https://drive.google.com/file/d/13nLFSd1ZCvKoaNqyc1FRw3dwxTRtL-Ly/view
-

Na Athuman Kajembe, Nachingwea
Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea, mkoani Lindi, Mohamed Hassan Moyo, ameonesha kukerwa baada ya kubaini ujenzi wa Kituo cha Afya cha Nammanga, Kata ya Ruponda, unaendelea bila kufuata Hati ya Makadilio Kiasi cha Kazi (BOQ) kama ilivyoainishwa na serikali.
Akiwa katika ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi huo, DC Moyo alisema serikali haiwezi kuvumilia wataalamu wanaojenga majengo ya umma bila kuzingatia taratibu, kanuni na viwango vilivyowekwa.
“Leo hii jamvi linafunikwa bila utaratibu, nondo za mita nane zinatumika badala ya nondo za mita 12 na mbao zinazotumika kujenga majengo mawili si zile zilizo kwenye BOQ, hili ni kosa kubwa,” alisema DC Moyo.
Alisema kitendo hicho kinaashiria matumizi mabaya ya fedha za umma na ujenzi wa miundombinu isiyokidhi viwango vya ubora.

“Naagiza TAKUKURU kuwakamata na kuwafikisha mahakamani wahandisi wote wanaohusika ili kujibu kwa nini wanajenga chini ya kiwango na kutumia vifaa visivyoidhinishwa”, alisema DC Moyo.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea ambaye pia ni Afisa Mipango, Joshua Mnyang’ali, alikiri kuwepo kwa makosa katika ujenzi huo na kumuomba DC Moyo msamaha mbele ya hadhira.
Hata hivyo, DC Moyo alisisitiza kuwa suala hilo litashughulikiwa kikamilifu kupitia ofisi za TAKUKURU ili kuhakikisha haki inatendeka na fedha za serikali hazipotei.
Inakumbukwa kuwa mradi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Nammanga umetengewa zaidi ya milioni 200 hadi kufikia Februari 2026, kiasi kinachotarajiwa kukamilisha ujenzi huo kwa viwango vinavyokubalika.


-

Na OWM (KAM) – DODOMA
Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) umepongezwa kwa hatua kubwa ilizochukua katika kuboresha upatikanaji wa huduma kwa wananchi, hususan utoaji wa fidia kwa wafanyakazi wanaokumbana na madhila ya ajali ama ugonjwa unaotokana na kazi.
Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu jana jijini Dodoma wakati wa ziara yake katika Ofisi za Makao Makuu ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) alipokutana na menejimenti na baadhi ya watumishi wa WCF kwa lengo la kujua majukumu ya Mfuko huo sambamba na kutoa maelekezo ya kiutendaji yanayolenga kuongeza tija na ufanisi.
Sangu alisema huduma hizo bora zimechangia kuimarisha imani ya wananchi kwa mfuko, ambapo wafanyakazi wanaopatwa na majanga kutokana na kazi wamekuwa wakipatiwa huduma kwa wakati na kwa kiwango kinachostahili hivyo kuongeza ufanisi na kupunguza usumbufu kwa wafanyakazi,
Katika hatua nyingine, Waziri Sangu ameitaka Menejimenti ya WCF kuendeleza ubunifu katika utekelezaji wa majukumu yao, ikiwemo kuongeza nguvu ya mifumo mipya ya kidijitali inayoboresha mbinu za utoaji huduma kwa wakati na ufanisi zaidi ili kufikia wananchi kwa haraka.
Awali, akizungumza, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Rahma Kisuo, amehamasisha Menejimenti ya Mfuko huo kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu majukumu na huduma zinazotolewa na Mfuko, ili kuongeza uelewa kwa waajiri wengi zaidi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa WCF Dkt. John Mduma alisema WCF imejipanga kuendelea kuboresha mifumo ya utoaji huduma ili kuhakikisha madai ya fidia yanashughulikiwa kwa wakati, uwazi na ufanisi zaidi.


-

Na Mwandishi Wetu
Wizara ya Maliasili na Utalii imesema ushindi wa Tanzania kwenye tuzo za World Travele Award 2025 ikiwemo tuzo kubwa ya Utalii wa safari bora duniani ni uthibitisho kuwa nchi ina vivutio vya utalii vinavyokubalika kimataifa.
Akizungumza Desemba 8, 2025 mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam, akitokea Bahrain, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dk. Hassan Abbas amesema ushindi huo unaonesha kuwa dunia imeitambua Tanzania kama kitovu bora cha utalii wa safari.
“Kwa mwaka wa pili mfululizo tumeshinda tuzo kubwa zaidi ya utalii wa safari duniani. Hii ni sawa na tuzo za Oscars kwa filamu au Grammy kwa muziki,” alisema Dk. Abbas.

Alisema kutokana na ushindi huo, nchi imepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa tuzo za dunia za utalii mwaka 2026, ambapo wadau wakubwa wa sekta hiyo duniani watakusanyika nchini.
Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Utalii Tanzania, Ephraim Mafuru, amewashukuru wadau wa utalii kwa kuipigia kura Tanzania, akisema ushindi huo umetokana na imani ya dunia kwa Serengeti na hifadhi nyingine.

“Tanzania imeshinda tuzo ya Hifadhi bora duniani kupitia Serengeti, pamoja na tuzo ya Utalii wa Safari Bora Duniani mafanikio haya yametokana na uboreshaji miundombinu ikiwemo barabara zaidi ya kilomita 2,800 ndani ya hifadhi na kuvifanya vivutio kufikika kwa urahisi,” alisema Mafuru.


-

Na Mwandishi Wetu
Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limewataka viongozi wa makundi ya mitandao ya kijamii, hususan WhatsApp, kudhibiti usambazaji wa taarifa za uchochezi, uvunjifu wa amani.
Wito huo umetolewa Desemba 8, 2025 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, SACP Safia Jongo, alipoungana na Mtandao wa Polisi Wanawake Tanzania (TPF-Net) mkoani humo kutoa msaada katika Kituo cha Afya Nyankumbu ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku 16 za Kupinga ukatili wa kijinsia.
Kamanda Jongo alisema mitandao ya kijamii, hususan makundi ya WhatsApp, isiruhusiwe kuwa majukwaa ya kusambaza chuki, vitisho, taarifa za upotoshaji na unyanyasaji wa kidijitali dhidi ya wanawake na wasichana.
Alisema wasimamizi wa makundi ya WhatsApp na watumiaji wa mitandao ya kijamii wanayo nafasi kubwa ya kudhibiti maudhui yanayokiuka maadili, sheria na kuchochea uvunjifu wa amani.
“Ni wajibu wao kuhakikisha mitandao haigeuki kuwa chanzo cha uhalifu na ukatili wa kijinsia,” alisema Kamanda Jongo.
Alizungumzia Mtandao wa TPF-Net unaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kupambana na ukatili unaotekelezwa kupitia majukwaa ya kidijitali, sambamba na kuhamasisha wananchi kutoa taarifa mapema wanapobaini au kukumbana na vitendo vya ukatili.
Aidha, amewataka wananchi kuepuka vitendo vya vurugu, uhalifu na uvunjifu wa amani, huku akisisitiza umuhimu wa kukomesha vitendo vyote vya ukatili, hususan unaofanywa mtandaoni dhidi ya wanawake na wasichana.

-

Na Vincent Mpepo
Walimu wanaosoma somo la Kifaransa kama mmoja ya somo la kufundishia wametakiwa kuwekeza nguvu nyingi na kujibidiisha kwani kuna fursa nyingi za ajira za ndani na nje ya nchi kupitia lugha hiyo.
Wito huo umetolewa mwishoni mwa wiki katika mijadala mbalimbali ya Siku ya Walimu wa Kifansa Duniani iliyofanyika katika Ukumbi wa Shule ya Sekondari Azania ambapo fursa za Lugha hiyo zilibabinishwa.
Mwenyekiti wa Chama cha Walimu wa Kifaransa Tanzania (TAFT), Dkt. Costantine Njalambaya alisema Kifaransa si tu lugha ya kujifunza, bali ni fursa ya ubunifu na chombo cha mshikamano kinachotumika kujieleza kupitia utamaduni na daraja linalounganisha watu.

Dkt. Njalambaya aliushukuru Ubalozi wa Ufaransa kwa msaada wa kifedha, ambao umewezesha sherehe hizo kufanyika na kwamba unasaidia kimarisha dhamira chama hicho kukuza ufundishaji wa lugha ya Kifaransa nchini Tanzania na kuendeleza jamii kielimu.
Aidha alizungumzia mipango na mikakati ambayo chama chake kimeiweka ili kuwafikia walimu wengi wa Kifaransa nchini mijini na vijijini ili kuongeza wigo wa walimu wa Kifansa nchini.
Mwalimu wa Kifaransa, Frola Musikula ambaye kwa sasa amestaafu, alisema kuna fursa nyingi kwa vijana ambao wanasoma Kifaransa na kutanabaisha kuwa kwa uzoefu wake amegundua wanafunzi wanaomliza Shule ya Msingi wengi wao wanapenda sana Kifaransa.

“Watoto wangu wawili wanafundisha Kifaransa na pia Kifaransa kimeniwezesha kugfanya kazi kwenye maeneo mengi ikiwemo sekta ya utalii na ualimu huko Zanzibar”, alisema Mwalimu Flora.
Alisema pamoja na kwamba amestaafu bado anafundisha Kifaransa kwa wanafunzi waliomaliza darasa la saba ambao wanajiandaa kuingia kidato cha kwanza katika kituo cha ‘Pugu Intercity Academy’.
Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo, Afisa Elimu Kata, Upanga Magharibi ambaye alimwakilisha Afisa Elimu Jiji la Dar es Salaam, Mwalimu Immaculata Ngure alisema wakati umefika kwa serikali kubadilika na kuongeza idadi ya walimu wa somo la kifaransa kutokana na umuhimu na faida za somo hilo katika nchi na kwa mtu mmojammoja.
“Uhamasishaji ufanyike ili kuhakikisha watoto wetu wanasoma lugha ya kifaransa”, alisema Mwalimu Immaculata.
Akizungumzia matumizi ya nyimbo katika ufundishaji alisema ni zana muhimu katika kusaidia kukuza uelewa na kuweka kumbukumbu hatahivyo alishauri uchaguzi wa nyimbo hizo ufanyike kwa makini ili kuwa na maudhui yanayofaa kwa kuwa siyo nyimbo zote zinaweza kutumika.
Makamu Mkuu wa Shule ya Sekondari Azania, Mwalimu Magreth Lawrance alisema shule hiyo ina darasa maalumu la Kifaransa na ameshukuru kusikia kuwa uongozi wa chama hicho unakusudia kufanya maboresho katika darasa hilo jambo ambalo ni jema.

“Sisi kama watanzania tumewasikia wenzetu kutoka Zanziobar na kilichotuunganisha ni Lugha ya Kifaransa kama ambvyo Mwalimu Nyerere alivyofanikiwa kuwaunganisha watanzania kwa kutumia Lugha”, alisema Mwalimu Magreth.
Aidha alishauri walimu wa shule nyingine kuanzisha somo hilo la Kifaransa kwa kuwa watoto wanapenda n ani fursa nzuri kwao.
Maadhimisho ya mwaka huu yenye kaulimbiu “Kuimba, Kucheza, Kufundisha: Lugha ya Kifaransa katika Muziki,” yanaangazia sanaa na michezo inavyotumika kwenye kufundisha lugha ya Kifaransa yamewakutanisha walimu, wahadhiri, wanafunzi wa lugha ya Kifaransa nchini yakihusisha bara na visiwani huku ikibanika kuwa Lugha hiyo ina ladha ya kipekee kwenye muziki hivyo ni rahisi kufundishika.



-

Mgeni Rasmi wa katika maadhimisho ya Siku ya Kifaransa Duniani, Afisa Elimu Kata ya Upanga Magharibi, Mwalimu Immaculata Ngure katika picha ya pamoja na meza kuu pamoja na walimu wa Kifaransa waliohudhuria katika maadhimisho hayo jana Katika Shule ya Sekondari Azania, jijini Dar es Salaam. (Picha na Vincent Mpepo).
Na Vincent Mpepo
Wadau wa lugha ya Kifaransa nchini wamekutana katika Shule ya Sekondari ya Azania kuadhimisha Siku ya Kifaransa Duniani, ikiwa ni sehemu ya kuienzi lugha hiyo adhimu na kubainisha fursa mbalimbali zinazopatikana kwa wanaojifunza Kifaransa.
Katika maadhimisho hayo yaliyofanyika jana jijini Dar es Salaam, wahadhiri, wakufunzi, walimu na wanafunzi wa lugha ya Kifaransa walisema bado kunahitajika hamasa zaidi kwa jamii ili kuongeza uelewa na mapenzi ya kujifunza lugha hiyo.
Mwenyekiti wa Chama cha Walimu wa Kifaransa Tanzania (TAFT), Dkt. Costantine Njalambaya, alisema Kifaransa si lugha ya kujifunza pekee, bali ni daraja la utamaduni, ubunifu na mshikamano linalowawezesha watu kujieleza na kuunganishwa kimataifa.

Mwenyekiti wa Chama cha Walimu wa Kifaransa Tanzania (TAFT), Dkt. Costantine Njalambaya akihutubia hadhara ya wanafunzi, wakufunzi, wahadhiri na wadau mbalimbali wa Lugha ya Kifaransa katika maadhimisho ya Lugha hiyo yaliyofanyika jana katika Shule ya Azania jijini Dar es Salaam. (Picha na Vincent Mpepo).
Alibainisha kuwa maadhimisho ya mwaka huu yenye kaulimbiu “Kuimba, Kucheza, Kufundisha: Lugha ya Kifaransa katika Muziki” yameangazia namna sanaa na michezo vinavyoweza kutumika kuboresha ufundishaji wa lugha hiyo.
Aidha, aliushukuru Ubalozi wa Ufaransa kwa msaada wa kifedha uliowezesha kufanyika kwa maadhimisho hayo, akisisitiza kuwa mchango huo umeendelea kuimarisha jitihada za chama hicho katika kukuza ufundishaji wa Kifaransa nchini.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Walimu wa Kifaransa Mkoa wa Dar es Salaam ambaye pia ni mwalimu wa Kifaransa katika Shule ya Sekondari Chang’ombe, John Daudi, alisema chama hicho kimepiga hatua kubwa, huku akishukuru serikali kwa ushirikiano inaotoa.
“Kwa mfano, mwaka jana tuliandaa Siku ya Walimu wa Kifaransa katika Kituo cha Utamaduni cha Kifaransa hapa Dar es Salaam, na mwaka huu tumefanya hapa Sekondari ya Azania,” alisema Mwalimu Daudi.
Naye Mgeni Rasmi wa maadhimisho hayo, Afisa Elimu Kata ya Upanga Magharibi, Mwalimu Immaculata Ngure, aliyemwakilisha Afisa Elimu wa Jiji la Dar es Salaam, alikipongeza chama hicho kwa juhudi za kuwaunganisha wadau wa lugha hiyo wakiwemo walimu, wakufunzi, wahadhiri na wanafunzi.

Afisa Elimu Kata ya Upanga Magharibi, Mwalimu Immaculata Ngure akihutubia washiriki wa maadhimisho ya Siku ya Walimu wa Kifaransa Duniani yaliyofanyika jana katika Shule ya Azania jijini Dar es Salaam. (Picha na Vincent Mpepo).
Alisema wakati umefika kwa serikali kuongeza idadi ya walimu wa somo la Kifaransa kutokana na umuhimu na manufaa yake kwa nchi na kwa mtu mmoja mmoja. Alisisitiza pia kuwepo kwa uhamasishaji zaidi ili watoto wawe na motisha ya kujifunza lugha hiyo.
Akizungumzia matumizi ya nyimbo katika ufundishaji wa lugha, Mwalimu Immaculata alisema nyimbo ni zana muhimu inayosaidia kuongeza uelewa na kuhifadhi kumbukumbu za kudumu kwa wanafunzi, hasa watoto.
Aidha, alieleza kuwa kuanzia mwaka huu Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA) limeanza kutahini wanafunzi wa shule za msingi katika lugha mbalimbali ikiwemo Kifaransa, Kichina na Kiarabu, akibainisha kuwa hatua hiyo ni fursa kubwa kwa wanafunzi kupata manufaa ya lugha hizo za kimataifa.
Katika maadhimisho hayo, mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwemo umuhimu wa kutumia muziki katika ufundishaji wa Kifaransa, ambapo ilibainika kuwa mbinu hiyo inachochea uelewa wa haraka na husaidia wanafunzi kukumbuka wanachojifunza kwa urahisi.
Maadhimisho ya mwaka huu yamewakutanisha walimu, wahadhiri na wanafunzi wa Kifaransa kutoka Tanzania Bara na Visiwani, yakionyesha kwa mara nyingine kuwa lugha hiyo ina mvuto wa kipekee katika muziki na hivyo kuwa rahisi kufundisha na kujifunza.


Sehemu ya washiriki wa maadhimisho ya Siku ya Walimu wa Kifaransa Duniani wakifuatilia mijadala hapo jana katika Ukumbi wa Shule ya Sekondari Azania. (Picha na Vincent Mpepo).
-

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Profesa Alex Makulilo akizungumza na hadhara ya wafanyakazi wa chuo hicho jana Kinondoni, jijini Dar es salaam.
Na Vincent Mpepo
Uongozi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) umesisitiza dhamira yake ya kuboresha mazingira ya kazi ili kuongeza tija na kuboresha utoaji wa huduma kwa wateja.
Akizungumza katika Mkutano wa Makamu Mkuu wa Chuo na wafanyakazi uliofanyika jana Kinondoni, jijini Dar es Salaam, Makamu Mkuu wa Chuo, Profesa Alex Makulilo, aliwataka wafanyakazi kufanya kazi kwa bidii na weledi ili kuboresha huduma kwa wateja na kupunguza malalamiko.
Alisema huduma bora kwa mteja ni msingi wa mafanikio ya taasisi yoyote, na hivyo amewataka wafanyakazi kutilia mkazo suala hilo, vinginevyo taasisi inaweza kukumbana na malalamiko ya mara kwa mara na kupoteza wateja.
Akizungumzia maendeleo ya Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET), Profesa Makulilo alisema mradi unaendelea vizuri licha ya changamoto katika baadhi ya vituo, ikiwemo kushindwa kwa baadhi ya wakandarasi kuendelea na kazi kutokana na sababu mbalimbali.
“Ufuatiliaji ulifanyika na kubaini kuwa wakandarasi hawawezi kuendelea na mradi,” alisema Profesa Makulilo.
Aliongeza kuwa taratibu zote za kisheria zilifuatwa katika kusitisha kandarasi hizo, na taratibu za kupata wakandarasi wapya zinaendelea kwa kushirikiana na wizara husika.
Vituo vya mikoa ambavyo utekelezaji wa mradi haukwenda vizuri ni Arusha, Mwanza na Kigoma, huku utekelezaji ukiendelea kwa ufanisi katika vituo vya Njombe na Mtwara.
“Kuchelewa kwa utekelezaji wa mradi kumetokana na changamoto mbalimbali za ndani na nje ya taasisi,” alifafanua Profesa Makulilo.
Aidha, alieleza kuwa uongozi umeimarisha mikakati ya kuhakikisha uendelevu wa mradi kwa kufanya uteuzi wa viongozi wapya watakaosimamia utekelezaji wake kwa ufanisi, huku akiwataka viongozi hao kutanguliza maslahi ya taasisi.
Kwa upande wake, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Huduma za Mikoa na Teknolojia za Kujifunzia, Profesa Leonard Fweja, alizungumzia uharibifu wa vituo vya Kahama na Kinondoni uliotokana na machafuko ya Oktoba 29.
Naye Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalamu, Profesa Saganga Kapaya, aliwashukuru wafanyakazi kwa kufanikisha mahafali ya 44 ya chuo hicho na kuwasisitiza kuendelea na moyo huo.
Akitoa taarifa kuhusu mrejesho wa mitaala kutoka Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), alisema kati ya mitaala 98 iliyowasilishwa, mitaala 21 ya marejeleo imerejeshwa na inakidhi vigezo vya ubora, huku 14 ikihitaji masahihisho madogo.
Aliwataka wakuu wa vitivo kuunda timu ndogo za kushughulikia masahihisho hayo na kuyawasilisha kwa wakati, akibainisha kuwa kazi hiyo inatakiwa kukamilika ifikapo 15/12/2025.
Wakati huohuo, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Mipango, Fedha na Utawala, Profesa Josiah Katani, aliwakumbusha wafanyakazi kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma, hususan suala la kuwahi na kuhudhuria kazini kwa wakati.
Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi (THTU) chuo hapo, Salatiel Chaula, aliushukuru uongozi wa chuo kwa ushirikiano wao katika kutatua changamoto za wafanyakazi, ikiwemo uboreshaji wa maslahi, na akawahimiza wafanyakazi kuendelea kujituma katika kazi.

Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi tawi (THTU) tawi la Chuo kikuu Huria cha Tanzania, Salatiel Chaula akisisitiza jambo wakati wa Mkutano wa Makamu Mkuu wa Chuo na wafanyakazi uliofanyika jana Kinondoni, jijini Dar es salaam. (Picha kwa hisani ya Kitengo Cha Mawasiliano na Masoko, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania).




Picha mbalimbali: Sehemu ya wafanyakazi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania wakati wa Mkutano wa Makamu Mkuu wa Chuo hicho na wafanyakazi uliofanyika jana Kinondoni, jijini Dar es salaam. (Picha kwa hisani ya Kitengo Cha Mawasiliano na Masoko, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania).

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko cha Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Dkt. Adam Namamba akisoma jumbe za wafanyakazi kutoka vituo vya mikoa nje ya Dar es salaam walioshiriki Mkutano wa Makamu Mkuu wa Chuo na wafanyakazi uliofanyika jana Kinondoni, jijini Dar es salaam. (Picha kwa hisani ya Kitengo Cha Mawasiliano na Masoko, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania).
-

Kulia ni Mkuu wa Polisi Wilaya ya Iramba SSP Brainer Robert akiteta Jambo na Muuguzi Mfawidhi Hospitali ya Wilaya ya Mkalama, Wilson Augustin (katikati) muda mfupi baada ya kupoke msaada uliotolewa na Askari wa Jeshi la Polisi Tanzania wanawake (TPF NET) Mkoa wa Singida katika Maadhimisho ya Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia ambapo wametoa msaada kwa wahitaji kwenye hospitali ya Wilaya Mkalama.

Pichani ni Askari wa Jeshi la Polisi Tanzania wanawake (TPF NET) Mkoa wa Singida wakijiandaa kwenda Wilaya ya Mkalama katika Maadhimisho ya Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia kwa lengo la kutoa msaada wa vitu mbalimbali kwa wahitaji katika hospitali ya Wilaya Mkalama tarehe 03/12/2025.
