Na Mwandishi Wetu

Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) anayesimamia Uhimilivu wa Kifedha na Uendeshaji wa Sekta ya Fedha, Sauda Msemo amesema sekta ya fedha nchini inapaswa kuendana na kasi ya ukuaji wa teknolojia duniani ili kulinda usalama wa kiuchumi na kuchochea maendeleo.

Msemo alitoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam wakati wa kongamano lililohusisha wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka katika taasisi zinazohusika na mnyororo wa fedha na teknolojia.

“Teknolojia inakua kwa kasi sana, taifa haliwezi kubaki nyuma, hatuwezi kuwa salama  kama hatutakuwa sehemu ya ukuaji huo na ni  lazima tushirikiane kukuza teknolojia yetu kwa kuzingatia vigezo vya usalama na uendelevu,” alisema Msemo.

Alisema katika juhudi za kuimarisha usimamizi wa bidhaa mpya za teknolojia ya kifedha, Benki Kuu ya Tanzania imeanzisha mazingira maalumu ya majaribio (sandbox), ambayo yanalenga kuwapa wabunifu fursa ya kujaribu bidhaa zao kabla ya kuziingiza rasmi sokoni.

“Hatutaki bunifu ziingie sokoni zikiwa hazijajaribiwa kisha zikaleta madhara bali tunataka ziwe katika mazingira salama kwa kujaribiwa, zikidhi vigezo, ndipo zihidhinishwe kwa ajili ya matumizi ya umma,” aliongeza Msemo.

Mwanzilishi na Mkurugenzi wa Impact Advisory, Angel Mbogoro, alisema kampuni yao imekuwa mstari wa mbele kusaidia taasisi na watu binafsi kujenga uwezo katika maeneo ya uongozi, teknolojia na uendelevu.

“Tumeona kuna pengo la utaalamu nchini ndiyo maana tumeanzisha programu za kuwajengea watu uwezo wa kuongoza taasisi, kutumia teknolojia na kuongeza ujasiri wao katika uwajibikaji ili kuchochea kasi ya maendeleo,” alisema Mbogoro.

Aidha, alibainisha changamoto ya viongozi kutotoa ushirikiano kwa wafanyakazi wao na pindi wanapoondoka ofisini hivyo kuacha pengo kubwa kwa kampuni kuajiri wataalamu kutoka nje ya nchi wakati wapo wenye uwezo lakini hawakuibuliwa.

Mkurugenzi wa Taasisi inayojihusisha na sanaa, uongozi kwa wasichana na mabadiliko ya tabia nchi, Small Hands Big Change, Akoth Okeyo, alisema teknolojia ina mchango mkubwa kwa vizazi vijavyo ikiwa watapatiwa elimu sahihi mapema.

Alisema watoto wanapaswa kufundishwa matumizi Chanya teknolojia ili kuwasaidia wasichana kupata taarifa kupitia akili unde (AI) kwa ajili ya miradi ya tabia nchi na kwamba anaamini teknolojia ni njia sahihi ya kuleta mabadiliko katika jamii.

Kongamano hilo liliibua hoja nyingi kuhusu umuhimu wa kushirikiana kati ya sekta ya umma na binafsi katika kukuza teknolojia bunifu zenye kuzingatia maslahi ya taifa, wadau walisisitiza kuwa ushirikiano wa pamoja ndiyo njia pekee ya kusukuma mbele ajenda ya maendeleo jumuishi na endelevu.

Posted in

Leave a comment