• Na Vincent Mpepo, Dodoma

    Washarika wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) wametakiwa kuendelea kumtolea Mungu sadaka bila kukata tamaa huku wakiziombea ili zifanye kazi yake na pia wapate baraka kupitia sadaka hizo.

    Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa Ujenzi wa Madarasa ya Watoto na Ofisi za Usharika  wa Betheli Dayosisi ya Dodoma, Makao Makuu Lilian Uroki wakati akihamasisha utoaji wa sadaka hiyo katika ibada ya kwanza usharikani hapo Jumapili.

    Alisema washarika wenyeji na wageni wanapaswa kufanyia kazi suala hilo na kwamba hawapaswi kuiita michango bali ni sadaka.

    “Ni muhimu sana kuhakikisha kabla ya kutoa unaziombea ili Mungu afanye kitu kwa ajili yako”, alisema Lilian

    Mhubiri wa Siku hiyo, ambaye ni Katibu wa Usharika huo, Dkt.Denis Ringo aliwaasa wakristo kutokujisahau kwa kuwanyenyekea watumishi badala ya Mungu aliyewatuma na kwamba wanatumika ili kusudi la Mungu litimie.

    “Ni hatari kumwamini aliueagizwa badala ya aliyemuagiza”, alisema Dkt.Ringo

    Alisema kuna wakati wakristo hujisahau hususani wanapopata kitu iwe ni baraka ya kichumi, kupanda cheo au manufaa fulani badala ya kumtumikia Mungu hurudi nyuma kwa sababu mbalimbali ikwemo madai ya kukosa muda wa kufanya zake na matokeo yake huwa ni kusahaulika.

    “Ni mara ngapi tunatumika kwa Bwana kwa nafasi zetu, vyeo vetu au hali njema tulizonazo?” Aliuliza Dkt.Ringo

    Alisema Mungu hutumia watu au vitu vya kawaida au vinyonge ili kusudi lake litimie badala ya watu wenye mamlaka au umaarufu ambao wakati mwingine hutumia nafasi zao ili tu wapate sifa na kusahau kuwa Mungu ndiye aliyewapa nafasi hizo.

    Alisema mkristo anapoitwa kutumika na ikiwa atatumika sawasawa na kusudi la Mungu atainuliwa na kuheshimishwa.

    Alisema wakristo wanapopitia katika nyakati ngumu busara, hekima, unyenyekevu na upole vitaendelea kuwa ndiyo silaha nzuri na kwamba Mungu anajua kesho yao hivyo waendelee kumtegemea yeye na wasiondoke katika kusudi la Mungu.

    Mchungaji kiongozi wa Usharika huo, Gershon Ngewe aliwashukuru washarika kwa sadaka mbalimbali ambazo wanaendelea kuzitoa na kuwaombea kwa Mungu ili afanyike Baraka kupitia sadaka hizo.

  • Sehemu ya wadahiliwa wapya waliohudhuria mafunzo elekezi katika Kituo cha Chuo Kikuu Huria cha Mkoa wa Arusha Leo, (Picha na Amos Majaliwa).

    Na Vincent Mpepo, Dodoma

    Wanafunzi wapya wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania waliodahiliwa katika shahada ya awali ya Mawasiliano ya Umma wameelezea matarajio yao katika muda watakaokuwa masomoni na kuainisha sababu za kukichagua chuo hicho.

    Wakizungumza katika nyakati tofauti kupitia mahojiano ya kimtandao hawakusita kuelezea hisia zao.

    Upendo Sumary wa kituo cha chuo hicho Mkoa wa Ruvuma ambaye ni mdahiliwa wa shahada ya mawasiliano ya umma alisema aliamua kusoma katika chuo hicho kwa kuwa ni chuo cha umma kinachotambulika kitaifa na kimataifa na kwamba anaamini kupitia chuo hicho atafikia ndoto zake.

    “Nimependa kusoma OUT kwa kuwa ni chuo chenye sifa nzuri ya ufundishaji na ninaamini kufanikisha ndoto zangu”, alisema Upendo.

    Alisema anategemea kufanya vyema katika masomo yake kwani atajitahidi kufuatilia masomo kwa kadiri ya uwezo wake na atakuwa makini ili afanikishe malengo yake.

    Esther Nurben wa Dar es salaam ambaye ni mdahiliwa wa shahada ya kwanza ya Mawasiliano kwa umma alisema alifikia uamuzi wa kusoma Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kutokana na sifa za kuaminika kwa kutoa wahitimu mahiri kwenye kwenye fani mbalimbali siyo tasnia ya habari pekee.

    “Ni mategemeo yangu kuwa nitahitimu shahada yangu kwa muda muafaka bila ya changamoto zozote”, alisema Ester.

    Alisema sababu nyingine muhimu ambayo ilimvutia kusoma chuo hicho ni fursa ya kuendelea na masomo huku anafanya kazi na unafuu wa ada.

    Anjela Mhilu wa Kituo cha Mkoa cha Ilala alisema aliamua kusoma katika chuo hicho ili kujiongezea maarifa na ujuzi kwenye programu aliyoomba na ni katika harakati za kujiongeza na kutafuta zaidi.

    Kwa upande wake, Abishagi Mpoki alisema uwezekano wa kufanyia mitihani mahali popote atakapokuwa hata akiwa na majukumu ya kikazi nje ya kituo chake cha kazi ndiyo sababu iliyomvutia kusoma Chuo Kikuu Huria cha Tanzania.

    “Elimu bora na kuniwezesha kusoma huku nafanya kazi ni kitu kilichonifanya nikichague chuo hiki”, alisema Abishagi.

    Mwandishi amebaini kuwa taarifa za matangazo ya chuo hicho zinaufikia umma kupitia matangazo kwa njia za mitandao ya kijamii, wanafunzi wanaoendelea na masomo na kupitia wahitimu wa chuo hicho ambao ni wafanyakazi katika taasisi mbalimbali za umma na binafsi.

    Ni ukweli usiopingika kuwa chuo hicho kina deni na wajibu wa kutimiza ili kuendana na matarajio ya wadahiliwa hao kwa kuboresha huduma zake ikiwemo huduma ya mtanado ambayo ndiyo uti wa mgongo wa elimu masafa, uboreshaji wa mifumo ya Tehama na huduma kwa wateja.

  • Na Tabia Mchakama

    Ujumbe wa watu 12 kutoka Eswatini ukiongozwa na Naibu Spika wa Bunge la Nchi hiyo Madala Mhlanga umezuru ofisi ndogo za Makao Makuu ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) Dar es salaam kwa lengo la kupata uzoefu wa masuala mbambali ya kibima ikiwemo usimamizi wa soko na maswala ya kisheria.

    Akiongoza kikao hicho kwa niaba ya Kamishna wa Bima Tanzania, Mkurugenzi wa Usimamizi kutoka TIRA, Christopher Mapunda aliwapitisha wageni hao katika mada mbalimbali ikiwemo hali ya soko la bima nchini, usimamizi wa soko la bima, sheria zinazotumika kusimamia soko la bima, mamlaka ya kamishna kwenye kusimamia soko la bima na mifumo ya tehama.

    Aidha mjadala ulijikita kwenye kwenye vipaumbele mbalimbali vya mamlaka vikiwemo utekelezwaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote (UHI) na Uanzishwaji wa konsotia ya bima ya kilimo (TAIC).

    Awali Naibu Spika wa Nchi hiyo Madala alieleza kuwa wapo katika mchakato wa uboreshaji wa sheria ya nchini humo na hivyo wamechagua Tanzania ikiwa ni miongoni mwa nchi za Afrika zinazofanya vizuri katika masuala ya bima ili kujifunza.

     “Zaidi tunaishukuru TIRA kwa elimu na uzoefu mliotupatia na tunahaidi kuendeleza ushirikiano kwa siku zijazo”, alisema Naibu Spika Madala.

    Baadhi ya wageni hao ni viongozi katika bunge la nchi hiyo, wizara ya fedha na mamlaka ya masuala ya huduma za fedha zisizo za kibenki ambapo waliungana na wataalamu wengine kutoka TIRA ili kubadilishana na kupeana uzoefu wa namna ya usimamizi na udhibiti katika soko la bima kwa pande zote mbili.

  • Na Anamaria John

    Utendaji mzuri wa kazi hupimwa kwa matokeo yanayopatikana, na ili matokeo yaonekane lazima kuwepo na waangalizi, wasimamizi na wafuatiliaji wa utekelezaji kutokana na kile walichokiona kwa macho na sio kusikia na kuangalia katika makaratsi.

    Moja ya vipimo hivyo vinaweza kuonekana kupitia thamani ya fedha iliyo tumika kwa kulinganisha na uhalisia wa kazi yenyewe.

    Katika masuala ya ujenzi wa miradi ya maji na kufikisha huduma ya maji kwa wananchi, Rais wa awamu ya sita Dkt. Samia Suluhu Hassan akamtwika dhamana Waziri wa Maji Jumaa Aweso (Mb) ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Pangani, mkoani Tanga kuiongoza wizara hii inayogusa maisha ya wananachi moja kwa moja ili kuhakikisha azma ya serikali ya kufikisha huduma ya maji kwa wananchi waishio vijijini na mjini inatimia bila kikwazo.

    Katika kufanikisha hilo Wizara ya Maji inatumia taasisi zake ambazo ni Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira kwa maeneo ya mijini, Wakala wa Usambazaji Maji Vijijini (RUWASA), Mfuko wa Taifa wa Maji, Pamoja na Chuo cha Maji ili kufanikisha huduma ya upatikanaji wa maji kwa maeneo ya vijijini kufika asilimia 85 na mijini asilimia 95 ifikapo mwezi Disemba 2025.

    Matokeo mazuri katika Sekta ya Maji kumechagizwa na usimamizi mzuri unaoitofautisha sekta hiyo ilipotoka na inapoelekea kupitia Kamati ya Kudumu ya Maji na Mazingira inayoongozwa na nahodha wake Mwenyekiti Jackson Kiswaga (Mb) ambaye ndiye mwakilishi wa wakazi wa Kalenga katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kamati hiyo inaundwa na jumla ya wajumbe 21 kutoka Bungeni.

    Moja ya kazi kubwa ya kamati hii ni ukaguzi wa miradi ya maji ili kujionea utekelezaji wake katika maeneo mbalimbali nchini ikilinganisha na bajeti ya mwaka wafedha husika, kiasi kilichotengwa na kutumika, kushauri na kuweka msukumo katika masuala yanayohusu maji safi na usafi wa mazingira.

    Kwa kipindi hiki kamati imetembelea miradi ya maji katika mikoa ya Tabora, Kigoma na Katavi ili kujionea utekelezaji wa miradi hiyo.

    Katika mkoa wa Tabora pamoja na sifa ya kuzalisha asali kwa wingi kwa upande wa suala la maji mkoa upo vizuri. Miradi iliyotekelezwa na kutoa huduma ya maji kwa wananchi na ile inayoendelea na utekelezaji wake ikiwemo Bwawa la Uyui ambapo kamati ilipata fursa ya kufanya ukaguzi.

    Bwawa hilo linajengwa kwa fedha za ndani na kiasi cha zaidi ya Shilingi bilioni nne na lina uwezo wa kuhifadhi maji kwa mwaka lita za ujazo bilioni 5.1 na likinufaisha zaidi ya wananchi elfu 90 na hivi sasa utekelezaji wa ujenzi wa bwawa hilo umefika asilimia 60 na kukamilika kwa bwawa hili kutaongeza hali ya upatikani wa maji katika mkoa wa Tabora.

    Umbali wa kutoka sehemu moja kwenda nyingine katika kukagua utekelezaji wa miradi ya maji hilo halikuwa kikwazo kwa wajumbe wa Kamati ya Maji na Mazingira, na safari iliendelea hadi mwisho wa reli mkoani Kigoma. Safari hii ilikuwa mahususi kufika kukagua ujenzi wa mradi wa maji Munanila-Nyakimue Wilayani Buhigwe, mradi ambao utanufaisha vijiji nane.

    Hadi sasa, katika mradi huu kazi zilizofanyika ni pamoja na ununuzi na ulazaji wa bomba, ujenzi wa nyumba tatu za mitambo ya kusukuma maji na ujenzi wa vituo vya umma vinne vya kuchotea maji.

    Hadi sasa mradi umefikia asilimia 67 huku fedha zilizoleta mabadiliko hayo ni za ndani kiasi cha Shilingi bilioni 14.9 na jambo la kutia moyo ni kuwa hadi kufikia Oktoba 2025 mradi huu unatarajiwa kuwa umekamilika.

    Aidha, kutokana na Kamati ya Maji na Mazingira kuona jiografia ya mkoa wa Kigoma ilipendekeza umuhimu wa kutumia chanzo cha ziwa Tanganyika kuwa chanzo cha uhakika cha maji kwa mkoa huo na mikoa jirani ikiwamo Katavi.

    Hivyo, Wajumbe wa kamati hiyo katika kuhakikisha huduma ya maji inafika kwa wananchi walipita pori la Kigoma kwenda Katavi kwa umbali wa kilomita 249 bila kukata tamaa, kwa mvua au jua.

    Wajumbe wa kamati walipata wasaa wa kuona kazi inayofanyika eneo la ujenzi wa mabwawa ya kutibu majitaka katika manispaa ya Mpanda. Maji safi yanapotumika kiasi kikubwa kinachobaki ni majitaka, huo ndio ukweli. Hivyo miundombinu ya majitaka nayo ni muhimu.

    Wataalam wamasuala ya huduma ya maji wanasema kuwa asilimia 80 ya majisafi hubadilika na kuwa majitaka hivyo kutokuwepo kwa miundombinu ya uchakataji majitaka kutaleta athari za kimazingira ambazo ni hatari kwa binadamu na viumbe wengine.

    Uchafunzi wa mazingira kutokana na majitaka unaweza kuwa ni chanzo cha kuharibu mazigira wezeshi kwa viumbe hai ikiwemo binadamu. Inaweza kuwa ni chanzo cha magonwa ya mlipuko kama kipindipindu.

    Mabwawa yaliyokaguliwa yana uwezo wa kupokea lita za ujazo 600,000 kwa siku na kutokana na mchakato wake, taka hizo zinaweza kuzalisha mbolea itakayoweza kutumika katika shughuli za kilimo. Thamani ya mradi ni kiasi cha Shilingi bilioni 1.197

    Mradi wa majitaka katika manispaa ya Mpanda umejikita katika matumizi ya magari na lengo la serikali ni kujenga mtandao ya majitaka moja kwa moja kutoka katika makazi ya wananchi kuelekea kwenye mabwawa hayo.

    Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira imeridhishwa na miradi ya maji katika mikoa ya Katavi, Kigoma na Tabora imetoa pongezi kwa Waziri wa Maji, Jumaa Aweso (Mb) na wataalam wa Sekta ya Maji nchini kwa kazi ya kuwafikishia wananchi huduma ya maji safi na salama.

    Juhudi hizo zinakwenda sanjali na adhma ya serikali ya kuwafikishia wananchi huduma hiyo muhimu kufikia asilimia 85 vijijini na 95 mjini ikiambana na na kauli mbiu inayotambulika kama “Kumtua mama ndoo ya maji kichwani” inatimia.

    Msisitizo umetolewa kuhusu utekelezaji wa miradi ya maji nchini ni kujenga  utamaduni wa kulinda na kutunza miundombinu na vyanzo vya maji na kila mwananchi aone ana wajibu wa kufanya hivyo faida ya kizazi cha sasa na badae.

    Utamaduni wa kulinda na kuhifadhi vyanzo na miundombinu ya maji utasaidia kuepuka athari hasi za mabadiliko ya tabia nchi yatakayosababisha ukame na changamoto ya nyingine za kimazingira.  Ni wazi kuwa kila mmoja anakiri kuwa ‘maji ndio uhai wetu’ kwa kuangalia umuhimu wake katika maisha yetu na viumbe hai wengine.

  • Na Gabriel Msumeno, Pwani

    Watanzania wametakiwa kushiriki kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 ili kutimiza haki yao ya kikatiba ya kuwachagua viongozi watakaowaongoza kwa kipindi kingine cha miaka mitano ijayo.

    Wito huo umetolewa na Mkimbiza Mwenge Kitaifa, Ismail Ali Ussi akiwa katika Wilaya ya Bagamoyo Mkoani Pwani ambako anaendelea kukimbiza Mwenge wa Uhuru.

    “Kila mtanzania mwenye umri wa kuanzia miaka 18 anapaswa kushiriki uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025”, alisema Ussi.

    Mwenge wa Uhuru umezindua miradi 5 na kuweka jiwe la Msingi kwenye mradi mmoja na kufanya  jumla ya miradi iliyotembelewa katika Wilaya ya Kibaha ikiwa na thamani ya zaidi yaTsh Milioni 748.

    Kauli mbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2025 inasema “Jitokeze kushiriki uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 kwa amani na utulivu”.

  • Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa Ismail Ali Ussi akipanda mti kama ishara ya kutunza mazingira na uboreshaji wa nishati ya jua katika Hospital ya Mchukwi.

    Na Gabriel Msumeno, Pwani

    Mwenge wa uhuru umezindua miradi sita ya maendeleo katika sekta za elimu na afya Wilayani Kibiti Mkoani Pwani yenye thamani ya shilingi milioni 600.

    Akizindua miradi hiyo, Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa  Ismail Ali Ussi aliwataka wananchi kuitunza ili iwe na manufaa kwa kizazi cha sasa na cha vizazi vijavyo ili kuboresha maisha.

    Miradi iliyozinduliwa ni ya ujenzi wa matundu sita ya vyoo na vyumba vinne vya madarasa katika Shule ya  Msingi Kibiti.

    Miradi mingine ni pamoja na uzinduzi wa mashine mbili za kisasa za kubangulia korosho  katika chama cha vijana cha Kibiti Cashernuts, uzinduzi wa nishati safi ya kupikia katika Shule ya Sekondari Kibiti na mradi wa maji katika kata ya Bungu.

    Aidha, Kionbgozi wa Mbio za Mwenge Kitafia alishiriki upandaji mti ikiwa ni ishara ya kutunza mazingira na uboreshaji wa nishati ya jua katika Hospital ya Mchukwi.

  • Sehemu ya wanakwaya wa USCF Mlimani CCT wakihudumu katika ibada ya kwanza katika anisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Usharika wa Mbezi Luis siku ya Jumapili, (Picha Vincent Mpepo).

    Na Vincent Mpepo

    Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam wameushukuru uongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Mbezi Luis kwa kuwapokea na kuwahudumia vizuri walipokua usharikani hapo kwa kambi Maalumu ya siku tatu.

    Shukrani hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kwaya ya USCF Mlimani CCT, Joshua Richard wakati wa ibada ya kwanza mbele ya washarika alipokuwa akitoa salamu za shukrani na kwamba wamefarijika kwa namna wa uongozi wa kanisa na vikundi mbalimbali walivyowakarimu.

    Alisema wametembelea sehemu nyingi kwa kambi lakini Usharika wa Mbezi Luis ni moja ya Sharika zilizowapokea na kuwakarimu vizuri kwani wameonja upendo na kujaliwa muda wote walipokuwa usharikani hapo.

    Alisema madhumuni ya kambi hiyo Maalumu ni kwa ajili ya maombi na masuala mbalimbli ya kiimani kwa vijana na kwamba ni utaratibu waliojiwekea kila mwaka wanafanya hivyo ikiwa ni sehemu ya kukulia kiimani kwani kanisani ndio mahali salama zaidi.

    “Vijana kujihusisha na masuala ya Mungu tunanakuwa salama zaidi kwani itatuepusha na mambo mengi yasiyofaa ikiwemo madawa ya kulevya”, alisema Richard

    Alisema vijana wakiandaliwa vyema kiroho familia, jamii na taifa kwa ujumla limepona kwa kuwa watajitambua na kuwa wanajamii wanatabua wajibu wao.

    Kambi hii ya maombi ilikuwa na vijana wa kike na wa kiume 132 tangu Ijumaa mpaka Jumapili, alisema Richard

    Mwalimu Gadielson Mfinanga katika mahubiri siku hiyo aliwakumbusha wakristo kutoruhusu changamoto wanozaopitia kubadili uhalisia wa Mungu katika maisha yao kwani kufanya hivyo kutawagharimu baada ya hali hiyo kuisha.

    Alisema Mungu ana tabia ya kuwabakiza watu ambao hata baada ya changamoto mbalimbali zinazowakabili wataedelea kutembea nao katika nyakati za huzuni au furaha.

    “Ni muhimu sana kuwathamini wengine bila kuwahukumu au kuwadharau kwani huwezi kujua ni wakati gani watakufaa”, alisema Mwalimu Mfinanga.

    Alisema matokeo ya kila mmoja na alivyo ni mjumuisho wa namna wa watu aliokutana nao katika maisha yake.

    Mchungaji Kiongozi wa Usharika wa Mbezi Luis, Godlsiten Nkya aliwashukuru vijana wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kwamba wanafanya kazi njema machoni pa Mungu.

    Aidha, aliwakumbusha wazazi wa Dar es salaam kujiuliza ikiwa vijana wao wanaosoma vyuoni hususani Chuo Kikuu cha Dar es salaam kama wanajishughulisha na masuala ya kiimani kwa kati ya vijana 132 walifika usharikani hapo hawakuzidi 10 kutoka Dar es salaam.

    “Ni wajibu wa wazazi kuwakumbusha vijana wao wasiende na maisha bila Mungu”, alisema Mchungaji Nkya.

    Alisema wakati vijana hao wakijishughulisha na kwaya na masuala ya kikanisa wapo wengine ambao wamejiingiza kwenye mambo yasiyofaa ikiwemo ulevi.

  • Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Edwin Mhede akihutubia wakati wa uzindizi wa programu tumizi ijulikanayo kama PFZ uliofanyika leo jijini Dar es salaam katika viwanja vya Soko Kuu la Kimataifa la Feri, (Picha na Vincent Mpepo).

    Na Vincent Mpepo

    Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) imezindua programu tumizi ijulikanayo kama PFZ itakayorahisisha shughuli za uvuvi na kuwanufaisha wadau mbalimbali kwenye mnyororo wa shughuli hizo ikiwemo wavuvi, wafanyabiashara, wachakataji, wachuuzi na wateja hivyo kuongeza tija itakayochochea ukuaji uchumi katika sekta ya uvuvi nchini.

    Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu hiyo Feri jijini Dar es salaam leo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Edwin Mhede alisema programu tumizi hiyo itasaidia wavuvi kufanya shughuli zao kwa uhakika na kuondokana na uvuvi wa kubahatisha.

    “Uvuvi ni moja ya sekta ambayo inakuwa kwa kasi ikizingatiwa kuwa asilimia 75 ya mazao yake yanauzwa kwenye soko la Ulaya na imeendela kutoa mchango mkubwa kwenye lishe na chakula”, alisema Dkt. Mhede.

    Alisema baada ya kufanyiwa mjaribio mfumo umeonesha matokeo mazuri ya uhakika wa zaidi ya asilimia 75 kutambua aina ya samaki anaowahitaji kwa mahitaji ya soko, umbali walipo na hali ya hewa ili kuwa na uhakika wa usalama wao wakiwa baharini.

    “Mvuvi atajisajili bure na atatakiwa kuweka taarifa zake za msingi ikiwemo taarifa leseni ili atambuliwe na taasisi mbalimbali na kwamba taarifa zake zitalindwa kwa mujibu wa sheria”, alisema Dkt. Mhede.

    Alisema programu tumizi hiyo itarahisisha upatikanaji wa taarifa za wavuvi na utambuzi wao utasaidia kudhibiti uvuvi haramu na kutoa fursa kwa taasisi za fedha kuwakopesha wanawake, vijana na wanaojishughulisha na shughuli za uvuvi.

    Alisema mfumo huo umefungamanishwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) hivyo kumhakikishia mvuvi kuwa na taarifa za hali ya hewa kitu kitakachomhakikishia usalama na namna bora ya kujilinda au kuepuka changamoto zitokanazo hali ya hewa hatarishi baharini.

    Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI), Dkt. Ismael Kimirei alisema shughuli za utafiti zilianza Mwaka 2011 kupitia Mradi wa kutafuta maeneo ya uvuvi baharini kwa msaada na ushirikiano kutoka Umoja wa Ulaya na Umoja wa Afrika.

    Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam alisema wavuvi watumie mfumo huo kwa kuwa ni wa serikali na kwamba anawapongeza watafiti wa Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) na Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi na Maliasili za Bahari (ZAFIRI) kwa kazi hiyo nzuri.

    Mkurugenzi wa jiji la Dar es salaam, Helihuruma Mabelya alisema Soko Kuu la Kimataifa la Feri ni moja ya chanzo kikubwa cha mapato kwa Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam na kwamba kwa kuthamini mchango huo halmashairi itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya matengenezo na ukarabati wa mindombinu ya msingi ili kujenga mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara na wateja.

  • Na Gabriel Alex Msumeno, Kibaha

    Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Phillip Mpango ameongoza wananchi na wakazi wa Mkoa wa Pwani katika sherehe za uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa zilizofanyika Leo katika viwanja vya Shirika la Elimu Kibaha.

    Akizungumza wakati wa sherehe hizo Dkt.Mpango amewataka watanzania kutumia vizuri haki yao ya kidemokrasia kwenye uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani utakaofanyika baadaye Oktoba 2025.

    “Kila mtanzania mwenye sifa atImize haki yake ya kikatiba KUmchangua kiongozi anayemtaka ili kuendelea kulinda amani na utulivu wa nchi yetu”, alisema Dkt Mpango.

    Aidha alibainishwa kuwa licha ya Mwenge wa Uhuru 2025 kuwa na kauli mbiu inayosema “Jitokeze kushiriki uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 kwa amani na utulivu”, umebeba ujumbe kwa watanzania kuhusu masula mengine ikiwemo lishe bora kwa afya imara, mapambano dhidi ya rushwa, VVU/UKIMWI, dawa za kulevya na ugonjwa wa Malaria.

    Sherehe hizo zilihudhuriwa na viongozi mbalimbal wa chama na serikali wakiwemo Waziri Mkuu, Naibu Waziri Mkuu, Rais Mstaafu wa Tanzania wa awamu ya nne Dkt.Jakaya Kikwete, Naibu Spika wa Bunge la Jumhuri ya Tanzania, wakuu wa taasisi za umma, vyombo vya ulinzi na usalama, watumishi wa serikali na taasisi binafsi, wasanii na wananchi kwa ujumla.

    Mwenge wa Uhuru utakimbizwa katika Mikoa 31 kwa muda wa siku 195 ukizindua miradi mbalimbali na katika Mkoa wa Pwani utazindua jumla ya miradi 64 yenye thamani ya shilingi Trilioni1.2.