Na Vincent Mpepo

Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kimeendesha mafunzo ya uelewa na utambuzi wa Lugha ya Alama kwa watumishi waendeshaji wanaohusika moja kwa moja na utoaji wa huduma kwa wateja ikiwemo viziwi ili kurahisisha mawasiliano na utoaji wa huduma.

Akifungua mafunzo hayo juzi jijini Dar es salaam, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Teknolojia za Kujifunzia na Huduma za Mikoa, Profesa Leonard Fweja alisema mafunzo hayo ni muhimu kwa kuwa yanadhihirisha dhamira ya chuo kutoa huduma ya elimu kuwa jumuishi na kwamba taarifa ndio nguzo ya mawasiliano miongoni mwa jamii.

“Kama tunavyofahamu katika jamii tupo watu wenye kila aina ya changamoto lakini huwa zipo namna za kupata suluhisho kwa changamoto hizo kupitia mawasiliano”, alisema Profesa Fweja.

Alisema mawasiliano hurahisisha utoaji na upokeaji wa huduma na kuwezesha akili kufanya kazi kwa ubora zaidi.

Mkuu wa Idara ya Isimu na Taaluma za Fasihi chuoni hapo, Dkt. Zelda Elisifa aliwataka waliohudhuria kuendelea kufanyia kazi walichofundishwa ili kukuza uelewa wao katika lugha hiyo kwani bila kufanya hivyo watasahau na mafunzo hayo hayatakuwa na tija.

Alisema chuo kimekusudia kujumuisha ukalimani wa Lugha ya Alama katika huduma na programu zote za chuo hicho kufikia Juni 2026.

“Ili kufanikisha jambo hili idara yangu iliona umuhimu wa kuwapa kipaumbele makatibu muhtasi na wafanyakazi wa mapokezi fursa hii ya ujuzi wa msingi wa Lugha ya Alama ya Tanzania (LAT)”, alisema Dkt. Elisifa.

Kwa upande wake, mshiriki wa mafunzo hayo kutoka Kurugenzi ya Huduma za Wanafunzi, Mwanawetu Mbonde alishukuru idara na Kitivo cha Sanaa na Sayansi za Jamii cha chuo hicho kwa kuandaa na kuendesha mafunzo hayo kwani yanawasaidia kupata msingi wa kuielewa Lugha ya Alama ambayo itawasaidia katika utoaji huduma na watu wa Makundi yote.

Mbonde alishauri mafunzo hayo yaongezewe muda na ikiwezekana yafanyikie nje ya eneo la kazi ili washiriki wapate kumakinika nayo tofauti na hilo inakuwa ngumu kwani wengine wanalazimika kwenda ofisini kufanya kazi na kurudi tena kitu ambacho kinapoteza makini kwa wafanyakazi hao.

Mtumishi wa Kurugenzi ya Maktaba ya chuo hicho, Khadija Katele alisema idadi ya washiriki kutoka kurugenzi hiyo iongezwe kwenye mafunzo wakati ujao kwa kuwa ni eneo linalohudumia watu wote ikiwemo viziwi.

Mafunzo hayo ya siku mbili yalikuwa na malengo mahususi matatu ambayo ni kuongeza ufahamu na uelewa kwa washiriki kuhusu uziwi, Lugha ya Alama na mahitaji ya msingi ya mawasiliano ya jamii ya viziwi.

Malengo mengine ni pamaja na kuwawezesha washiriki kuwa na mbinu za msingi za mawasliano ya kila siku na viziwi ili kuondoa vizuizi vya mawasiliano na viziwi katika jamii ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania na kuwapa washiriki mikakati ya kutengeneza mazingira wezeshi kwa mawasiliano jumuishi.

Posted in

Leave a comment