
Na Vincent Mpepo, Dodoma
Watumishi wa Idara ya Masomo ya Habari na Ukutubi chini ya Kitivo cha Sanaa na Sayansi za Jamii, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, wametakiwa kufanyia kazi changamoto mbalimbali za wanafunzi na masuala mengine kwa wakati.
Hayo yalisemwa na Mkuu wa Idara, Dkt. Henry Mambo, wakati akifunga kikao kazi cha idara hiyo cha siku nne kilichofanyika katika kituo cha Mkoa cha chuo hicho cha Dodoma.

Dkt. Mambo alisisitiza kuwa watumishi wa idara hiyo wanatakiwa kushughulikia majukumu yao ya msingi, ikiwemo kufundisha, kufanya tafiti na kazi nyingine zitazosaidia maendeleo ya idara, kitivo na chuo kwa ujumla.
Mhadhiri Mwandamizi Athumani Samzugi aliwataka watumishi wa Idara hiyo kushikamana na kusaidiana kitaaluma, akisisitiza umuhimu wa kufanya tafiti za pamoja kutokana na masomo yanayofanana katika idara.
Mratibu wa masomo ya Ukutubi katika Idara hiyo, Ntimi Kasumo, aliwakumbusha watumishi hao kuendana na mabadiliko ya kiutendaji, ikiwemo katika usahihishaji, uwekaji wa kumbukumbu za matokeo na uwasilishaji kwa wakati.
Aidha, aliwashauri wahadhiri wanaofundisha programu za uzamili kutoa alama kwa wakati ili kuendana na utendajikazi wa menejimenti ya chuo hicho.





















