
Na Cosmas Msuha
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, TAKUKURU Mkoani Rukwa imefanikiwa kudhibiti vitendo vya rushwa katika miradi ya maendeleo yenye thamani ya shilingi bilioni 1.7 kwa kipindi cha Oktoba hadi Disemba mwaka 2025.
Mkuu waTAKUKURU Mkoa wa Rukwa, Mzalendo Widege aliyasema hayo katika taarifa yake kwa umma ambapo inaonesha kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2026, TAKUKURU Mkoani humo imepanga kufuatilia matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo pamoja na mali za watuhumiwa ili kufidia hasara zinazotokana na vitendo vya rushwa.
Alisema katika kuboresha utekelezaji wa miradi, TAKUKURU ilitoa mapendekezo kadhaa ikiwemo matumizi ya wahandisi waliosajiliwa, matumizi ya vifaa vya kujikinga kwa mafundi, kutangaza zabuni mapema kupitia mfumo wa NeST pamoja na kuimarisha vikao katika eneo la mradi na utunzaji wa nyaraka.
Katika hatua nyingine, alisema TAKUKURU ilifanikiwa kumrejesha mkandarasi aliyekuwa ameacha ujenzi wa bweni na madarasa katika Shule ya Sekondari Mzindakaya.
“Mradi huo wenye thamani ya shilingi milioni 380 ulisimama kwa miezi miwili kuanzia Oktoba hadi Novemba 2025 kutokana na mkandarasi huyo kuwa na zabuni nyingi, alisema Widege.
Sanjali na hayo alitoa taarifa ya kuhusu uchambuzi wa mifumo ambapo taasisi hiyo imefanya tathmini ya ukusanyaji mapato katika Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo na usimamizi wa Jumuiya za Maji ngazi ya Jamii katika Wilaya ya Sumbawanga, ambapo mapendekezo yametolewa na ufuatiliaji unaendelea.
Katika taarifa yake alibainisha jumla ya malalamiko 64 yalipokelewa katika kipindi hicho ambapo kati ya hayo, malalamiko 35 sawa na asilimia 55 yalihusu rushwa, huku 29 sawa na asilimia 45 hayakuhusu rushwa.
“Malalamiko yasiyohusu rushwa yalifungwa baada ya ushauri, wakati yale yanayohusu rushwa uchunguzi unaendelea”, alisema Widege.
Akizungumzia suala la elimu kwa umma, TAKUKURU imeendesha semina 19, mikutano ya hadhara 15, maonesho matano, kuimarisha klabu 10 za wapinga rushwa na kufungua klabu moja mpya na kudai kuwa hatua hiyo imeongeza mwitikio wa wananchi kutoa taarifa za vitendo vya rushwa.
Widege aliwataka wananchi kuepuka vitendo vya rushwa na kuendelea kutoa taarifa kupitia simu ya bure 113 au namba ya Mkuu wa TAKUKURU Mkoa 0738150186.











