
Na Mwandishi Wetu
Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, watumishi wanawake wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) wametoa msaada wa vitu, mahitaji na vifaa mballimbali kwa watoto wa Kituo cha kulea watoto yatima na waliofanyiwa ukatili cha Shalom kilichopo Kidenge B, Kata ya Msangani, Halmashauri ya Mji wa Kibaha, mkoani Pwani.
Msaada huo unajumuisha mifuko 50 ya saruji, matofali 1,000 pamoja na mahitaji mbalimbali.

Akizungumza hivi karibuni wakati wa kukabidhi msaada huo, Meneja wa Udhibiti na Viwango wa Mamlaka hiyo Bi. Sultana Seiff, alisema wanawake wa e-GA wameamua kusherehekea siku hiyo na watoto wahitaji katika jamii na kukichagua kituo hicho ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii.
Bi. Seiff alisema baada ya kuwasiliana na kituo hicho na kupata changamoto mbalimbali zinazohitaji utatuzi ikiwemo ujenzi wa uzio ili kuhakikisha usalama wa watoto katika kituo hicho waliamua kuchangia vifaa vya ujenzi pamoja na mahitaji mengine muhimu kwa watoto.
“Napenda kuwasilisha salamu kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa e-GA ambaye ametuwezesha wanawake wa mamlaka hii kufika hapa Kibaha”, alisema Bi. Seiff.
Alisema mbali na vifaa vya ujenzi wametoa mahitaji mengine muhimu ikiwemo chupi za kuzuia mkojo kwa watoto yaani pampers, maziwa ya watoto wachanga, sukari na mahitaji mengine ya msingi kwa watoto wa kituo hicho.
Kwa upande wake, mbeba maono wa kituo hicho, Bi. Lilian Mbise, aliwashukuru wanawake wa Serikali Mtandao kwa kujitoa kwao kufika na kuwaona watoto hao pamoja na na msaada huo.
Alisema kwa niaba ya kituo anaishukuru sana Mamlaka ya Serikali Mtandao kupitia wanawake ambao wameacha shughuli zao na familia zao na kwenda kuwaunga mkono.
“Msaada huu wa saruji na tofali utasaidia sana katika ujenzi wa uzio,” alisema Bi. Mbise.
Akielezea historia ya kituo hicho alisema kilianzishwa Mei Mosi mwaka 2016, kikiwa na watoto wawili, lakini sasa kinahudumia watoto 66 wa kike na wa kiume, yatima na waliofanyiwa ukatili wa aina mbalimbali ambao hufikishwa kituoni hapo kupitia taratibu za kiserikali.


















