
Na Vincent Mpepo
Imeelezwa kuwa matatizo mengi wayapatayo wakristo katika jamii muda mwingine ni kutokana na kiburi au kupuuzia sauti ya Roho Mtakatifu ndani yao wanapofanya maamuzi katika masuala mbalimbali.
Hayo yameelezwa jana na Mwinjilisti, Thomas Mwakatobe wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT) Usharika wa Buguruni wakati akihuburi katika ibada ya Siku ya Bwana ya Utatu Mtaa wa Kwembe na kusisitiza kuwa athari za kupuuza sauti ya Roho Mtakatifu ni kubwa kwani mara nyingi huwa ni majuto.
Alisema kwa mkristo aliyemkiri Bwana kuwa Mwokozi wa maisha yake kuna namna ambayo Roho Mtakatifu hufanya kazi ndani yake ikiwemo kumkumbusha, kumshauri na wakati mwingine kumpa tahadhari za mambo anayokusudia kuyafanya na ikiwa atatii ni wazi kuwa atafanya maamuzi sahihi.
“Roho Mtakatifu ni ukamilifu wa Mungu Mwenyewe na kuna nguvu ambayo huiachilia kwetu ikiwa tutatembea katika kusudi la Bwana”, alisema Mwinjilisti Mwakatobe.
Alisema Roho Mtakatifu yupo kwa ajili ya kuwakumbusha, kuwapa nguvu na kuwafundisha na kwamba hawawezi kutenda kazi ya Mungu pasipo nguvu za Roho Mtakatifu ndani yao.
“Mara ngapi Roho Mtakatifu amekusemesha kwa namna mbalimbali hata kupitia ndoto na ulifanya nini kutii au kupuuza sauti hiyo?, aliuliza Mwinjilisti Mwakatobe
Alisema miujiza inayotendeka ni kutokana na nguvu za Roho Mtakatifu na kwamba mtu yeyote asijaribu kumwekea mikono mtu mwingine ikiwa hana nguvu ya Roho Mtakatifu kwani atapata shida.
Aidha aliwataka washarika kumakinika na ibada wakiwa kanisani badala ya kuwepo tu kama picha huku mawazo yao yapo nje ya ibada.
Kwa upande mwingine aliwaasa vijana wa vikundi vya kusifu na kuabudu kutengeneza kwanza mambo yao kabla ya kwenda mbele za Mungu na kwamba makosa yao yanaweza kusababisha uwepo wa Mungu kutojidhihirisha katika ibada.

MwinjilistI Kiongozi wa Mtaa wa Kwembe, Emeline Mnzava aliwakumbusha wazazi kuendelea kuwahimiza watoto kujisomea kwa ajili ya maandalizi ya mitihani ya kupima ufahamu ambayo itafanyika kwa watoto wa mwaka wa kwanza.
Mwinjilsti Mnzava aliwashukuru washarika kwa kuendelea kumtolea Mungu kupitia sadaka mbalimbali ikiwemo ile ya ujenzi wa kituo cha watoto wennye mahitaji Maalumu Kitopeni Bagamoyo na kuwa kazi hiyo si ya bure na kwamba hakuna aliyewahi kumtolea Mungu akaachwa.
“Pamoja na kuwa tumeshatoa bado tunaalikwa kuendelea kumtolea Mungu hata kwa kuanzia kwa cha kiwango cha shilingi 1,000 kwani bado rasilimali fedha inahitajika”, alisema Mwinjilisti Mnzava
Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi Mtaani hapo, Exaud Mchome aliwajulisha washarika kuwa kazi ya ujenzi inaendelea vizuri na aliwakumbusha waliohaidi katika awamu ya kwanza ya utoaji ya Januari-Juni 2025 kukamilisha ahadi zao hadi kufikia mwishoni mwa Mwezi Juni kupisha awamu ya pili na mavuno.
“Pesa zilizopatikana zimefanya kazi na kila mmoja anaweza kujionea kwa kutembelea eneo la ujenzi”, alisema Mzee Mchome.
Alisema kipaumbele cha kwanza kwa sasa katika Mtaa wa Kwembe ni ujenzi.
Mjumbe wa Kamati ya Malezi mtaani hapo, Chiristina Bukuku aliwakumbusha wazazi na walezi kuhusu maandalizi ya vijana watakaoshiriki katika Tamasha la Twen’zetu Kwa Yesu kuwahi siku ya Jumamosi kwa ajili ya usafiri wa pamoja ulioandaliwa.
“Mnapaswa kufika hapa kanisani saa 12 kasoro atakayechelewa na akiachwa atalazimika kusafiri mwenyewe”, alisisitiza Bukuku.
Leave a comment