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Geita, SP Severia Nauyo, alisema ziara hiyo imelenga kuwajengea wanafunzi uelewa kuhusu namna Polisi Jamii inavyotekeleza majukumu yake ya kutoa elimu kwa wananchi, kuimarisha ushirikiano kati ya Jeshi la Polisi na jamii, pamoja na kushirikisha makundi mbalimbali katika kuzuia uhalifu na kuimarisha usalama.
SP Nauyo aliwapongeza wanafunzi hao wa Kidato cha Nne kwa kuonyesha uthubutu na utayari wa kujifunza kuhusu majukumu ya Jeshi la Polisi, hususan namna Dawati la Jinsia na Watoto linavyopokea na kushughulikia malalamiko na migogoro ya kijamii kwa kuzingatia sheria, taratibu na haki za wahusika.
Aidha, aliwahimiza wanafunzi hao kuwa mabalozi wa amani kwa kutoa taarifa kwa walimu, wazazi, walezi na Jeshi la Polisi pindi wanapoona viashiria vya uhalifu, ukatili wa kijinsia, unyanyasaji wa watoto au vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama na amani katika jamii.
Kwa upande wao, wanafunzi wa Shule ya Sekondari Ludete walilishukuru Jeshi la Polisi kwa kuwapatia elimu hiyo muhimu, wakieleza kuwa imewaongezea uelewa kuhusu majukumu ya Dawati la Jinsia na Watoto pamoja na umuhimu wa kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kudumisha amani, usalama na utulivu.
Pia walilipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kutoa huduma kwa wananchi kwa weledi, haki na bila ubaguzi, jambo ambalo limeendelea kuimarisha imani ya jamii kwa Jeshi hilo.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limeendelea kuimarisha usalama barabarani kwa kutoa elimu kwa madereva wa magari madogo na makubwa wanaofanya kazi katika kampuni za GGML na Capital Drilling.
Elimu hiyo ilitolewa katika eneo la Shift Change Site, Kata ya Nyalwanzaja, Tarafa ya Busanda, Wilaya ya Geita, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kupunguza ajali na kuongeza uelewa wa madereva kuhusu umuhimu wa kuzingatia sheria za usalama barabarani.
Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mkaguzi wa Polisi, INSP Gabriel Rwehimbiza, aliwataka madereva kuhakikisha wanamiliki leseni halali za udereva na kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za uendeshaji wa magari ndani ya mgodi ili kuzuia ajali na kulinda maisha yao pamoja na ya watumiaji wengine wa barabara.
Alisema madereva wanapaswa kuwa mabalozi wa usalama kwa kuwaelimisha wenzao kuhusu umuhimu wa kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani.
Aidha, alionya kuwa hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya madereva watakaobainika kukiuka sheria, ikiwemo kufungiwa leseni za udereva kwa mujibu wa vifungu vya 33 na 34 vya Sheria ya Usalama Barabarani, Sura ya 168, Marejeo ya mwaka 2023.
Kwa upande wake, Mkufunzi wa IHET, Steven Reuben, amelipongeza Jeshi la Polisi kwa kuendelea kutoa elimu inayochangia kuongeza uelewa wa madereva kuhusu usalama na nidhamu ya uendeshaji wa magari ndani ya mgodi.
Reuben aliwataka madereva kuhakikisha abiria wote wanaotumia magari wanafunga mikanda ya usalama, kuzingatia viwango vya mwendo vilivyowekwa na kudumisha umbali salama wanapokuwa karibu na magari makubwa ya mgodini ili kupunguza hatari ya ajali.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limeendelea kutoa wito kwa madereva wote kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani wakati wote, likisisitiza kuwa kufuata sheria ni msingi wa kulinda maisha, mali na kuhakikisha mazingira salama ya kazi na usafiri.
Kikosi cha Usalama Barabarani kwa kushirikiana na uongozi wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (UDART) kilifanya kikao kazi na madereva wa mabasi ya mwendokasi katika ukumbi wa Chuo cha Teknolojia cha Dar es salaam (DIT) ili , kujadili na kuweka mikakati ya kupunguza ajali zinazotokea katika mfumo wa usafiri wa mabasi yaendayo haraka.
Katika kikao hicho, ilielezwa kuwa kati ya asilimia 65 na 70 ya ajali zinazohusisha mabasi ya mwendokasi husababishwa na makosa ya kibinadamu, ikiwemo ulevi, uzembe na mwendo kasi usiozingatia sheria huku asilimia zilizobaki ni ajali kutokana na changamoto za miundombinu pamoja na hitilafu za kiufundi katika baadhi ya magari.
Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Kinondoni, SSP Adamson Mwangamilo, alisisema ni muhimu kufunga viashiria vya mwanga kwenye vizuizi barabarani ili kuongeza usalama, huku akiwahimiza wananchi kutumia daraja la juu la waenda kwa miguu eneo la Kimara Mwisho badala ya kuvuka barabara kiholela, hatua itakayosaidia kupunguza ajali na msongamano wa magari.
Kwa upande wake, Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Ilala (RTO), SSP Salum M. Morimori, alionya kuwa vitendo vya uzembe, ulevi wakati wa kuendesha, pamoja na kukaidi taa na alama za usalama barabarani havitavumiliwa.
Aliwataka madereva kuzingatia kanuni za udereva wa kujihami ili kupunguza ajali, hususan katika maeneo yenye msongamano mkubwa kama Kivukoni na Msimbazi.
Naye Mkurugenzi wa UDART, Pius Ng’ingo, aliahidi kushughulikia changamoto za kiufundi zinazohusu mabasi ya mwendokasi na kuimarisha usimamizi wa nidhamu kwa madereva na watumishi wote ili kuongeza usalama wa huduma zinazotolewa.
Akizungumza kwa niaba ya madereva, Nassoro Hoza aliahidi ushirikiano wa karibu na Jeshi la Polisi pamoja na uongozi wa UDART katika kutekeleza kaulimbiu ya “Utii wa Sheria Bila Shuruti”, akisema madereva watazingatia udereva wa kujihami ili kulinda maisha ya abiria, watumiaji wengine wa barabara na vyombo vya usafiri wanavyoviendesha.
Kikao hicho ni sehemu ya juhudi zinazoendelea za Jeshi la Polisi na UDART za kuimarisha usalama barabarani, kupunguza ajali na kuhakikisha huduma za usafiri wa mabasi ya mwendokasi zinaendelea kutolewa kwa usalama na ufanisi.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Kinondoni, kupitia Kitengo cha Ushirikishwaji wa Jamii, limetoa msaada wa mahitaji mbalimbali kwa vituo vya kulelea watoto wenye mahitaji maalumu vya New Life na Huruma Children Home, vilivyopo Wilaya ya Kinondoni, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ustawi wa watoto hao na kudumisha mahusiano mema kati ya Jeshi la Polisi na jamii.
Mkuu wa Kitengo cha Ushirikishwaji wa Jamii Mkoa wa Kinondoni, ACP Ally Shughuli Wendo, aliyemwakilisha Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, SACP Mtatiro Kitinkwi, aliongoza ziara hiyo akiwa ameambatana na maafisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali.
Katika ziara hiyo, Jeshi la Polisi lilikabidhi msaada uliojumuisha unga, mchele, sukari, mafuta ya kula, taulo za kike, pampasi na mahitaji mengine muhimu kwa ajili ya kusaidia malezi na ustawi wa watoto wanaolelewa katika vituo hivyo.
Akizungumza kwa niaba ya watoto wanaolelewa katika vituo hivyo, Abdul Issa alilishukuru Jeshi la Polisi kwa msaada huo, akieleza kuwa umewaletea faraja na matumaini, huku ukidhihirisha moyo wa kujitolea na kuwajali watoto wenye mahitaji maalumu.
Alisema mchango huo una umuhimu mkubwa katika kuboresha mazingira ya malezi na kukidhi baadhi ya mahitaji muhimu ya kila siku ya watoto hao.
Ziara hiyo ni sehemu ya shughuli za ushirikishwaji wa jamii zinazotekelezwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Kinondoni, zenye lengo la kuimarisha uhusiano kati ya Polisi na wananchi, pamoja na kuhamasisha jamii kushiriki katika kuwasaidia watoto na makundi mengine yenye mahitaji maalumu.