
Na Mwandishi Wetu
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amewataka Watanzania kuendelea kudumisha amani na kutopuuza viashiria vya uvunjifu wa amani, akisisitiza kuwa vinaweza kuchafua taswira ya taifa.
Dkt. Nchemba alitoa wito huo jana wakati wa ibada maalumu ya kilele cha harambee iliyofanyika Usharika wa Amani, mjini Singida, katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kati.
Alisema ulinzi wa taifa ni jukumu la kila Mtanzania, hivyo wananchi wanapaswa kuendelea kuhamasishana kulinda amani na kutoa taarifa mapema kuhusu viashiria vinavyoweza kuhatarisha usalama wa nchi.
“Sasa hivi hatupaswi kupuuzia viashiria vya uvunjifu wa amani hapa nchini. Hatutakiwi kuvipuuza kwa sababu vinaweza kulitia doa taifa letu,” alisema Dkt. Nchemba.
Harambee hiyo, ambayo ni ya nne kufanyika, ililenga kukusanya Sh. bilioni 1.4 kwa ajili ya kuboresha huduma za afya, elimu, utumishi na uinjilisti katika Dayosisi ya Kati. Jumla ya Sh. bilioni 1.331 zilipatikana kupitia michango ya fedha taslimu na ahadi.
Dkt. Nchemba alisema kiasi kilichobaki cha Sh. milioni 69 kitakamilishwa ndani ya wiki ijayo kupitia utekelezaji wa ahadi mbalimbali zilizotolewa pamoja na timu aliyoiunda kusimamia zoezi hilo.
Akihubiri katika ibada hiyo, Mkuu wa Kanisa la KKKT, Askofu Dkt. Alex Gehazi Malasusa, alisema harambee hiyo imewapa waumini nafasi ya kumshukuru Mungu kwa baraka na mafanikio aliyowajalia.

“Kila tunachokifanya kinapaswa kumtukuza Mungu. Mali na fedha zetu ziwe za halali na zisipatikane kwa kuwaonea au kuwakanyaga wengine,” alisema Askofu Malasusa.
Kwa upande wake, Askofu wa KKKT Dayosisi ya Kati, Dkt. Cyprian Hilinti, alisema kanisa linaendelea kuwaombea viongozi wa nchi kila Jumapili pamoja na kuombea amani na maridhiano kati ya makundi mbalimbali ya jamii, ikiwemo makabila, wakulima na wafugaji, pamoja na vyama vya siasa.
“Tunatamani kuona msamaha ukitawala katika nyanja mbalimbali za maisha. Msamaha ni dawa,” alisema Dkt. Hilinti.
Aliongeza kuwa tangu kuanzishwa kwa harambee hiyo miaka minne iliyopita, Dayosisi imeanzisha majimbo manane mapya, sharika 27, imepokea waumini wapya 17,364 na kupata wachungaji wapya 65.
Akizungumzia huduma za jamii, alisema Dayosisi pia imefanikiwa kusajili shule mbili mpya za sekondari na shule moja ya msingi inayotoa elimu kwa lugha ya Kiingereza, huku akiwashukuru waumini wote kwa kujitolea na kuchangia maendeleo ya kanisa na jamii.
























