
Na Mwandishi Wetu, Songea
Jeshi la Polisi kupitia Kitengo cha Usalama Barabarani Mkoa wa Ruvuma limeendelea kutoa elimu ya usalama barabarani kwa wanafunzi wa Shule ya Awali na Msingi ya Good Shepherd Montessori iliyopo Mjimwema, Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma.
Elimu hiyo ilitolewa na watendaji wa Dawati la Elimu kutoka Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Ruvuma ikiwa ni sehemu ya juhudi za Jeshi la Polisi za kujenga uelewa kwa jamii, hususan watoto, kuhusu matumizi sahihi na salama ya barabara.
Akizungumza wakati wa utoaji wa elimu hiyo, Mkaguzi wa Polisi (Insp.) Nelson Mwambashi aliwataka wanafunzi kuzingatia kanuni za matumizi salama ya barabara wanapokuwa barabarani ili kujiepusha na ajali.
Alisema wanafunzi wanapaswa kujenga utamaduni wa kutembea pembeni mwa barabara na kutumia vivuko maalum pamoja na taa za barabarani wakati wa kuvuka.
Naye Mkaguzi wa Polisi (Insp.) Bahati Festo aliwakumbusha wanafunzi namna sahihi ya kutembea barabarani, kuvuka kwa usalama pamoja na kutambua alama muhimu za usalama barabarani zinazowaongoza watembea kwa miguu.
Kwa upande wake, Koplo Samwel Saguli aliwataka wanafunzi kuwa mabalozi wa elimu hiyo kwa wenzao na jamii zinazowazunguka kwa kuelekeza matumizi sahihi ya alama za barabarani na kuonya dhidi ya kucheza barabarani.
Alisema tabia ya kucheza barabarani inaweza kusababisha ajali zisizo za lazima zinazopelekea majeraha, ulemavu au hata vifo.
Naye Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Joshua Sonsoge, alilishukuru Jeshi la Polisi Mkoa wa Ruvuma kwa kuendelea kutoa elimu ya kinga kwa wanafunzi, akisema hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa na nidhamu ya matumizi ya barabara kwa watoto wakiwa shuleni na hata wanapokuwa nyumbani.



















