• Na Vincent Mpepo, Kwembe

    Jamii imetakiwa kuwakumbuka wahitaji na wenye mahitaji maalumu katika huduma mbalimbali ikiwemo mavazi, chakula na mahitaji mengine ya msingi ili waendelee kuishi vyema kimwili na kiroho kama sehemu ya wanajamii.

    Wito huo umetolewa Jumapili na Mwalimu Israel Mmari katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT) Mtaa wa Kwembe wakati akihamasisha uchangiaji wa sadaka maalumu ya udiakonia kwa kwa ajili ya ujenzi wa kituo kipya kituo cha watoto wenye mahitaji maalumu kinachotarajiwa kuhamishiwa Kitopeni Bagamoyo kutoka Kijichi jijini Dar es salaam kutokana na mahali kilipo sasa kuwa siyo salama.

    Alisema bado kuna namna ambapo kila mtu kwa nafasi yake au familia au mashirika iwe ya umma na binfasi yanatakiwa kuwakumbuka wahitaji kwa namna moja au nyingine ili kuwasadia katika kuhakikisha mahitaji yao ya msingi yanapatikana.

    “Kuna mahali ambapo maombi peke yake hayasaidii ni lazima ufanye kitu cha ziada ikiwemo sadaka na matendo ya huruma”, alisema Mwalimu Mmari.

    Alibainisha wahitaji wengine ambao wanahitaji misaada mbalimbali ya kibinadamu katika jamii kuwa ni pamoja na watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu, wajane, wafungwa na wagonjwa.

    Aidha aliitahadharisha jamii dhidi ya matumizi mabaya ya mitanadao ya kijamii na kwamba wapo ambao huitumia vibaya kuharibu wasifu na sifa za wengine.

    “Wapo watu ambao hugharimia mambo yanayowaumiza wengine kupitia mitandao ya kijamii”, alisema Mwalimu Mmari.

    Aidha aliwakumbusha wazazi na walezi kujuenga mazingira mazuri na wezeshi kwa watoto wao ili wakue katika namna njema badala ya mazingira ambayo yatakuwa magumu kwao.

    Mwalimu wa Shule ya Jumaipili, Thomas Lukindo akifundisha watoto kama alivyoonekana na mpiga picha wetu Siku ya Jumapili katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Mtaa wa Kwembe, (Picha na Vincent Mpepo).

    Uchunguzi uliofanywa na mwandishi umebaini kuwa matendo ya huruma kwa wanajamii huwa yanafanyika nyakati za mifungo ya kiimani mfano Kwaresma kwa wakristo na Mwezi Mtukufu wa Ramadani kwa waislamu wakati kiuhalisia mahitaji kwa watu wa Makundi Maalumu yapo muda wote.

    Mwandishi anadhani ifike  mahali jamii ione kuwa mahitaji kwa wahitaji ni sehemu ya maisha ya kila siku na siyo siku za mifungo au msimu tu hivyo jamii ibadilike na kuwathamini wahitaji nyakati zote na ikibidi wafanye kwa kudhamiria kutoka ndani siyo kwa maonesho na kujitangaza kama inavyofanyika sasa.

    Mwalimu Joyce Kamugisha wa shule ya Jumapili akifundisha watoto katika ibada katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT), Mtaa wa Kwembe, (Picha na Vincent Mpepo).

  • Sehemu ya wanafunzi na walimu kutoka Norway wakifurahia zawadi kutoka Idara ya Sosholojia na Ustawi wa Jamii zilizotolewa leo katika hafla fupi ya kuwaaga katika ukumbi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania leo jijini Dar es salaam, (Picha na Vincent Mpepo,OUT).

    Na Vincent Mpepo, OUT

    Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kimeelezea kuridhishwa kwake na huduma za walimu na wanafunzi kutoka Norway ambao walikuwa nchini katika mafunzo kwa vitendo ikiwa ni utekelezaji wa matakwa ya ushirikiano kati ya chuo hicho na vyuo vikuu kutoka nchini Norway.

    Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Idara ya Sosholojia na Ustawi wa Jamii ya Chuo hicho, Dkt.Mariana Makuu wakati wa hafla fupi ya kuwaaga walimu na wanafunzi iliyofanyika leo katika ukumbi wa chuo hicho jijini Dar es salaam na kuhudhiriwa na wanataaluma na wanafunzi wa pande zote mbili.

    Alisema idara yake imepokea mrejesho chanya kutoka shule ambako wanafunzi na walimu hao walikuwa wanafanya mafunzo kwa vitendo na kwamba wameelezea kuridhishwa na huduma zilizofanyika kwa ajili ya walimu na watoto.

    “Walimu wametoa shukrani kwa ujuzi na maarifa mliyoyatoa ya namna ya kuwahudumia watoto wenye mahitaji maalumu”, alisema Dkt.Mariana.

    Aidha alisema ushirikiano uliooneshwa na wanafunzi na wasimamizi wao umerahisisha kazi ya utekelezaji na tathimini ya kazi hiyo.

    Akizungumza kwa niaba ya walimu kutoka Norway, Mwalimu Anne Gutteberg alisema kwa muda aliokaa Tanzania amepata uzoefu na kujifunza mambo mbalimbali ikiwemo utofatui wa kiutamaduni kati ya Norway na Tanzania.

    “Imekuwa fursa nzuri kwa wanafunzi kutoka Norway kujifunza kwa vitendo na kubadilisha uzoefu,” alisema Mwalimu Anne.

    Akitoa shukrani kwa niaba ya idara, Mkufunzi Msadizi, Fauzia Kitenge alisema washiriki kutoka Norway wamefanya kazi nzuri kwa juhudi na maarifa kitu ambacho kimeleta matokeo mazuri kupitia kazi zao.

    Mkufunzi Msadizi, Idara ya Sosolojia na Ustawi wa Jamii ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania. Fauzia Kitenge akitoa neno la shukrani kwa wageni kutoka Norway,kushoto ni Mkuu wa Idara hiyo, Dkt.Mariana Makuu. (Picha na Vincent Mpepo).

    Naye Mwanafunzi kutoka Norway, Ina Fagerdal aliwashukuru wenyeji wao ambao ni idara ya sosholojia na ustawi wa jamii kwa ukarimu na msaada wao wa karibu katika muda wote waliokuwa hapa nchini.

    Mwanafunzi Ina Fagerdal kutoka Norway akielezea uzoefu wake katika mafunzo kwa vitendo alipokwa hapa nchini, (Picha na Vincent Mpepo).

  • Na Tabia Mchakama

    Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imeshiriki na kudhamini tuzo katika Mkutano wa Wadau wa elimu ulioandaliwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Bi. Rosemary Sinyamule uliofanyika mwanzoni mwa wiki hii jijini Dodoma.

    Katika Mkutano huo, Kamishna wa Bima Dkt. Baghayo Saqware aliitaka jamii kukata bima kutokana na manufaa yake katika ulinzi wa afya zao, mali zao na za mali za serikali.

    “Bima ni sehemu ya kujiongezea kipato kwa kuwa wakala wa bima”, alisema Kamishna Dkt. Saqware.

    Mgeni Rasmi wa Mkutano huo alikuwa Dkt. Doto Biteko ambaye kutokana na majukumu mengine aliwakilishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Bi. Rosemary Sinyamule.

    Mkutano huo uaneda sanjali na utekelezaji wa kauli mbiu isemayo ‘Uwajibikaji Wangu ni Msingi wa Kuinua Ubora wa Elimu na Ufaulu Dodoma’ na ulihudhuriwa na wadau mbalimbali wa elimu zaidi ya 2,000.

    Waliotunukiwa tuzo hizo ni walimu, wanafunzi, shule na Wilaya, zilizofanya vizuri katika mitihani ya darasa la nne, darasa la saba, kidato cha nne na kidato cha Sita kwa mwaka 2024 katika Mkoa wa Dodoma.

    Tuzo hizo zinatajwa kuwa chachu na hamasa kwa waliofanya vizuri na inatarajiwa kuwa chachu kwa wengine kuongeza bidii katika mitihani ijayo hivyo kuinua kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi kiwilaya, kimkoa na kitaifa.

  • Hawa Mikidadi, Morogoro

    Katibu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Morogoro, Nuru Ngereja amewaomba waandishi wa habari kuendeleza ushirikiano na chama chake ili kuwatumikia wananchi katika utekelezaji wa ilani ya chama.

    Kauli hiyo aliitoa Tarehe 24.03.2025 wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake ikiwa ni sehemu ya kujitambulisha na kuwatambua waandishi wa habari wa mkoa huo.

    “Katika kipindi ambacho nitakuwepo hapa ninaamini tutafanya kazi pamoja”, alisema Ngereja.

    Alisema kupitia kalamu zao wana kila sababu ya kushirikiana na chama ili kufanikisha utatuzi wa changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii ya wana Morogoro.

  • Mwalimu Israel Mmari wa KKKT Usharika wa Mji Mpya akihubiri jana katika Ibada katika Mtaa wa Kwembe (Picha na Vincent Mpepo).

    Na Vincent Mpepo, Kwembe

    Wakristo wametakiwa kuombea akili kwa kuwa ndiyo inayowezesha watu kufanya maamuzi katika masuala mbambali  iwe katika ngazi ya mtu binafsi, ngazi za familia, jamii na taifa kujiepusha na majanga au matokeo ya matumizi mabaya ya akili ambayo mara nyingi huwaingiza watu kwenye majuto na shida.

    Wito huo umetolewa leo na Mwalimu Israel Mmari wa Kanisa la Kiinjili la Kiutheri (KKKT) Usharika wa Mji Mpya jijini Dar es salaam wakati akihubiri katika Mtaa Kwembe na kwamba siyo kila matatizo dawa yake ni maombi au kufunga.

    Alisema zipo changamoto ambazo kimsingi zimetokana na matumizi mabaya ya akili na kutotambua majira na nyakati hivyo wakati mwingine kuaomba na kufunga ni kujitesa kwa kuwa shida imeanzia kwenye akili iliyofanya maamuzi mabaya.

    Alisema kila kitu katika maisha kimefungwa na nyakati na nyakati ni kibebeo cha mafanikio ambayo Mungu huachilia katika mafanikio ya mwanadamu hivyo busara, hekima na akili sahihi husaidia kufanya maamuzi sahihi kwa wakati husika ili kuwa na matokeo chanya.

     “Kuna majira na nyakati kwa ajili ya kujiliwa kwako na hata kama hukufanya maandalizi Mungu huachilia baraka zake sasa inategemea akili yako imetambuaje na kutumia vyema baraka hizo kwa nyakati hizo”, alisema Mwalimu Mmari.

     “Kabla ya mabaya Mungu huwa na tabia ya kutanguiza mema sasa akili na hekima zinaweza kuamua vyema kwa ajili ya baadaye lakini akili isiyoweza kuamua vyema huleta majanga”, alisema Mwalimu Mmari.

    Akitolea mifano ya ushoga, usagaji na wanaume wanaoishi na wanawake waliowazidi umri kwa kigezo cha kulelewa kuwa hayo yote ni matumizi mabaya ya akili na kwamba wanaotenda hayo wamefikia mwisho wa namna za kutumia akili zao.

    “Hata baadhi ya matatizo katika taasisi za umma, binafsi na kwa watu binafsi wakati mwingine yanatokana na uzembe wa baadhi ya waliopewa dhamana kutotumia akili ipasavyo katika maamuzi fulani”, alisema Mwalimu Mmari.

    Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi, Exaud Mchome aliwajulisha washarika wa Mtaa huo hatua ya ujenzi wa kanisa ambapo imefikia kwenye kuezeka na kwamba tayari kamati yake imeshalipia mabati kwa ajili ya jengo hilo.

    Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi, Exaud Mchombe akifafanua jambo wakati akizungumza na washarika wa KKKT Mtaa wa Kwembe Jana (Picha na Vincent Mpepo)

    Alisema kila mmoja anatakiwa kuwa sehemu ya historia katika ujenzi wa jengo hilo na aone fahari kwa jambo hilo la kumjengea Mungu mahali pa kuabudia. 

    Aidha, aliwakumbusha viongozi mbalimbali katika mtaa huo kuendelea kuwa mfano kwa washarika ili kuongoza vyema katika masuala mbalimbali ikiwemo uchangiaji katika ujenzi na kwamba kiongozi mzuri ni yule anayeongoza kwa mfano na matendo yake.

    “Kimsingi hakuna masikini anayeweza kukiri kuwa hana cha kumtolea Mungu kwa kuwa wema wake bado ni ushahidi kuwa bado tunapaswa kumrudishia yeye hata kwa kidogo alichotujaalia”, alisema Mchome.

    Katika hatua nyingine, wawakilishi wa watoto wa shule ya Jumapili katika ibada hiyo huku masuala mbalimbali yakiwekwa mikononi mwa Mungu ikiwemo amani na usalama wa nchi hususani wakati taifa likielekea kwenye uchaguzi mkuu, waliwaombea viongozi mbalimbalimbali wa dini na wa kisiasa ili waongoze kwa hekma za kimungu.

    Wawakilishi wa watoto wa Shule ya Jumapili ambao walifanya maombi kwa niaba ya wenzao jana katika Mtaa wa Kwembe, nyuma yao ni Mwinjilisti Kiongozi wa KKKT Mtaani hapo, Emeline Mzava. (Picha na Vincent Mpepo).

    Maombi mengine yalielekezwa kwenye mamlaka mbalimbali zinazohusika na utoaji wa haki ikiwemo mahakama na magereza, ustawi wa familia na mtoto, umoja wa makanisa na Uchumi wa nchi.

    Mwinjilisti Kiongozi wa Mtaa huo, Emeline Mzava aliwakumbusha washarika wa Mtaa huo kuwa mawakili wema katika utoaji wa sadaka ya mfuko wa elimu na kwamba ikiwa kila mmoja atakuwa mwaminifu katika sadaka hiyo itasadia sekta ya elimu.

    Kwaya ya akinababa ya KKKT Mtaa wa Kwembe ikihudumu katika ibada ya Jumapili. (Picha na Vincent Mpepo).

  • Na Cartace Ngajiro, Tanga

    Menejimenti ya Bandari ya Tanga imewahakikishia wadau wa bandari hiyo kuendelea kutoa ushirikiano katika masuala mbalimbali ya kibandari ikiwa ni pamoja na utoaji huduma bora kwa wateja ili kuongeza tija na ufanisi.

    Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Meneja wa Bandari ya Tanga Bw. Peter Millanzi hivi karibuni wakati akifunga kikao cha maboresho ya Bandari ya Tanga ‘Tanga Port Improvement Committee’ kilichofanyika jijini Tanga katika ukumbi wa mikutano ulipo katika jengo la Bandari House.

    “Ushirikiano uliopo uendelee kuwepo kwani ndio chachu ya mafanikio katika bandari hiyo kiufanisi”, alisema Millanzi.

    Aidha aliwaahidi wadau hao kufanyia kazi na kupatikana kwa ufumbuzi kwa changamoto zilizopo ili kuendelea  kuvutia wateja zaidi kutumia bandari hiyo.

  • Na Vincent Mpepo, Dar es salaam

    Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Profesa Elifas Bisanda amewapongeza wakuu wa idara chuoni hapo kwa kufanya kazi kwa bidiii hivyo kuendelea kukifanya chuo hicho kutoa huduma nzuri.

    Pongezi hizo alizitoa jana jijini Dar es salaam wakati wa Mhadhara wa Kitaaluma na kusaini makubaliano na kati ya chuo chake na Chuo Kikuu cha Blelefeld cha Ujerumani ambapo miongoni mwa masuala katika makubaliano hayo ni ushirikiano katika tafiti.

    Profesa Bisanda alisema wakuu wa idara ndiyo watekelezaji wakuu wa shughuli za kitaaluma chuoni hapo kwa kuwa wana majukumu ya kusimamia mitaala na ufundishaji.

    “Nitumie fursa hii kuwapongeza wakuu wa idara kwa kazi nzuri wanayofanya ambayo inaendelea kukifanya chuo hiki kuendelea na majukumu yake ya msingi”, alisema Profesa Bisanda.

    Alisema Ujerumani ni miongoni mwa nchi zilizoendelea katika masuala mengi ikiwemo sayansi na teknolojia hivyo kushirikiana nao kunatoa fursa ya kunufaika katika masuala mbalimbalki ikiwemo ujuzi na maarifa katika tafiti.

    Akiwasilisha mada kuhusu namna ya kuratibu timu ya watafiti, Profesa.Dr. Tobias Hecker wa Chuo Kikuu cha Blelefeld cha Ujerumani alisema ni muhimu sana kwa Mtafiti Mkuu  kutambua uwezo, sifa na ubunifu kwa kila mtafiti ili atumie talanta hizo katika kufanikisha utafiti.

    Alisema jambo jingine muhimu ni kwa mtafiti mkuu ni kujishusha na kuwa kiwango sawa na watafiti wengine kwani kufanya hivyo kutasaidia upatikanaji wa mawazo kutoka kwa watafiti wote bila kujali kiwango cha elimu walichonacho.

    Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania anayeshughulikia Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalamu, Profesa Alex Makulilo alisema makubaliano hayo na vyuo vikuu vya Ujerumani ni ya awamu ya tatu na kwamba mara zote utekelezaji wake umekuwa ni wa uhakika.

    “Ni muhimu kubadilishana uzoefu ili kukuza na kuongeza maarifa na ujuzi katika kuratibu timu za utafiti”, alisema Profesa Makulilo.

    Naibu Makamu Makamu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania anayeshughulikia Huduma za Mikoani naTeknolojia ya Kujifunzia, Profesa Leonard Fweja alishauri wanataaluma kuungana na kufanya tafiti badala ya kufanya mmojammoja.

    “Ushirikiano katika utafiti una tija kwa kuwa unasaidia kupunguza gharama na ni rahisi kutumia maarifa, ujuzi na ubunifu wa mwngine katika kuboresha na kupata matokeo mazuri zaidi”, alisema Profesa Fweja.

  • Kijana Junior Allen Mwangoka miaka (22) amepotea. Mara ya ya mwisho alivaa jeans ya sky blue na t-shirt ya dark blue yenye nembo ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania na mpaka sasa  ana zaidi ya wiki mbili. Ukimwona toa taarifa kituo cha polisi jirani nawe, au wasiliana kwa +255 652 064 311.

  • Na Vincent Mpepo, OUT

    Wahadhiri, wakufunzi na wanafunzi katika taasisi za elimu ya juu wameishauri serikali kuhusu utekelezaji wa sera, kanuni na haki za watu wenye mahitaji maalumu ikiwemo watoto wenye ulemavu ili kufanya maisha yao yawe mazuri.

    Ushauri huu umetolewa na wataalamu hao wakati wa tathimini ya mradi wa NOREC unaohusisha wahadhiri, wakufunzi na wanafunzi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Chuo cha Ualimu Elimu Maalumu Patandi na vyuo vikuu vya Norway iliyofanyika kwa siku mbili jijini Dar es salaam.

    Mkuu wa Idara ya Ustawi wa Jamii wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania Dkt. Mariana Makuu alisema watoto wenye mahitaji maalumu wanahitaji kuthaminiwa kwani wakipata huduma hizo zikiambatana na upendo wanaweza kusonga mbele na kufanya vitu vya tofauti kwa jamii zao.

    “Alisema jamii inatakiwa kutambua haki za watoto wenye mahitaji maalumu na kujua kuwa watoto hao ni binadamu kama binadamu wengine wana roho na uhai na wakithaminiwa hali zao zinabadilika”, alisema Dkt.Makuu.

    Alisema kupitia mradi huo wa NOREC kumekuwa na mabadiliko chanya hususani katika Shule ya Msingi Uhuru Mchangayiko ambapo watoto walioanza nao katika mradi hivi sasa wameanza madarasa ya kawaida na wengine wamefaulu kwenda sekondari.

    Mkufunzi wa Chuo cha Ualimu Elimu Maalumu Patandi, Leah Makundi aliikumbusha kuajili walimu wa mahitaji maalumu ili kuwapunguzia walimu mzigo wa kufundisha watoto wengi ikwemo wenye ulemavu.

    Alisema vyuo vya elimu maalumu ikwemo Patandi vinazalisha walimu wengi lakini wanaoajiriwa ni wachache huku uhitaji wao kwenye shule za elimu maalumu ni mkubwa ili watoto wenye mahitaji maalumu wapate haki yao.

    “Natambua juhudi za serikali katika kuhakiksha inatengeneza mazigira rafiki kwa jamii hususani watoto wenye mahitaji maalumu niwaombe waangalie na upande wa ajira ”, alisema Bi Makundi.

    Kwa upande wake, Mkufunzi wa Chuo cha Ualimu Elimu Maalumu Patandi, Anita Kway alizungumzia changamoto za upatikanaji elimu kwa watoto wenye ulemavu ambazo zinatokana na muktadha, upungufu wa vifaa saidizi na kukosekana kwa kwa walimu wenye maarifa ya ufundishaji watoto wenye ulemavu mchanganyiko.

    “Changamoto nyingine ni uwiano usio sawa kati ya wanafunzi na walimu, ukosefu wa rasilimali watu na fedha pamoja na miundombinu stahiki kwa watoto wenye ulemavu”, alisema Bi.Kway

    Mwakilishi wa wanafunzi kutoka Norway, Tora Rosnes alisema uwepo wao nchini Tanzania wamejifunza vitu vingi ikiwemo ari na utayari wa wanafunzi wenye mahitaji maalumu kujifunza na namna walimu wanavyoweza kuchangamana na wanafunzi wakati wa kufundisha.

    “Changamoto nilizokutana nazo ni pamoja na utofauti wa kiutamaduni kati ya nchi yangu na hapa Tanzania hususani Lugha na mimi sijui Kiswahili”, alisema Tora.

    Aidha alisema anafurahishwa na uwepo wa nyimbo nyingi na michezo mbalimbali ya watoto na kitu cha pekee anachoondoka nacho ni furaha.

  • Na Vincent Mpepo, OUT

    Jamii imetakiwa kuwatambua na kuwathamini watoto wenye mahitaji maalumu ili kuwajengea uwezo na kujiamini kitu kitakachosaidia ustawi wao kimalezi, kimakuzi na kitaaluma.

    Wito huo umetolewa na Mkuu wa Idara ya Ustawi wa Jamii wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania Dkt. Mariana Makuu wakati wa tathimini ya mradi wa NOREC unaohusisha wahadhiri, wakufunzi na wanafunzi wa vyuo Tanzania na Norway iliyoanza jana katika ukumbi wa chuo hicho jijini Dar es salaam.

    Alisema jamii inatakiwa kutambua haki za watoto wenye mahitaji maalumu na kujua kuwa watoto hao ni binadamu kama binadamu wengine wana roho na uhai na wakithaminiwa hali zao zinabadilika.

    “Tumeshuhudia pale Uhuru Mchangayiko watoto tulioanza nao katika mradi huu wa NOREC sasa hivi wameshaanza madarasa ya kawaida na wengine wamefaulu kwenda sekondari”, alisema Dkt.Makuu

    Alisema watoto wenye mahitaji maalumu wanahitaji kuthaminiwa kwani wakipata huduma hizo zikiambatana na upendo wanaweza kusonga mbele na kufanya vitu vya tofauti kwa jamii zao.

    Mwanafunzi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania na Mtumishi wa Taasisi ya Mafunzo ya Afya na Sayansi Shirikishi Huruma iliyopo Kilimanjaro, John Kihine alisema Tanzania tuna sera nzuri zinazowahakikishia ulinzi watu wenye mahitaji maalumu ikiwemo watoto wenye ulemavu shida ni utekelezaji.

    Alitolea mfano sera ya elimu inayosema mtoto hatakiwi kuchapwa viboko zaidi ya vinne na anayetakiwa kufanya hivyo ni Mwalimu Mkuu na mwalimu mwingine akimchapa anapaswa kuandika kwa nini amemchapa na akahoji ikiwa sera ingesema mtoto hatakiwi kuchapwa badala yake atafutiwe adhabu nyingine ingefuatwa.

    “Jambo lingine ambalo tunaweza kulifanya ili kuleta matokeo mazuri kwa watu wenye ulemavu ni kuhakiksha tunaendelea kuwa na miundombinu mizuri itakayofanya wao kupata huduma stahiki kama elimu na afya”, alisema Kihine.

    Mkufunzi wa Chuo cha Ualimu Elimu Maalumu Patandi, Leah Makundi aliitaka jamii kuendelea kuwathamini watoto wenye mahitaji maalumu kwa kuwa wanastahili kupata haki zao kama watoto wengine.

    Alisema anatambua juhudi za serikali katika kuhakiksha inatengeneza mazigira rafiki kwa jamii hususani watoto wenye mahitaji maalumu na kuitaka kuajili walimu wa mahitaji maalumu ili kuwapunguzia walimu mzigo wa kufundisha watoto wengi ikwemo wenye ulemavu.

    “Patandi tunazalisha walimu wengi sana lakini wanaoajiriwa ni wachache huku uhitaji wao kwenye shule za elimu maalumu ni mkubwa ili watoto wenye mahitaji maalumu wapate haki yao”, alisema Mkufunzi Makundi.

    Mkuu wa Kitivo cha Sanaa na Sayansi za Jamii cha Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Dkt. Dunlop Ochieng, alisema utekelezaji wa makubaliano ya mradi huo wa ushirikiano kati ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Chuo cha Ualimu Elimu Maalumu Patandi na vyuo vikuu vya Norway yanaenda sanjali na matakwa ya mikataba ya kimataifa na sheria za nchi kuhusu haki za watoto na watu wenye ulemavu.