Afisa Polisi Jamii Mkoa wa Singida, ACP Richard Mwaisemba amewataka wananchi wa Kata ya Makanda, Wilaya ya Manyoni, kuitii sheria na kanuni za uchaguzi mkuu 2025 bila kushurutishwa ili kulinda amani na usalama katika maeneo yao.
Akihitimisha mafunzo ya Polisi Jamii kwa vijana 32 wa kijiji cha Magasai, ACP Mwaisemba amesisitiza umuhimu wa uadilifu, nidhamu na kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuzuia uhalifu.
Viongozi wa jamii wamepongeza mafunzo hayo na kuomba yaendelezwe kwa kuwahusisha vijana zaidi.
Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka watumishi wa Hazina ndogo mkoani Kigoma kufanya kazi kwa bidii, maarifa, weledi na kuzingatia kanuni katika majukumu yao.
Wito huo aliutoa wakati wa mazungumzo na watumishi hao alipotembelea Mkoa huo hivi karibuni ambapo alipata fursa ya kuzungumza na watumishi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Hazina ndogo.
Alisema kufuatia juhudi zinazofanywa na serikali katika kuboresha mazingira ya kazi na namna bora ya kuwahudumia wananchi wake watumishi hao wanatakiwa kufanya kazi kiueledi.
“Serikali inafanya kazi kubwa kwa kuweka mazingira wezeshi kwa watoa huduma na kuboresha miundombinu katika sekta zote ili wananchi wapate huduma bora kwa wakati na bila upendeleo” Dkt. Nchemba.
Mkuu wa Hazina Ndogo Mkoa wa Kigoma, Frank Msaki aliishukuru serikali kwa kazi kubwa katika Kanda ya Kigoma kuhakikisha huduma muhimu zinapatokana kwa wananchi na kwa wakati.
“Sisi wasaidizi wake, tutaendelea kutoa huduma kwa kufuata misingi ya haki na uwajibikaji”, alisema Msaki..
Kwa upande wake, Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Mkoa wa Kigoma, Beatus Nchota alisema usimamizi mzuri wa ukusanyaji wa mapato katika Mkoa wa Kigoma unatokana na mwitikio mkubwa wa walipa kodi kufuatia elimu ya mlipa kodi wanayoitoa mara kwa mara kwa wafanyabiashara wa Mkoa huo.
Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria cha Tazania anayeshughulikia Mipango, Fedha na Utawala, Profesa Josiah Katani ni miongoni mwa waliofika katika zoezi la upimaji afya mapema jana. Anayeonekana nyuma yake ni Mkurugenzi wa Rasilimali watu na Utawala wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Francis Badundwa na Profesa Cosmas Mnyanyi. (Picha kwa hisani ya Dkt. Adamu Namamba).
Na Vincent Mpepo
Wafanayakazi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania wametakiwa kujali afya zao kwa kupima na kupata ushauri wa kitabibu ili kujua changamoto zinazowakabili mahali pa kazi na namna ya kukabiliana nazo.
Mkurugenzi wa Rasilimali watu na Utawala wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Francis Badundwa alitoa wito huo jana ofisini kwake Kinondoni jijini Dar es salaam wakati wa mahojiano na mwandishi wetu na kuwataka wafanyakazi hao kutumia fursa ya siku tano ya uwepo wa watumishi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) kwa zoezi hilo la upimaji afya.
Alisema kumekuwa na mwitikio mdogo wa wafanyakazi katika zoezi hilo la upimaji licha ya kukiri kuwa masuala afya ni masuala binafsi.
“Natambua wengi huenda kipima hospitali moja kwa moja ambapo watapata vipimo, majibu na tiba”, alisema Badundwa.
Kwa upande wake, Dkt. Pricila Michael kutoka Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) alianisha majukumu ya taasisi yake kuwa ni ukaguzi wa afya unahusisha upimaji wa vipimo vya awali kwa mwajiriwa mpya, upimaji wa afya wa mara kwa mara na vipimo wakati mtumishi anapomaliza muda wake wa ajira kwa kustaafu, kuachishwa au kuhama.
“Madhumuni ya kufanya zoezi hili la ukaguzi wa afya ni kutaka kujua hali ya mtumishi kiafya”, alisema Dkt.Pricila.
Alibainisha aina ya vipimo wanavyohusika navyo kuwa ni pamoja na vya uzito, urefu, shikizo la damu, hali ya lishe na uwezo wa kuona mbali ili kujua hali ya afya ya mwajiriwa kwa ujumla na mazungumzo na Daktari.
Mkaguzi wa Afya wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA), Peter Kilimuhano alisema watumishi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania walipe kipaumbele zoezi hili la upimaji wa afya kwa kuwa ni muh9mu kwa afya zao.
Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) ni chombo cha kusimamia usalama na afya mahala pa kazi kwa kuhakikisha kwamba waajiri wote nchini wanaweka miundo na mifumo inayohakikisha usalama na afya mahala pa kazi vinalindwa.
Mkuu wa mkoa Arusha Kenani Kihongosi mapema wiki hii aliwaongoza wananchi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi CCM Mkoa wa Arusha kwenye Ofisi za Chama Cha Mapinduzi wilaya ya Arusha, kumdhamini Mgombea Urais wa Chama hicho Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Rais wa awamu ya sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Wananchi walioambatana na Kihongosi ni kutoka makundi mbalimbali ya kijamii wakiwemo wajasiriamali, mama lishe na baba lishe, vijana wanaojishughulisha na usafiri wa bajaji na pikipiki maarufu kama Bodaboda pamoja na wananchi wengine,
Sababu za kumuunga mkono zinatajwa kuwa ni kutokana na mafanikio makubwa yaliyoshuhudiwa Mkoani Arusha kwa kipindi cha Miaka minne ya uongozi wake.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Acp Pili Misungwi amekabidhi pikipiki mbili kwa watendaji wa dawati la jinsia na watoto Wilaya ya Kimara na Kinondoni. Makabidhiano hayo yamefanyika leo katika kituo cha Polisi Oystebay ambapo yamehudhuriwa na maofisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali Mkoa wa kinondoni.
Watendaji wa dawati la jinsia na watoto waliokabidhiwa pikipiki hizo wamepewa elimu na matumizi sahihi ya vyombo hivyo ambvyo ni kwa ajili ya kuhakikisha wanawafikia wananchi kila eneo kwa haraka na kuwapatia huduma za kutanzua ukatili wa kijinsia.
Mgombea urais wa Chama Cha Kijamii (CCK), David Mwaijojele, ameahidi iwapo atapewa ridhaa na watanzania kuiongoza nchi, serikali yake itahakikisha wafanyakazi wanajengewa nyumba wakiwa bado kazini ili kuondoa hofu ya maisha magumu baada ya kustaafu.
Akizungumza mara baada ya kuchukua fomu ya kugombea urais akiwa na Mgombea mwenza Masoud Ali bdallah katika ofisi za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Mwaijojele alisema serikali ya CCK imejipanga kuweka mfumo wa makato maalum ya kodi kwa wafanyakazi walioko kazini ambayo yatatumika kuwajengea nyumba kabla hawajastaafu.
“Tumeona mara nyingi wafanyakazi waliopo kwenye ajira sasa hivi wanaogopa kustaafu kwa sababu ya mazingira wanayoishi mtu anafanya kazi miaka mingi lakini hana hata kiwanja, hana nyumba na anapofikiria kuacha kazi anajiuliza ataishije”, alisema Mwaijojele.
Alisema iwapo wananchi waiamini CCK na kuipa dhamana ya kuobgoza kitaweka mazingira wezeshi ya kuwakatia kodi kwa kiwango kidogo wakiwa kazini ili zisaidie katika ujenzi wa nyumba hizo kabla hawajastaafu.
Mwaijojele alionhgeza kuwa lengo la mpango huo ni kuandaa mazingira salama ya ustaafu kwa watumishi wa umma na sekta binafsi ili nafasi zao zichukuliwe na vijana huku waliostaafu wakiendelea kuishi maisha ya heshima na hadhi.
Sanjali na hilo, Mwaijojele alisema serikali ya CCK pia ina mikakati thabiti ya kuwawezesha wananchi wa kawaida kupitia mfumo wa kuweka akiba ya kiasi kidogo cha fedha, ambapo serikali itawaunga mkono kwa kuwapatia mitaji ya kujiendeleza.
“Hata kama mtu unaweka mia mia kwa siku, tunataka mwisho wa mwaka uweze kupata msaada kutoka serikalini hata kama una kibanda cha chumba kimoja, CCK itakusaidia uweze kukipanua hii ni kwa wafanyabiashara, wajasiriamali wadogo, wachimba madini, waandishi wa habari na wananchi wote kwa ujumla”,alisema Mwaijojele.
Akizungumzia mchakato wa kuchukua fomu, Mwaijojele aliishukuru Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa kuratibu zoezi hilo weledi akidai kuwa kuwa tume imekuwa ikishirikiana bega kwa bega na wagombea wote tangu hatua za awali.
“Ninawashukuru sana Mwenyekiti wa Tume, Mkurugenzi na jopo zima la Tume pamoja na wafanyakazi wote kwa kazi nzuri mnayoifanya tumekuwa tukishirikiana nanyi bega kwa bega katika kila hatua na tunathamini sana jambo hilo,” alisema Mwaijojele.
Mwaijojele alibainisha vipaumbele vya CCK kuwa ni kilimo cha kisasa, elimu, afya, ajira, pamoja na ustawi wa vijana na wazee.
Alisema CCK inalenga kuleta mageuzi ya kweli kwa watanzania wote kwa kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Mkuu wa Ushirikishwaji wa Jamii Mkoa wa Kinondoni, ACP Ally Wendo amezindua kituo cha polisi kinachohamishika cha Kuzidi maeneo ya Goba, Kinzudi jijini Dar es salaam.
Uzinduzi huo ulifanyika juzi na ulihudhuriwa na maafisa wa jeshi hilo, wakaguzi, askari wa vyeo mbalimbali, viongozi wa serikali ya mtaa na wananchi wa mtaa huo.
Katika uzinduzi huo, wananchi walipewa elimu ya ukatili wa kijinsia, aina zake, namna ya kutanzua uhalifu, kuanzisha vikundi vya ulinzi shirikishi katika mItaa, kuchangia pesa ya ulinzi pamoja na kutoa taarifa za wahalifu na uhalifu.
Katika hatua nyingine, ACP Wendo ameupongeza uongozi wa serikali ya mtaa wa Kinzudi na wananchi kwa ushirikiano uliofanikisha kukamilika kwa kituo hicho kidogo cha polisi.
ACP Wendo alifanya uzinduzi huo kwa niaba ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni SACP Mtatiro Kitikwi na aliwataka wananchi kuendelea kushirikiana na jeshi la polisi na kuwapa ushirikiano askari watakaopangiwa majukumu katika kituo hicho.
Wadahiliwa wa Shahada za Uzamili na Uzamivu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania Mkoa wa Dar es salaam wameelezea mipango na mikakati yao binafsi ili kuhakikisha wanamaliza masomo yao kwa wakati na kwa mafanikio.
Wakizungumza na mwandishi wetu katika mahojiano, wadahiliwa hao walionesha kufurahia mafunzo elekekezi yaliyotolewa na chuo hicho kwani yamewafungua kuona namna ya usomaji chuoni hapo.
Mwanaidi Salim, mdahiliwa wa Shahada ya Uzamili katika Eilimu, Sera na Mipango alisema mafunzo elekezi aliyoyapata yamemsaidia kutambua mifumo ya kujifuza na kujifunzia huku akidai kuwa vitu vingi vimerahishishwa.
“Kila kitu kipo mtandaoni kuanzia masomo na sehemu ya kuhifadhi taarifa za malipo”, alisema Mwanaidi.
Alisema wameelekezwa kuwatambua waratibu wa programu ambao ndio waongoza njia katika safari yao ya masomo kwa kuwa wana taarifa muhimu katika programu wasomazo.
Kwa upande wake, Beatus Kamugisha mdahiliwa wa Shahada ya Uzamili ya Usimamizi wa Maktaba na Habari alisema amejipanga vyema kuanza masomo na kwamba mafunzo elekekezi yamemsaidia kujua namna ya kusoma hususani kwa mfumo wa elimu huria na masafa ambao nyezo yake kuu ni mtandao.
“Tumefundishwa mifumo ya kusomea, matumizi ya programu tumizi kama vile Zoom na namna ya kutoa mrejesho kwa walimu kwa kazi za darasani”, alisema Kamugisha.
Mdahiliwa wa Shahada ya Uzamivu katika masuala ya kibenki na mifumo ya malipo katika Kitivo cha Usiamizi wa Biashara, William Fidelis alisema mafunzo elekezi n muhimu lakini kuna sehemu ya wajibu kati ya mwanafunzi na msimamizi wa utafiti.
“Mafunzo elekezi yametoa matumaini na mwanga kwa wadahiliwa hususani sisi ambao ni watu wazima kwa kuwa tumepata miongozo itakayotusaidia kuenenda katika safari ya masomo”, alisema William.
Alisema elimu ya utu uzima ina changamoto hususani elimu huria na masafa ambayo mwanafunzi anasoma kwa namna ya kutokakaa darasani ambapo atatakiwa kuwa makini zaidi ili aendane na matakwa ya asomeacho kwa miongozo iliyopo.
“Uthabiti na usaidizi wa msimamizi kwa mwanafunzi ndio kitu muhimu ili kuhakikisha kuwa hakuna anayemfelisha mwingine”, alisema William.
Mratibu wa Idara Usimamizi na Kumbukumbu wa Kurugenzi ya Masomo ya juu chuoni hapo, Mhadhiri Mary Ogondiek alielezea wajibu wa mwanafunzi na msimamizi katika mchakato wa utafiti huku akiwataka wanafunzi kujenga utaratibu wa mawasiliano ya mara kwa mara na wasimamizi wao.